Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 12/1 kur. 25-30
  • Kusitawisha Urafiki Ulio Bora Zaidi Katika Ulimwengu Wote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusitawisha Urafiki Ulio Bora Zaidi Katika Ulimwengu Wote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Aina ya Urafiki Wenye Thamani
  • Wale Ambao Yehova Anafanya Urafiki Nao
  • Epuka Urafiki Utakaoshindwa
  • Yehova-Mtu Umjuaye Tu au Rafiki Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
    Amkeni!—1996
  • “Nimewaita Rafiki”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 12/1 kur. 25-30

Kusitawisha Urafiki Ulio Bora Zaidi Katika Ulimwengu Wote

“Nawe, Israeli, [u] mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu.”​—ISAYA 41:8, Biblia ya New World Translation.

1. Ni jambo gani linalofanya urafiki wa kweli usishindwe?

RAFIKI wa kweli ni mwenye thamani kama nini! Lakini ni nini msingi wa kuwa na rafiki wa kweli? Ni nini kinachotegemeza urafiki wenye kuendelea? Ni jambo fulani ambalo halishindwi kamwe, hata linafanya rafiki wa kweli asishindwe kamwe. Ni jambo gani? Ni sifa ambayo mtume Paulo alitaja aliposema, “Upendo haushindwi kamwe”!—1 Wakorintho 13:8, NW.

2. Kitenzi ambacho neno la Kigiriki “rafiki” limetolewa kwacho kina maana gani ya pekee?

2 Katika Maandiko ya Kiebrania, neno linalotafsiriwa “upendo” linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kupenda.” (Kumbukumbu la Torati 6:4, 5; linganisha Mathayo 22:37, NW.) Na katika Septuagint Version ya Kigiriki, kitenzi kinachotafsiri “unapaswa kupenda” katika maandishi ya Kiebrania ni a·ga·panʹ. Lakini, katika tafsiri hiyo ya kale na katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno linalotafsiriwa “rafiki” halitegemei kitenzi hicho bali ni neno la Kigiriki phi’los, linalotokana na kitenzi kinachomaanisha “kuwa na shauku ya upendo kwa ajili ya.” Kwa hiyo, kulingana na Kigiriki cha kwanza, shauku ya upendo inaonyeshwa kuelekea rafiki au kati ya marafiki. Hata katika lugha ya Kiswahili neno “rafiki” linatoa maana ya “mpendwa.”

3. Ikilinganishwa na upendo wa Mungu kwa ajili ya ulimwengu wa wanadamu, wanafunzi wa Yesu walishikamanishwa naye kwa upendo wa aina gani?

3 Kwa hiyo kitenzi cha Kigiriki ambacho neno “rafiki” linatolewa kinatoa maana yenye uchangamfu na ya uhusiano wa karibu sana kuliko upendo unaomaanishwa na kitenzi a·ga·pan’, kinachoonekana katika andiko la Kigiriki la Yohana 3:16, ambapo Yesu anatajwa kuwa akisema: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Kwa hiyo upendo (Kigiriki, a·gaʹpe) huo wa Yehova Mungu ni mpana kuweza kutia ndani ulimwengu wote wa wanadamu, jamii ya kibinadamu ijapokuwa na hali ya dhambi. Lakini Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu aliwaambia mitume wake waaminifu 11 kwamba walikuwa wameshikamanishwa pamoja naye kwa aina ya upendo iliyo changamfu zaidi, ya ukaribu zaidi.

Aina ya Urafiki Wenye Thamani

4. Ni kwa kufanya nini wanafunzi wa Yesu wangeendelea kuwa “rafiki” zake, na uhusiano huo wa karibu ungewaingiza katika cheo gani?

4 Yesu aliwaambia mitume hao kwamba wangeendelea kuwa “rafiki” zake wakiendelea kufanya mambo aliyokuwa amewaamuru wafanye. Akionyesha kwamba ingetia ndani ukaribu waliopendelewa kuwa nao ulioletwa na kutumainiana kwao, alisema: “Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:14, 15) Katika kusema hayo, Yesu alitumia neno phi’los kwa kila mmoja wa mitume hao.

5. Urafiki unaotajwa katika Mithali 18:24 unategemea nini, na uhusiano huo ni thabiti jinsi gani?

5 Kulingana na Mithali 18:24, mtu yule mwenye hekima aliyeongozwa kwa roho ya Mungu alisema: “Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe; lakini yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.” Urafiki huo hautegemei uhusiano wa kimwili; unategemea kuthamini ustahili hakika wa ambaye urafiki umefanywa pamoja naye. Ndiyo, huenda watu wa ukoo wa kimwili wakatengana kwa sababu mbalimbali za kichoyo, lakini rafiki imara hatakuwa mwenye kuyumba-yumba na atashikamana na urafiki wake zijapokuwa hali zenye majaribu au zilizo ngumu, au hali zenye kuyajaribu sana mawazo ya moyoni ambazo huenda zikasitawi.

6. Tunakumbushwa juu ya urafiki wa nani wenye nguvu, na Daudi aliulipaje urafiki huo baadaye?

6 Katika hilo tunaweza kumfikiria Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli aliyekataliwa, na kumfikiria Daudi, ambaye Yehova Mungu alikuwa amechagua na kupaka mafuta awe mfalme wa Israeli. Urafiki wao uliendelea mpaka kufa kwa Yonathani kwenye uwanja wa pigano. Aliposikia habari hizo zenye kusikitisha, Daudi alitoa kilio kilichoandikwa katika 2 Samweli 1:17-27. Akionyesha jinsi uhusiano wake na Yonathani ulivyokuwa mwororo, Daudi alisema: “Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani, ndugu yangu, ulikuwa ukinipendeza sana; upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu, kupita upendo wa wanawake.” Urafiki wa jinsi hiyo haungesahauliwa bila kulipwa. Ndio uliomfanya Mfalme Daudi amwonyeshe rehema Mefiboshethi, mwana wa Yonathani aliyebaki.​—2 Samweli 9:1-10.

7. (a) Je! urafiki kama ule wa Daudi na Yonathani umemalizika, hasa katika huu “umalizio wa mfumo wa mambo”? (b) Urafiki wa namna hiyo unamwingiza mtu katika mtajo gani wa uhusiano wa karibu, kama Yesu alivyoeleza mitume wake waaminifu?

7 Aina hiyo ya urafiki wenye thamani haijamalizika duniani. Leo, katika huu “umalizio wa mfumo wa mambo” wakati ‘upendo wa walio wengi umepoa,’ uchangamfu wa urafiki huo wa upendo unaonwa kati ya mashahidi wa Yehova Mungu walio wakfu na kubatizwa ambao wanatoa ushuhuda wa Ufalme aliotabiri Yesu. (Mathayo 24:3-14, NW) Marafiki wana maelekeo ya kuambiana siri kwa sababu wanatumainiana. Kumbuka kwamba Yesu alipokuwa akizungumza usiku sana na wale mitume 11 walioshikamana naye, yeye alisema: “Nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:14, 15) Ndiyo, mambo ya kiroho ya Neno la Mungu ambayo hayana budi kutimizwa au kutekelezwa kwanza yangefunuliwa kwa “rafiki” za kweli wa Bwana, Yesu Kristo, waliozaliwa kwa roho. Halafu “rafiki” hao wangekuwa na pendeleo na daraka la kufunua hayo yaliyokuwa siri takatifu kufikia wakati huo kwa wanaotaka kuingia katika uhusiano wa kirafiki pamoja na Yehova Mungu, ambaye mambo hayo ya siri yanatokana naye.

8. Yehova anatolea nani uhusiano wa karibu pamoja naye, na Yesu alitajaje agano linalohusika katika uhusiano huo wa karibu?

8 Ndivyo Yehova ameshughulika na waabudu wake waliozaliwa kwa roho ambao wameingizwa katika agano jipya kupitia Mpatanishi, Yesu Kristo. Alipokuwa akianzisha Chakula cha Jioni cha Bwana, Yesu alisema: “Kikombe hiki kinamaanisha lile agano jipya kwa uwezo wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.” (Luka 22:20, NW) Hayo yalikuwa kupatana na Zaburi 25:14, inayosema: “Siri ya [Yehova] iko kwao wamchao, naye atawajulisha agano lake.” Wanaoingia katika uhusiano wa kirafiki pamoja na Yehova Mungu na Mpatanishi wake, Yesu Kristo, wanapewa maarifa yasiyo ya kawaida kama nini!

Wale Ambao Yehova Anafanya Urafiki Nao

9. Je! tunapita cheo kwa kufikiri kwamba Yehova angefanya urafiki na viumbe duni vya kibinadamu, na ni maandiko gani ya Biblia tunayoweza kuonyesha kuthibitisha jibu hilo?

9 E, lakini je, kweli Aliye Juu Zaidi na Mungu Mweza Yote anaweza kuwa Rafiki yetu wa kibinafsi? Je! kweli kweli amejinyenyekeza kufikia kadiri hiyo awe Rafiki yetu? Si kupita cheo kufikiri hivyo. Katika barua waliyoandikiwa Waisraeli wa kiroho kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka 70 W.K., Yakobo aliandika hivi: “Maandiko yale yakatimizwa yaliyonena, Ibrahimu alimwamini [Yehova], ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa Mungu.” (Yakobo 1:1; 2:23; Mwanzo 15:6; Wagalatia 6:16) Katika ‘andiko’ moja la Kiebrania ambalo Yakobo alitaja hapo tunasoma ombi hili lililotolewa kwa Mungu na Mfalme Yehoshafati wakati usalama wa Yerusalemu ulipokuwa umehatirishwa na wavamizi wengi: “Si wewe, Ee Mungu wetu, uliyewafukuza wenyeji wa nchi hii mbele ya watu wako Israeli, ukawapa wazao wa Ibrahimu rafiki [“mpendwa,” NW] hata milele?” (2 Mambo ya Nyakati 20:7) Hapa tunaona kwamba neno la msingi la Kiebrania linalotafsiriwa “rafiki” linamaanisha “mpendwa” (NW). Bila shaka, Ibrahimu alikuwa mpendwa wa Yehova, Mungu aliyemwita atoke Uru wa Wakaldayo na kumwingiza katika Nchi ya Ahadi. Akiwa mpendwa hivyo, Ibrahimu alikuwa mwanamume ambaye Yehova angeweza kufanya urafiki naye, au kumfanya rafiki Yake.

10. Katika Isaya 41:8, ni nani aliyejisemea juu ya urafiki, na Ibrahimu alipewa msimamo wa pekee pamoja na Mungu kwa msingi wa nia gani yake kuelekea Yehova?

10 Lakini, katika Isaya 41:8 Yehova alijisemea akatumia maneno haya yenye kutia moyo wazao wa Ibrahimu wakiwa taifa: “Nawe, Israeli, [u] mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu.” Mungu Aliye Juu Zaidi aliheshimu urafiki huo pamoja na Ibrahimu akampa mgawo wa kuwa babu mwenye kutokeza wa Yesu Kristo, aliye Mwokozi wa wanadamu wote, kutia Ibrahimu mwenyewe. Mzao huyo wa Ibrahimu hakuwa rafiki tu wa Yehova Mungu, bali aliizidi hali ya kuwa hivyo kwa maana yeye ni Mwana mpendwa wa Mungu.​—Yohana 3:16.

11. Ni kwa sababu gani urafiki na Yehova hauna budi kujaribiwa?

11 Kwa yote yaliyotangulia, tunaweza kukata shauri gani? Kwamba inawezekana kwa viumbe wa kibinadamu hapa chini, yaani, “mahali pa kuweka miguu” ya Yehova, kuwa rafiki zake. (Isaya 66:1) Bila shaka, urafiki wetu wenye thamani pamoja naye katika ulimwengu huu wa kale utajaribiwa, kwa maana Shetani Ibilisi, “mungu wa huu mfumo wa mambo,” atajaribu kuuvunja.​—2 Wakorintho 4:4, NW.

12. Kama Ayubu wa nchi ya Uzi, tunapaswa kuazimia kufanya nini juu ya urafiki wetu na Aliye Juu Zaidi?

12 Fikiria kisa cha yule mwanamume mwenye kutokeza wa nyakati za kale mwenye kuitwa Ayubu, ambaye juu yake mwanafunzi Yakobo aliye Mkristo alisema: “Tazama! Tunawatangaza wenye furaha wale ambao wamevumilia. Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu na mmeona matokeo aliyoleta Yehova, kwamba Yehova ni mwororo sana katika upendo wenye shauku na ni mwenye rehema.” (Yakobo 5:11, NW) Ayubu hakuwa mtu wa kuwaziwa tu bali aliishi kweli kweli katika nchi ya Uzi. Ibilisi alitia shaka juu ya kama urafiki wa Ayubu kuelekea Mungu ulikuwa wenye ubora unaodumu, na Yehova akamruhusu Shetani amjaribu Ayubu vikali sana. Kupitia misiba yenye kuvunja moyo aliyomletea Ayubu, Shetani alijitahidi kumfanya amkane Yehova. Lakini Ayubu alikataa kumuunga mkono Ibilisi kwa kutomkana Mungu. Kama angalimkana, Ayubu angalikufa akiwa upande wa Shetani katika lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Tofauti yake, Ayubu alithibitisha Shetani Ibilisi kuwa mwongo mkubwa. Hapa duniani, Yesu Kristo alithibitisha jambo ilo hilo. Lakini namna gani sisi leo? Wale wanaothamini sana urafiki wa Yehova wameazimia kutegemeza upande wake wa ugomvi huu unaohusu ulimwengu wote. Nao watafanya hivyo mpaka Shetani na mashetani wake watakapotupwa ndani ya shimo lisilo na mwisho hatimaye na kunyamazishwa kabla ya Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo.​—Ufunuo 20:1-4.

13. Urafiki pamoja na Yehova Mungu na Mwanaye mzaliwa-pekee unachukua nafasi gani, na ni mwendo gani tunaopaswa kufuatia ili tusipangwe katika hesabu ya “wazinzi” wa mfano?

13 Hakuna urafiki unaopita ule wa pamoja na Mungu Yehova, Aliye Juu Zaidi. Urafiki pamoja na Mwana wa Mungu aliye mzaliwa-pekee ndio unaochukua nafasi ya pili. Uhusiano huo wa kupendeza pamoja nao unamaanisha uzima wa milele katika furaha tele. Kwa haki wanadai utii wetu kamili. Hatuwezi kuwa tukishirikiana na ulimwengu huu wa kale uliohukumiwa maangamizi na wakati uo huo tusitawishe urafiki pamoja na Yehova na Mwanaye. Kwa njia ya kiroho, hatutaki kupangwa katika hesabu ya wazinzi, kulingana na Yakobo 4:4, andiko linalotaja jambo hilo waziwazi na kusema: ‘ Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” Maneno hayo yalielekezwa kwa Waisraeli wa kiroho wa karne ya kwanza W.K., lakini pia yanahusu Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika ulimwengu huu, au mfumo huu wa mambo wa karne ya 20.

Epuka Urafiki Utakaoshindwa

14. Kuhusu urafiki, Mashahidi wa Yehova wanaepukaje kupatwa na yaliyotabiriwa katika Zekaria 13:4-6?

14 Kwa sababu ya kutojifanya rafiki za ulimwengu huu wa kale uliopotoka na wenye jeuri, Mashahidi wa Yehova wanasingiziwa, kuonewa, na kuteswa. Ndivyo ilivyokuwa kwa shahidi mkuu zaidi wa Yehova aliyepata kuwa duniani, Yesu Kristo, nao hawamzidi yeye. (Ufunuo 1:5; 3:14) Kwa sababu kwa unyofu wanaendelea kurekebisha kufikiri kwao kulingana na Neno la Rafiki yao aliye bora zaidi, Yehova Mungu, hawapatwi na yanayosimuliwa kiunabii katika Zekaria 13:4-6, ambapo pameandikwa hivi: “Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba manabii, kila mmoja wao, atayaonea haya maono yake atoapo unabii; wala hawatavaa joho la nywele ili kudanganya watu; bali atasema, Mimi si nabii kamwe; mimi ni mkulima wa nchi; kwa maana nalifanywa mtumwa tokea ujana wangu. Na mtu atamwambia, Je! jeraha hizi ulizo nazo kati ya mikono yako ni nini? Naye atajibu, Ni jeraha nilizotiwa katika nyumba ya rafiki [“wapendwa,” NW] zangu.”

15. Ni kwa sababu gani viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamevaa majoho ya pekee mbele ya watu, nao wamefanya urafiki wa kujitafutia faida yao wenyewe pamoja na nani?

15 Kwa karne nyingi sasa, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamevaa ‘majoho’ kwa kusudi la kuvuta fikira kwenye kazi yao ya kidini na kwa kusudi la kuheshimiwa wao binafsi kwa kujitofautisha na washiriki wa makundi yao. Viongozi wa kidini wanafanya hivyo, ingawa hakuna ushuhuda hata mmoja wa kuthibitisha kwamba Yesu Kristo na mitume wake na waevanjeli aliotuma walivaa wakati wo wote majoho rasmi ya kidini ili kuvuta fikira kwenye cheo chao na kukikweza. Sasa tumo ndani ndani sana katika “umalizio wa mfumo wa mambo” ulioanza wakati wa kumalizika kwa “majira ya Mataifa,” au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” katika mwaka 1914. (Mathayo 24:3; Luka 21:24, UV; NW) Kwa muda mrefu viongozi wa kidini wamejaribu kuwa rafiki bora zaidi wa sehemu za kibiashara, kijeshi, na kisiasa za ulimwengu huu. Wamefanya hivyo kwa ajili ya faida yao wenyewe ya kichoyo na bila kusumbuliwa na dhamiri. Lakini urafiki wao wa kichoyo hautaendelea sana!

16. (a) Kulingana na unabii wa Biblia, “rafiki” za ulimwengu watafanyia nini jamii ya viongozi wa kidini hivi karibuni? (b) Hata wajapokuwa katika cheo kingine, hatimaye viongozi wa kidini hawatakosa kupatwa na nini?

16 Viongozi wa kidini na wanadini wao pia wanajikuta katika kizazi kilichofanya maendeleo makubwa ya kisayansi. Uhusiano wa kilimwengu unaharibiwa kabisa chini ya mkazo wa nyakati hizi. Viongozi wa kidini, ujapokuwa msimamo wanaodai wanao na Mungu wa mbingu, hawajapata kibali yo yote kutoka kwake juu ya mpango wa mambo wa kibiashara, kijeshi na kisiasa, nao hawatoi faraja yo yote kwa hali ya ulimwengu yenye kuwa mbaya zaidi. Karibuni, “rafiki” zao wa kilimwengu watafanywa watambue kwamba viongozi wa kidini hawafai kitu, ndiyo, ni mzigo kwao, ni wawongo katika unabii wao kwamba kutakuwa nyakati bora za kufanikiwa kimwili bila ya kutegemea Ufalme wa Yehova mikononi mwa Kristo. Hakika, “rafiki” hao wa kilimwengu mwishowe watasukumwa waonyeshe hasira yao kamili ya kwamba wameacha kuwatumaini viongozi wa kidini, wanawadharau, hata kuwachukia. Watawaangamiza kwa jeuri au angalau wawavue majoho yao rasmi ya kikazi na kuwafanya wawe watu wa kawaida, wenye cheo cha kawaida tu, kama inavyosimuliwa katika Zekaria 13:4-6. Lakini kubadilishwa huko kwa cheo chao hakutawazuia wasiangamizwe pamoja na Babuloni Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo sura za 17 na 18. “Rafiki” za kilimwengu za viongozi wa kidini hawatawasaidia hata.

17. Ni urafiki gani unaostahili kusitawishwa, na kwa muda gani?

17 Kwa sababu ya hayo, ni jambo la maana kama nini kuepuka urafiki wa kichoyo wa aina isiyofaa! Lakini urafiki bora zaidi katika ulimwengu unapaswa uwe wenye thamani kwetu kama nini! Unastahili kusitawishwa nasi milele.

Wewe Una Mawazo Gani?

◻ Wanafunzi wa Yesu wanaweza kuendelea kuwa rafiki zake kwa kufanya nini tu?

◻ Tunajuaje kwamba wanadamu wanaweza kufurahia urafiki wa Yehova, naye anakubali nani wawe na uhusiano wa karibu naye?

◻ Ni kwa sababu gani urafiki pamoja na Mungu hauna budi kujaribiwa?

◻ Kwa habari ya urafiki, Mashahidi wa Yehova wanaepukaje kupatwa na yaliyotabiriwa katika Zekaria 13:4-6?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Daudi na Yonathani walifurahia urafiki wenye thamani wa kutoka moyoni. Wewe pia unaweza kuufurahia

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ibrahimu alikuwa ‘rafiki ya Yehova.’ Na wewe je?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki