Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 2/22 kur. 25-27
  • Muziki Waweza Kweli Kuniumiza?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Muziki Waweza Kweli Kuniumiza?
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nguvu za Muziki
  • Usiofaa kwa Masikio na Macho
  • Je! Waweza Kukudhuru?
  • Jilinde na Muziki Usiofaa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Je, Utafanya Maamuzi Yenye Hekima?
    Amkeni!—2011
  • Ninaweza Kuwa na Usawaziko Jinsi Gani Kuhusu Muziki?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Muziki Wangu Una Ubaya Gani?
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 2/22 kur. 25-27

Vijana Wanauliza . . .

Muziki Waweza Kweli Kuniumiza?

TOM alikuwa mvulana wa kawaida mwenye miaka 14—mwanafunzi bora aliyependa kufanyia mema jirani zake. Lakini baada ya kununua mfumo wa stereo wenye bei, alianza kusikiliza muziki wenye mdundo mzito.

Tom akawa mpweke kabisa katika chumba chake. Akumbuka baba yake: “Nilikuwa nikisema, ‘Huwezi kukaa humo wakati wote na kusikiliza stereo yako.’” Lakini Tom aliendelea kusikiliza. Kisha, siku moja ya majira ya baridi, alimchoma mamake kisu akamuua kisha akajiua. “Waambieni wazazi wachunge muziki wanaosikiliza watoto wao,” aonya baba ya Tom mwenye huzuni nyingi. Siku kadhaa kabla ya mauaji hayo, Tom alikuwa ameimba kwa kurudia-rudia wimbo juu ya “damu na kuua mamako.”

Je! ni kisa chenye kupita kiasi? Hakika. Na ingawa mambo mengine bila shaka yalishiriki sehemu katika msiba huo, huo watoa uthibitisho wa jambo ambalo vijana wengi huelekea kupuuza: Muziki unaweza kukuathiri wewe! Huenda wewe usiwe shabiki wa muziki wenye mdundo mzito, wala haielekei kwamba wewe utakwenda huku na huku ukifanya vituko vyenye jeuri. Hata hivyo, muziki unaweza kukuathiri kwa njia ambazo hata huenda using’amue.

Nguvu za Muziki

Muziki una nguvu. Kwelikweli, unaweza kutokeza namna zote za hisia za kibinadamu—kuanzia na huzuni na huruma hadi upendo na shangwe. Muziki unaweza kutuliza mtu na kumchochea hasira. Unaweza kuchochea ujitoaji na kuendeleza upotovu. Basi, si ajabu kwamba tokea nyakati za kale, muziki umekuwa chombo chenye nguvu cha “Mungu wa dunia hii,” Shetani Ibilisi.—2 Wakorintho 4:4.

Kutoa kielezi: Muda mfupi baada ya Waisraeli kuokolewa kutoka utumwa katika Misri, waliacha ibada ya Yehova kwa ajili ya ile ya ndama wa dhahabu. Ni nini kilichoambatana na mwenendo wao wenye aibu? Ni muziki wa kutojizuia uliopotoka! (Kutoka 32:1-6, 17, 18) Na wakati Mfalme Nebukadreza mwenye majivuno alipoamuru raia zake waabudu sanamu ya kipagani, alitafutaje kuchochea watu wake kwenye harara ya kizalendo na kidini? Kwa kutumia muziki wenye kuchochea!—Danieli 3:1-7.

Kwa hiyo, twapaswa kutarajia Shetani atumie muziki kuongoza watu vibaya leo. Yeye ni “mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi.” (Waefeso 2:2) Muziki mwingi wa leo huonyesha roho ya uasi ya Shetani. Na si ajabu, kwa kuwa kwa sehemu kubwa zaidi huandikwa na wale ambao Biblia husema ‘waenenda katika ubatili wa nia zao, ambao akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu.’ Kwelikweli, ikiamuliwa kwa mitindo yao ya maisha, waimbaji, wanamuziki, na watungaji wapendwao na wengi ‘wamekufa ganzi.’—Waefeso 4:17-19.

Hivyo kusikiliza muziki wao kwaweza kutokeza hatari halisi kwa vijana Wakristo. Si kwamba muziki wote upendwao na wengi ni mbaya au kwamba muziki wa roki ndio muziki pekee ambao wahitaji kujitahadharishia.a Muziki usiofaa waweza kupatikana miongoni mwa mitungo ya kikawaida na opera pia. Lakini ingawa nyakati zilizopita muziki ulidokeza ukosefu wa adili, muziki mwingi wa leo huendeleza ufasiki kwa ujasiri usio na kifani.

Usiofaa kwa Masikio na Macho

Fikiria muziki wenye mdundo mzito—namna hususa ya muziki wa roki wenye kudhuru sana ambao kwa kawaida hupigwa kwa sauti kubwa kupita kiasi. Bendi za muziki wenye mdundo mzito hutumia kwa majivuno majina kama Poison, Skid Row, Guns N’ Roses, na Slayer. Gazeti Time lilisema hivi: “Majina ya bendi pekee hutokeza picha za jeuri, mateso na kifo.” Inaweza kusemwa hivyohivyo juu ya ile michoro yenye kuogofya ambayo hupamba vifuko vya santuri kubwa na ambayo mara nyingi huonyesha ishara za kishetani.

Lakini vipi muziki wenyewe? Huo hutumia majina kama vile “Nyama na Damu” na “Hamu ya Uharibifu” na una maneno ambayo hutukuza kuona raha kwa kuumiza wengine, unajisi, na mauaji ya kimakusudi. Hivyo haishangazi kwamba kitabu cha mwongozo cha muziki wenye mdundo mzito Stairway to Hell huuita muziki wenye mdundo mzito “ushindi wa utovu wa adabu, mwendo wa kasi, utumizi wa moja kwa moja wa maneno [machafu], kutojali kijeuri.” Pia mara nyingi muziki wenye mdundo mzito umefungamanishwa na utumizi mbaya wa dawa za kulevya, Ushetani, na kujiua miongoni mwa wasikilizaji wao. Hata hivyo, kulingana na ripoti za vyombo vya habari, muziki wenye mdundo mzito unazidi kukubaliwa na watu wengi zaidi.

Muziki mwingi wa rapu (au, hipu-hopu) vilevile hupita kiasi sana.b Lasema gazeti Time: ‘Washairi wa rapu . . . katika maneno yao huitisha moto wa vita dhidi ya polisi au ngono yenye kuonyeshwa waziwazi yenye kuwaka kibiriti.’ Kusema kweli, maneno ya nyimbo nyingi za rapu ni machafu mno yasiweze kunukuliwa hapa. Akirejezea wimbo mmoja kama huo, msichana mmoja tineja alisema hivi: “Neno la kwanza lilitoka—nami nikashtuka!”

Hata hivyo, muziki mwingi wa roki ambao husikilizwa na watu wengi vilevile haufai kwa masikio ya Mkristo. Ingawa nyimbo nyingi kati ya zile 40 zenye kupendwa zaidi si zenye ufidhuli kama rapu au muziki wenye mdundo mzito, bado nyingi huendeleza kwa werevu—au waziwazi—ukosefu wa adili kingono na mazoea mengine yasiyo ya Kikristo. Vidio za muziki, zenye kupendwa sana na vijana, huzidisha nguvu za muziki kwa kuongeza picha zenye nguvu. Kati-ka uchunguzi mmoja wa vidio za muziki, asilimia 57 ilionekana kuwa na jeuri, na asilimia 75 ilikuwa na tamasha zenye kuonyesha ngono. Mavazi yenye kuchochea nyege na dansi zenye kuchochea nyege ni mambo yaliyoonekana kuwa yakionyeshwa mara nyingi katika muziki wa vidio.

Je! Waweza Kukudhuru?

Badala ya kuwa wenye kuburudisha na wenye kufaa, muziki mwingi unaoendelezwa leo kwa wazi ni ‘wa kidunia, kibinadamu [kinyama, NW], kishetani.’ (Yakobo 3:15) Ingawa hivyo, kwa kushangaza, si vijana wote Wakristo ambao huona tatizo lolote katika kusikiliza nyimbo kama hizo au kutazama vidio hizo. “Huhitaji kujali juu ya maneno ya muziki wa rapu,” abisha msichana mmoja kijana. “Kwa vyovyote hata huwezi kuyaelewa!” Yeyote ambaye amejaribu kuelewa maneno ya muziki wa rapu aweza kukubali ya kwamba kuna kweli fulani katika jambo hilo.

Vijana hawafahamu sikuzote zile maana zilizofichwa za nyimbo zenye kupendwa sana. Katika uchunguzi mmoja, matineja waliambiwa waeleze yaliyokuwamo katika baadhi ya nyimbo zenye kupendwa sana. Vijana wengi hawakutambua hata kidogo vile vichwa vya werevu vya ngono, jeuri, dawa za kulevya, na Ushetani vilivyoenea katika muziki wao. Hivyo The Journal of the American Medical Association lilifikia mkataa huu: “Hakuna uthibitisho kwamba muziki huu una matokeo yoyote ‘yenye kudhuru’ juu ya tabia ya wabalehe.”

Ingawa hivyo, Biblia huonyesha vingine. Kwanza, inatuambia kwamba “mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema.” (1 Wakorintho 15:33) Sasa, je, wewe ungetumia saa nyingi ukishirikiana na au ukisikiliza mtu fulani ambaye anatumia maneno machafu sana, anayekuhimiza utumie dawa za kulevya, anayetetea ibada ya Shetani, au anayeeleza kindani sana ngono yenye upotovu? Bila shaka sivyo! Basi kwa nini maneno hayo yasiwe yenye kudhuru kadiri hiyohiyo kwa sababu tu yanaambatana na muziki au yanaambatana na mdundo? Wakati vichwa kama hivyo vinapoimbwa tena na tena, vinaweza tu kukuathiri! “Je! mtu aweza kutia moto kifuani pake, na nguo zake zisiteketezwe?”—Mithali 6:27.

Kwa sababu hiyo Biblia hutuhimiza hata tusitaje mambo yenye ukosefu wa adili, achia mbali kuyarudia tena na tena. (Waefeso 5:3-5; Wafilipi 4:8) Mtu anayepuuza kanuni hiyo hakika “atavuna uharibifu.” (Wagalatia 6:8) “Nyimbo hizo hukufanya ufikiri,” akubali kijana mmoja aitwaye Jodie. “Tamaa mbaya zikiisha kuamka, zinaichochea zaidi akili yako.” Baada ya kusikiliza wimbo mmoja wa rapu ambao ulieleza kindani sana ngono yenye upotovu, kijana mmoja alikiri hivi: “Sikuweza hata kidogo kuuondoa akilini mwangu.”

Na vipi kusikiliza nyimbo zenye mdundo mzito ambazo huhubiri kifo, dawa za kulevya, au Ushetani? Kijana mmoja Mkristo alianza kusikiliza muziki wenye mdundo mzito na upesi akashikwa na kichaa cha kifo. Ni jitihada zenye kuazimia tu za wazazi wake na rafiki Mkristo aliyekomaa zilizoweza kumponyoa na uangamivu wa kiroho na wa kimwili.

Nyakati nyingine, mawazo hugeuka kuwa vitendo. (Yakobo 1:14, 15) Na muziki mwingi wa leo umetungwa kwa werevu na kwa uangalifu ujaze akili yako mawazo mabaya. Ni kweli, ikiwa wewe umelelewa kulingana na viwango vya Biblia, haielekei kwamba utaua kimakusudi au ufanye ngono yenye ukosefu wa adili kwa sababu tu umeisikia katika wimbo. Lakini kuna njia nyingine unazoweza kuvutwa vibaya. Vijana wengine Wakristo wameanza kuvaa mavazi na kutumia mitindo ya nywele ya kiajabu inayotumiwa na wanamuziki wa roki na rapu. Usemi, ishara, na mtazamo wa vijana hao kwa wazi huonyesha kwamba wao wanavutwa na yale wanayosikia.

“Vijana husema kwamba muziki hauwaathiri,” asema mvulana mmoja Mwafrika Kusini. “Lakini unampa Shetani njia ya kuingia maishani mwako—kuyadhibiti.” Ajua hivyo kutokana na yaliyompata binafsi, aeleza hivi: “Ule muziki niliosikiliza ulikuwa juu ya uwasiliano na roho, dawa za kulevya, na ngono.” Alijiondoaje katika athari hizo zenye kudhuru za muziki mpotovu?

“Nilitupa muziki wangu wote. Lilikuwa badiliko kubwa kuketi katika chumba chenye utulivu. Lakini lilinifanya kuwa mtu bora zaidi.” Je! wewe wahitaji kuchukua hatua kama hiyo—si lazima kutupa muziki wako wote, lakini angalau kujiondolea rekodi ambazo kwa wazi ni zenye kushusha tabia?—Linganisha Matendo 19:19.

Hiyo haimaanishi kukataa kabisa muziki, bali kujifunza kuwa mteuzi! Jinsi ya kufanya hivyo itazungumzwa katika makala ya wakati ujao.

[Maelezo ya Chini]

a Ona “Vijana Wauliza . . . Muziki Wangu Una Ubaya Gani?” katika toleo la Februari 8, 1993.

b Maneno “muziki wa roki” yametumiwa hapa kwa yoyote ya aina mbalimbali ya muziki upendwao sana miongoni mwa vijana.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je! kujaza akili yako jumbe za kifo, uharibifu, na ushushaji tabia kingono kutakusaidia au kutakudhuru?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki