Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Shule Matatani Nilikuwa nikingoja kwenye kituo cha basi wakati mtu fulani aliponipa toleo la “Shule Matatani.” (Desemba 22, 1995) Limethibitika kuwa lenye mafaa zaidi kuliko kitabu fulani kizima ambacho nilisoma hivi majuzi juu ya habari hiyo. Nitashukuru sana nikiletewa nyumbani andikisho la Amkeni!
V. C., Marekani
Ile sehemu inayohusu Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilinikumbusha wakati ambapo nilikuwa shuleni. Nilipaswa kutoa ripoti kwa njia ya hotuba lakini sikujua Kiingereza sana wakati huo. Nilipomaliza kutoa ripoti hiyo, mwalimu wangu aliniambia kwamba alivutiwa sana na kwamba ni mimi pekee niliyesimama vizuri na kuwaangalia wasikilizaji. Niliweza kufanya hivyo kwa sababu ya mazoezi bora tupatayo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwenye Jumba la Ufalme.
G. A., Marekani
Sikujua kwamba makala hizo zingetokeza hisia zenye nguvu ndani yangu. Nilipokuwa shuleni, wazazi wangu walijishughulisha tu na mambo yao wenyewe na hivyo hawakunisaidia. Tokeo likawa kwamba kuna pindi ambazo nilikuwa mpweke sana shuleni. Kwa sababu ya makala kama hizi, natambua kwamba Yehova hupenda vijana naye hataki wahisi wakiwa wapweke katika ulimwengu huu.
M. M., Marekani
Mali Ile makala “La Kwanza Katika Mali” (Desemba 22, 1995) ilikuwa nzuri sana. Nimeisoma mara tatu. Natamani kama nini kwamba hali zangu zingeniruhusu niwe mishonari! Makala hiyo pia ilinifanya nitambue kwamba kuna watu wengi ambao hawana mafaa ambayo sisi tunayo na bado wao ni wenye furaha. Ni kikumbusho cha wakati ufaao kama nini!
D. L., Marekani
Miamba Inayoruka Siku chache tu zilizopita, nilijiuliza tofauti iliyoko kati ya nyota yenye kuruka na meteoriti. Ebu wazia jinsi nilivyoshangaa niliposoma hiyo makala “Miamba Inayoruka” (Desemba 8, 1995), ambayo ilieleza jambo lilo hilo. Asanteni kwa kutangaza makala zinazotujulisha uumbaji wa Yehova.
R. P., Uswisi
Kujifunza Kutokana na Andrew Nimetoka tu kusoma ile makala kuhusu kijana mwenye tatizo la Down’s syndrome, “Kile Tulichojifunza Kutokana na Andrew.” (Desemba 8, 1995) Sisi pia tuna mtoto mwenye tatizo la kiakili, na maelezo mengi ya wazazi wa Andrew yaonyesha jinsi sisi wenyewe twahisi. Mara nyingi ni vigumu sana kwa ndugu zetu Wakristo kung’amua magumu ya kipekee ambayo kuwa na mtoto punguani hutokeza na ile mikazo ya kihisia moyo ambayo hupata familia. Kwa hiyo asanteni kwa makala hiyo.
J. B., Uingereza
Nahisi hii ni mojayapo makala nzuri zaidi na yenye kugusa hisia zaidi ambayo mmepata kutangaza. Katika kurasa tatu pekee, hali yote ya jinsi tupaswavyo kuwaona wale wenye upungufu ilionyeshwa. Ilitoa somo kubwa sana kuhusu mahusiano ya kibinadamu.
M. L., Hispania
Mapema mwaka huu mke wangu alizaa mtoto mwenye Down’s syndrome. Kama ilivyo na wazazi wa Andrew, tulipatwa na kile ambacho wazazi wengi wamehisi wajuapo ya kwamba mtoto wao hajiwezi—uguo na huzuni na vilevile maswali kuhusu wakati wa sasa na wakati ujao. Kwa upande wetu, tumefaulu kukubali hali ya kutojiweza ya mtoto wetu. Karibuni atakuwa na miezi sita, naye anakua vizuri. Siku moja baada ya kuzaliwa kwa huyo mtoto, mke wangu alifurahia zaidi ziara nyingi za ndugu na dada zetu Wakristo. Kwa kweli tulihisi kile kinachomaanishwa na kuwa na familia ya kiroho. Pamoja na upendo wa ndugu na dada zetu, kuna Yehova. Asanteni kwa makala hiyo.
G. C., Ufaransa