Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 11/22 kur. 12-14
  • Je, Kuwa Rafiki ya Mungu Kutanisaidia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kuwa Rafiki ya Mungu Kutanisaidia?
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Urafiki na Mungu
  • “Tumaini Langu Tokea Ujana Wangu”
  • Mungu Hutusaidia Kufuata Njia Inayofaa
  • “Mwamba wa Moyo Wangu”
  • Kusitawisha Urafiki Ulio Bora Zaidi Katika Ulimwengu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
    Amkeni!—1996
  • Mbona Rafiki Yangu Ananitendea Hivi?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 11/22 kur. 12-14

Vijana Huuliza. . .

Je, Kuwa Rafiki ya Mungu Kutanisaidia?

VIJANA wengi leo hukulia chini ya mikazo ambayo ingalikuwa isiyoaminika kwa kizazi kilichopita. Waanzilishi wa uchunguzi wa kitaifa wa vijana 160,000 walieleza hivi: “Matineja watuambia kwamba mwingi wa msukosuko wao hutokana na misongo ambayo wao huhisi kutomudu; kutokana na kivunja-moyo na huzuni ambayo hukumba kujitumaini kwao; na kutokana na wazazi ambao hawahangaikii matatizo yao.” Huenda vilevile ukahisi kwamba wengine hawaelewi hata kidogo jinsi maisha yawezavyo nyakati nyingine kuwa yenye kuumiza kwa kijana.

Bila shaka, huenda ukawa na rafiki wa karibu ambaye waweza kumtegemea kwa utegemezo wa kihisia-moyo, na jambo hili laweza kuleta kitulizo fulani. Lakini, je, si kweli kwamba kuna matatizo yenye kuumiza ambayo ni lazima uyakabili ukiwa peke yako? Ni kweli kama nini kwamba nyakati nyingine ni ‘moyo wako tu huijua huzuni ya nafsi yako.’ (Mithali 14:10) Lakini kuna Mtu Fulani ambaye hukuelewa kabisa, naye hutoa urafiki wake. Vijana wengi wamepata kwamba urafiki wake ni msaada mkubwa hata katika nyakati zenye maumivu zaidi.

Urafiki na Mungu

Msichana mmoja aliulizwa alichomshukuru Yehova Mungu kwacho zaidi. Jibu lake: “Kwamba twaweza kumjua na kuwa marafiki wake wa siri.” Naam, yawezekana kuwa na urafiki ulio bora zaidi katika ulimwengu wote mzima! Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Mwenyezi-Mungu ni msiri wa watu wanaomcha.”—Zaburi 25:14, Habari Njema kwa Watu Wote.

“Usiri na Yehova” (New World Translation)—ni fursa yenye thamani kama nini! Neno la Kiebrania la asili lawasilisha wazo la maongezi ya wazi, ya kindani pamoja na mtu fulani ambaye ni rafiki wa pekee. Hivyo, ni uhusiano wa karibu wenye kutegemea upendo, usiri wa hali ya juu unaotokana na kutumainiana. Ukiwa rafiki ya Mungu, unahisi kwamba ustahiki wako kwa kweli ukiwa mtu unathaminiwa na mmoja huyu ambaye anakuelewa kwelikweli. Lakini ni yapi manufaa ya urafiki huu?

“Tumaini Langu Tokea Ujana Wangu”

Vijana wengi, licha ya kujishaua kwa nje, kindani hukosa kujitumaini. “Natoa maoni yangu na mtu fulani atatoa yake na kuyabadili yale yangu kabisa,” akaguna Judy mwenye umri wa miaka 13. “Sina uhakika kabisa kujihusu.” Hata hivyo, Rafiki yetu wa kimbingu, huandaa katika Neno lake lililoandikwa, Biblia, mwongozo hususa wa maisha yenye ufanisi. Kwa kweli, shauri linalotolewa katika kitabu cha Biblia cha Mithali limeandikwa ili kumpa ‘kijana maarifa na uwezo wa kufikiri,’ likimwezesha kunyoosha mapito yake. (Mithali 1:1-4; 3:1-6) Hili laweza kukupa tumaini lililoje! Waweza kujua njia bora zaidi ya kuishi.

Biblia, pamoja na misaada ya kusoma Biblia kama vile gazeti hili, huandaa shauri kuhusu karibu kila upande wa maisha—kuanzia na jinsi ya kuchagua marafiki hadi mtazamo ufaao kuelekea wazazi wako. (Mithali 1:8, 9; 13:20) Wale wanaofuata mwelekezo kama huo basi waweza “kuepukana na tanzi za mauti.” (Mithali 14:27) Kwa kielelezo, msichana anayeitwa Mae aliona dada yake wa kimwili akidharau kanuni za Biblia. Dada huyo alikufa kifo cha mapema chenye kuhuzunisha kwa sababu ya mtindo-maisha wake wa uovyo-ovyo. Mae alieleza hivi jinsi alivyoweza kukinza ukosefu wa adili kama huo: “Naweza kutafakari waziwazi kuhusu kanuni za Yehova juu ya adili, na hili huniimarisha. Kanuni hizi hunisaidia kuona jinsi Yehova alivyo kihalisi na kwamba njia yake ni bora zaidi.”

Hata hivyo, Yehova akiwa rafiki, yatia ndani mengi zaidi ya kujifunza viwango vyake tu. Waweza kuona upendezi wake wa kibinafsi katika maisha yako. Biblia hueleza kuhusu Mfalme Daudi, aliyefunzwa na Mungu tokea ujana wake. Daudi akawa rafiki ya Mungu, na ingawa alipatwa na “mateso mengi,” kwa kweli alimwona Mungu akitenda maishani mwake. Daudi alizungumza kuhusu “miujiza” ya Mungu kwa niaba yake na kuhusu “nguvu” za Yehova, zikitumika maishani mwake. Kutokana na maono ya kibinafsi kama hayo, Daudi aliandika hivi: ‘Ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, tumaini langu tokea ujana wangu.’ (Zaburi 71:5, 17, 18, 20) Waweza kuwa na tumaini hilihili unapohisi baraka ya Yehova maishani mwako. Ujitahidipo kufuata mwongozo wake—licha ya matatizo—hakika utakuwa ukitembea na Mungu katika uhusiano wenye kuhazinika.—Linganisha Mwanzo 6:9.

Mungu Hutusaidia Kufuata Njia Inayofaa

Kukiwa na vishawishi na misongo yote iliyopo maishani, kufuata mwongozo wa Mungu si rahisi. Jambo hili lilikuwa kweli kwa Peggy, ambaye akiwa kijana alikuwa mraibu wa dawa za kulevya na kahaba. Aliweza kushinda uraibu wake na kufanya mabadiliko ya maadili kwa kujifunza Biblia, na hivyo akasitawisha urafiki na Mungu. Lakini Peggy aliendelea kukabili misongo ileile ambayo ilikuwa imemfanya atafute kitulizo kupitia kwenye dawa za kulevya. Alipoulizwa jinsi alivyoendelea kukinza, yeye alijibu hivi: “Naweza kusema tu ni kupitia roho ya Yehova.”

Peggy alijua kwamba Mungu hutoa roho yake takatifu, au kani tendaji, kwa marafiki wake na kwamba hii yaweza kuwapa nguvu ili kuishi kwa viwango vyake. (Matendo 5:32; 1 Wakorintho 6:9-11) “Kuna nyakati sasa ambazo mimi hurudiwa na hisia hizo za zamani, hasa ninapokuwa peke yangu,” Peggy akubali, “lakini mara mimi huanza kusali. Ule uwezo wa kushinda matatizo haya unasisimua zaidi kuliko chochote nilichopata kutimiza maishani mwangu.” Yatia moyo kama nini kujua kwamba akiwa rafiki, Mungu aweza kutusaidia “kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo, kwa kadiri ya nguvu itendayo kazi ndani yetu.”—Waefeso 3:20.

Roho ya Mungu hutusaidia kusitawisha sifa kama vile ustahimilivu, upole, na kujidhibiti. (Wagalatia 5:22, 23) Pia, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, wazee, au wachungaji, waliowekwa rasmi na roho takatifu, wameandaliwa na Mungu ili kutoa msaada wenye kutumika. Peggy aongezea hivi: “Nilikuwa na utegemezo mwingi kutoka kutanikoni, hasa kutoka kwa wazee. Ulikuwa msaada mkubwa mno.”

“Mwamba wa Moyo Wangu”

“Rafiki hupenda nyakati zote, na huwa ndugu katika nyakati za shida.” Ndivyo inasema Mithali 17:17 katika The Basic Bible. Rafiki huhitajika hasa katika “nyakati za shida.” Mtunga-zaburi Asafu alipatwa na msukosuko mkali wa kihisia-moyo, hata hivyo alikuwa amemkaribia Mungu akiwa rafiki. Hivyo, hata ingawa ‘moyo wake ulipoona uchungu’ kwa maumivu ya ndani, yeye alisema hivi: “Mungu ni mwamba wa moyo wangu.” (Zaburi 73:21, 26, 28) Yehova, ambaye kwa kweli alielewa vile Asafu alivyokuwa akihisi, alimpa utegemezo wa kihisia-moyo. Yehova alikuwa uvutano wenye kusawazisha juu ya Asafu ili kwamba asipoteze tumaini na ujasiri.

Rafiki yetu wa kimbingu vivyo hivyo aweza kuwa kwako kama msingi wa mwamba wakati wa taabu. Tineja mmoja alifahamu hili kupitia ono la kibinafsi. Bonnie alipokuwa na umri wa miaka 13, baadhi ya wasichana katika shule yao ya sehemu za mashambani walianzisha fununu mbaya, yenye uchongezi kumhusu. Kwa Bonnie ilionekana kana kwamba kila mtu aliamini uwongo huu. Wengi wa wanadarasa wenzake walishughulika naye kwa ubaridi, hata kumwita majina yenye kumshushia heshima. “Siku nyingi nilikuja nyumbani na kulia,” akaeleza Bonnie. “Hata nilihisi kujiua kwa sababu niliumia vibaya sana kindani.” Huyu msichana aliwaendea baadhi ya marafiki wake ili kupata utegemezo. “Nilijaribu kuongea na watu, lakini walionekana kutoelewa. Walifanya tatizo langu kuonekana kana kwamba si kitu. Nyakati nyingine nilijihisi mpweke sana.” Ni nini kilichomfanya asikate tumaini akiwa katikati ya mvurugiko kama huo? Yeye aendelea: “Isingalikuwa ni kwa sababu ya Yehova, ningalijiua. Nampenda sana. Yeye ni rafiki yangu bora kuliko wote.” Sasa ajua kwamba ni urafiki wake pamoja na Mungu ambao ulimsaidia kuvumilia ono hilo lenye kuvunja kihisia-moyo.

Kujua kwamba Yehova huelewa hali zetu na anajua kile ambacho kilitukia hasa ni faraja kubwa wakati wengine hawatuonyeshi hangaiko ambalo huenda tukatarajia. Pia, kujua kwamba Rafiki yetu ni “Baba wa rehema nyororo” ni msaada mkubwa tunapotendwa bila fadhili au hata kutendwa vibaya. Nyakati nyingine mioyo yetu wenyewe huenda ikatuhukumu, lakini “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4, NW; 1 Yohana 3:20) Kuwa na maoni ya Yehova kuelekea jambo kwaweza kuwa jambo lenye kufariji kwelikweli. Kwa kielelezo, mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 13 alitendwa vibaya kwa ukatili na wanaume watatu. “Baadaye, niliona haya sana nami nilijilaumu kwa yale yaliyonipata,” yeye akakubali. “Nilishuka moyo sana.” Kisha alianza kufanya utafiti katika vichapo vyenye kutegemea Biblia vya Watch Tower Society kuhusu habari ya kulalwa kinguvu. “Niliposoma habari hii, singeweza kuzuia hisia-moyo zangu nami nikalia. Nilihisi kana kwamba mzigo mzito ulikuwa umeondolewa mabegani pangu. Nilikuwa jeruhi. Kwa kutegemea Yehova, familia, na marafiki, niliweza kushinda kipindi hiki chenye msukosuko.” Maneno hayo yenye kutegemea Biblia yaliandaa utegemezo kama nini!

Urafiki pamoja na Mungu waweza kusaidia katika njia nyingi! Twaweza kuwa na tumaini halisi maishani, twaweza kusitawisha nguvu za ndani ili kufuata njia ya Mungu, na kuwa na utegemezo kama wa mwamba wakati wa taabu. Lakini twaweza kujengaje urafiki kama huo? Makala ya wakati ujao katika mfululizo huu itaeleza.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mungu aweza kuwa ‘mwamba wa moyo wako’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki