Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Maonyesho ya Roki Singeweza kuepuka kufikiri kwamba makala “Vijana Huuliza . . . Je, Nihudhurie Maonyesho ya Roki?” (Desemba 22, 1995) ilikuwa na upendeleo kiasi fulani. Nilihudhuria onyesho la roki pamoja na mama yangu. Ilikuwa bendi ya kale, na umati ulikuwa na mwenendo mzuri. Lakini makala hiyo haikuonyesha hata uwezekano wa kupata onyesho lifaalo.
S. A., Marekani
Makala hiyo ilikazia hatari ziwezazo kutokea za maonyesho ya roki. Hata hivyo, hatukushutumu kabisa kuhudhuria matukio hayo. Tuliwaeleza wasomaji: “Ukifikiria kwenda kwenye maonyesho [ya roki], pata habari zifaazo.” Hivyo habari ilitolewa kusaidia vijana na wazazi wafanye uamuzi wenye usawaziko.—Mhariri.
Nataka kuwashukuru kwa makala hiyo. Majuma kadhaa tu kabla ya kupata gazeti hilo, baadhi yetu tulikwenda kwenye onyesho fulani. Hakukuwa na udhibiti, na wengi huko walilewa; hapakuwa mahali panapofaa Wakristo. Nilijifunza kutokana na kosa langu na natumaini wengine walijifunza pia.
M. E., Marekani
Kosta Rika Ningependa kufanya rekebisho fulani kuhusu makala “Kosta Rika—Nchi Ndogo, Unamna Mwingi.” (Julai 8, 1995) Mlitaarifu kwamba “karibu asilimia 27 ya ardhi imehifadhiwa, ulinganifu ulio mkubwa zaidi kuliko nchi nyingineyo ulimwenguni.” Hata hivyo, kulingana na World Almanac, Ekuado imetenga kando asilimia 40 ya eneo lote layo la bara kwa ajili ya uhifadhi.
M. E., Ekuado
Asante kwa rekebisho hilo.—Mhariri.
Mali Nilitoa machozi ya shangwe niliposoma makala “La Kwanza Katika Mali.” (Desemba 22, 1995) Roho ya ushirikiano ya washiriki wenu katika Mali ni yenye kuimarisha imani. Nimewasiliana na Mashahidi wa Yehova ili waanze kunifundisha Biblia. Ni azimio langu kushirikiana na washiriki wenu katika kumwabudu Mungu.
D. C. A., Nigeria
Ugonjwa wa Tourette Nataka kuwashukuru kwa makala yenu “Ugumu wa Kuishi na Ugonjwa wa Tourette.” (Desemba 22, 1995) Dalili zangu zilitoweka mwishoni mwa ubalehe wangu. Lakini mambo hayajakuwa mazuri kwa wote. Makala hii itakuwa msaada wenye thamani kwao na familia zao.
Y. L., Ufaransa
Najua mvulana fulani ambaye ana ugonjwa huo, na hadi sasa nimemwepuka kwa sababu niliona aibu kuwa pamoja naye. Sikuwa nimetambua kamwe kwamba huenda anahisi aibu kuuhusu kuliko nihisivyo!
P. M., Italia
Nimekuwa na tatizo hili tangu nilipokuwa na miaka mitano, nalo limenifanya niwe na huzuni sana. Nina mitetemo ya kimisuli na ya sauti. Wala wazazi wangu wala mimi hatukuweza kufahamu ni kwa nini mitetemo hii ilitokea; walikuwa na wasiwasi kwamba labda kulikuwa na kasoro fulani katika njia waliyonilea. Nimesali kwa Yehova anisaidie kufahamu, naye amejibu sala yangu kupitia makala hii. Nilitiwa moyo sana kusoma maono ya wengine miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ambao wamekuwa na tatizo lilo hilo.
Y. K., Japani
Nimeishi katika hali hii kwa karibu maisha yangu yote, lakini ilikuwa tangu 1983 tu kwamba nimejua ilikuwa nini. Nilipokuwa mtoto, mara nyingi wengine walinicheka. Lakini akina ndugu na dada kwenye Jumba la Ufalme sikuzote walikuwa wenye upendo na wakaikubali kuwa sehemu yangu. Baadaye, nilimpenda mwanamume mmoja mchanga Mkristo. Yeye alifahamu vizuri sana tatizo langu. Ingawa baba yangu alifikiri ndoa yetu haitadumu, nafurahi kusema kwamba miaka 30 baadaye tungali tumeoana kwa furaha. Mume wangu sikuzote hunitendea kama dhahabu na hajaruhusu kamwe tatizo langu limsumbue au kumwaibisha.
F. H., Kanada