Mambo Ambayo Kimbunga Andrew Hakingeweza Kuharibu
KUNA vimbunga, kisha kuna vimbunga vyenye uharibifu mkubwa sana.a Vingine huonwa tu kuwa upepo mwingi mkali, ukileta mvua kubwa na kung’oa miti. Kisha kulikuwa na Kimbunga kiitwacho Andrew katika Florida kusini (Agosti 24, 1992) na Louisiana (Agosti 26, 1992), Kimbunga Iniki katika Kauai, Hawaii (Septemba 12, 1992), na Tufani Omar katika Guam (Agosti 28, 1992).
Vimbunga hivyo vilileta uharibifu uliopata kuwa mabilioni ya dola. Watu wengi walikufa katika Florida. Maelfu ya familia ziliachwa bila makao. Wenye mashirika ya bima walikuwa wakizunguka-zunguka katika makao yaliyoharibiwa wakiwatafuta wenyewe na kuwaandikia hundi za malipo ya bima.
Ripoti moja kutoka Halmashauri ya Kutoa Misaada ya Fort Lauderdale ya Mashahidi wa Yehova ilisema kwamba makao 518 kati ya 1,033 ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo yangeweza kurekebishwa. Ikiwa uwiano huo ungetumiwa kwa ujumla, hilo lingemaanisha kwamba angalau asilimia 50 ya makao yote yaliyokumbwa na kimbunga Andrew yaliharibiwa. Baadaye, wale waliofanikiwa kuwa na makao yaliyofaa bado kukaliwa walikuwa wakijaribu kukausha fanicha yao na mapazia na kusafisha tope jeupe lililofanyizwa na dari lililoangushwa na furiko la mvua lililopita ndani ya paa zilizoharibiwa. Wengi waliona vigumu kutazama makao yao yaliyoharibiwa. Wale waliokumbwa vibaya zaidi ni wale waliokuwa wakiishi katika makao ya kukokotwa na gari au trela.
Kimbunga Andrew Hakikuacha Yeyote
Mmojawapo wenzi wawili waliooana waliopatwa na hayo walikuwa Leonard na Terry Kieffer. Walipoenda kuzuru tena makao yao ya kukokotwa na gari katika Jiji la Florida, iliwabidi wajitambulishe wenyewe kwenye kituo cha ukaguzi cha kijeshi ili kuingia eneo hilo. Kile walichoona kilikuwa makao ya kukokotwa na gari yaliyoonekana kana kwamba yamepigwa na mamia ya mabomu yenye nguvu nyingi—bila kuacha mashimo yoyote ya bomu. Miti iling’olewa. Mabati ya aluminiamu yaliyokunjika, yaliyokuwa kuta na paa za makao, yalizungushwa kwenye miti na kuning’inia kwenye matawi kana kwamba yalikuwa mapambo yasiyofaa ya kisherehe. Waya za umeme zilikuwa zimeanguka kila mahali, miti ya umeme ikikatwa kama vijiti vya kiberiti. Magari yalivingirishwa na kuvunjwa-vunjwa.
Bob van Dyk, ambaye makao yake mapya yalitangazwa kuwa yasiyofaa kukaliwa, alieleza hali ya makao yake hivi: “Dari liliporomoka, li-kivunja vitu vinavyoweza kuvunjika, likikunja vitu vinavyoweza kukunjwa na kutuogopesha sisi, tunaoweza kuogopa.”
Mali za kibinafsi, vitu vya kuchezea, nguo, picha, vitabu, vilitapakaa kila mahali vikitukumbusha kwa huzuni mtindo-maisha wa hapo mbeleni. Paka mweusi mpweke alizurura-zurura katika mabomoko hayo. Aliwakodolea macho akina Kieffer. Mijusi midogo walikimbia-kimbia juu ya ile iliyokuwa mali ya mtu ya thamani. Uvundo wa chakula chenye kuoza, kilichomwagika kutoka friji zilizovunjika, ulienea hewani. Katika kila upande kulikuwa na uharibifu mkubwa—wote ukisababishwa na upepo mwingi, wenye nguvu, ukiwa na mwendo wa zaidi ya kilometa 260 kwa saa.
Lilikuwa jambo la kutamausha kabisa kwa wenye nyumba na wakazi wazo. Baada ya miaka mingi ya kulea familia na kushiriki maisha zao katika makao yao ya pekee, wao walikuja baada ya dhoruba kupata kila kitu kimevunjwa-vunjwa na kutawanywa. Akina Kieffer walikuwa wameokoa baadhi ya mali yao katika ziara ya mapema, lakini walitamauka sana wasiweze kutafuta kwa uangalifu kuona kile kilichobakia katika rundo hilo. Hata hivyo, walithamini kwamba bado walikuwa hai na waliweza kumtumikia Mungu.
Kimbunga Andrew hakikuacha chochote. Sehemu za maduka, viwanda, mabohari—vyote vilipatwa na msiba huo wa asili. Stadi za ujenzi za mwanadamu duni hazikuzuia uharibifu huo.
Ubora na Ubovu wa Asili ya Kibinadamu
Msaada ulianza kuja Florida kutoka nchini kote huku mashirika ya msaada yalipojipanga. Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, lilitenda mara hiyo na kuteua halmashauri ya kutoa msaada ili ifanye kazi nje ya Jumba la Kusanyiko la Fort Lauderdale. Pia walitoa kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa, chakula, na vifaa vya dharura. Kama tokeo, Mashahidi walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kutenda baada ya hali hiyo na walianza kutafuta wenye kujitolea. Kwa kweli, wengi walikuja bila kuombwa waje.
Wafanyakazi Mashahidi waliwasili kutoka California, Carolina Kaskazini, Oregon, Jimbo la Washington, Pennsylvania, Missouri, na sehemu nyingi nyinginezo. Halmashauri ya Ujenzi wa Kimkoa ya Virginia ambayo kwa kawaida hujenga Majumba ya Ufalme ilituma kikundi cha Mashahidi 18 ili warekebishe paa. Iliwachukua muda wa saa 18 kusafiri kwa gari hadi huko. Wafanyakazi wa kutoa msaada walichukua likizo au wakaomba siku kadhaa na kusafiri hadi upande mwingine wa nchi, mamia na hata maelfu ya kilometa, ili kuwafikia Mashahidi wenzi waliokuwa katika taabu.
Kikundi kilichotoka eneo la Charleston katika Carolina Kusini kilitoa msaada wenye thamani kubwa. Wao walikuwa wamepata ujuzi kutokana na Kimbunga Hugo huko nyuma katika 1989. Walijua yale ambayo wangeweza kutazamia na upesi wakapanga ugavi wa misaada, kutia na jenereta za umeme na vifaa vya ujenzi. Katika muda wa majuma mawili wafanyakazi wa kujitolea walikuwa wamekausha makao yapatayo 800 na kurekebisha paa nyingi.
Wenzi wa ndoa wengi wasio Mashahidi na majirani walinufaika na msaada uliotolewa na timu za Mashahidi wenye kurekebisha. Ron Clarke kutoka Homestead Magharibi aliripoti: “Wenzi wasioamini wamevutiwa kwelikweli na yote hayo. Wamekuwa wenye machozi, wakivutiwa sana na yale ambayo Mashahidi wamewafanyia tayari.” Kuhusu mume asiyeamini wa Shahidi mmoja, yeye aliongeza: “Yeye [mume huyo] ana mchachao tu—Mashahidi wako huko sasa wakimwekea paa lake.”
Shahidi mwingine alisema juu ya majirani zake wasio Mashahidi ambao alienda kuwaangalia kila usiku. Walisema kwamba walikuwa sawasawa. Katika siku ya tano, mke alikosa kuvumilia akaanza kulia. “Sisi hatuna nepi zozote kwa ajili ya mtoto. Chakula cha mtoto karibu kimalizike. Hatuna chakula na maji ya kutosha.” Mume wake alihitaji lita 20 za petroli lakini hangeweza kuipata mahali popote. Siku hiyohiyo, Shahidi huyo alileta vitu vyote walivyohitaji kutoka kwa depo ya Jumba la Ufalme la kutoa msaada. Mke huyo alilia akiwa mwenye shukrani. Mume wake alitoa upaji kwa ajili ya kazi ya kutoa misaada.
Wazee na watumishi wa huduma wa kundi walikuwa na sehemu ya maana kwa kufanya kazi pamoja katika kupanga misaada kwenye Majumba ya Ufalme mbalimbali yaliyorekebishwa katika eneo la msiba. Walifanya kazi nyingi kuwatafuta Mashahidi wote na kujua mahitaji yao. Kwa kutofautisha, ofisa wa Jeshi la Angani alinukuliwa akisema kuhusu jitihada ya kuandaa misaada katika eneo jingine hivi: “Machifu wote wanataka tu wawe machifu, lakini hakuna yule anayetaka kufanya kazi chafu zisizopendeza.”
Misiba inaweza kutokeza sifa zilizo bora na zilizo mbovu za watu. Mfano mmoja wa sifa mbovu ni uporaji. Familia moja ya Mashahidi waliamua kwamba angalau wangeliweza kuokoa friji yao na mashine ya kufua nguo ili itumiwe kwenye kituo cha kuandaa misaada kwenye Jumba la Ufalme la huko. Walienda kwenye jumba hilo kutafuta kilori kidogo. Waliporudi, waporaji walikuwa wameiba vyombo hivyo viwili!
Mmoja aliyeshuhudia hali alisema: “Tuliposafiri kupitia barabara zisizo na watu, tuliona makao yenye ishara zenye kuonya waporaji. Baadhi ya ishara hizo zilisema, ‘Waporaji Lazima Wafe’ na, ‘Waporaji Watapigwa Risasi.’ Nyingine ilisema, ‘Waporaji wawili wamepigwa risasi. Mmoja wao amekufa.’ Maduka yalikuwa yameporwa.” Kulingana na sajenti mmoja wa Kikosi cha Anga cha 82, angalau mporaji mmoja alikuwa amekamatwa na kunyongwa na watu.
Wengi walikamatwa. Inaonekana kwamba katika msiba wowote wahalifu wako tayari kuvamia kama tai-wala-mizoga. Na hata wale waitwao eti watu wa kawaida hushiriki katika kupora. Dini, uungwana, na maadili, na maadili huonekana yakitoweka chini ya shawishi la kupata vitu bila kulipa.
Amkeni! liliambiwa kwamba mwanzoni askari-jeshi wachache hata walinyang’anywa bunduki zao zisizo na risasi na waporaji wenye silaha. Baadhi ya askari-jeshi walisikika wakisema kwamba waliona kituo cha kutoa misaada cha Jumba la Ufalme kuwa chemchemi katika jangwa “kwa sababu,” kama walivyosema, “ninyi watu hambebi bunduki.”
“Msikae Kitako”
Mashahidi wa Yehova wamejifunza nini kutokana na maono yao ya misiba ya asili? Kufanya upya utendaji wa kiroho upesi iwezekanavyo. Ed Rumsey, mwangalizi katika Homestead, aliliambia Amkeni! kwamba Majumba ya Ufalme mawili yaliyo mahali pamoja yalikuwa tayari kwa ajili ya mikutano siku ya Jumatano kufuatia kimbunga cha Jumatatu. Sehemu ya paa ilikuwa imeng’oka, dari lilikuwa limeporomoka, na maji yalikuwa yameingia. Wenye kujitolea walifanya kazi upesi ili kuweka yale Majumba ya Ufalme tayari kwa ajili ya mikutano na kuyatumia kuwa vituo vya uelekezi ambavyo kutoka kwavyo kazi ya kutoa misaada ingeelekezwa katika eneo lao lililokumbwa. Meko yalitayarishwa ili milo iweze kupewa waliopatwa na msiba na wafanyakazi wa kutoa misaada.
Fermín Pastrana, mzee kutoka Kundi la Princeton la Kihispania, aliripoti kwamba familia saba katika kundi lake la Mashahidi 80 walikuwa wamepoteza makao yao kabisa. Ni utatuzi gani aliokuwa amedokezea Mashahidi wenzi? “Huzunikeni ikiwa mwahitaji kuhuzunika. Lakini msikae kitako. Iweni watendaji katika kusaidia wengine, na, kwa kadiri iwezekanavyo, tokeni mwende katika huduma. Msikose mikutano yetu ya Kikristo. Tatueni yale yanayoweza kutatuliwa, lakini msisumbukie yale yasiyotatulika.” Kama tokeo, upesi Mashahidi walikuwa wakihubiri na kupeleka masanduku ya kutoa misaada nyumba kwa nyumba. Kimbunga Andrew hakikuwa kimepeperushia mbali bidii yao.
‘Wakati Mwingine Tutahama!’
Sharon Castro, mwanamke mwenye miaka 37 kutoka mji wa Cutler Ridge aliambia Amkeni! hadithi yake: “Baba yangu aliamua tusihame. Alihisi kwamba kwa kuwa kimbunga cha wakati uliopita kiligeukia mbali bila kupiga pwani ya Florida, kile cha Andrew kingefanya vivyo hivyo. Hata hangeimarisha madirisha kwa mbao. Jambo zuri ni kwamba, ndugu yangu alikuja na kusisitiza wazibe madirisha kwa mbao kadha zilizogandamizwa. Bila shaka yoyote, hatua yake iliokoa maisha zetu. Madirisha yetu yangelivunjwa, na tungelikatwa-katwa vipande.
“Karibu saa 10:30 usiku, umeme ulipotea. Kelele za nje zilihofisha. Ilikuwa kama sauti ya gari-moshi kubwa sana. Kulikuwa na kishindo, miti na majengo yalipovunjika na kuporomoka. Baadaye tuling’amua kwamba sauti nyembamba ya kuogofya ilikuwa ile ya misumari mirefu katika paa letu iliyokuwa ikilegea. Orofa la juu lilipeperushwa, na kiasi kikubwa cha paa letu kilibebwa pia. Mwishowe, sisi sote 12, kutia na mama yangu mgonjwa sana na nyanya yangu mwenye miaka 90, tulilazimika kujibanza katika chumba cha katikati kisicho na madirisha. Tulihisi wenye uhakika kwamba tungefia humo.”
Alijifunza somo gani kutokana na ono hilo? “Wakati mwingine wakituambia tuhame, tutahama—bila maswali. Tutasikiliza maonyo. Pia nimejifunza kushiriki na kuishi na vitu vichache sana. Na ninajua ni vema kulia, kuhuzunika, na kukabili uhalisi wa mambo.”
Maitikio ya Magazeti
Hata magazeti yaliona jinsi Mashahidi walivyojipanga vizuri. Savannah Evening Press lilikuwa na kichwa kikuu “Mashahidi wa Yehova Wapata Kuwa Wanakaribishwa Katika Florida Kusini,” na The Miami Herald likajulisha: “Mashahidi Washughulikia Walio Wao—na Wengineo.” Lilisema: “Hakuna yeyote katika Homestead anayefunga mlango Mashahidi wa Yehova wanapobisha juma hili—hata ingawa bado wana milango ya kufunga. Mashahidi wenye kujitolea wapatao 3,000 kotekote nchini wamekutana kwenye sehemu ya msiba, kwanza kusaidia walio wao, kisha kusaidi wengineo. . . . Shirika lolote la kijeshi laweza kutamani ule utaratibu, nidhamu na ubora wa kazi wa Mashahidi.”
Mashahidi wamezoea kupanga kazi ya kulisha watu wengi kwenye makusanyiko na mikusanyiko. Zaidi ya hiyo, wamepanga mamia ya Halmashauri ya Ujenzi wa Kimkoa kotekote ulimwenguni ili kujenga Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko yaliyo makubwa. Hivyo, wana wafanyakazi waliozoezwa na walio tayari kuchukua hatua wanapojulishwa kwa muda mfupi.
Hata hivyo, kuna jambo jingine—mtazamo wao. Ripoti hiyohiyo iliendelea hivi: “Hakuna kupiga ubwana. Hakuna watu wanaopigania ukubwa. Badala yake, wafanyakazi wanaonekana wenye furaha na wenye kushirikiana sana hata kuwe joto, wawe wachafu au wamechoka kadiri gani.” Hilo lilielezwaje? Shahidi mmoja alijibu: “Hilo linatokana na uhusiano na Mungu ambao hutusukuma kuonyesha upendo wetu kwa wengine.” Hilo ni jambo jingine ambalo kimbunga Andrew hakingeweza kupeperusha mbali, upendo wa Kikristo wa Mashahidi.—Yohana 13:34, 35.
Ulinganisho wenye kupendeza ni kwamba ilionekana kwamba Mashahidi walijifunza kutokana na miti. Mmoja aliyeshuhudia alisema: “Niliposafiri huku na huku, niliona kwamba mamia ya miti mikubwa ilikuwa imeng’olewa na kuangushwa hadi chini. Kwa nini? Miti hiyo ilikinza sana upepo mwingi kwa sababu ya ukubwa wayo, na ilikuwa na mizizi iliyoenea pote lakini yenye kina kifupi. Kwa upande ule mwingine, miti mingi ya mivumo iliyo myembamba ilibaki imesimama. Ilinepa kwa upepo, baadhi yayo ikipoteza matawi yayo, lakini miti mingi ilibaki imetiwa mizizi kwenye udongo.”
Mashahidi walikuwa na mizizi yenye kina kirefu ya imani katika Neno la Mungu na walibadilikana katika maitikio yao. Mali na makao havikuwa vya maana sana. Angalau walikuwa hai na wangeweza kuendelea kumtumikia Yehova kujapokuwa na taabu. Uhai ulikuwa jambo ambalo kimbunga Andrew hakikuweza kuwanyang’anya.
Hiyo Hufanywaje?
Kampuni ya Anheuser Busch ilitoa upaji wa lori nzima ya maji ya kunywa. Dereva alipowasili, aliuliza maofisa ni wapi anapaswa kupeleka maji hayo. Aliambiwa kwamba watu pekee waliokuwa na mpango ni Mashahidi. Kwa kweli, katika muda wa juma moja baada ya kimbunga Andrew kupiga, ugavi wa malori 70 ulikuwa umewasili kwenye Jumba la Kusanyiko la Fort Lauderdale la Mashahidi wa Yehova.
Mmoja mwenye kujitolea huko aliripoti: “Kwa hiyo sisi tulipokea lori nzima la maji ya kunywa. Tuliyaweka mara hiyo pamoja na chakula kingine ambacho tulikuwa tukipeleka kwenye vituo vya ugawanyaji kwenye Majumba ya Ufalme. Yaligawanywa miongoni mwa akina ndugu na majirani katika sehemu hiyo waliokuwa na uhitaji.” Kampuni ya karatasi katika Jimbo la Washington ilitoa sahani za karatasi 250,000.
Hapo mwanzoni, wenye mamlaka wa jiji walikuwa wakiwatuma wenye kujitolea wasio Mashahidi kwenye Majumba ya Ufalme, wakisema, ‘Wao tu ndio watu walio na mpango mzuri.’ Hatimaye majeshi yalikuja na kuanza kuweka vituo vya kuandaa misaada ya chakula na maji na majiji ya hema.
Kituo cha mwanzoni cha Mashahidi kiliwekwa na halmashauri ya kuandaa misaada kwenye Jumba la Kusanyiko la Fort Lauderdale, lililo kilometa 60 hivi kaskazini mwa eneo lenyewe la msiba kuzunguka Homestead. Ili kupunguza kazi kubwa, eneo la kituo cha msingi Lilianzishwa kwenye Jumba la Kusanyiko la Jiji la Plant karibu na Orlando, kilometa zipatazo 400 kaskazini-magharibi mwa eneo la msiba. Vifaa vingi vya msaada vilipelekwa huko ili vipambanuliwe na kupakiwa. Halmashauri iliagiza mahitaji yayo kutoka kwa Jiji la Plant kila siku, na malori makubwa yalitumiwa kusafiri kwa muda wa saa tano kufika Fort Lauderdale.
Kisha kituo hicho cha kutoa misaada kilitoa ugavi wa chakula, vifaa, maji, jenereta, na mahitaji mengine kwa Majumba ya Ufalme matatu yaliyokuwa yamerekebishwa katikati ya sehemu ya msiba. Huko, Mashahidi wenye uwezo walipanga wafanyakazi wa ujenzi na wa usafi waweze kuzuru mamia ya makao yaliyohitaji uangalifu. Meko na mistari ya chakula ilianzishwa pia kwenye uwanja wa Jumba la Ufalme, na mtu yeyote alikaribishwa aje apate msaada. Hata baadhi ya askari-jeshi walifurahia milo na baadaye walionwa wakitia upaji katika masanduku ya michango.
Wanaume walipokuwa wakishughulika kurekebisha makao, baadhi ya wanawake walikuwa wakitayarisha milo. Wengine walikuwa wakizuru watu wowote walioweza kuwapata ili kushiriki nao maelezo ya Biblia ya misiba ya asili na pia kuwapa bure masanduku ya misaada wale waliokuwa na uhitaji. Mmoja wa hao alikuwa Teresa Pereda. Kao lake liliharibiwa, na madirisha ya gari lake yakavunjwa—na bado gari hilo lilibeba masanduku ya misaada tayari kwa majirani zake. Mume wake, Lazaro, alishughulika kufanya kazi kwenye mojawapo Majumba ya Ufalme.—Mhubiri 9:11; Luka 21:11, 25.
Kwa wengi wasio na makao, malazi mengine yalipatikana katika makao ya Mashahidi yasiyoharibiwa na Andrew. Wengine walikaa katika trela zilizokodiwa au kutolewa kwa ajili ya kusudi hilo. Wengine walihamia kwenye majiji ya hema yaliyoanzishwa na majeshi. Wengine waliyaona makao yao kuwa yasiyofaa kitu na wakahamia kwa marafiki na watu wa ukoo katika sehemu nyingine za nchi. Hawakuwa na makao wala kazi. Hakukuwa na umeme, maji, na mifereji ya kuondoa maji machafu—kwa hiyo walitumia utatuzi ulio bora zaidi.
Somo moja ambalo wote walijifunza lilielezwa vema na Shahidi mmoja mwenye kusema Kihispania: “Tuna shukrani sana kwa somo tulilojifunza kuhusu miradi yetu maishani. Wajua, unaweza kufanya kazi kwa miaka 15 au 20 kujenga makao yako, kurundika mali, na kisha katika saa moja tu, yote yaweza kutoweka. Hilo linatusaidia kutambulisha miradi yetu ya kiroho, kufanya maisha yawe sahili zaidi na kufikiria kwelikweli juu ya kumtumikia Yehova.”
Ni kama vile ambavyo mtume Paulo alisema: “Mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo. Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo.”—Wafilipi 3:7, 8.
Misiba ya asili ni sehemu ya maisha katika ulimwengu wetu wa sasa. Tukitii maonyo kutoka kwa wenye mamlaka, huenda angalau tukaokoa uhai wetu. Labda makao na mali zitapotea, lakini uhusiano wa Mkristo pamoja na “Mungu wa faraja yote” wapaswa uimarishwe. Hata ikiwa huenda wengine wakaangamia katika msiba, Yesu aliahidi ufufuo kwa ajili yao katika ulimwengu mpya wa Mungu katika dunia iliyorudishwa—dunia ambayo haitaona kamwe taabu na kifo kinacholetwa na misiba ya asili.—2 Wakorintho 1:3, 4; Isaya 11:9; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:3, 4.
[Maelezo ya Chini]
a Kimbunga ni “tufani ya chamchela inayofanyizwa juu ya Bahari ya Atlantiki Kaskazini ambacho katika hicho upepo mwingi hupata mwendo zaidi ya kilometa 121 kwa saa.” (The Concise Columbia Encyclopedia) Tufani ni “kimbunga kinachotokea katika magharibi mwa Pasifiki au Bahari ya China.”—The American Heritage Dictionary of the English Language.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Alistaajabishwa Kabisa
Kikundi cha Mashahidi wazungu 11 walisafiri kutoka Tampa, Florida, ili kusaidia katika kazi ya kuandaa misaada. Walipata ugavi na wakaanza kurekebisha paa la Shahidi mweusi. Wakati mpwa wake asiye Shahidi alipowasili, hangeweza kuamini macho yake—alistaajabishwa kabisa kupata kwamba kikundi cha Mashahidi wazungu walikuwa wamefika kabla yake na walikuwa wakirekebisha makao ya mjomba wake. Alivutiwa sana hivi kwamba hata alisaidia katika kazi ya ujenzi.
Alisema kwamba wakati mwingine Mashahidi wakija kwenye nyumba yake, angewaomba funzo la Biblia. Alipokuwa akizungumza na kikundi cha Tampa, ilidhihirika kwamba alitoka eneo lao. Bila kukawia mmoja wa wazee katika kikundi hicho alifanya mipango ya funzo la Biblia juma lililofuata! Kama vile Shahidi mmoja alivyosema, hilo lilithibitisha kwamba si lazima tu ugonge milango ili kutoa ushahidi—unaweza kugonga paa!
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kimbunga Andrew hakikuacha chochote, na majengo machache yalisimama
Makao ya kukokotwa na gari ya akina Kieffer—na yale yaliyobakia
[Picha katika ukurasa wa 16]
Rebecca Pérez, mabinti wake, na wengine 11 waliokoka katika nafasi hii ndogo
Majeshi yaliingilia ili kuzuia uporaji (juu kulia); maduka yaliyoporwa (kulia)
Kimbunga kilirarua paa, na magari yalitupwa huku na huku
[Picha katika ukurasa wa 17]
Misaada ilipangwa kwenye Majumba ya Ufalme
Makao ya kukokotwa na gari yalizungushwa kwenye miti; vitu vya kuchezea vya mtoto vimeachwa juu ya godoro; Fasihi ya Biblia imo miongoni mwa mabaki hayo; Mashahidi, kama vile Teresa Pereda, walipeleka ugavi kwa majirani wao
Vifaa vya ujenzi vilivyotolewa kuwa upaji. Kupambanua nguo
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wenye kujitolea kutoka kotekote United States walisaidia katika kazi ya kutoa misaada