Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 3/22 kur. 4-8
  • Babu na Nyanya—Shangwe na Magumu Yao

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Babu na Nyanya—Shangwe na Magumu Yao
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Daraka la Babu na Nyanya
  • Mikazo ya Familia
  • Upendo na Staha—Ndizo Funguo!
  • Kile Ambacho Babu na Nyanya Wanaweza Kutoa
  • Kuishi Pamoja kwa Upendo
    Amkeni!—1995
  • Ni Yapi Baadhi ya Hayo Matatizo?
    Amkeni!—1995
  • Babu na Nyanya Wanapokuwa Wazazi
    Amkeni!—1999
  • Kwa Nini Niwajue Vyema Babu na Nyanya?
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 3/22 kur. 4-8

Babu na Nyanya—Shangwe na Magumu Yao

“Ninapenda kuwa babu au nyanya! Unafurahia wajukuu wako bila kuhisi ukiwa na daraka kuwaelekea. Unatambua kwamba unaathiri maisha yao lakini hatimaye huchangii uamuzi wa mwisho. Wazazi wao watafanya hivyo.”—Gene, ambaye ni babu.

NI KITU gani kinachoweza kuchochea shauku hiyo unapokuwa babu au nyanya? Watafiti wanasema kwamba mambo ambayo kwa kawaida wazazi hudai kiasili kutoka kwa watoto wao yaweza kutokeza mkazo mkubwa sana. Kwa sababu kwa kawaida si lazima babu na nyanya wadai mambo hayo, wanaweza kufurahia uhusiano usio na mkazo pamoja na wajukuu wao. Kama asemavyo, Arthur Kornhaber, M.D., wako huru kuwapenda wajukuu wao “kwa sababu tu ni wajukuu wao.” Nyanya mmoja anayeitwa Esther asema hivi: “Nilipokuwa na watoto wangu, nilijihusisha sana na kila kitu walichofanya. Nikiwa nyanya, nahisi nikiwa huru kufurahia na kuwapenda wajukuu wangu tu.”

Kisha mtu anapokuwa na umri mkubwa anapata hekima na ufahamu zaidi. (Ayubu 12:12) Babu na nyanya wamepata uzoefu wa miaka mingi katika kulea watoto, kwa kuwa wao si wachanga tena. Wakiwa wamejifunza kutokana na makosa yao, wanaweza kuwa na ufahamu zaidi wa kushughulikia watoto kuliko waliokuwa nao walipokuwa na umri mdogo zaidi.

Hivyo Dakt. Kornhaber amalizia kwa kusema: “Kifungo kinachofaa na chenye upendo kati ya babu na nyanya na wajukuu ni cha lazima ili vizazi vyote vitatu vipate afya ya kihisia-moyo na furaha. Kifungo hiki ni haki ya kuzaliwa ya kiasili kwa watoto, . . . urithi walioachiwa na wazee wao ambao hunufaisha kila mmoja katika familia.” Vivyo hivyo jarida Family Relations lasema: “Babu na nyanya wanaoshiriki na kuelewa daraka lao husitawisha hali njema na imani zaidi.”

Daraka la Babu na Nyanya

Babu na nyanya wanaweza kutimiza madaraka mengi yenye thamani. “Wanaweza kuwategemeza watoto wao waliofunga ndoa,” asema Gene. “Nafikiri kwa kufanya hivyo, wanaweza kukomesha baadhi ya hali ngumu ambazo huwapata wazazi wachanga.” Babu na nyanya pia wanaweza kufanya mengi zaidi kuwategemeza wajukuu wao wenyewe. Mara nyingi babu na nyanya ndio husimulia matukio fulani ambayo humfahamisha mtoto historia ya familia. Mara nyingi, pia babu na nyanya hutimiza daraka la maana katika kupitisha urithi wa kidini wa familia.

Katika familia nyingi, babu na nyanya hutumikia wakiwa washauri wanaoaminiwa. “Huenda kukawa na mambo ambayo watoto watakuambia ambayo hawajihisi huru kuyazungumzia pamoja na wazazi wao,” asema Jane, aliyetajwa katika makala ya kwanza. Kwa kawaida wazazi hufurahia msaada huo wa ziada. Kulingana na uchunguzi mmoja, “zaidi ya asilimia 80 ya vijana waliwaona babu na nyanya yao kuwa marafiki wao wa karibu. . . . Idadi kubwa ya wajukuu waliokomaa hudumisha mawasiliano kwa ukawaida pamoja na babu na nyanya yao wa karibu.”

Babu au nyanya mwenye upendo aweza kuwa mtu wa maana sana hasa kwa mtoto ambaye amekosa malezi yanayofaa nyumbani. “Nyanya yangu ndiye aliyekuwa mtu wa maana zaidi maishani mwangu nilipokuwa mchanga,” aandika Selma Wassermann. “Nyanya yangu ndiye aliyenilea. Nyanya yangu alikuwa mwenye kufikika na tayari daima kunibeba kwenye paja lake ili kunifariji na kunipa uhakikishio zaidi. . . . Nilijifunza mambo ya maana zaidi kunihusu kutoka kwa nyanya yangu—kwamba nilipendwa na kwa hiyo napendeka.”—The Long Distance Grandmother.

Mikazo ya Familia

Ingawa hivyo, hali ya kuwa babu au nyanya haikosi kuwa na mikazo na matatizo. Kwa kielelezo, mzazi mmoja, akumbuka akibishana vikali na mama yake kuhusu njia inayofaa ya kumfanya mtoto apige mbweu. “Jambo hilo lilisababisha kuvunjika kwa uhusiano wetu kwenye pindi ambayo ningeweza kudhurika kwa urahisi.” Kwa kueleweka, wazazi wachanga wanataka wazazi wao wakubali njia wanayolea watoto wao. Hivyo madokezo kutoka kwa wazazi wao wenye nia njema yaweza kusikika kuwa uchambuzi unaoharibu mambo.

Katika kitabu chake Between Parents and Grandparents, Dakt. Kornhaber asema juu ya wazazi wawili wenye tatizo jingine la kawaida. Mzazi mmoja asema hivi: “Mimi huingiliwa kila siku na wazazi wangu, nao hukasirika wanapokuja nyumbani na kunikosa. . . . Hawanifikirii—hisia zangu na haki yangu ya kuwa na faragha.” Mwingine alalamika akisema: “Wazazi wangu wanataka kumtawala msichana wangu mdogo. Wanataka kujihusisha katika kila jambo linalohusu maisha ya Susie. . . . Tunafikiria kuhama.”

Nyakati nyingine babu na nyanya pia hulaumiwa kwa kuwaendekeza wajukuu wao kwa kuwapa zawadi nyingi sana. Bila shaka, ukarimu ni jambo la kiasili kwa babu na nyanya kama ilivyo kupumua, lakini wengine huvuka mipaka katika jambo hili. Hata hivyo, nyakati fulani, malalamiko ya wazazi yaweza kutokana na wivu. (Mithali 14:30) “Wazazi wangu walikuwa wakali sana kunielekea,” akiri Mildred. “Inapohusu watoto wangu wao huwaonyesha ukarimu na [kuwaendekeza]. Nina wivu kwa sababu hawajabadili hata kidogo namna wanavyonitendea.” Hata nia au sababu iwe nini, inaweza kusababisha matatizo ikiwa babu au nyanya haheshimu mapendezi ya wazazi kuhusu kuwapa wajukuu zawadi.

Hivyo babu na nyanya watakuwa wenye hekima kutumia busara wanapoonyesha ukarimu. Biblia inaonyesha kwamba hata kitu kizuri kinapokuwa kingi sana chaweza kuwa kibaya. (Mithali 25:27) Ikiwa huna hakika ni zawadi za aina gani zinazofaa, shauriana na wazazi. Kwa njia hii ‘utajua jinsi ya kuwapa zawadi zilizo njema.’—Luka 11:13.

Upendo na Staha—Ndizo Funguo!

Kwa kusikitisha, babu na nyanya fulani hulalamika kwamba kazi yao ya kutunza na kulea watoto haithaminiwi. Wengine huhisi kwamba hawapewi muda wa kutosha kuwa na wajukuu wao. Lakini babu na nyanya fulani husema kwamba watoto wao wakubwa wamewaepuka kabisa bila hata kuwaeleza sababu. Mara nyingi matatizo hayo yanayoleta uchungu yanaweza kuepukwa ikiwa washiriki wa familia wataonyeshana upendo na staha. Biblia husema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, . . . hautafuti masilahi yao wenyewe, haupati kuwa wenye kuchokozeka. . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.”—1 Wakorintho 13:4, 5, 7.

Labda wewe ni mzazi mchanga na Nyanya atoa dokezo au maoni yenye kuudhi, ijapokuwa ana nia njema. Je, kweli una sababu nzuri ya “kuwa mwenye kuchokozeka”? Kwa vyovyote, Biblia huonyesha kwamba daraka la mwanamke Mkristo mwenye umri mkubwa ni kufundisha “wanawake vijana . . . kuwapenda waume zao, kuwapenda watoto wao, kuwa timamu katika akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani.” (Tito 2:3-5) Na je, si ni kusudi lako, la babu na la nyanya kutimiza lengo lile lile—la kuwapa watoto wenu vitu vilivyo bora zaidi? Kwa kuwa upendo “hautafuti masilahi yao wenyewe,” labda itakuwa bora kufikiria mahitaji ya mtoto—si kufikiria hisia zako tu. Kufanya hivyo kwaweza kuwasaidia mwepuke “kuchochea shindano juu ya mtu na mwenzake” kuhusu mambo madogo yenye kuudhi.—Wagalatia 5:26, kielezi-chini New World Translation of the Holy Scriptures—With References.

Ni kweli, unaweza kuhofia ukarimu mwingi sana utamharibu mtoto wako. Lakini kwa kawaida babu au nyanya hawi na nia mbaya anapokuwa akionyesha ukarimu. Wataalamu wengi wa utunzaji-watoto wanakubali kwamba jinsi unavyomzoeza na kumtia nidhamu mtoto wako kutakuwa na matokeo makubwa zaidi kuliko kuingiliwa kati pindi kwa pindi na babu au nyanya. Daktari mmoja ashauri kwamba: “Inasaidia kuwa na ucheshi.”

Ukiwa na hangaiko halali kuhusu suala fulani la utunzaji wa mtoto, usiwazuie kabisa wazazi au wakwe zako kuwasiliana na watoto wako. Biblia husema: “Pasipo mashauri makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Katika ‘wakati unaofaa,’ uwe na mazungumzo mazito na ufunue mahangaiko yako. (Mithali 15:23) Mara nyingi, masuluhisho yanaweza kupatikana.

Je, wewe ni babu au nyanya? Basi ni muhimu kuwastahi wazazi wa mjukuu wako. Bila shaka, ungehisi kuwa na daraka la kusema ikiwa ungeona kwamba mjukuu wako yuko hatarini. Lakini ijapokuwa ni jambo la kiasili kwako kumpenda na kumtunza mjukuu wako, wazazi—wala si babu na nyanya—ndio wenye daraka la kulea watoto wao. (Waefeso 6:4) Biblia huwaamuru wajukuu wenu wawastahi na kuwatii wazazi wao. (Waefeso 6:1, 2; Waebrania 12:9) Hivyo, jiepushe kuwapatia wazazi wao mashauri mengi kupita kiasi na ambayo hawajaomba au kuhujumu mamlaka ya wazazi.—Linganisha 1 Wathesalonike 4:11.

Kweli, kutojihusisha, kunyamaza—na pengine kungojea ukiwa na wasiwasi jambo fulani litokee—na kuacha watoto wako wafanye kazi yao wakiwa wazazi haliwi jambo rahisi sikuzote. Lakini kama asemavyo Gene, “isipokuwa waombe shauri, utahitaji kukubaliana na kile ambacho wazazi wanahisi kuwa bora kwa watoto wao.” Jane asema: “Ninakuwa mwangalifu kutosema, ‘Hivi ndivyo inavyopasa kufanywa!’ Kuna njia nyingi tofauti-tofauti za kufanya mambo, na ikiwa unashikilia sana maoni yako, inaweza kusababisha matatizo.”

Kile Ambacho Babu na Nyanya Wanaweza Kutoa

Biblia inaonyesha kwamba kuwa na wajukuu ni baraka kutoka kwa Mungu. (Zaburi 128:3-6) Kwa kupendezwa na wajukuu wako, unaweza kuathiri sana maisha yao, ukiwasaidia wasitawishe kanuni za kimungu. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 32:7.) Katika nyakati za Biblia mwanamke mmoja aliyeitwa Loisi alitimiza fungu la maana katika kusaidia mjukuu wake wa kiume, Timotheo, akue na kuwa mtu wa Mungu mwenye kutokeza. (2 Timotheo 1:5) Vivyo hivyo, unaweza kupata shangwe wajukuu wako wanapokubali kuzoezwa kimungu.

Pia unaweza kuwa chanzo cha upendo na shauku inayohitajiwa sana. Kweli, huenda usiwe mtu mwenye kuzungumza sana kwa shauku. Hata hivyo, upendo wa kimungu waweza kuonyeshwa pia kwa kupendezwa kwa moyo mweupe na bila ubinafsi na wajukuu wako. Mwandishi Selma Wassermann asema hivi: “Kupendezwa na mambo ambayo mtoto anakuambia . . . kwa hakika kutaonyesha kwamba unajali. Kuwa msikilizaji mzuri, bila kuingilia kati, kutokuwa mchambuzi—yote haya huonyesha staha, shauku, uthamini mkubwa.” Kwa mjukuu, uangalifu huo wenye upendo waweza kuwa mojawapo ya zawadi bora kabisa ambazo babu na nyanya waweza kutoa.

Kufikia hapa mazungumzo yetu yamekazia madaraka ya kidesturi ya kuwa babu au nyanya. Hata hivyo, babu na nyanya wengi wa kisasa, hubeba mzigo mzito zaidi.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Nilijifunza mambo ya maana zaidi kunihusu kutoka kwa nyanya yangu—kwamba nilipendwa na kwa hiyo napendeka”

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Madokezo kwa Babu na Nyanya Wanaoishi Mbali

• Waombe wazazi wakupelekee kanda za vidio au picha za wajukuu.

• Wapelekee wajukuu wako “barua” zilizorekodiwa katika kaseti. Kwa watoto wadogo, jirekodi mwenyewe ukisoma hadithi za Biblia au ukiimba nyimbo za kubembeleza mtoto.

• Wapelekee wajukuu postikadi na barua. Ikiwezekana, uwe unawaandikia barua kwa ukawaida.

• Ikiwa unaweza kulipia gharama, wasiliana na wajukuu wako walio mbali kwa kuwapigia simu. Unapoongea na watoto wadogo, anzisha mazungumzo kwa kuuliza maswali sahili, kama vile, “Ulikula nini asubuhi?”

• Ikiwezekana, fanya ziara za kawaida, na fupi.

• Fanya mipango na wazazi wa wajukuu wako wakutembelee. Panga shughuli za kujifurahisha, kama vile kwenda kuwatazama wanyama, kwenye majumba ya ukumbusho, na kwenye bustani.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Babu na nyanya wengi husaidia kutunza wajukuu wao

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mkazo waweza kutokea kuhusu njia za kulea watoto

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mara nyingi babu na nyanya hutimiza fungu fulani katika kupitisha historia ya familia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki