Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 6/1 kur. 24-26
  • Yehova-Mtu Umjuaye Tu au Rafiki Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova-Mtu Umjuaye Tu au Rafiki Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Urafiki na Mungu
  • Matakwa ya Urafiki
  • Urafiki na Yehova Ni wa Maana Kadiri Gani Kwako?
  • Kusitawisha Urafiki Ulio Bora Zaidi Katika Ulimwengu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
    Amkeni!—1996
  • “Nimewaita Rafiki”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 6/1 kur. 24-26

Yehova-Mtu Umjuaye Tu au Rafiki Yako?

“JOHN, je, naweza kukujulisha kwa rafiki yangu? Huyu ni—samahani, jina lako ni nani tena?”

Je! umepata kusikia mazungumzo ya aina hiyo yenye kuleta aibu? Yanaandaa mfano wa jinsi watu wengine hutumia vibaya lile neno “rafiki.” Kwa kweli wao humaanisha ‘mtu wamjuaye tu’ au nyakati nyingine hata hawamaanishi hivyo. Kumjua tu Bwana Kamau anayeishi upande ule mwingine wa barabara ni jambo moja; kuwa rafiki yake ni jambo jingine lililo tofauti kabisa.

Kamusi moja hufasili “mtu umjuaye tu” kuwa “mtu ambaye umeshirikiana naye kijamii lakini ambaye huna shauku ya kibinafsi yenye nguvu kwake.” Inaonyesha “kuwa na kufahamiana, ukaribu, ushirika, na kutakia mema kidogo kuliko RAFIKI.”

Ukosefu huo wa shauku ya kibinafsi yenye nguvu husaidia kueleza ni kwa nini sisi hukosa kutoa uangalifu mwingi kwa yale yanayowapata watu tuwajuao tu, huku tukihusika kwa kupendezwa na maisha ya rafiki zetu. Tunashiriki shangwe zao na majonzi yao, tukiruhusu mambo hayo yatuathiri sana. Pasipo shaka, ni lazima tuwe wenye uangalifu tusiruhusu uhusiano wa kihisia-moyo utuongoze vibaya ili tuingilie mambo yao ya faragha.—1 Petro 4:15.

Kuwa na shauku ya kibinafsi yenye nguvu kwa rafiki zetu hueleza pia ni kwa nini sisi hujaribu kwa kawaida kuwapendeza. Mtu tumjuaye tu anapoona mwenendo wetu kuwa wenye kuchukiza au usiofaa, kuchukizwa kwake hakuelekei sana kutusukuma tugeuke. Lakini rafiki aweza kuwa na uvutano wenye nguvu kweli kweli, iwe ni katika mambo ya mavazi, mwenendo, au mwelekeo.

Kwa habari ya kutumainiana, shauku, staha, na uaminifu-mshikamanifu, urafiki hutaka daraka la kadiri ya juu kuliko kujuana tu kunavyotaka. Yeye atakaye urafiki, asitake kuwa na daraka lolote, kwa kweli ataka kuwa na mtu amjuaye tu, wala si rafiki. Rafiki wa karibu hufurahi kutimiza yale madaraka yanayoletwa na ile shauku ya kibinafsi yenye nguvu, wakitambua kwamba madaraka hayo huwapa nafasi ya kuthibitisha urafiki wao.

Urafiki na Mungu

Akiwa Muumbaji, Yehova ndiye Baba wa kimbingu wa ainabinadamu naye hustahili kupendwa, kutiiwa, na kustahiwa. Lakini yeye ataka wanadamu wafanye hivyo kwa sababu ya shauku ya kibinafsi yenye nguvu, si kwa sababu ya kutaka kutimiza wajibu tu. (Mathayo 22:37) Yeye awataka pia wampende akiwa Rafiki. (Zaburi 18:1) Kwa kuwa “yeye alitupenda sisi kwanza,” yeye mwenyewe ameweka msingi mkamilifu kwa ajili ya urafiki wa jinsi hiyo.—1 Yohana 4:19.

Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walimjua Yehova. Swali lilikuwa ni: Je! wangekubali toleo lake la urafiki? Kwa huzuni, hawakulikubali. Kufuatia kwao kwa ubinafsi kujitegemea bila Mungu kulidokeza ukosefu wa shauku ya kibinafsi yenye nguvu. Wakiwa na nia ya kukubali baraka za ule urafiki aliokuwa akiwatolea, hawakuwa na nia ya kuyatimiza madaraka ya urafiki huo. Ilikuwa kana kwamba walitaka kuonea sha-ngwe starehe na usalama wa makao yao ya Paradiso bila kuwa na nia ya kulipa kodi.

Sisi sote, baadhi yetu kwa kadiri kubwa zaidi ya wengine, tumeirithi roho hiyo ya kutothamini na ya kujitegemea. (Mwanzo 8:21) Kwa mfano, vijana wengine wameruhusu tamaa yao ya kiasili ya kujitegemea iwafanye wasithamini wazazi wao. Hiyo imetokeza mvunjiko wa urafiki wenye thamani kubwa zaidi ambao wapasa kuwako kati yao na wazazi wao kwa muda wote wa maisha. Hata hivyo, jambo hilo hata liwe ni la kuhuzunisha jinsi gani, mvunjiko wa urafiki wetu na Baba yetu wa kimbingu ni wenye uzito zaidi. Kwa kweli, waweza kusababisha kifo!

Matakwa ya Urafiki

Bila kutumainiana, hakuna uhusiano wowote uwezao kudumu kwa muda mrefu, iwe ni pamoja na wanadamu au pamoja na Mungu. Mzee wa ukoo Abrahamu alielewa hilo, na kwa sababu hiyo alionyesha tena na tena kwamba alimtumaini Mungu kabisa. Soma Mwanzo 12:1-5 na 22:1-18, na uone mifano miwili yenye kutokeza ya kumtumaini kwake Yehova. Naam, “Abrahamu alimwamini Mungu, na kwa imani yake akakubaliwa kuwa mtu mwadilifu.” Hiyo ndiyo sababu “akaitwa rafiki wa Mungu [Yehova, NW].”—Yakobo 2:23, HNWW.

Takwa la ziada ili kuwa na urafiki na Mungu ni kutimiza wajibu mbalimbali unaoletwa na urafiki huo. Kwa sababu ya cheo chetu duni kwa kulinganishwa na cheo cha Yehova, yafuatana kwamba wajibu huo mbalimbali ni mkubwa kuliko jinsi ambavyo ungekuwa katika urafiki wa kibinadamu. Huo unazidi kutaka kwetu kumpendeza katika mambo fulani tu—kama vile tungefanya na rafiki wa kibinadamu. Unatia ndani kutaka kwetu kumpendeza katika mambo yote. Yesu, Mwana wa Mungu na rafiki yake wa karibu zaidi, alionyesha hilo aliposema hivi juu ya Yehova: “Nafanya sikuzote yale yampendezayo.”—Yohana 8:29.

Hivyo, urafiki na Yehova, au na Mwana wake, haupatikani bila madaraka fulani; unategemea kuishi kwetu kulingana na matakwa ya urafiki ambayo wao wameweka. (Ona Zaburi 15:1-5.) Yesu alionyesha hilo kwa wazi katika mazungumzo pamoja na wanafunzi wake. “Ninyi mmekuwa rafiki zangu,” akawaambia, “mkitenda niwaamuruyo.”—Yohana 15:14.

Takwa jingine la urafiki ni kuwa na uwasiliano wa waziwazi na wa unyofu. Siku ya kifo chake, Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu hivi: “Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:15) Kwa kushiriki mawazo yake pamoja na rafiki zake, Yesu alikuwa akifuata mfano wa Baba yake wa kimbingu, ambaye juu yake Amosi 3:7 husema hivi: “Hakika Bwana MUNGU [Yehova, NW] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.”

Je! hilo si jambo la kawaida miongoni mwa rafiki? Huenda tusihisi msukumo wowote kushiriki mambo tuliyoyaona pamoja na Bwana Kamau aishiye upande ule mwingine wa barabara. Na kwa hakika zaidi tusingetaka kumwambia mawazo na hisia zetu za ndani kabisa. Kwa vyovyote vile, yeye ni mtu tumjuaye tu. Lakini tukiwa na rafiki zetu, mara nyingi ni vigumu hata kungojea kuwaambia mambo ya jinsi hiyo!

Ni vivyo hivyo katika urafiki wetu na Mungu. Ni vigumu kwetu kungojea kumkaribia katika sala, kumfunulia mahitaji yetu, tamaa zetu, na hisia zetu za ndani kabisa. Bila shaka, uwasiliano ukiwa kutoka upande mmoja tu, urafiki utaisha upesi. Kwa hiyo ni lazima sisi pia tuwe na nia ya kumruhusu Mungu aseme nasi. Twafanya hilo kwa kusikiliza kwa uangalifu Neno lake lililoandikwa, kutafakari juu ya shauri lake, na kisha kulitumia kwa njia iliyo bora zaidi.

Urafiki na Yehova Ni wa Maana Kadiri Gani Kwako?

Ili kukusaidia ujibu swali hilo, fikiria aina ya pekee ya urafiki wa kibinadamu. Ikiwa wewe ni kijana, labda unapendezwa na urafiki ambao ungeweza kuongoza kwenye ndoa. Bila shaka, unatambua kwamba kumjua tu yule atakayekuwa mwenzi wa ndoa sio msingi ufaao wa ndoa. Kujuana kwapasa kwanza kugeuke kuwe urafiki. Halafu urafiki huo waweza kukuzwa na kufinyangwa uwe uhusiano wa karibu zaidi utakaofanyiza hatimaye msingi ufaao wa ndoa yenye furaha.

Sasa fikiria. Watu wengi hujitahidi kadiri gani ili kukuza urafiki wa aina hiyo? Wao hutumia wakati na pesa nyingi kadiri gani ili kuuanzisha na kisha kuudumisha? Wao hutumia wakati mwingi kadiri gani wakiufikiria? Wao hufanya mipango—au huonyesha nia ya kubadili mipango—kwa kadiri gani kwa kusudi la kuufanyia maendeleo au kuudumisha uhusiano huo?

Kisha jiulize hivi: ‘Hilo hulinganikaje na jitihada zangu za kuukuza urafiki na Muumba wangu au kuufanyia maendeleo na kuuimarisha? Mimi hutumia wakati mwingi kadiri gani kufanya hivyo? Urafiki na Yehova huwa katika mawazo yangu kwa kadiri gani? Mimi ninafanya mipango—au ninaonyesha nia ya kubadili mipango—kwa kadiri gani kwa kusudi la kuufanyia maendeleo na kisha kuudumisha uhusiano huo?’

Wakristo wachanga wapaswa kufahamu kabisa kwamba urafiki wote wa kibinadamu, kutia na ule ambao hatimaye huongoza kwenye ndoa, ni wa pili kwa maana kutoka kwa ule urafiki ambao wanahitaji kuwa nao pamoja na Muumba wao. Hiyo ndiyo sababu wanasihiwa hivi kwenye Mhubiri 12:1: “Mkumbuke muumba wako siku za ujana wako.” Wengi wanafanya hivyo kwa kutumikia peupe wakiwa wahudumu wa Mungu, hesabu yao yenye kuongezeka daima wakiwa wahubiri wa wakati wote, au mapainia.

Ijapokuwa ile tabia ya kutojali na kule kuchukia dini kunakowazunguka, hao hutetea Yehova kwa ujasiri wanaposikia masuto na mashtaka bandia yakitolewa dhidi yake. Je! Yehova hapaswi kwa haki kutazamia hilo kutoka kwa rafiki zake? Je! hatungetazamia hilo kutoka kwa rafiki zetu? Na je, isingefurahisha mioyo yetu kupata rafiki zetu wakifanya hivyo kwa bidii na kwa usadikisho?—Linganisha Mithali 27:11.

Naam, urafiki na Mungu—sawa ule pamoja na wanadamu—huleta madaraka ambayo ni lazima yatimizwe ikiwa urafiki utadumu. Mtu asiye na nia ya kukubali madaraka hayo, au asiye tayari kujiweka wakfu kwa Mungu na kisha kuutekeleza, huenda kwa kweli akamjua Yehova. Hata hivyo, bado anahitaji kuona zile shangwe za kuwa na Yeye akiwa Rafiki.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Abrahamu alimtumaini Mungu na kwa hiyo akaitwa rafiki wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki