Vijana Huuliza...
Je, Naweza kwa Kweli Kuwa Rafiki ya Mungu?
KUWA rafiki ya Mungu? Haiwezekani, ndivyo aaminivyo Doris mwenye umri wa miaka 20. “Najihisi nikiwa na thamani ndogo sana na asiyestahiki kupendwa na yeyote,” aomboleza mwanamke huyu mchanga. “Mimi hata huepuka kusali kwa Yehova Mungu kwa sababu sifikiri nastahili kuwa mbele zake.” Katika hisia zao za ndani, baadhi ya vijana huhisi kutostahiki kabisa urafiki wa Mungu. Ingawa huenda wakathamini wazo la kuwa rafiki ya Mungu, wao huhisi huo ni usioweza kufikilika kwao. Je, umepata kuhisi hivyo?
Nyakati nyingine, udhaifu wake mwenyewe huenda ukamfanya kijana ahisi kutostahiki hata kumkaribia Mungu. Mathalani, chukua kielelezo cha Michael mchanga. Yeye asema kwamba kabla ya kuja kung’amua njia za kimungu, yeye “alijawa na karibu kila wazo na tendo lenye dhambi na lenye kuumiza lililopo.” Hata hivyo, lile alilojifunza kutokana na funzo lake la Biblia lilimfanya atambue huzuni na udhiko alilokuwa akimsababishia Mungu. Yeye alieleza hivi: “Kila mkutano wa kutaniko ulifanya angalau moja ya kasoro zangu dhahiri kwangu. . . . Singeweza kuona kimbele msamaha wa Yehova kwa dhambi zangu zilizoonekana kutoisha licha ya uhakika wa kwamba singeweza hata kujisamehe.”
Katika visa vingine, njia ambayo kijana anatendewa na wengine yaweza kumfanya ahisi asiyestahiki urafiki wa Yehova. Mathalani, Doris, aliyenukuliwa mapema, aliachwa na mama yake akiwa mtoto mdogo. Yeye alifunua hivi: “Sifikiri mtu yeyote anipenda. Ikiwa mama yangu na familia yangu mwenyewe iliniacha, kuna uwezekano gani wa yeyote mwingine kunijali?” Wakati kijana anapokuwa ametendewa katika njia ya kudai na ya matukano tangu utotoni, anaweza kuamini kwa unyofu kwamba Mungu hangeweza kumtaka awe rafiki kamwe.
Kwa upande mwingine, huenda ikawa kijana alikuwa na urafiki na Mungu lakini, kwa sababu ya udhaifu, aangukia dhambi nzito. Hili lilimpata Tracy. “Nahisi kuaibika sana,” aomboleza msichana huyu mwenye umri wa miaka 21, “umivu langu na hatia haivumiliki. Nimemuumiza sana Baba yangu, Yehova.”
Labda unajipata katika hali inayofanana na mojapo zilizotoka kutajwa. Lakini kuna tumaini: Mungu anaweza kuwa rafiki yako!
Sababu Inayofanya Uweze Kuwa Rafiki ya Mungu
Ni kweli kwamba matendo ya dhambi yanaweza kuzuia mtu kuwa rafiki ya Mungu. Kwa kupendeza, Baba yetu mwenye upendo amechukua hatua ya kwanza kutusaidia. “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi,” akaandika mtume Paulo. (Warumi 5:8) Kupitia kifo chake, Yesu alilipa fidia ili kufidi wenye uthamini kutokana na umiliki kamili wa dhambi. (Mathayo 20:28) Hivyo, huyo mtume aongezea hivi: “Tulikuwa maadui wa Mungu, lakini alitufanya marafiki wake kupitia kifo cha Mwanaye.”—Warumi 5:10, Today’s English Version.
Kabla ya kuja kung’amua viwango vya Yehova, vijana fulani, kama Michael aliyetajwa mapema, huenda walijihusisha katika utendaji-makosa mbaya. Lakini, kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu, mtu aweza kusamehewa dhambi za wakati uliopita, haidhuru dhambi hizi zilikuwa nzito kadiri gani. Biblia hutoa uhakikishio huu wenye kuchangamsha moyo: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu.” (1 Yohana 1:9) Hata hivyo, mtu lazima achukue hatua kuonyesha Mungu kwamba yeye anathamini utakasaji huo. Mtume Paulo ataarifu kanuni ambayo yaweza kutumiwa: ‘“Komeni kugusa kitu kisicho safi,” asema Yehova, “nami nitawakaribisha ndani. Na mimi nitakuwa baba kwenu.”’ (2 Wakorintho 6:17, 18, New World Translation) Ni jambo lenye kugusa moyo kama nini kujua kwamba mtu akigeuka kutoka utendaji-makosa kama huo na kuwa mwenye kutubu kikweli, Mungu yuko tayari kumpokea ndani ya upendeleo Wake akiwa rafiki.
Namna gani vijana ambao wamelelewa katika mazingira yenye matukano? Tambua kwamba Mungu haoni watu kuwa wenye hatia kwa sababu walifanyiwa mambo dhidi ya kutaka kwao. Watu hao walikuwa majeruhi badala ya washiriki katika dhambi. Kumbuka pia, kwamba ustahiki wako ukiwa mtu hautegemei hukumu ya mwanadamu mwingine. Yehova aweza kuwa Rafikiyo licha ya hali zako. Maureen alilelewa na mama Mkristo katika nyumba iliyojaa jeuri kwa sababu ya baba yake aliyekuwa mraibu wa alkoholi. Na bado yeye alisema hivi: “Katikati ya hali hii ngumu, kwa njia fulani niliweza kusitawisha uhusiano pamoja na Yehova. Nilikuja kumjua kuwa Mmoja ambaye hangeniacha kamwe.”
Namna Gani Ukiangukia Dhambi Nzito?
Doug, ambaye alilelewa na wazazi wenye kumwogopa Mungu, alijiingiza katika ukosefu wa adili katika ngono kwenye umri wa miaka 18. Hii ilikuwa kwa sababu ya mashirika yake mabaya. “Nilijua ilikuwa kosa, lakini niliendelea kufanya kwa sababu nilitaka kuwa na wakati mzuri,” Akaungama Doug. Wakati fulani baadaye, Doug aliona ubatili wa mwenendo wake. Yeye alikiri hivi: “Nilianza kuona kwamba waliokuwa eti rafiki zangu walikuwa tu wakinitumia ili kupata fedha zangu au kuwa na wakati mzuri.” Kisha yeye alianza kuchukua hatua za kurudisha urafiki wa Yehova. Lakini kizuizi kikubwa kilizuia maendeleo yake.
“Jambo kuu lililofanya iwe vigumu kurudi lilikuwa kwamba nilihisi kutostahiki kabisa,” Doug akafunua moyo wake. “Nilihisi kwamba yote niliyokuwa nimefanya yalikuwa mabaya machoni pa Yehova. Kujua jinsi alivyo mwema na kadiri ambavyo alinivumilia, ilionekana hakukuwa na namna ambavyo yeye angetaka kunisamehe kwa sababu nilikuwa tu mbaya mno.” Walakini, Doug aliweza kuruka kiunzi hiki kwa msaada wa mzee wa kutaniko na kwa kufikiri kwa uzito simulizi la Biblia la Manase.
Manase alikuwa nani? Mfalme wa Yuda la kale. Biblia huonyesha kwamba alikuwa amefundishwa kumpenda Yehova na baba yake aliyemwogopa Mungu, Hezekia. Lakini baada ya baba yake kufa na yeye kuwa mfalme katika umri wa miaka 12, yeye alifikiri angeweza sasa kufanya kama alivyotaka. Yeye alimwacha Yehova na kufuata ibada ya Baali. Ibada hiyo ilikuwa na karamu zilizokosa adili mno na ngono zisizozuiwa. Manase “alifanya kwa kiwango kikuu yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, ili kumchukiza.” Kupitia wanenaji waaminifu, “Yehova aliendelea kusema na Manase na watu wake, lakini hawakutoa uangalifu.” Kisha, ukiwa wonyesho wa hukumu ya Yehova, Manase alichukuliwa hadi Babiloni akiwa mfungwa aliyefungwa kwa pingu.—2 Mambo ya Nyakati 31:20, 21; 33:1-6, 10, 11, NW.
Manase alipowaza juu ya matendo yake ya wakati uliopita na kuyalinganisha na yale aliyokumbuka kuhusu sheria za Yehova, alilemewa na hatia na kuomba msamaha. Yeye alijinyenyekeza mbele za Mungu na “akaendelea kusali Kwake.” Na Mungu “akakubali kusikia sihi yake Naye akakubali ombi kwa ajili ya upendeleo na kumrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake.” Ndiyo, ‘Baba wa rehema nyororo’ alikuwa tayari kuruhusu mtenda-dhambi huyu mwenye kutubu aje karibu naye tena. Baada ya kupokea rehema hiyo, Manase, kwa ono la kibinafsi, sasa “alikuja kujua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.”—2 Mambo ya Nyakati 33:12, 13, NW; 2 Wakorintho 1:3.
Ikiwa Yehova angeweza kumkubali tena Manase, hakika angeruhusu kijana mpotovu leo apate tena uhusiano pamoja Naye ikiwa huyo kijana anaonyesha mtazamo wa kutubu. Doug aliitikia msaada wa wachungaji wa kiroho katika kutaniko lake. Yeye alisaidiwa kuona waziwazi kwamba Mungu “hatatafuta kosa kwa wakati wote, wala hataendelea kuchukizwa hata wakati usio dhahiri.”—Zaburi 103:9, NW.
Baki Ukiwa Rafiki ya Mungu
Mara tu Mungu anapokuwa Rafiki yako, lazima uthamini uhusiano huu ili kuudumisha. Msichana mmoja aliyebatizwa mwenye umri wa miaka 18 alikuja kuwa mama asiyeolewa. Hata hivyo, alisaidiwa kunyoosha mambo pamoja na Yehova. (Ona Isaya 1:18.) Jambo kuu la kurudia kwake hali nzuri? “Nilijifunza kwamba Yehova alikuwa Baba mwenye upendo na si mfishaji,” yeye akaeleza. “Nilitambua kwamba alikuwa ameumizwa na kile nilichokuwa nimefanya. Ni jambo la maana sana kumwona Mungu kama Rafiki, mtu aliye na hisia, na si Roho fulani inayowaziwa tu ya kutolewa ibada lakini isiyopendwa kikweli kamwe.” Kama Manase, yeye alisukumwa kujitia kikamili katika ibada ya Yehova. (2 Mambo ya Nyakati 33:14-16) Hili limethibitika kuwa ulinzi kwake. Yeye ashauri vijana wengine hivi: “Endeleeni kujikakamua kumsifu Yehova hata kama hali yawa ngumu. Yehova kwa upendo atanyoosha vijia vyenu tena.”
Ni jambo la maana pia kwamba utafute urafiki na wale walio rafiki za Mungu. Hata hivyo, epuka kama tauni, wale ambao kwa wazi hawana staha kwa kanuni za kimungu. (Mithali 13:20) Linda mchanga alijiingiza katika ukosefu wa adili katika ngono pamoja na kijana fulani ambaye urafiki wake ulikuja kuwa “jambo la maana zaidi ya chochote.” Baada ya kupata kwake nafuu kiroho, Linda alikiri hivi: “Unaweza kuharibu maisha yako yote kwa kutokuwa na uhusiano huo wa kibinafsi kati ya Yehova na wewe.”
Je, wewe una uhusiano kama huo? Ikiwa sivyo, fanyia kazi kuupata. Linda anafanyia muhtasari thamani ya kuwa na urafiki wa Mungu kwa kusema hivi: “Jambo la maana kuliko yote katika ulimwengu wote ni uhusiano mwema wa kibinafsi pamoja na Yehova. Hakuna mvulana au msichana au kitu kinginecho chote katika ulimwengu huu kilicho muhimu zaidi kuliko huo. Ikiwa urafiki pamoja na Yehova hauko, basi hakuna chochote kilicho na maana.”
[Picha katika ukurasa wa 15]
Huenda vijana fulani wakahisi kuwa wasiostahiki kuwa rafiki za Mungu