Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 12/22 kur. 17-19
  • Je, Nihudhurie Maonyesho ya Roki?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Nihudhurie Maonyesho ya Roki?
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuujaribu Huo Muziki
  • Ukosefu wa Udhibiti
  • Uwezo wa Mazingira
  • Jilinde na Muziki Usiofaa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ninaweza Kuwa na Usawaziko Jinsi Gani Kuhusu Muziki?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Ninaweza Kuwekaje Muziki Mahali Pao Panapofaa?
    Amkeni!—1993
  • Muziki Waweza Kweli Kuniumiza?
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 12/22 kur. 17-19

Vijana Huuliza. . .

Je, Nihudhurie Maonyesho ya Roki?

Bendi ijulikanayo sana inakuja mjini kwenu. Tikiti zauzwa kwa haraka, kwa hiyo lazima uamue sasa. Je, utahudhuria?

MUZIKI wenye kujenga katika mazingira yafaayo waweza kuwa wenye kufurahisha. Kwa vyovyote, Yehova Mungu alituumba tukiwa na uwezo wa kufurahia muziki, na unamna-namna mwingi wa muziki unakubalika kwake.

Miongoni mwa vijana leo, muziki unaopendelewa sana kwa kawaida ni muziki wa roki katika namna zao nyingi. Wengi huufurahia zaidi unapochezwa wakiwepo mahali unapochezwa. Hata hivyo, miongoni mwa mambo mengine, ripoti za fujo na mwenendo usiodhibitiwa kwenye maonyesho ya roki hutokeza maswali mazito kwa vijana wenye kumhofu Mungu. Ni nini hasa huendelea kwenye maonyesho ya roki? Je, lingekuwa wazo zuri kuhudhuria mmoja?

Kuujaribu Huo Muziki

Kwanza ebu tufikirie muziki wenyewe. Muziki waweza kuonyesha—na kuamsha—namna nyingi za hisia. Katika nyakati za Biblia, watu wa Mungu mara nyingi walitumia muziki kuonyesha upendo wao kwa Mungu. (Zaburi 149:3; 150:4) Muziki pia ulitumiwa kuonyesha shangwe, msisimko, na huzuni. (Mwanzo 31:27; Waamuzi 11:34; 1 Samweli 18:6, 7; Mathayo 9:23, 24) Ingawa hivyo, kwa kusikitisha, muziki haukuwa sikuzote wenye kujenga hata katika nyakati za Biblia. Muziki mpotovu, wenye ashiki huenda ulichangia kuchochea baadhi ya Waisraeli kutenda dhambi wakati taifa hilo lilipopiga kambi kwenye Mlima Sinai.—Kutoka 32:1-6, 17, 18, 25.

Kusema kweli, mwingi wa muziki wa roki vivyohivyo huchochea mambo mabaya—ukosefu wa adili katika ngono, dawa za kulevya, uasi, uwasiliani-roho. Hili halimaanishi ujiepushe kabisa na muziki, lakini Biblia huambia Wakristo “mkihakiki ni nini impendezayo Bwana.” (Waefeso 5:10) Kwa hiyo ni lazima uwe mteuzi na mwenye utambuzi kuhusiana na muziki.a

Uchaguzi wako wa muziki hukuathirije? Je, hukufanya uhisi furaha, utulivu au mwenye amani? Au hukufanya uhisi hasira, uasi, au kushuka moyo? Mwanamume mmoja Mkristo katika Denmark akumbuka siku alizokuwa shabiki wa mdundo mzito, aina ya muziki wa roki. Yeye asema hivi: “Ningeusikiliza nilipokuwa nikifanya kazi. Na kama nilifanya kosa, ningekasirika mno hivi kwamba ningevunja-vunja kitu nilichokuwa nikikifanyia kazi na kukitupa kwa hamaki!” Kijana mwingine akiri hivi: “Nilisikiliza muziki wa rapu na mdundo mzito mwingi ambao ulitukuza ngono na mtindo-maisha wa kilimwengu. Muziki huu ulijaza akili yangu, na tokeo lilikuwa kutamani mambo waliyokuwa wakiimba kuyahusu.” Sasa ikiwa mrekodio mmoja tu waweza kuwa na athari kama hiyo, wazia uwezo wa wonyesho ambao upo pale!

Fikiria pia: Muziki huo utakuwa wenye sauti kubwa kadiri gani? Ni kweli, watu wana mapendezi tofauti kuhusiana na hili. Nayo Biblia haikatazi muziki wenye sauti ya juu ya kiasi. Kwani, kwenye kuwekwa wakfu kwa hekalu la Sulemani, wapiga tarumbeta pekee walikuwa 120! (2 Mambo ya Nyakati 5:12) Lazima hiyo ilikuwa sauti ya juu mno! Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya mpaazo wa sauti kubwa wa sifa kwa Mungu na muziki wa roki wenye kupasua masikio. Katika hicho kisa cha mwisho, hali ya sauti kubwa mara nyingi hutumiwa kuchochea umati kuingia katika roho ya kutojizuia kabisa. Lakini Biblia yashutumu “sherehe zenye kelele,” au “karamu zenye vurugu.” (Wagalatia 5:21; Byington) Na staha kwa mwili wako ingekataza kusikiliza muziki wa kiasi cha sauti ya juu mno hivi kwamba unajiweka katika hatari ya kuharibu kusikia kwako.—Warumi 12:1.

Jambo jingine la kufikiria latokezwa kwenye Ayubu 12:11. Hapo Biblia huuliza hivi: “Je! sikio silo lijaribulo maneno, kama vile kaakaa lionjavyo chakula?” Kupatana na hili, unapaswa ‘kujaribu’ maneno ya huo wimbo! Kijana mmoja Mkristo akiri hivi: “Nilianza kusikiliza maneno ya baadhi ya nyimbo nilizopenda, na kwa mshangao wangu hayakufaa kwa Mkristo kuyasikiliza. Niliona likiwa jambo la muhimu kuuharibu muziki huo.” (1 Wakorintho 14:20; Waefeso 5:3,4) Pata onyo kimbele pia, kwamba wanamaonyesho wengi hutumia maonyesho ya roki ili kuendeleza matoleo yao ya karibuni zaidi—muziki ambao huenda ulikuwa tofauti kabisa na ule wa hapo awali, labda ulikuwa muziki wenye kujenga zaidi.

Kwa kuongezea, unapaswa kuwa na uhakika kwamba huo muziki hauna madokezo ya kishetani—jambo ambalo kihususa ni mashuhuri sana katika namna za muziki wa mdundo mzito. Wanabendi wa mdundo mzito wanajulikana sana kwa kujipamba wenyewe na kaseti zao kwa mifano ya kishetani na mapambo ya kishetani. (Yakobo 3:15) Kuhudhuria maonyesho yanayofanywa na kikundi kama hicho hakungempendeza Mungu hata kidogo, ambaye hutuamuru ‘tumpinge Ibilisi!”—Yakobo 4:7.

Ukosefu wa Udhibiti

Ni nini ambacho huenda kitukie kwenye maonyesho yenyewe? Msichana mmoja tineja aitwaye Stacey alikwenda pamoja na rafiki zake kuona bendi ambayo walihisi ilicheza muziki usio na hatia kwa kadiri fulani. Lakini maonyesho yalipofika katikati, mwimbaji mwenye kuongoza bendi alimwigiza mvumbuaji wa habari za roho waovu na kualika wasikilizaji waungane naye katika kujaribu kuwasiliana na ulimwengu wa roho! Je, ulikuwa mzaha tu? Labda. Lakini kwa kuwa Biblia yashutumu uwasiliani-roho katika njia yoyote ile, Stacey na rafikize walihisi wakiwajibika kuondoka mara moja.—Mambo ya Walawi 19:31; Kumbukumbu la Torati 18:10-13; Ufunuo 22:15.

Vijana wengine Wakristo wamekuwa na mambo waliyojionea kama hayo yenye kutesa, kwa kuwa ingawa uwasiliani-roho ulio dhahiri huenda ukatukia mara chache kwenye maonyesho ya roki, mwenendo usiodhibitiwa ni wa kawaida. Kwenye wonyesho mmoja bendi ilisaidia kuchochea fujo ambayo ilitokeza kuumia kwa watu 60 na uharibifu wa zaidi ya dola 200,000! Na kwenye wonyesho mwingine tena, vijana watatu walivunjwa-vunjwa hadi kifo. Ni kweli, maonyesho mengi ya roki hayamalizikii katika fujo, maumizo, au vifo. Lakini kuna uhitaji ulio wazi wa tahadhari. Mithali 22:3 husema hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”

Kwa hiyo ukifikiria kwenda kwenye maonyesho, pata habari zifaazo. Je, hiyo bendi ina sifa ya kuchochea mwenendo usioweza kudhibitiwa? Bendi hiyo huvutia aina gani ya wasikilizaji? (1 Wakorintho 15:33) Utumizi wa alkoholi na dawa za kulevya huendelezwa kwa kiwango gani? Namna gani jumba la maonyesho lenyewe? Je, limepata kuwa na matatizo ya usalama katika wakati uliopita? Kutakuwa na mipango gani ya kuketi? Wakati watu huketi mahali popote wanapotaka, uwezekano wa mtu kuumizwa huongezeka sana.

Matumizi mabaya ya dawa za kulevya na alkoholi yameenea sana kwenye maonyesho ya roki. “Watu hawaji kwa ajili ya muziki,” akasema mwanamume mmoja Mkristo aliyetoka katika hali ya kupumbazika ambaye katika ujana wake alihudhuria wonyesho uliofanywa na bendi ya asili ya roki. “Wanakuja kulewa.” Yeye aliamua kwamba huo ulikuwa wonyesho wake wa mwisho wa roki. Msichana mmoja Mkristo aliye tineja anaripoti vivyohivyo: “Nakumbuka nikienda kwenye wonyesho ambapo bendi ‘yenye kutumia mawazo mapya’ ilikuwa ikicheza. Lilikuwa jambo lenye kuogofya mno! Watu walikuwa wakivuta bangi. Lugha ilikuwa mbaya mno, na wengi hapo walionekana kama waabudu wa Shetani kwa sababu ya jinsi walivyokuwa wamevalia.” Hata mahali ambapo dawa za kulevya na alkoholi vimekatazwa kabisa, si jambo lisilo la kawaida kwa wengi katika wasikilizaji kuja wakiwa wamelewa tayari. Je, kuhudhuria tukio kama hilo kunaweza kupatana na amri ya Biblia ya “kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi”?—Tito 2:12.

Uwezo wa Mazingira

Ingawa hivyo, huenda ukahisi kwamba hakuna uhitaji wa kuwa na wasiwasi juu ya jinsi wale walio kando yako wanavyotenda mradi hujiungi nao katika fujo mwenyewe. Hata hivyo, mazingira yako hukuathiri. Kwenye Waefeso 2:2 (New World Translation), Biblia inasema juu ya “mamlaka ya hewa, ile roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kuasi.” Ona kwamba ulimwengu huu una “roho,” au mtazamo wa akilini ulioenea sana. Iko kila mahali, imeenea kama hewa yenyewe. Lakini tazama pia kwamba roho hii, au mtazamo, ina “mamlaka”—uwezo wa kubadili mawazo yako, hisia na mwenendo—ikiwa utajiachilia kwayo! Huwezi hata kidogo kupumua hewa hii yenye uwezo na usiathiriwe!

Katika visa vingi maonyesho ya roki ni kujiweka kabisa chini ya uvutano wa roho ya ulimwengu. Mtu anaweza kuvutwa kwa urahisi ndani ya ile hali iliyochafuka ambayo kwa kawaida huenea—au katika kupiga mayowe na kupunga mikono ambako humalizikia kwenye kuheshimu wachezaji kunakokaribia ibada. Kusifu huko kwa kupita kiasi hupokonya heshima ambayo ni ya Mungu kupatana na haki. Huwa ni ibada ya sanamu, jambo ambalo linashutumiwa waziwazi katika Maandiko. (1 Wakorintho 10:14; 1 Yohana 5:21) Je, unataka kujihatarisha kwa kujihusisha nayo?

Ni jambo lisiloweza kuleta bishano kusema kwamba maonyesho yaliyo mengi ya roki huhusisha hatari ambazo hufunika manufaa zozote ambazo huenda mtu akapata kwa kuyahudhuria. Bila shaka, wazazi wako wana haki ya kufanya uamuzi wa mwisho kama utaruhusiwa kuhudhuria au kutohudhuria wonyesho fulani. Lakini ikiwa una uhuru wa kufanya uamuzi huo mwenyewe, chagua kwa hekima. Kuna njia nyingi za kujifurahisha ambazo ni zenye kujenga na hazihusishi zile hatari za kuhudhuria maonyesho ya roki.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Vijana Huuliza . . . ” juu ya muziki zinazopatikana katika matoleo ya Amkeni! ya Februari 8, Februari 22, na Machi 22, 1993.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Alkoholi, dawa za kulevya, na mwenendo wenye fujo ni mambo ya kawaida kwenye maonyesho ya roki

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki