Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 12/1 kur. 4-7
  • Kuandaa Kitulizo Katikati ya Magofu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuandaa Kitulizo Katikati ya Magofu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Accra—“Siku ya Noa Ndogo”
  • San Angelo—“Ilisikika Kana Kwamba Ulimwengu Ulikuwa Ukiisha”
  • Kobe—“Uharibifu wa Mbao, Lipu, na Miili ya Binadamu”
  • Kitulizo cha Kudumu Karibuni!
  • Msiba wa Ghafula wa Japani—Jinsi Watu Walivyoukabili
    Amkeni!—1995
  • Kukua Pamoja Katika Upendo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kazi ya Kutoa Msaada
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Mambo Ambayo Kimbunga Andrew Hakingeweza Kuharibu
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 12/1 kur. 4-7

Kuandaa Kitulizo Katikati ya Magofu

JITIHADA za mwanadamu za kuandaa kitulizo baada ya msiba kwa hakika zastahili sifa. Programu nyingi za kitulizo zimesaidia kujenga nyumba, kuunganisha tena familia, na zaidi ya yote, kuokoa uhai.

Msiba upigapo, Mashahidi wa Yehova hutumia—nao wanathamini—maandalizi yoyote yanayofanywa kupitia programu za kilimwengu za kutuliza. Wakati huohuo, wana wajibu wa Kimaandiko wa “[kuwatendea] mema . . . hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10) Ndiyo, Mashahidi huhisi kana kwamba wana uhusiano wa kijamaa; wanaonana kuwa “familia.” Hiyo ndiyo sababu wanaitana “ndugu” na “dada.”—Linganisha Marko 3:31-35; Filemoni 1, 2.

Kwa hiyo, msiba unapoathiri ujirani, wazee miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wanafanya jitihada zenye bidii ili kuhakikisha mahali alipo na mahitaji ya kila mshiriki wa kutaniko na kufanya mipango ya kutoa msaada unaohitajiwa. Fikiria jinsi hilo lilivyokuwa kweli katika Accra, Ghana; San Angelo, Marekani; na Kobe, Japani.

Accra—“Siku ya Noa Ndogo”

Mvua ilianza kunyesha saa tano hivi usiku, na ilimwagika bila kukoma kwa muda wa saa kadhaa. “Ilikuwa ikinyesha kwa nguvu sana hivi kwamba familia yangu haikuweza kulala,” asema John Twumasi, mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika Accra. Gazeti la habari Daily Graphic liliiita “Siku ya Noa ndogo.” “Tulijaribu kupeleka baadhi ya vitu vya thamani kwenye orofa ya juu,” John aendelea kusema, “lakini tulipoufungua mlango wa kwenda kwenye ngazi, maji ya furiko yakaingia ndani.”

Wenye mamlaka walitoa onyo kwamba watu wahame, lakini wengi walisitasita, wakihofu kwamba nyumba iliyoachwa bila watu—hata ikiwa imejawa na maji—ingeweza kuvutia waporaji. Watu fulani hawakuweza kuondoka hata ikiwa walitaka kufanya hivyo. “Mama yangu nami hatukuweza kufungua mlango,” asema msichana aitwaye Paulina. “Maji yaliendelea kupanda, kwa hiyo tulisimama juu ya mapipa ya mbao na kushikilia boriti la paa. Hatimaye, karibu saa 11:00 alfajiri, jirani zetu walituokoa.”

Upesi ilipowezekana, Mashahidi wa Yehova walianza kazi. Dada Mkristo anayeitwa Beatrice aeleza hivi: “Wazee katika kutaniko walikuwa wakitutafuta, nao walitukuta katika nyumba ya Shahidi mwenzetu, ambapo tulikuwa tumekimbilia. Siku tatu tu baada ya furiko, wazee na washiriki wa kutaniko vijana walikuja kutusaidia na kuzoa matope kutoka ndani na nje ya nyumba yetu. Watch Tower Society ilitoa sabuni, viuaviini, rangi, magodoro, mablanketi, nguo, na mavazi kwa ajili ya watoto. Akina ndugu walitutumia chakula kwa siku kadhaa. Nilichochewa sana!”

John Twumasi, aliyenukuliwa mapema, aripoti hivi: “Niliwaambia wale wapangaji wengine kwamba Sosaiti yetu ilikuwa imetutumia sabuni na viuaviini—vya kutosha kuosha jengo zima. Wapangaji wapatao 40 walisaidia kuosha. Niliwapa jirani zangu baadhi ya hizo sabuni, kutia na mtu mmoja ambaye ni kasisi katika kanisa la mahali hapo. Wafanyakazi wenzangu walifikiri kwa kukosea kwamba Mashahidi wa Yehova huonyesha upendo kwa watu wao tu.”

Ndugu na dada Wakristo walithamini sana ule msaada wenye upendo waliopewa. Ndugu Twumasi amalizia hivi: “Ingawa vitu nilivyopoteza katika furiko vilikuwa vya thamani kubwa zaidi kifedha kuliko vifaa vya kutuliza, familia yangu nami twahisi kwamba kwa sababu ya uandalizi huo wenye kugusa moyo kutoka Sosaiti, tumepata vingi zaidi kuliko vile ambavyo tulipoteza.”

San Angelo—“Ilisikika Kana Kwamba Ulimwengu Ulikuwa Ukiisha”

Pepo za chamchela zilizoharibu San Angelo Mei 28, 1995, ziling’oa miti, zikavunja vigingi vya umeme, na kuangusha waya za umeme kuvuka barabara. Pepo zilivuma kufikia mwendo wa kilometa 160 kwa saa, zikiharibu mali za umma. Nyumba zaidi ya 20,000 zilikosa umeme. Kisha mvua ya mawe ikaja. Huduma ya Halihewa ya Kitaifa iliripoti “mawe-mvua yenye kipenyo cha sentimeta nne,” kisha “mawe-mvua yenye kipenyo cha sentimeta kumi,” na hatimaye “mawe-mvua yenye kipenyo cha sentimeta kumi na mbili.” Sauti ya mawe-mvua yaliyokuwa yakianguka ilikuwa yenye kushinda masikio. Mkazi mmoja alisema hivi: “Ilisikika kana kwamba ulimwengu ulikuwa ukiisha.”

Utulivu wenye kuogofya ulifuata hiyo dhoruba. Watu walitoka polepole katika nyumba zao zilizoharibiwa ili wachunguze madhara. Miti iliyokuwa ingali ikisimama ilikuwa imeponolewa. Nyumba zilizokuwa zingali zikisimama zilionekana kana kwamba zilikuwa zimechunuliwa. Katika maeneo fulani mawe-mvua yalifunika ardhi chungu kwa chungu kufikia kina cha meta moja. Maelfu ya madirisha ya nyumba na magari yalikuwa yamevunjwa katika hiyo dhoruba, hivi kwamba sasa kulikuwa na vipande vya vioo vilivyokuwa vikimetameta pamoja na mawe-mvua yaliyofunika ardhi. “Nilipofika nyumbani,” mwanamke mmoja asema, “Niliketi tu ndani ya gari langu katika njia ya gari nikalia. Madhara yalikuwa mabaya sana, yalinishinda tu.”

Programu za kutuliza na hospitali ziliandaa msaada wa kifedha haraka, vifaa vya majenzi, matibabu, na mashauri. Kwa kustahili pongezi, watu wengi ambao wao wenyewe walikuwa wahasiriwa wa hiyo dhoruba walifanya yale ambayo waliweza ili kuwasaidia wengine.

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalichukua hatua vilevile. Aubrey Conner, mzee katika San Angelo, aripoti hivi: “Mara tu hiyo dhoruba ilipoisha, tulikuwa tukipiga simu tukijaribu kujua hali za ndugu na dada wote. Tulisaidiana wenyewe na jirani zetu wasio Mashahidi kuweka mbao kwenye madirisha, kuweka plastiki kwenye paa, na kuzifanya nyumba zikinge halihewa kwa kadiri ambavyo tungeweza. Kisha tukafanyiza faili juu ya kila mtu kutanikoni ambaye nyumba yake iliathiriwa. Karibu nyumba mia moja zilihitaji kurekebishwa, na vifaa vilivyoandaliwa na mashirika ya kutuliza havikutosha. Kwa hiyo tulinunua vifaa zaidi na kuwa tayari kwa ajili ya kazi. Kwa ujumla, Mashahidi 1,000 walijitolea kusaidia, karibu 250 kila mwisho-juma. Walikuja kutoka umbali unaofikia kilometa 740. Wote walifanya kazi bila kuchoka, mara nyingi katika halihewa yenye joto la digrii 40 Selsiasi. Hata dada mwenye umri wa miaka 70 alifanya kazi nasi miisho-juma yote isipokuwa mmoja, na huo ulikuwa wakati nyumba yake mwenyewe ilikuwa ikirekebishwa. Kwenye mwisho-juma huo alikuwa kwenye paa yake mwenyewe akisaidia kurekebisha!

“Mara nyingi tulisikia maneno kutoka kwa watazamaji kama, ‘Je, isingekuwa vema ikiwa dini nyingine zingewafanyia washiriki wao hili?’ Jirani zetu walivutiwa kuona kikundi cha wajitoleaji 10 hadi 12 (kutia na dada) kikifika mapema asubuhi ya Ijumaa kwenye nyumba ya Shahidi mwenzetu, wakiwa tayari kurekebisha au hata kuijenga upya paa yote bila malipo. Katika visa vingi kazi ilimalizwa katika mwisho-juma mmoja. Nyakati nyingine, wajenzi wasio Mashahidi wangekuwa wameendelea sana katika kurekebisha paa fulani wakati kikundi chetu kilipofika kwenye nyumba ya jirani. Tungeondolea mbali paa ya zamani na kujenga upya paa yetu na kuondoa uchafu kwenye uwanja kabla hawajamaliza paa yao. Nyakati nyingine walisimamisha kazi yao ili watuangalie tu!”

Ndugu Conner amalizia hivi: “Sote tutakosa mambo yaliyoonwa tuliyofurahia pamoja. Tumekuja kujuana kutoka upande tofauti kwa kuonyesha na kuonyeshwa upendo wa kidugu kuliko hapo mbele. Twahisi kwamba hii ni sampuli tu ya jinsi itakavyokuwa katika ulimwengu mpya wa Mungu, ndugu na dada wakisaidiana kwa sababu wanataka kufanya hivyo kikweli.”—2 Petro 3:13.

Kobe—“Uharibifu wa Mbao, Lipu, na Miili ya Binadamu”

Wakazi wa Kobe walipaswa kuwa tayari. Kwa kweli, kila Septemba 1 wao huadhimisha Siku ya Uzuiaji wa Msiba. Watoto wa shule hujizoeza mazoezi ya matetemeko ya dunia, wanajeshi hufanya mazoezi ya kazi za uokoaji kwa kutumia helikopta, na idara za wazima-moto huleta machine zao za matetemeko bandia ya dunia, ambazo katika hizo wajitoleaji hujizoeza stadi zao za kusalimika ndani ya sanduku linalotoshana na chumba ambalo hutetemeka na kutikisika kama tu tetemeko halisi la dunia. Lakini wakati tetemeko halisi la dunia lilipotokea katika Januari 17, 1995, matayarisho yote yalionekana kuwa yasiyofaa kitu. Makumi ya maelfu ya paa zilianguka—jambo ambalo halikutukia kamwe katika mashine za matetemeko bandia ya dunia. Magari-moshi yalipinduka; visehemu vya barabara kuu viliatuka; mabomba ya maji na gesi yalipasuka; nyumba zilianguka kana kwamba zilifanyizwa kwa bango. Gazeti Time lilifafanua mandhari hiyo kuwa “uharibifu wa mbao, lipu, na miili ya binadamu.”

Kisha ikaja mioto. Majengo yaliwaka huku wazima-moto waliotamauka walikuwa wamekwama katika magari yaliyosongamana kwa kilometa nyingi. Wale walioifikia hiyo mioto mara nyingi walikuta kwamba hakuna maji yaliyoweza kupatikana kutoka katika mfumo wa maji wa jiji uliokuwa umeharibika. “Siku ya kwanza ilikuwa yenye hofu tupu ya ghafula.” alisema ofisa mmoja. “Sijapata kamwe kuhisi nikiwa bila nguvu hivyo maishani mwangu, nikijua kwamba kulikuwa na watu wengi sana waliokuwa wamezikwa katika nyumba hizo zilizokuwa zikichomeka. Na nikijua kwamba singeweza kufanya lolote kuhusu hilo.”

Kwa ujumla, watu 5,000 hivi waliuawa, na majengo yapatayo 50,000 yalikuwa magofu. Kobe ulikuwa na thuluthi moja tu ya chakula ulichohitaji. Ili kupata maji baadhi ya watu waligeukia kuzoa maji machafu chini ya mabomba ya maji yaliyopasuka. Wengi wa wale wasio na nyumba wakakimbilia vibanda, ambavyo baadhi yavyo vilipima chakula, vikimpa kila mtu chakula kidogo sana kama sehemu ndogo ya mchele kwa siku. Upesi kutoridhika kukaenea. “Wenye mamlaka hawajafanya chochote,” akalalamika mwanamume mmoja. “Tukiendelea kuwategemea tutakufa njaa.”

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika Kobe na maeneo ya karibukaribu yakajitayarisha yenyewe mara moja. Rubani wa helikopta aliyejionea kazi yao alisema hivi: “Nilienda kwenye eneo la msiba siku ya tetemeko nikakaa juma moja huko. Nilipofika kwenye kibanda kimoja, kila kitu kilikuwa shaghalabaghala. Hakuna kazi yoyote ya kitulizo iliyokuwa ikifanywa. Mashahidi wa Yehova peke yao ndio walioharakisha kufika mahali hapo, wakishughulikia jambo moja baada ya jingine.”

Kwa kweli, kulikuwa na kazi nyingi ya kufanya. Majumba ya Ufalme kumi yalionwa kuwa yasiyofaa kutumiwa, na Mashahidi zaidi ya 430 hawakuwa na nyumba. Nyumba nyingine 1,206 walimokuwa wakiishi zilihitaji kurekebishwa. Si hayo tu bali pia familia za Mashahidi 15 waliokuwa wamekufa katika huo msiba zilihitaji sana faraja.

Mashahidi 1,000 hivi kutoka nchini kote walitoa wakati wao ili wasaidie katika kazi ya kurekebisha. “Tulipokuwa tukifanya kazi katika nyumba za wanafunzi wa Biblia ambao bado hawakuwa wamebatizwa,” asema ndugu mmoja, “nyakati zote tuliulizwa, ‘tulipe kiasi gani kwa ajili ya yote haya?’ Tulipowaambia kwamba hiyo kazi ilikuwa ikitegemezwa na makutaniko, walitushukuru, wakisema hivi, ‘Yale ambayo tumejifunza ni halisi sasa!’”

Wengi walivutiwa na itikio la upesi na la kikamili la Mashahidi kwa huo msiba. “Nilivutiwa sana,” asema rubani aliyenukuliwa mapema. “Mwaitana ‘ndugu’ na ‘dada.’ Nimeona jinsi mnavyosaidiana; ninyi watu kwa kweli ni familia.”

Mashahidi wenyewe walijifunza masomo yenye thamani kutokana na hilo tetemeko. Dada mmoja alikiri hivi: “Sikuzote nimehisi kuwa kadiri tengenezo linavyokuwa kubwa, ndivyo inavyokuwa vigumu kuonyesha hangaiko la kibinafsi.” Lakini utunzaji mwororo aliopokea ulibadili mtazamo wake. “Sasa najua kwamba Yehova anatujali si tukiwa tengenezo tu bali pia tukiwa watu mmoja-mmoja.” Hata hivyo, kitulizo cha kudumu kutoka kwa misiba kiko mbele.

Kitulizo cha Kudumu Karibuni!

Mashahidi wa Yehova wanatazamia wakati ambapo uhai na maishilio ya binadamu hayatakatizwa tena na msiba. Katika ulimwengu mpya wa Mungu, mwanadamu atafundishwa kushirikiana na mazingira ya dunia. Wanadamu waondoapo mazoea yenye ubinafsi, hawataelekea kuathiriwa na hatari za kiasili.

Zaidi, Yehova Mungu—Muumba wa kani asilia—atahakikisha kwamba familia yake ya kibinadamu na uumbaji wa kidunia hautishwi tena kamwe na kani za asili. Kisha dunia itakuwa paradiso kwelikweli. (Isaya 65:17, 21, 23; Luka 23:43) Unabii wa Ufunuo 21:4 utatimizwa kwa utukufu: “Atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Beatrice Jones (kushoto) aonyesha jinsi yeye na wengine walivyoungana pamoja ili wapite katikati ya maji ya furiko

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kazi ya kitulizo baada ya pepo za chamchela

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki