Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 3/15 kur. 4-6
  • Waweza Kufurahia Urafiki Wenye Kudumu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waweza Kufurahia Urafiki Wenye Kudumu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vielelezo vya Kibiblia vya Urafiki
  • Jinsi ya Kukuza Urafiki
  • Kudumisha Urafiki Ukiwa Umeshikamana
  • Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
    Amkeni!—1996
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Urafiki?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • “Wakashikamana na Kuwa Marafiki wa Karibu Sana”
    Igeni Imani Yao
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 3/15 kur. 4-6

Waweza Kufurahia Urafiki Wenye Kudumu

KUNA vizuizi kwa urafiki. Kwa hakika, Biblia ilitabiri kwamba katika hizi “siku za mwisho” hakungekuwa na upendo, shauku ya asili, na uaminifu-mshikamanifu. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:12) Hali hizi zimesababisha pigo la upweke lisilo na kifani. Mtu mmoja alisema: “Ujirani wangu uko kama safina ya Noa. Ikiwa hujafunga ndoa, unatengwa.” Lawama zote za jambo hilo haziwezi kuwekewa watu wapweke. Katika sehemu fulani za ulimwengu, matatizo ya urafiki wenye kudumu hutia ndani mambo kama vile watu kuhama-hama, kuvunjika kwa familia, majiji yasiyo na urafiki na yenye hatari, na upungufu uonekanao katika wakati wa pumziko.

Mkaaji wa jijini wa siku ya kisasa huenda akashirikiana na watu wengi zaidi katika juma moja kuliko wale ambao mkaaji wa kijijini wa karne ya 18 aliona kwa mwaka mmoja au hata kwa maisha yake yote! Hata hivyo, mara nyingi mahusiano leo ni ya kijuu-juu. Wengi hujihusisha kabisa katika kuungana na watu wengine kijamii na kujaribu kujifurahisha. Ingawa hivyo, twapaswa kukubali kwamba kujifurahisha kwenye ubatili pamoja na washirika waliochaguliwa isivyofaa ni kama kutumia miiba kwa ajili ya moto. Mhubiri 7:5, 6 lasema: “Heri kusikia laumu ya wenye hekima, kuliko mtu kusikia wimbo wa wapumbavu; maana kama mlio wa miiba chini ya sufuria, ndivyo kilivyo kicheko cha mpumbavu. Hayo nayo ni ubatili.” Miiba hutokeza moto mwangavu na wenye kelele kwa muda mfupi, lakini hautoi joto la kutosha. Vivyo hivyo, waandamani wenye kelele, wachekao huenda wakatukengeusha kwa muda mfupi tu, lakini hawataondoa upweke wote na kutosheleza uhitaji wetu wa marafiki wa kweli.

Ufaragha hutofautiana na upweke. Ufaragha fulani ni muhimu kwetu kujiburudisha na hivyo kuwa na mengi zaidi ya kutoa tukiwa rafiki. Wanapokabiliwa na upweke, wengi mara moja hugeukia aina fulani ya kitumbuizo cha kielektroni. Ripoti ya uchunguzi fulani ilipata kwamba moja ya maitikio ya kawaida zaidi kwa upweke ni kutazama televisheni. Hata hivyo, watafiti walifikia mkataa kwamba kutazama televisheni kwa muda mrefu ni moja ya mambo mabaya zaidi tuwezayo kufanya wakati tuna upweke. Hiyo husitawisha kutokuwa watendaji, uchoshi, na fantasia, ikiwa kibadala kibaya cha mahusiano ya kibinafsi na watu wengine.

Kwa hakika, ufaragha waweza kuwa wenye thamani sana ikiwa twatumia wakati wetu tukiwa peke yetu kwa njia yenye kujenga. Twaweza kufanya hilo kwa kusoma, kuandika barua, kutengeneza vitu, na kupumzika. Ufaragha wenye kujenga hutia ndani kusali kwa Mungu, kujifunza Biblia, na kuitafakari. (Zaburi 63:6) Hizi ni njia za kumkaribia Yehova Mungu, yule ambaye atakuwa Rafiki yetu mkubwa kupita wote.

Vielelezo vya Kibiblia vya Urafiki

Ingawa ni vizuri kuwa mwenye urafiki na watu wengi, Biblia hutukumbusha kwamba “yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.” (Mithali 18:24) Sote twahitaji marafiki wachache wa karibu zaidi ambao hutujali kikweli, ambao urafiki wao hutupa shangwe, nguvu, na amani. Ingawa huenda urafiki huo wa kweli ukawa vigumu kupatikana leo, vielelezo vya kale vinatajwa hasa katika Biblia. Kwa mfano, kulikuwa na urafiki wenye kutokeza kati ya Daudi na Yonathani. Twaweza kujifunza nini kutokana nao? Kwa nini urafiki wao ulidumu?

Jambo moja ni kwamba Daudi na Yonathani walikuwa na mapendezi ya maana yaliyofanana. La maana zaidi, wao walikuwa na ujitoaji wenye kina kwa Yehova Mungu. Alipoona imani ya Daudi katika Mungu na matendo yake katika kutetea watu wa Yehova, “roho [“nafsi,” New World Translation] ya Yonathani, ikaambatana na roho [“nafsi,” NW] ya Daudi, Yonathani akampenda kama roho [“nafsi,” NW] yake mwenyewe.” (1 Samweli 18:1) Basi, upendo wa wote wawili kwa Mungu, husaidia kufunganisha marafiki wawili pamoja.

Yonathani na Daudi walikuwa watu thabiti walioishi kulingana na kanuni za kimungu. Hivyo wangeweza kuheshimiana. (1 Samweli 19:1-7; 20:9-14; 24:6) Kwa hiyo tumebarikiwa kikweli ikiwa tuna marafiki wenye kumhofu Mungu ambao wanaongozwa na kanuni za Kimaandiko.

Kuna mambo mengine yaliyochangia urafiki wa Daudi na Yonathani. Uhusiano wao ulikuwa wa moyo mweupe na wazi, na kila moja alimtumaini mwenzake. Kwa uaminifu-mshikamanifu Yonathani alitanguliza mapendezi ya Daudi. Yeye hakuwa na wivu kwa kuwa Daudi alikuwa ameahidiwa ufalme; badala ya hivyo, Yonathani alimtegemeza kihisia-moyo na kiroho. Na Daudi alikubali msaada wake. (1 Samweli 23:16-18) Katika njia zifaazo Kimaandiko, Daudi na Yonathani walijulishana hisia zao za urafiki. Urafiki wao wa kumhofu Mungu ulitegemea uthamini na shauku ya kweli. (1 Samweli 20:41; 2 Samweli 1:26) Ulikuwa usioweza kuvunjika kwa sababu wanaume wote wawili walibaki waaminifu kwa Mungu. Kutumia kanuni hizo kwaweza kutusaidia kujenga na kudumisha urafiki wa kweli.

Jinsi ya Kukuza Urafiki

Je, unatafuta marafiki wa kweli? Huenda usihitaji kutafuta mbali. Wengine miongoni mwa washiriki wako wa kawaida wanaweza kuwa marafiki wako, na huenda wakahitaji urafiki wako. Hasa kuhusiana na Wakristo wenzako, ni jambo la hekima kutumia shauri la mtume Paulo la ‘kupanuka.’ (2 Wakorintho 6:11-13, NW) Hata hivyo, usihuzunike ikiwa kila jitihada ya kufanya urafiki haitokezi kifungo bora. Kwa kawaida kukuza urafiki huchukua wakati, na si kila uhusiano utakuwa na kina kilekile. (Mhubiri 11:1, 2, 6) Bila shaka, ili kufurahia urafiki wa kweli, hatupaswi kuwa watu wenye ubinafsi, na twahitaji kufuata shauri la Yesu: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

Ni nani wanaohitaji urafiki wako? Kando na wale wa umri wako, namna gani wachanga zaidi au wazee-wazee? Urafiki wa Daudi na Yonathani, Ruthu na Naomi, na Paulo na Timotheo ulihusisha tofauti kubwa ya umri. (Ruthu 1:16, 17; 1 Wakorintho 4:17) Je, waweza kupanua urafiki wako kwa wajane na watu wengine ambao hawajafunga ndoa? Fikiria pia juu ya wale ambao ni wapya katika ujirani wenu. Huenda waliacha ushirika wa wengi au marafiki wao wote kwa kuhama au kubadili njia yao ya maisha. Usingojee wengine wakutafute. Ikiwa wewe ni Mkristo, fanya urafiki wenye kudumu kwa kutumia shauri la Paulo: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.”—Warumi 12:10.

Twaweza kuwazia urafiki kuwa namna fulani ya kutoa. Yesu alisema kwamba tukizoea kutoa, watu watatupatia. Alitaja pia kwamba kuna furaha nyingi zaidi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea. (Luka 6:38; Matendo 20:35) Je, umekutana na watu wa malezi mbalimbali? Mikusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova imethibitisha kwamba watu wa tamaduni tofauti-tofauti wanaweza kufanyiza urafiki wa kweli na wenye kudumu wanapomwabudu Mungu pamoja.

Kudumisha Urafiki Ukiwa Umeshikamana

Kwa kuhuzunisha, wale waonwao kuwa marafiki nyakati fulani husababishiana maumivu. Porojo zenye kudhuru, kuvunjwa kwa utumainifu, ukosefu wa uthamini—haya ni baadhi ya mambo ambayo ni yenye kuumiza sana yanapotokana na mtu ambaye ulimwona kuwa rafiki wa kweli. Ni nini kiwezacho kufanywa katika hali kama hizo?

Weka kielelezo chema. Fanya kila jambo uwezalo ili kuepuka kusababisha maumivu yasiyotakikana. Katika mahali fulani ni jambo la kawaida kwa marafiki kufanyiana mzaha juu ya makosa ya kila mmoja. Lakini kutenda kwa ukali, au kwa ujanja hakutavuta karibu marafiki, hata kama eti “wanafurahia.”—Mithali 26:18, 19.

Fanya kazi kwa bidii ili kudumisha urafiki. Kutoelewana huzuka nyakati fulani wakati marafiki wanapotarajia mengi zaidi kutoka kwa kila mmoja. Yaelekea rafiki aliye mgonjwa au mwenye shughuli nyingi mno kwa sababu ya tatizo zito hataweza kuonyesha uchangamfu mwingi kama kawaida. Basi, katika wakati kama huo jaribu kuwa mwenye kufahamu na mwenye kutegemeza.

Tatueni matatizo haraka na kwa fadhili. Ikiwezekana fanyeni hivyo faraghani. (Mathayo 5:23, 24; 18:15) Hakikisha rafiki yako ajua kwamba unataka kudumisha uhusiano mzuri. Marafiki wanyoofu husameheana. (Wakolosai 3:13) Je, utakuwa rafiki wa namna hiyo—mmoja ambaye anaambatana kwa ukaribu kuliko ndugu?

Kusoma na kufikiri juu ya urafiki ni mwanzo tu. Ikiwa tuna upweke, na tuchukue hatua ifaayo, na hatutakuwa wenye upweke kwa muda mrefu. Tukijitahidi sana, tutafanya marafiki wa kweli. Tutafanyiza kifungo cha kipekee na baadhi yao. Lakini hakuna mtu awezaye kuchukua mahali pa Mungu, Rafiki mkuu kupita wote. Ni Yehova pekee awezaye kujua, kufahamu, na kututegemeza kikamili. (Zaburi 139:1-4, 23, 24) Isitoshe, Neno lake hutoa tumaini zuri ajabu la wakati ujao—ulimwengu mpya ambao itawezekana kuwa na marafiki wa kweli milele.—2 Petro 3:13.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Daudi na Yonathani walifurahia urafiki wa kweli, nasi pia twaweza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki