Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 8/22 kur. 22-27
  • Msiba wa Ghafula wa Japani—Jinsi Watu Walivyoukabili

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Msiba wa Ghafula wa Japani—Jinsi Watu Walivyoukabili
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kipindi cha Maafa
  • Kuponea Chupuchupu na Misiba
  • Hali Yenye Kutamausha
  • Mashahidi Waitikia Mara Moja
  • Programu ya Kutoa Msaada Yaanzishwa
  • Zaidi ya Msaada wa Kimwili
  • Kupangwa ili Kujenga Upya
  • Ishara ya Nyakati
  • Tetemeko la Haiti—Imani na Upendo Zadhihirika
    Amkeni!—2010
  • Matetemeko Makubwa Zaidi Yanatazamiwa
    Amkeni!—2010
  • Kuandaa Kitulizo Katikati ya Magofu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • “Upendo Wao Ulitugusa Moyo Sana”
    Amkeni!—2017
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 8/22 kur. 22-27

Msiba wa Ghafula wa Japani—Jinsi Watu Walivyoukabili

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA JAPANI

WAKATI mmoja Kobe, Japani, lilikuwa jiji la bandari lenye kunawiri lenye wakazi 1,500,000. Lakini kwa sekunde 20, tetemeko la dunia lenye kipimo cha 7.2 katika kipimo cha Richter liliharibu sehemu kubwa yalo kuwa magofu. Makumi ya maelfu ya nyumba na majengo yalibomolewa kabisa au kuharibiwa, na zaidi ya watu 300,000 waliachwa bila makao.

Msiba ulikumba Januari 17, 1995, mwaka mmoja kamili baada ya tetemeko la dunia lililoharibu Northridge, California, Marekani, na kuua watu 61. Tetemeko la Kobe lilitoa yapata mara mbili nishati za mtikisiko mwingi kuliko hilo lilivyotoa. Idadi ya waliokufa zaidi ya 5,500 ililifanya hilo kuwa tetemeko baya zaidi kupita yote katika Japani tangu 1923, wakati watu wapatao 143,000 waliuawa katika tetemeko kubwa ambalo lilikumba Tokyo na Yokohoma.

Kipindi cha Maafa

Mnamo saa 11:46 ya alfajiri hiyo yenye kuhuzunisha, Ryuji alikuwa akichuuza magazeti ya habari katika kitovu cha Jiji la Kobe. Bado kulikuwa na giza. Ghafula kulikuwa na kelele kama ya gari-moshi lililokuwa likipita kwenye reli ya juu. Barabara na majengo zilivingirika kama vile mawimbi ya bahari. Kisha stima zote zikazimika.

Barabara kuu za juu ziliporomoka, zikiangusha magari kwenye barabara zilizoko chini. Reli zilikunjwa kama mkeka, na magari-moshi yaliondoshwa kwenye reli. Majengo ya zamani ya mbao yaliporomoka, na makao ya orofa mbili ghafula yalionekana kama jengo la orofa moja. Wengi wa wakazi wa Kobe walitikiswa kutoka usingizini.

Mara mioto ikawaka, na safu nzima za majengo zilichomeka. Wazima-moto walitazama bila la kufanya, kwa sababu tetemeko lilikuwa limeharibu mfumo wa ugavi wa maji. Kwa muda mfupi, ile ngano ya kwamba majengo ni yenye kukinza tetemeko la dunia ilikuwa imevunjiliwa mbali.

Kuponea Chupuchupu na Misiba

Katika eneo lililoathiriwa na tetemeko moja kwa moja, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 3,765 walioshirikiana na makutaniko 76. Kufikia asubuhi iliyofuata tetemeko, ilikuwa imebainika kwamba Mashahidi 13 na washirika ambao hawajabatizwa 2 walikuwa wameuawa. (Mhubiri 9:11) Wakati huo idadi ya waliokufa iliyotolewa na polisi ilikuwa 1,812, lakini mnamo juma moja ilipanda hadi zaidi ya 5,000. Kwa sababu Mashahidi walikuwa wamewatafuta kwa haraka wale wanaoshirikiana nao katika makutaniko yao, idadi yao ya waliokufa ilibaki vilevile.

Mume wa Misao alikuwa ameondoka mapema kwenda kazini. “Yapata saa moja baadaye, nyumba ilitikisika,” akasema Misao. “Vigae vya paa vilianguka kunizunguka. Kigae kikubwa cha kati cha paa kiliangukia mto mahali kichwa cha mume wangu kilikuwa kimelala saa moja tu kabla ya hapo.” Vitoto vya meza na rafu ya vitabu viliangukiana juu tu ya Misao. Hili lilimwokoa kutokana na kufunikwa chini ya vigae vya paa.

Paka aliyekuwa akitoa mlio alimwamsha Hiromasa, mvulana wa shule mwenye umri wa miaka 16. Alipokuwa akimfungulia huyo paka atoke nje, tetemeko lilikumba. Aliporudi alipata mama yake chini ya televisheni na rafu ya vitabu. Alipata kitulizo kilichoje kumpata akiwa hai! Hiromasa aliomba tochi kutoka kwa majirani na kumwokoa mamaye. Maelfu wana masimulizi ya kuponea chupuchupu. Lakini Mashahidi wengine walipatwa na misiba yenye kuhuzunisha.

Hiroshi na Kazu Kaneko walifunikwa chini ya maporomoko ya makao yao. Washiriki wa kutaniko la Kikristo walikimbia huko ili kuwaokoa. Ilikuwa mpaka saa 4:00 asubuhi kwamba Hiroshi aliokolewa na kupelekwa hospitalini. Lakini Kazu alikuwa amekufa walipomwondoa baadaye.

Miyoko Teshima, mwenye umri wa miaka 24 na aliyebatizwa kwa yapata miaka miwili tu, alikuwa na mradi wa utumishi wa wakati wote. Asubuhi ya hilo tetemeko, msichana huyo alikuwa amelala katika jengo la orofa ya kwanza wakati orofa ya pili ilipoporomoka. Miyoko alifunikwa chini ya paa na mbao za dari. Wazazi wake na majirani walijaribu kuondoa maporomoko lakini hawakuweza. Mama yake, ambaye ni mwanafunzi wa Biblia, aliwasiliana na Mashahidi wa Yehova, ambao walikuja kusaidia.

Miyoko alipoondolewa chini ya maporomoko baada ya karibu saa saba, bado alikuwa hai. Wazee watatu Wakristo walibadilishana na daktari na muuguzi katika taratibu ya kukanda moyo ili kurejesha upumuaji wa kawaida, lakini Miyoko alikufa. Baba yake, ambaye alipinga imani yake, alisukumwa na hisia na jitihada za Mashahidi kumwokoa bintiye, naye alikubali ombi la bintiye la hapo awali la kuzikwa na Mashahidi.

Takao Jinguji, mzee mmoja Mkristo, aliishi katika orofa ya kwanza ya jengo fulani la zamani pamoja na mkeye na binti yao. “Wakati mtikisiko ulipokumba,” yeye alisema, “sakafu iliyo juu ilituporomokea, nami nilinasika chini ya rafu ya vitabu. Hatimaye, niliweza kujinasua na kuanza kujaribu kutoka nje ya hilo jengo. Ghafula nilisikia sauti. Alikuwa Shahidi jirani, aliyekuwa amekuja kututafuta.”

Hatimaye Takao alipofaulu kutoka nje, aliona moto kutoka kwa majengo yaliyozunguka ukienea kuelekea makao yake. Hivyo alitambaa kurudi kwenye maporomoko na kujaribu kumwondoa mke wake bila kufanikiwa. Lakini ilikuwa kuchelewa mno. Eiko, mke wake wa miaka 26, na binti yake Naomi walikuwa wameuawa. Licha ya hili, alianza kusaidia washiriki wengine wa kutaniko lake. “Hakuna lolote ningeweza kufanyia familia yangu,” akasema baadaye, “hivyo niligeuza uangalifu wangu ili kusaidia wengine. Nilipata kitulizo kupata kwamba wote katika kutaniko letu walikuwa salama.”

Hali Yenye Kutamausha

Maelfu walipata makao katika shule mbalimbali na majengo ya umma. Wakihofu tetemeko la baadaye, wengine walipiga kambi nje ama walilala katika magari yao. Reli na njia kuu ziliharibiwa, na barabara zilizokuwapo kwa ajili ya kusafirisha ugavi wa msaada zilijawa na maelfu ya magari. Kwa siku kadhaa wengi walikuwa na chakula kichache ama hawakuwa nacho. Lakini kwa kupendeza, hakukuwa na ripoti za uporaji-maduka, na wengi walishiriki kile chakula kichache walichokuwa nacho.

“Hii yafanana na baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili,” akasema mwanamume mmoja mzee-mzee akiwa amejifunga blanketi, machozi yakimtiririka mashavuni. Waziri mkuu wa Japani, Tomiichi Murayama, alikagua uharibifu na kuripoti hivi: “Sijapata kuona jambo kama hili. Hili lavuka mawazio yoyote ya binadamu.”

Mashahidi Waitikia Mara Moja

Keiji Koshiro, mzee Mkristo, alipotembelea mjini Kobe asubuhi ya tetemeko na kuona uharibifu mbaya sana, alirudi nyumbani na kupanga kutaniko la mahali pale lipike chakula kwa ajili ya Wakristo wenzao waliokuwa wameathiriwa vibaya sana. Kufikia jioni, alikuwa akipeleka vyakula na vinywaji kwa makutaniko yaliyoko katikati ya Kobe akitumia gari. Asubuhi iliyofuata, vyakula na maji zaidi viliandaliwa. Kwa kuwa msongamano wa magari ulikuwako, Mashahidi walipanga msafara wa pikipiki 16 kupeleka ugavi wa msaada.

Wengine wengi pia mara moja walichukua hatua ya kwanza kuwatafuta na kuwasaidia ndugu zao Wakristo. Tomoyuki Tsuboi na mzee mwingine Mkristo waliondoka kwa pikipiki kuelekea Ashiya, jiji lifuatalo Kobe ambalo lilikuwa pia limeharibiwa vibaya. Kwenye Jumba la Ufalme mjini Ashiya, walipata kwamba mwangalizi asafiriye, Yoshinobu Kumada, alikuwa tayari ameanzisha kituo cha kutolea msaada huko.

Uwasiliano wa simu ulifanywa ili kujulisha akina ndugu uhitaji, na upesi ugavi ulikuwa ukikusanywa. Muda si muda magari tisa yaliyobeba mablanketi, chakula, na maji yalikuwa njiani kuelekea Ashiya. Ugavi huu ulipelekwa kwenye Majumba ya Ufalme mawili jijini, ambapo kati ya watu 40 na 50 walikuwa wamekimbilia. Wengine walipata makao katika nyumba za waamini wenzao. Siku iliyofuata Mashahidi katika eneo lililo karibu walitayarisha milo kwa ajili ya watu 800. Chakula kilichoandaliwa kwa wale wenye uhitaji kilikuwa kingi, hivyo Mashahidi walikishiriki pamoja na majirani waliokuwa na uhitaji.

Kotekote katika eneo lililoathiriwa na tetemeko, Mashahidi wa Yehova mara moja walikuja kuwasaidia waamini wenzao. Jambo hili lilivuta watazamaji wengi. Juma moja baada ya tetemeko, rubani wa helikoputa alimfikia Shahidi mmoja katika Yokohama na kusema hivi: “Nilienda kwenye eneo la msiba siku ya tetemeko na kukaa huko kwa juma moja. Mashahidi wa Yehova walikuwa ndio pekee yao waliokimbilia eneo hilo. Nilivutiwa sana.”

Programu ya Kutoa Msaada Yaanzishwa

Mara moja ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, iliyoko Ebina, Japani, ilipeleka wawakilishi wanne Kobe ili kupanga kazi ya kutoa msaada. “Mara moja tulikubaliana kutafuta Majumba ya Ufalme ambayo hayakuharibiwa na kupeleka ugavi wa msaada humo,” mwakilishi mmoja akaripoti. “Majumba sita yalipatikana, na kwa muda upatao saa tano haya yalijaa pomoni. Ugavi mwingine ulipelekwa kwenye Majumba ya Kusanyiko mawili makubwa ya Mashahidi wa Yehova yaliyo karibu.”

Akaunti ya benki kwa ajili ya hazina ya msaada ilifunguliwa, na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kotekote Japani yaliarifiwa. Kwa kipindi cha siku tatu za kazi, dola milioni moja zilitolewa zikiwa upaji. Fedha hizo ziligawanywa haraka kwa ajili ya utumizi wa wale wenye uhitaji.

Makutaniko yaliambiwa yangeweza kuchukua ugavi uliohitajika kwenye vituo vilivyowekwa vya kutolea msaada. Wazee katika kila kutaniko walipanga ugawaji wa ugavi kwa washiriki wenye uhitaji wa makutaniko yao. Washiriki wa familia za Mashahidi wasioamini hawakupuuzwa. Baba ya mzee Mkristo mmoja katika eneo lililoathiriwa—ambaye hapo awali hakupendelea Mashahidi wa Yehova—alisikika akijisifu kwa simu kwa mtu fulani wa ukoo hivi: “Watu kutoka dini ya mwanangu huja na kutusaidia!”

Zaidi ya Msaada wa Kimwili

Mara, mikutano ya Kikristo ilipangwa tena. Kutaniko moja lilikusanyika kwenye bustani kwa ajili ya mikutano hiyo Jumanne, siku ya tetemeko. Kufikia Jumapili makutaniko mengi katika eneo lililoathiriwa yalikuwa na Funzo la Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida, ama katika vikundi vidogo ama katika Majumba ya Ufalme ambayo hayakuharibiwa kabisa. Kwa kufaa, Mnara wa Mlinzi wa Desemba 1, 1994, uliosomwa juma hilo, ulizungumzia pendeleo la kutumia rasilimali “kusaidia watu waliopatwa na misiba ya kiasili.” Mwanamke mmoja kwenye mkutano alisema hivi: “Kwa mara ya kwanza, sisi ni wapokeaji wa misaada. Nimejawa na shukrani ambazo siwezi kueleza kwa maneno. Mara tukirudia hali ya kawaida, nitatimiza fungu langu la kuwa mpaji.”

Wawakilishi kutoka ofisi ya tawi walitumia pikipiki kutembelea eneo lililofikwa mno. “Lilikuwa ono lenye kugusa moyo kuona akina ndugu wakiwa na machozi,” mmoja wao akaripoti. “Walikuwa wakituambia, ‘Hatulii kwa sababu tumepoteza kila kitu lakini kwa sababu mioyo yetu imeguswa nanyi akina ndugu mliokuja kututembelea kutoka mbali Ebina.’”

Mnamo muda wa saa 24 za tetemeko, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, Marekani, pamoja na ofisi za tawi katika sehemu zote za ulimwengu zilipeleka jumbe zilizoonyesha hangaiko. Jumbe nyingi kama hizo zilipokewa katika siku zilizofuata. Faksi kutoka Kutaniko la Wŏnju West, Jamhuri ya Korea, ambalo lilikuwa limepoteza washiriki 15 katika mlipuko wa bomu la moto miaka miwili mapema, hasa ilikuwa yenye kugusa hisia.a Ilimalizia hivi: “Maumivu ya ndugu zetu katika Kobe ni maumivu na uchungu wetu. Tafadhali mkumbuke, kama vile tulivyopata kuona, hamko peke yenu mnapokuwa katika dhiki. Ndugu wapendwa, msife moyo!”

Wawakilishi wa tawi walifanya mipango kwa ajili ya utegemezo wa kiroho wenye kuendelea. Kwa kielelezo, waangalizi wasafirio zaidi walipewa mgawo wa muda katika eneo la Kobe ili kuandaa kitia-moyo. Na wazee Wakristo kutoka sehemu nyingine za Japani pia walialikwa kutembelea Kobe kwa juma moja ama kwa majuma kadhaa ili kuandaa utegemezo wa kiroho na kihisia-moyo kwa wale waliokuwa wakiteseka.

Kukiwa na utunzi na kitia-moyo kama hicho kutoka kwa waamini wenzao ulimwenguni pote, Mashahidi katika eneo lililoathiriwa walidumisha mtazamo chanya na wenye uthamini. Baada ya kuhudhuria mkutano wa kwanza baada ya tetemeko, Shahidi mmoja alisema hivi: “Tulikuwa wenye hangaiko kidogo mpaka jana, kwa kuwa hatukuwa na mahali pa kwenda. Lakini kuja hapa na kusikia mpango wenye fadhili ambao umefanywa kwa faida yetu, kutia ndani kufuliwa nguo, maandalizi ya kuoga, na utumizi wa Jumba la Kusanyiko kama makao ya muda, kwa kweli umetuliza mahangaiko yetu. Kwa kweli hili ni tengenezo la Mungu!”

Kwa kweli, kukazia utajiri wa kiroho kumesaidia hao Mashahidi kukabili hali. Mwanamke mmoja katika miaka yake ya mapema ya 20 alisema hivi: “Mama yangu alinifunza tangu wakati nilikuwa na miaka mitatu kuweka tumaini langu katika Yehova. Mazoezi yake na yale yapokewayo kupitia kutaniko la Kikristo yamenisaidia kustahimili ono hili lenye kuhuzunisha.”

Kupangwa ili Kujenga Upya

Karibu nyumba 350 za Mashahidi zilibomolewa ama kuharibiwa; mia moja kati ya hizi zilikuwa za kibinafsi. Zaidi ya nyumba 630 zaidi za Mashahidi zilihitaji marekebisho madogo. Pia, Majumba ya Ufalme kumi yaliharibiwa hivi kwamba hayangeweza kutumiwa.

Haraka, mipango ilifanywa ili kujenga upya Majumba ya Ufalme kwa makutaniko ambayo yalipoteza yao. Na zile Halmashauri za Ujenzi wa Kimkoa 11 katika Japani kila moja ilipanga vikoa vya watu 21 kurekebisha nyumba zilizoharibiwa za Mashahidi.

Ishara ya Nyakati

Matetemeko ya dunia yanatukia kwa ukawaida mkubwa zaidi. “Mwaka jana pekee,” likaonelea gazeti Maclean’s, “kulikuwa na matetemeko kadhaa [katika Japani] makubwa kuliko hilo la Kobe.” Moja lilikuwa kuu likiwa na ukubwa wa 8.1, lakini lilikumba eneo lenye idadi ndogo ya watu katika kaskazini.

Ongezeko la matetemeko ya dunia halishangazi Mashahidi wa Yehova. Kwani, baada tu ya tetemeko kutikisa nyumba yao katika Kobe, Atsushi mwenye umri wa miaka mitano alitembea akizunguka akisema hivi: “Kutakuwa na matetemeko ya nchi mahali mahali”! (Marko 13:8) Alikuwa amejifunza unabii huu kutokana na mama yake. Yesu Kristo alitia ndani matetemeko ya dunia yakiwa sehemu ya “ile ishara ya kuwapo [kwake] na umalizio wa mfumo wa mambo.” (NW) Sehemu nyingine za ishara hiyo yatia ndani vita, upungufu wa chakula, magonjwa ya kipuku, na kupoa kwa upendo wa wengi.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5, NW.

Tetemeko la Kobe ni uthibitisho zaidi tu wa kwamba tunaishi katika siku za mwisho wa ulimwengu huu. Kwa furaha, hilo ni sehemu ya ishara ya Yesu inayoendelea kutimizwa sasa ambayo huthibitisha kwamba karibuni ulimwengu huu utabadilishwa na ule ulio mwadilifu.—1 Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Amkeni! la Aprili 22, 1993, kurasa 25-27.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Takao Jinguji alipoteza familia yake katika magofu haya

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kituo cha gari-moshi kilichoharibiwa

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Barabara ya juu iliyoporomoka

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashahidi mara moja walianzisha programu ya kutoa msaada kwa ajili ya majeruhi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki