Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 4/15 kur. 19-24
  • Jilinde na Muziki Usiofaa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jilinde na Muziki Usiofaa!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Matumizi Mabaya ya Muziki
  • Uhitaji wa Kujihadhari
  • Muziki wa Rapu (Maongezi)—Muziki wa Uasi
  • Muziki Wenye Mdundo Mzito—Ngono, Jeuri, na Ushetani
  • Kuvuna Kile Unachopanda
  • Jilinde
  • Muziki Wangu Una Ubaya Gani?
    Amkeni!—1993
  • Muziki Waweza Kweli Kuniumiza?
    Amkeni!—1993
  • Je, Utafanya Maamuzi Yenye Hekima?
    Amkeni!—2011
  • Ninaweza Kuwekaje Muziki Mahali Pao Panapofaa?
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 4/15 kur. 19-24

Jilinde na Muziki Usiofaa!

“Angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.”—WAEFESO 5:15, 16.

1. Kwa nini muziki waweza kuitwa “zawadi ya kimungu”?

“MUZIKI . . . ni zawadi ya kimungu.” Ndivyo alivyoandika Lulu Rumsey Wiley katika kitabu chake Bible Music. Kutoka nyakati za mapema zaidi, wanaume na wanawake wenye kumhofu Mungu wametambua hisia hiyo. Kupitia muziki, mwanadamu ameonyesha hisiamoyo zake za ndani kabisa—shangwe, huzuni, hasira, na upendo. Hivyo muziki ulishiriki sehemu ya maana katika nyakati za Biblia, ukiwa umetajwa kotekote katika kitabu hicho kitakatifu.—Mwanzo 4:21; Ufunuo 18:22.

2. Muziki ulitumiwaje kumsifu Yehova katika nyakati za Biblia?

2 Muziki ulitokezwa kwa njia bora zaidi katika ibada ya Yehova.a Baadhi ya maneno ya sifa yenye ubora wa hali ya juu zaidi yaliyopata kutolewa kwa Yehova Mungu wakati wowote ule yalitumiwa katika muziki mwanzoni. “Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo,” akaandika mtunga zaburi Daudi. (Zaburi 69:30) Muziki ulitumiwa wakati wa upweke ukiandamana na fikira za sala. “Nakumbuka wimbo wangu usiku, nawaza moyoni mwangu, roho yangu ikatafuta,” akaandika Asafu. (Zaburi 77:6) Katika hekalu la Yehova, muziki ulipangwa kwa kadiri kubwa. (1 Mambo ya Nyakati 23:1-5; 2 Mambo ya Nyakati 29:25, 26) Nyakati nyingine, vikundi vikubwa sana vya kimuziki vilipangwa, kama vile wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu, wakati wapiga tarumbeta 120 walipotumiwa. (2 Mambo ya Nyakati 5:12, 13) Hatuna rekodi yoyote juu ya jinsi muziki huo wenye fahari ulivyosikika, lakini kitabu The Music of the Bible huonelea hivi: “Halitakuwa jambo gumu kutoa maoni juu ya matokeo ya ujumla ya muziki wa Hekalu wakati wa pindi zenye uzito . . . Ikiwa mmoja wetu angeweza kusafirishwa hadi miongoni mwa mandhari moja kama hiyo, hisi yenye nguvu sana ya kicho na fahari isingeepukika.”

Matumizi Mabaya ya Muziki

3, 4. Zawadi ya muziki ilitumiwaje vibaya na watu wa Mungu na majirani wao wapagani?

3 Hata hivyo, muziki haukutumiwa sikuzote kwa njia hiyo yenye ubora wa juu sana. Kwenye Mlima Sinai, muziki ulitumiwa kuchochea ibada ya sanamu ya ndama wa dhahabu. (Kutoka 32:18) Pindi nyingine muziki ulifungamanishwa pia na mwenendo wa ulevi na hata umalaya. (Zaburi 69:12; Isaya 23:15) Majirani wapagani wa Waisraeli walikuwa na hatia iyo hiyo ya kutumia vibaya zawadi hiyo ya kimungu. “Katika Foiniki na Siria,” yasema The Interpreter’s Dictionary of the Bible, “karibu muziki wote uliopendwa sana ulionyesha ibada ya Istari, yule kijimungu-kike cha uzazi. Hivyo, muziki uliopendwa sana ulikuwa kwa ukawaida utangulizi wa karamu za kingono.” Wagiriki wa kale vilevile walitumia muziki kuandamana na “dansi za kiashiki” zilizopendwa sana.

4 Naam, muziki una nguvu za kuchochea, za kusisimua, na za kuvuta. Miongo kadhaa iliyopita, kitabu cha John Stainer The Music of the Bible kilifikia hatua hata ya kudai hivi: “Hakuna ufundi mwingine ulio na uvutano wenye nguvu sana juu ya jamii ya kibinadamu wakati huu kama ufundi wa Muziki.” Muziki waendelea kuwa na uvutano wenye nguvu leo. Kwa hiyo, aina ya muziki isiyofaa yaweza kuwa yenye hatari ya kweli kwa vijana wanaomhofu Mungu.

Uhitaji wa Kujihadhari

5. (a) Muziki una sehemu gani kubwa katika maisha ya matineja wengi? (b) Maoni ya Mungu ni nini juu ya vijana kujifurahisha wenyewe?

5 Ikiwa wewe ni kijana, basi wajua vema jinsi muziki ulivyo wa maana—hasa namna-namna za muziki unaopendwa au wa roki—kwa vijana wengi wa rika lako. Muziki umeitwa “sehemu ya umetaboli wa matineja” (jambo la muhimu sana kwa matineja). Imekadiriwa kwamba katika miaka yake sita ya mwisho shuleni, kijana wa kawaida katika United States atasikiliza zaidi ya muda wa saa nne za muziki wa roki kwa siku! Hilo kwa hakika laonyesha ukosefu wa usawaziko. Si kwamba kuna ubaya wowote na kufurahia jambo fulani linalokufanya uhisi vizuri au uwe mwenye furaha. Kwa hakika, Yehova, Muumba wa muziki wenye kufurahisha, hawatazamii vijana wawe wenye uchungu na huzuni. Kwa kweli, yeye huwaamuru watu wake hivi: “Mfurahieni BWANA [Yehova, NW], shangilieni, enyi wenye haki. Pigeni vigelegele vya furaha; ninyi nyote mlio wanyofu wa moyo.” (Zaburi 32:11) Neno lake husema hivi kwa vijana: “Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako.”—Mhubiri 11:9.

6. (a) Kwa nini vijana wanahitaji kujihadhari katika uchaguzi wao wa muziki? (b) Kwa nini muziki mwingi leo ni wenye kutokubalika zaidi kuliko muziki wa vizazi vilivyotangulia?

6 Hata hivyo, kuna sababu nzuri ya wewe kuwa mwenye kujihadhari katika uchaguzi wako wa muziki. Mtume Paulo alisema kwenye Waefeso 5:15, 16: “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.” Vijana wengine huenda wakapinga, kama msichana mmoja mchanga alivyopinga: “Wazazi wetu waliweza kusikiliza muziki wao walipokuwa vijana. Kwa nini sisi tusiweze kusikiliza wetu?” Baadhi ya muziki ambao wazazi wako walisikiliza walipokuwa umri wako huenda ikawa ulikuwa na sehemu zao zisizokubalika. Vinapochunguzwa kwa ukaribu, viwango vingi vinavyopendwa na wengi huwa na idadi yenye kushangaza ya vidokezo vya kingono na marejezeo yaliyofichwa ya ukosefu wa adili. Lakini jambo lililokuwa likidokezwa tu wakati mmoja sasa husimuliwa waziwazi. Mwandikaji mmoja aonelea hivi: “Watoto sasa wanashambuliwa na ujumbe mbalimbali unaoeleza mambo waziwazi kwa kadiri ambavyo utamaduni wetu haujapata kuona wakati wowote.”

Muziki wa Rapu (Maongezi)—Muziki wa Uasi

7, 8. (a) Muziki wa rapu ni nini, na ni nini kinachosababisha upendwe sana? (b) Ni nini huenda kikamtambulisha mtu kuwa mfuasi wa mtindo-maisha wa rapu?

7 Kwa mfano, fikiria kule kuenea sana kwa muziki wa rapu. Kulingana na gazeti la Time, muziki wa rapu umekuwa “kwa hakika, badiliko kubwa la mdundo duniani pote” na unapendwa sana katika Brazili, Ulaya, Japani, Urusi, na United States. Mara nyingi bila muziki wowote, maneno yao yanatamkwa, si kuimbwa, mdundo wenye nguvu ukiandamana nayo. Lakini, ni mdundo huo wenye kusukuma unaoonekana kuwa ndiyo siri ya mafanikio makubwa ya kibiashara ya muziki wa rapu. “Ninaposikiliza muziki wa rapu,” asema kijana mmoja Mjapani, “ninahisi kusisimuka, na ninapocheza dansi, ninajihisi kuwa huru.”

8 Maneno ya rapu—mara nyingi yakiwa mchanganyiko usio na busara wa maneno machafu na maongezi yasiyo na ufasaha—yaonekana kuwa ndiyo sababu nyingine ya muziki wa rapu kupendwa sana. Tofauti na maneno ya zamani ya roki, ambayo mengi yayo hukazia hasa habari ya kimahaba ya matineja, maneno ya rapu yana ujumbe mzito zaidi. Rapu nyingine hulaumu ukosefu wa haki, ubaguzi wa rangi, na ukatili wa polisi. Lakini, nyakati nyingine sehemu za kurudiwa-rudiwa zenye maneno yanayopatana hunenwa katika lugha chafu zaidi, yenye kushtua sana iwazikavyo. Muziki wa rapu huonekana pia kuwa uasi dhidi ya viwango vya mavazi, mapambo, na adili za kingono. Haishangazi kwamba, muziki wa rapu umekuja kuwa mtindo-maisha wa aina yao wenyewe. Wafuasi wao hutambulishwa kwa ishara zao za mikono zenye kupita kiasi, maongezi yao yasiyo na ufasaha, na mavazi yao—suruali kubwa-kubwa za aina ya jeans, viatu vya kuchezea vinavyofika juu ya vifundo vya miguu, ambavyo havikufungwa kamba, mikufu ya dhahabu, kofia za wachezaji besiboli, na miwani ya jua.

9, 10. (a) Vijana wanapaswa wafikirie mambo gani ili kuamua kama muziki wa rapu na mtindo-maisha wao ‘unampendeza Bwana’? (b) Baadhi ya vijana Wakristo hawaonekani kuchukua nini kwa uzito?

9 Kwenye Waefeso 5:10, Wakristo huambiwa “[wahakiki] ni nini impendezayo Bwana.” Ukifikiria ile sifa ambayo muziki wa rapu umejifanyia wenyewe, je, unafikiri muziki huo ‘ungempendeza Bwana’ kadiri ambavyo waweza kujishirikisha nao? Je! kijana Mkristo angetaka kutambulishwa na mtindo-maisha unaoonwa kuwa haukubaliki hata na walimwengu wengi? Ona vile mwandikaji mmoja wa maoni alivyosimulia maonyesho fulani ya muziki wa rapu: “Wanamuziki hao wa rapu walishindana kuwa wenye kushtua zaidi kwa maneno machafu ya kingono na yenye kueleza mambo waziwazi. . . . Wacheza dansi wanaume na wanawake waliiga vitendo vya ngono jukwaani.” Kuhusu maonyesho fulani yenye kutokeza, mwendelezi mmoja wa maonyesho alisema hivi: “Kila neno kutoka kinywani mwao ni (la aibu).”

10 Hata hivyo, muziki uliochezwa usiku huo haukuonwa hata kidogo kuwa tofauti sana na muziki wa kawaida wa rapu. Mkurugenzi wa jumba la maonyesho hayo alisema hivi: “[Muziki] unaosikia ni rapu ya kawaida—sawasawa na ule wanaonunua dukani.” Ni jambo la kusikitisha kama nini kwamba miongoni mwa wale vijana 4,000 na zaidi waliohudhuria maonyesho hayo mlikuwamo wengine wanaodai kuwa Mashahidi wa Yehova! Yaonekana kwamba wengine hawachukui kwa uzito uhakika wa kwamba Shetani ndiye “mfalme wa uwezo wa anga.” Yeye hutawala ‘roho ile [au, mtazamo mkuu wa kiakili] itendayo kazi sasa katika wana wa kuasi.’ (Waefeso 2:2) Ungetumikia masilahi ya nani ikiwa ungejihusisha na muziki wa rapu au na mtindo-maisha wa rapu? Ni kweli, muziki mwingine wa rapu hauna habari nyingi isiyokubalika. Lakini, je, ni jambo la kiakili kuanza kupendezwa na aina yoyote ya muziki ambayo sanasana huudhi viwango vya Kikristo?

Muziki Wenye Mdundo Mzito—Ngono, Jeuri, na Ushetani

11, 12. Muziki wenye mdundo mzito ni nini, na muziki huo hutokeza mambo gani yasiyokubalika?

11 Namna nyingine ya muziki inayopendwa sana ni ile yenye mdundo mzito. Mdundo mzito unahusisha zaidi ya roki yenye mdundo mzito yenye sauti ya juu. Ripoti moja katika The Journal of the American Medical Association yasema hivi: “Muziki wenye mdundo mzito . . . una mdundo wenye sauti ya juu unaopigapiga na una maneno mengi yanayotukuza chuki, matumizi mabaya, upotovu wa kingono, na ushetani wa mara kwa mara.” Kwani, majina yenyewe ya baadhi ya bendi zinazopendwa zaidi yanathibitisha hali ya kushusha heshima ya aina hiyo ya roki. Yanatia ndani maneno kama vile “sumu,” “bunduki,” na “kifo.” Hata hivyo, muziki wenye mdundo mzito waonekana wenye upole zaidi unapolinganishwa na ule mdundo mzito unaokaribia sana ile roki ya punki (inayoonyesha kutoridhika na jamii) na ule mdundo mzito unaokazia vichwa vya kifo—namna nyinginezo zaidi za muziki wenye mdundo mzito. Majina ya bendi hizo hutumia kwa faida zao maneno kama vile “mtu mla nyama ya mwanadamu” na “tanzia.” Vijana katika mabara mengi huenda wasing’amue jinsi majina hayo yalivyo yenye kuchukiza kwa sababu yamo katika Kiswahili au lugha nyingine ya kigeni.

12 Muziki wenye mdundo mzito umefungamanishwa tena na tena na kujiua kwa matineja, kushuka moyo, na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. Uhusiano wao na mwenendo wa jeuri ulimfanya mshauri mmoja wa redio aupatie jina la fumbo la “muziki wa kutumia kuwaua wazazi wako.” Ni uhusiano wao na ushetani unaowahofisha wazazi wengi—na maofisa wa polisi. Mpelelezi mmoja alidai kwamba vijana fulani waliojihusisha na ibada ya kishetani waliingizwa katika uwasiliani-roho kupitia muziki huo. “Hawajui wanachojihusisha nacho,” akamalizia.

13. Ni nini hatari ya kuhusika na muziki wenye mdundo mzito?

13 Hata hivyo, vijana Wakristo hawapaswi ‘kukosa kujua fikira za Shetani.’ (2 Wakorintho 2:11) Kwani, “kushindana kwetu . . . ni . . . juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.” (Waefeso 6:12) Lingekuwa jambo la kipumbavu kama nini, kwa mtu kuwaalika roho waovu maishani mwake, kupitia uchaguzi wake wa muziki! (1 Wakorintho 10:20, 21) Hata hivyo, ni wazi kwamba vijana Wakristo kadhaa hupenda sana muziki huo. Wengine wameamua kutumia njia za kisiri ili kuridhisha hamu zao za kimuziki. Msichana mmoja mchanga aungama hivi: “Nilikuwa nikisikiliza muziki wenye mdundo mzito, nyakati nyingine karibu usiku kucha. Nilikuwa nikinunua magazeti ya [mashabiki wa] muziki wenye mdundo mzito na kuwaficha wazazi wangu kwa kuyaweka katika vibweta vya viatu. Niliwaambia wazazi wangu uwongo. Najua Yehova hakupendezwa na mimi.” Alirekebishwa fikira na makala moja katika gazeti la Amkeni! Ni vijana wengine wangapi ambao huenda bado wakanaswa na mtego wa muziki huo?

Kuvuna Kile Unachopanda

14, 15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba kusikiliza muziki usiofaa kutatuathiri isivyofaa? Toa kielezi.

14 Usipunguze hatari ya muziki huo. Ni kweli, huenda usiwe na mwelekeo wa kumwua mtu au kutenda ukosefu wa adili katika ngono kwa sababu tu ulisikiliza wimbo mmoja. Hata hivyo, Wagalatia 6:8 husema hivi: “Yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu.” Kusikiliza muziki ulio wa kidunia, wa kinyama, na hata wa kishetani kwaweza kukuathiri kwa njia isiyofaa. (Linganisha Yakobo 3:15.) Profesa mmoja wa muziki Joseph Stuessy ananukuliwa akisema hivi: “Muziki wowote unaathiri hali zetu, hisiamoyo zetu, mitazamo yetu, na mwenendo wetu wa mwisho . . . Yeyote asemaye, ‘Naweza kusikiliza muziki wenye mdundo mzito, lakini hauniathiri,’ hasemi kweli hata kidogo. [Muziki huo] unaathiri tu watu tofauti-tofauti katika viwango tofauti-tofauti na njia tofauti-tofauti.”

15 Kijana mmoja Mkristo akiri hivi: “Nilihusika sana katika muziki wenye mdundo mzito unaokaribia roki ya punki hivi kwamba utu wangu mzima ulibadilika.” Punde alianza kupata matatizo na roho waovu. “Mwishoni nilitupilia mbali rekodi na tepu zangu nikaachiliwa na roho waovu.” Kijana mwingine akiri hivi: “Muziki niliokuwa nikisikiliza ulihusisha ama uwasiliani-roho, dawa za kulevya, ama ngono. Vijana wengi husema huo hauwaathiri, lakini unawaathiri. Nilikuwa karibu nimeacha kweli kabisa.” Mithali moja husema hivi: “Je! mtu aweza kutia moto kifuani pake, na nguo zake zisiungue?”—Mithali 6:27.

Jilinde

16. Ni nini laweza kusemwa juu ya watungaji na waimbaji wa muziki mwingi wa leo?

16 Paulo aliwaandikia Wakristo katika Efeso la kale hivi: “Basi nasema neno hili, tena nashuhudia katika Bwana, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao.” (Waefeso 4:17, 18) Je! hilo haliwezi kusemwa juu ya watungaji na waimbaji wa muziki mwingi wa leo? Zaidi ya wakati mwingine wowote, muziki wa aina zote huonyesha uvutano wa “mungu wa dunia hii,” Shetani Ibilisi.—2 Wakorintho 4:4.

17. Vijana wanaweza kujaribuje, au kutahinije, muziki?

17 Kuhusu “siku za mwisho,” Biblia ilitabiri hivi: “Watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu.” (2 Timotheo 3:1, 13) Basi, zaidi ya wakati mwingine wowote, utahitaji kuwa mwangalifu sana juu ya muziki unaochagua. Mara nyingi, kichwa kibaya ndicho huonyesha kwamba rekodi haifai. Ayubu 12:11 huuliza hivi: “Je! sikio silo lijaribulo maneno, kama vile kaakaa lionjavyo chakula?” Katika njia iyo hiyo, wewe waweza kutahini muziki kwa kusikiliza sehemu kwa kutumia sikio lenye kuchambua-chambua. Muziki huo unaamsha hisi gani ndani yako? Je! unachochea mwenendo wa kishenzi, wenye kushusha heshima—roho ya sherehe yenye kelele za ulevi? (Wagalatia 5:19-21) Namna gani maneno au mashairi ya muziki? Je! yanachochea ukosefu wa adili katika ngono, utumizi mbaya wa dawa za kulevya, au mabaya mengine ambayo “ni aibu hata kuyanena”? (Waefeso 5:12) Biblia husema kwamba mambo hayo hayapasi ‘kutajwa kamwe’ miongoni mwa watu wa Mungu, licha ya kuunganishwa na mdundo na kurudiwa tena na tena. (Waefeso 5:3) Namna gani mapambo ya kifuniko? Je! yanatia ndani vikao vya kishetani au picha zinazoamsha nyege?

18. (a) Huenda baadhi ya vjiana wakahitaji kufanya mabadiliko gani kwa habari ya muziki? (b) Vijana wanaweza kuanzaje kupenda muziki ufaao zaidi?

18 Labda unahitaji kufanya mabadiliko fulani katika namna ya muziki unaochagua. Ikiwa una rekodi, tepu, na sahani za santuri zenye muziki usio na adili na wa kishetani unapaswa kuziondolea mbali mara moja. (Linganisha Matendo 19:19.) Hiyo haimaanishi kwamba huwezi kufurahia muziki; si muziki wote upendwao sana ambao haukubaliki. Vijana wengine wamejifunza pia kupenda aina nyingine mbalimbali za muziki na sasa hufurahia muziki fulani ulio bora sana, wa kitamaduni, wa jezi ulio na mdundo mwepesi, na namna nyinginezo za muziki. Tepu za Kingdom Melodies zimewasaidia vijana wengi waanze kupendezwa na muziki wa kiokestra (muziki wenye sauti mbalimbali) wenye kujenga.

19. Kwa nini ni jambo la muhimu kuweka muziki mahali pao?

19 Muziki ni zawadi ya kimungu. Lakini kwa vijana wengi, unakuwa kishughulishaji akili kisichofaa. Hao ni kama Waisraeli wa zamani waliofurahia kucheza “kinubi, na zeze, na matari, na filimbi, . . . lakini [hawakuangalia] kazi ya BWANA [Yehova, NW].” (Isaya 5:12) Fanya shabaha yako iwe kuweka muziki mahali panapoufaa na kuacha utendaji wa Yehova uwe hangaiko lako kuu. Uwe mteuzi na mwangalifu juu ya muziki unaochagua. Hivyo utaweza kutumia vizuri—wala si vibaya—zawadi hiyo ya kimungu.

[Maelezo ya Chini]

a Taifa la Israeli laonekana lilikuwa bora zaidi katika ufundi wa muziki. Masimulizi yenye kuchongwa mwambani ya Ashuru hufunua kwamba Mfalme Senakeribu alitaka wanamuziki Waisraeli kama ushuru kutoka kwa Mfalme Hezekia. Grove’s Dictionary of Music and Musicians yasema hivi: “Kutaka wanamuziki kama ushuru . . . kwa kweli halikuwa jambo la kawaida.”

Je! Wakumbuka?

◻ Kwa nini muziki waweza kuitwa zawadi ya kimungu?

◻ Muziki ulitumiwaje vibaya katika nyakati za kale?

◻ Muziki wa rapu na wenye mdundo mzito unatokeza hatari zipi kwa vijana Wakristo?

◻ Vijana Wakristo wanawezaje kuwa waangalifu katika uchaguzi wao wa muziki?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Katika nyakati za Biblia, mara nyingi muziki ulitumiwa ikiwa njia ya kumletea Yehova sifa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki