Vijana Huuliza . . .
Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
“Rafiki yangu nami tulishiriki mapendezi na utendaji mwingi pamoja; tulifurahia kutumia wakati pamoja. Lakini ghafula urafiki wetu ukawa baridi na baridi zaidi. Hilo lilinifanya nihisi nikiwa nimeshuka moyo sana.”—Maria.
UMEPATA rafiki hatimaye, mtu anayekuelewa na asiyekuhukumu. Kisha, ghafula, urafiki wenu waanza kupotea. Wajaribu kuuokoa, lakini bila mafanikio.
Rafiki mwaminifu-mshikamanifu ni mwenye thamani sana. (Mithali 18:24) Na kumpoteza kwaweza kuleta maumivu sana. Biblia hutuambia kwamba wakati Ayubu alipoachwa na marafiki wake, yeye aliomboleza hivi: “Watu wa mbari yangu wamekoma, na rafiki zangu niwapendao wamenisahau.” (Ayubu 19:14) Huenda ukahisi huzuni kama hiyo ikiwa hivi majuzi urafiki uliokuwa nao ulizorota. Kama Patrick mchanga alivyosema, “unahisi kana kwamba mtu uliyempenda amekufa.” Lakini namna gani ikiwa karibu kila urafiki ambao umepata kuwa nao umekosa kufaulu?
Urafiki Uvunjikao Upesi
Kitabu Adolescence kilichoandikwa na Eastwood Atwater chaonelea kwamba urafiki wa matineja “huelekea kutokuwa imara, ukiwa na mabadiliko ya ghafula yenye kutazamisha na hisia chungu wakati urafiki unapokoma.” Ni nini kifanyacho urafiki wa matineja kuwa wenye kuvunjika upesi sana? Sababu moja ni kwamba unapozidi kuwa mkubwa, hisia, maoni, miradi, na mapendezi yako huanza kubadilika. (Linganisha 1 Wakorintho 13:11.) Unaweza kujipata ukienda mbele—au kubaki nyuma—ya marika wako katika mambo fulani.
Kwa hiyo marafiki wanapokua, nyakati fulani uhusiano wao wa karibu unadidimia pole kwa pole—si kwa sababu wamekasirikiana, bali kwa sababu wanasitawisha miradi, mapendezi, na viwango tofauti. Huenda ikawa vema zaidi uhusiano ukome. Unapokuwa mkubwa na kuanza kuchukua mambo ya kiroho kwa uzito, huenda ukatambua kwamba baadhi ya marafiki wako wa zamani hawakuwa wenye uvutano ujengao. (1 Wakorintho 15:33) Unawajali, lakini hufurahii uandamani wao kama ulivyoufurahia zamani.
Mambo Ambayo Hudhuru Urafiki
Hata hivyo, namna gani ikiwa wewe hupoteza marafiki daima—mahusiano ambayo ungependa kudumisha? Kwa wazi, ingeweza kumaanisha kwamba una kasoro za kiutu unazopaswa kushinda. Kwa kielelezo, wivu hudhuru urafiki. Wazia kwamba una rafiki ambaye ni tajiri zaidi, mwenye kipawa zaidi, mwenye kuvutia zaidi, au mwenye kupendwa na wengi kuliko wewe. Je, wewe hukasirishwa na uangalifu zaidi ambao yeye aweza kupata? “Husuda [“wivu,” NW] ni ubovu wa mifupa.” (Mithali 14:30) “Nilionea wivu kwelikweli umashuhuri wa rafiki yangu na vitu vyote alivyokuwa navyo ambavyo sikuwa navyo,” akiri Keenon mchanga, “na hilo liliathiri urafiki wetu.”
Umiliki waweza kuwa kitabia kingine chenye kuharibu. Vipi ukijua kwamba rafiki anatumia wakati mwingi zaidi pamoja na wengine na wakati mchache zaidi pamoja nawe? Kijana mmoja alikiri hivi: “Nilikuwa na wivu hata wakati wengine walipozungumza na baadhi ya marafiki wangu.” Huenda ukaona ushirika wa rafiki yako pamoja na wengine kuwa tendo la usaliti.
Kutaka ukamilifu kwaweza pia kuharibu urafiki. Kwa kielelezo, wapata kujua kwamba rafiki ameporojesha kukuhusu, labda akifunua mambo ya siri. (Mithali 20:19) “Siwezi kumtumaini tena kamwe!” unapaaza sauti kwa hasira.
Urafiki—Kupokea au Kutoa?
Ikiwa wivu, kuwa mwenye kumiliki, au kutaka ukamilifu kumeleta mkazo juu ya urafiki wako, jiulize, ‘Mimi nataka nini kutokana na urafiki?’ Je, unafikiri kwamba urafiki humaanisha kuwa na mtu aliye tayari kutii amri yoyote, namna ya mtumishi wa kufanya lolote utakalo? Je, unatafuta urafiki ili upate sifa, kupendwa na wengi, au kupata faida? Je, unatazamia ujitoaji usiohusisha mwingine kutoka kwa rafiki, kukiwa na fursa ndogo kwa wengine katika huo uhusiano? Basi unahitaji kurekebisha maoni yako juu ya urafiki.
Kutokana na mafundisho ya Biblia twajifunza kwamba mahusiano mazuri pamoja na wengine hutokana, si na kupokea, bali hutokana na kutoa! Kwenye Mathayo 7:12, Yesu Kristo mwenyewe alisema: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” Ni jambo la asili kutazamia mambo fulani kutoka kwa marafiki. Kitabu Understanding Relationships chakiri hivi: “Kwa kawaida sisi hutazamia rafiki awe mtu ambaye ni mfuatiaji wa haki, mwenye kusema mambo wazi, mwenye kuonyesha shauku, atuambiaye siri au matatizo yake, atupaye msaada tunapouhitaji, atutumainiye na pia . . . aliye tayari kusuluhisha kutokubaliana.” Hata hivyo, huo sio mwisho wa mambo. Kitabu hicho chaongeza hivi: “Haya ndiyo mambo ambayo watu hutazamia rafiki awafanyie na kutazamia kumfanyia rafiki vilevile.”—Italiki ni zetu.
Ona jinsi Yesu mwenyewe alivyowatendea wale waliokuwa karibu naye. Yeye aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki.” Lakini je, urafiki wa Yesu pamoja na wanafunzi wake ulitegemea kile ambacho wangemfanyia? Kinyume na hilo. Yeye alisema: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13, 15) Ndiyo, msingi wa kweli wa urafiki ni upendo wenye kujidhabihu! Upendo unapokuwa msingi, uhusiano waweza kusalimika mabishano na matatizo.
Matatizo Yanapozuka
Kwa kielelezo, wazia kwamba rafiki yako ana fedha zaidi, akili, au kipawa kukushinda. Upendo usio na choyo hukusaidia kufurahi pamoja na rafiki yako. Kwa vyoyote, “mwenye upendo hana wivu,” yasema Biblia.—1 Wakorintho 13:4, HNWW.
Au tuseme rafiki yako asema au kufanya jambo ambalo laumiza hisia zako. Je, yamaanisha kwamba urafiki wenu utaisha? Si lazima iwe hivyo. Mtume Paulo alikasirika sana wakati rafiki yake Marko alipomwacha katika safari ya kimishonari. Alikasirika sana hivi kwamba alikataa kumruhusu Marko aandamane naye katika safari yake iliyofuata! Paulo hata alirushiana maneno makali na binamu ya Marko, Barnaba, juu ya jambo hilo. Ingawa hivyo, miaka mingi baadaye, Paulo alisema kwa upendo kuhusu Marko, hata kumwalika Roma ili amhudumie. Bila shaka walikuwa wametatua tofauti zao.—Matendo 15:37-39; 2 Timotheo 4:11.
Kwa nini usijaribu kufanya jambo lilo hilo matatizo yazukapo katika urafiki wako? Usiache mambo yazorote. (Waefeso 4:26) Kabla ya kuhukumu haraka au kufanya mashtaka kwa hasira, sikiliza ayasemayo rafiki yako juu ya suala hilo. (Mithali 18:13; 25:8, 9) Labda kumekuwa na kutoelewa jambo fulani. Lakini namna gani ikiwa rafiki yako kwa kweli ana hatia ya kuonyesha ukosefu wa ufahamu? Kumbuka kwamba rafiki yako ni binadamu mwenye udhaifu tu. (Zaburi 51:5; 1 Yohana 1:10) Nasi sote tuna hatia ya kusema na kufanya mambo ambayo baadaye hujuta.—Linganisha Mhubiri 7:21, 22.
Hata hivyo, unaweza kueleza wazi kiasi ambacho vitendo vya rafiki yako vimekuumiza. Hilo laweza kumsukuma rafiki yako aombe radhi yenye unyoofu. Kwa kuwa upendo “hauhesabu mabaya,” labda waweza kusahau jambo hilo. (1 Wakorintho 13:5) Akitazama nyuma kwa urafiki uliopotea, Keenon mchanga asimulia: “Ikiwa ningaliupata tena, singalitazamia ukamilifu kutokana na urafiki wetu. Ningalisikiliza zaidi na kumtegemeza na kutofanya kasoro zake kuwa kubwa. Sasa naelewa kwamba kinachofanya urafiki ufanikiwe ni kujitahidi kupitia mitihani na magumu.”
Lakini vipi ikiwa rafiki yako hatumii wakati mwingi nawe kama wakati uliopita au kama utakavyo? Je, yaweza kuwa umekuwa mwenye kumiliki wakati na uangalifu wa rafiki yako kupita kiasi? Hilo laweza kuzima urafiki. Watu wenye mahusiano yenye kufanikiwa hupatiana kiwango cha uhuru wa kufanya mambo watakayo. (Linganisha Mithali 25:17.) Wao huruhusu nafasi ya kutosha ya kufurahia watu wengineo! Kwa vyovyote, Biblia hutia moyo Wakristo “wapanuke” katika urafiki wao. (2 Wakorintho 6:13, NW) Kwa hiyo rafiki anapofanya hilo, hakuna haja ya kumwona kuwa anakosa uaminifu-mshikamanifu.
Kwa hakika, si wazo zuri kutegemea kupita kiasi mtu mmoja hususa. (Zaburi 146:3) Ni jambo la hekima kusitawisha urafiki pamoja na watu wasio marika wako, kama vile wazazi wako, wazee, na watu wazima wengine wenye kujali wachukuao daraka. Ana asimulia hivi kwa upendo: “Mama yangu ndiye rafiki yangu bora zaidi. Naweza kuzungumza naye kuhusu karibu kila jambo.”
Urafiki Wenye Kudumu Waweza Kufurahiwa!
Biblia husema kwenye 1 Petro 3:8: “Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu.” Ndiyo, onyesha fadhili, huruma, uaminifu-maadili, na hangaiko la kweli kwa wengine, nawe sikuzote utavutia marafiki! Ni kweli, urafiki wenye kudumu wahitaji jitihada na azimio. Lakini thawabu hufanya jitihada istahili.
Kwa kupendeza, Biblia hueleza juu ya Daudi na Yonathani. Wao walifurahia urafiki wenye kutokeza. (1 Samweli 18:1) Waliweza kushinda wivu usio na maana na kasoro za kiutu. Hilo liliwezekana kwa sababu wote Daudi na Yonathani waliweka urafiki na uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu juu ya vitu vinginevyo vyote. Fanya vivyo hivyo, nawe hutakuwa na tatizo kudumisha marafiki wenye kumhofu Mungu!
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mara nyingi urafiki huvunjika wakati mmoja anapohisi ni kukosa uaminifu-mshikamanifu kuwa na marafiki wengine