Ulimwengu Wetu Unaobadilika—Wakati Ujao Una Nini kwa Kweli?
IKIWA ulimwengu wetu utabadilika uwe bora, tuna mambo gani ya kuchagua? Chaguo moja ni kuamini kwamba watawala na viongozi wa ulimwengu hatimaye watakuwa wenye kujali masilahi ya wengine na kuanza kuongoza ainabinadamu kwenye njia za kuvumiliana, kuelewana, na amani.
Hiyo inamaanisha kuamini kwamba ukabila na utukuzo wa taifa utaondolewa na mahali pazo pachukuliwe na mtazamo wa kimataifa ambao waweza kuleta upatano ulimwenguni.
Pia inahusisha kuamini kwamba viongozi wa nchi za kibepari watatambua kwamba kusudi la kupata faida pekee ni wazo lisilofaa katika ulimwengu ambamo wengi hawana kazi, makao, na wana madeni makubwa ya matibabu.
Kwa kuongezea inamaanisha kuamini kwamba watengenezaji wote wa silaha wa ulimwengu wataanza kutamani amani ya ulimwengu na hivyo watafua panga zao ziwe majembe ya plau.
Zaidi ya hiyo, inamaanisha kwamba wahalifu wa ulimwengu, kutia na wakuu wa Mafia, wakuu wa magenge ya uhalifu ya Mashariki, na wakuu wa biashara ya dawa za kulevya katika Amerika Kusini, watatubu na kuanza kuwa na mwenendo mwema!
Kwa maneno mengine, inamaanisha kuamini katika hali kamilifu iliyofanyizwa na mwanadamu—ndoto isiyowezekana. Ikiwa yote hayo yatatukia bila msaada wa Mungu, basi tumo katika hali ileile iliyoelezwa na mwanahistoria Paul Johnson katika kitabu chake A History of the Modern World. Aliandika kwamba mojawapo maovu yanayochangia “ushinde na misiba yenye kuleta kifo” katika karne hii ni “itikadi ya kiburi kwamba wanaume na wanawake wangeweza kusuluhisha mafumbo yote ya ulimwengu wote mzima kwa ujuzi wao wenyewe.”—Linganisha Isaya 2:2-4.
Hata hivyo, kuna chaguo zuri kwa badiliko linalofaa. Hilo ni kuamini kwamba Muumba wa dunia, Mwenye sayari yetu, Fundi-Mbuni-Ujenzi Mkuu, Yehova Mungu, ataingilia mambo ya kibinadamu ili kuokoa kazi yake ya ustadi. Historia ya Biblia huonyesha kwamba Mungu amechukua hatua nyakati za kale ili kuendeleza makusudi yake, na unabii wa Biblia huonyesha kwamba karibuni atachukua hatua tena ili kutimiza kusudi lake la kwanza kwa ainabinadamu na dunia.—Isaya 45:18.
Chanzo cha Pekee cha Habari Inayotegemeka
Chanzo cha pekee cha maarifa halisi juu ya yale yaliyo katika wakati ujao wa ainabinadamu kinaelezwa katika maneno ya Biblia ya nabii Isaya: “Kumbukeni mambo ya zamani za kale; maana mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado.”—Isaya 46:9-11.
Kwa nini Yehova Mungu ana ujuzi wa kimbele wa matukio yatakayoathiri ainabinadamu hivi karibuni? Isaya tena ajibu: “Kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” Mawazo ya Mungu juu ya wakati ujao wa ainabinadamu yanaelezwa katika Biblia.—Isaya 55:9.
“Nyakati za Hatari Zilizo Ngumu Kushughulika Nazo”
Neno la Mungu, Biblia, limetabiri nini kwa ajili ya kizazi chetu? Mtume Paulo Mkristo alionya: “Lakini jua hili, kwamba katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa.” (2 Timotheo 3:1, New World Translation) Tangu 1914 na Vita ya Ulimwengu 1, tumekuwa tukiishi katika nyakati ambazo zimezidi kuwa za hatari. Ubinafsi, pupa, na tamaa ya uwezo ya mwanadamu imemwongoza kufanya maovu mabaya zaidi na zaidi si dhidi ya mwanadamu mwenzake tu bali pia dhidi ya uumbaji wa asili wenyewe. Kutokujali kwa mwanadamu kuelekea mazingira yake kunatisha kuwapo kwa watoto wake na wajukuu wake wakati ujao.
Hatari hiyo kuu ilikaziwa na aliyekuwa rais wa Chekoslovakia, Vaclav Havel, aliyeandika kuhusu hali katika nchi hiyo. Kwa kweli, maneno yake yanatumika ulimwenguni pote: “Hayo ni matokeo tu ya . . . mtazamo wa mwanadamu kuelekea ulimwengu, kuelekea uumbaji wa asili, kuelekea wanadamu wengine, kuelekea uhai wenyewe. Hayo ni matokeo . . . ya kiburi cha mwanadamu wa kisasa, anayeamini kwamba anaelewa kila kitu na anajua kila kitu, anayejiita mkuu wa uumbaji wa asili na wa ulimwengu. . . . Hayo ndiyo yaliyokuwa mawazo ya mwanadamu aliyekataa kutambua kitu chochote . . . kilicho juu kuliko yeye.”
Al Gore, aliyetangulia kunukuliwa aliandika: “Nina uhakika kwamba watu wengi wamepoteza imani yao juu ya wakati ujao, kwa sababu karibu katika kila jambo la ustaarabu wetu tunaanza kutenda kana kwamba wakati ujao wetu umo mashakani sana sasa hivi kwamba inaonekana ikifaa kukaza akili hasa juu ya mahitaji yetu ya sasa na matatizo ya muda mfupi.” (Earth in the Balance) Kwa kweli inaonekana kwamba wengi wanatazamia mabaya kwa wakati ujao.
Hali hiyo imetokea kwa sababu kwa sehemu maneno yanayofuata ya Paulo yametimizwa: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”—2 Timotheo 3:2-5.
Njia Nyingine Bora
Lakini Mungu amekusudia kwamba mambo yatabadilika kwenye dunia hii—yawe bora. Ameahidi kwamba ataleta “mbingu mpya na nchi [dunia, NW] mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.” (2 Petro 3:13) Ili kurudisha dunia hii iliyochafuliwa kwenye hali ya Paradiso, Yehova Mungu lazima kwanza ‘atawaharibu wale waiharibuo dunia.’ (Ufunuo 11:18) Hilo litatendekaje?
Ikitumia maneno ya ufananisho, Biblia huonyesha kwamba Mungu karibuni atatia katika mioyo ya sehemu za kisiasa, kutia na Umoja wa Mataifa, wazo la kuharibu uwezo na ufanisi wa labda kani isiyofaa zaidi katika historia ya ainabinadamu—uvutano wa kitaifa na wa kugawanya wa dini duniani pote.a Kulingana na Martin van Creveld, katika kitabu chake The Transformation of War, “inaonekana tunaweza kutazamia kwamba mitazamo, itikadi, na ushupavu wa kidini utakuwa na sehemu kubwa zaidi katika kuchochea mizozo ya kijeshi kuliko vile umechochea, angalau katika Magharibi, kwa miaka 300 iliyopita.” Labda kwa sababu ya kuingilia siasa, dini itateseka mikononi mwa mamlaka za kisiasa. Hata hivyo, mamlaka hizo zitakuwa zikitimiza mapenzi ya Mungu bila kujua.—Ufunuo 17:16, 17; 18:21, 24.
Kisha, Biblia yaendelea kuonyesha kwamba Mungu atageuza fikira zake kwenye sehemu za kisiasa za kihayawani zenye ubinafsi za mfumo wenye ufisadi wa Shetani na kupigana nazo katika vita yake ya mwisho, au vita ya Har–Magedoni. Baada ya kuondolewa kwa mifumo ya kisiasa isiyo na huruma na mchochezi wayo mkuu, Shetani, njia itakuwa wazi kwa ulimwengu mpya wenye amani ambao Mungu ameahidi.b—Ufunuo 13:1, 2; 16:14-16.
Kwa muda wa karibu miaka 80, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakihubiri kutoka nyumba kwa nyumba kuhusu mabadiliko hayo yanayokuja. Katika wakati huo, wao pia wameona na kuhisi mabadiliko mengi ambayo ainabinadamu imeleta. Wamepitia magereza na kambi za mateso za Wanazi kwa sababu ya kanuni zao zinazotegemea Biblia. Wameona taabu na kuteseka kwa maisha katika sehemu nyingi za Afrika, kutia ndani vita vya wenyewe kwa wenyewe na ugomvi wa kikabila. Wamevumilia minyanyaso mikononi mwa mifumo mingi ya kisiasa na ya kidini kwa sababu ya kutokuwamo kwao na bidii yao ya utendaji wa kuhubiri. Na bado, kujapokuwa hayo yote, wameona baraka ya Mungu juu ya kazi yao ya elimu ya ulimwenguni pote huku wakikua kuanzia maelfu machache katika 1914 hadi milioni nne unusu hivi katika 1993.
Sababu za Kuwa na Mtazamo Mzuri
Badala ya kushindwa na mtazamo mbaya, Mashahidi wana mtazamo mzuri kwa sababu wanajua kwamba mabadiliko bora na yaliyo makuu zaidi yatatendeka duniani hivi karibuni. Matukio tangu 1914 yametimiza unabii mbalimbali ambao Yesu alitoa, yakitia alama kuwapo kwake kusikoonekana katika uwezo wa Ufalme na kuonyesha kwamba tumo katika wakati wa mwisho wa kuwa na “mvurugo wa ulimwengu mpya” wenye kuletwa na binadamu, kama vile mwandikaji Mfaransa alivyoeleza mataraja ya wakati ujao wa karibuni katika Le Monde. Yesu alisema: “Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:7-32.
“Utaratibu wa ulimwengu mpya” wa mwanadamu unaweza kuharibiwa na upungufu wa asili ya kibinadamu—kufuatia makuu, tamaa ya uwezo, pupa, ufisadi, na ukosefu wa haki. Ulimwengu mpya wa Mungu utahakikisha kuwa kuna haki. Kuhusu yeye imeandikwa: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.
“Utaratibu wa ulimwengu mpya” wa mwanadamu unapatwa na yale McGeorge Bundy, mtaalamu wa U.S. wa mwongozo wa nchi za kigeni, aliita “hisi zisizofaa za utukuzo wa taifa ambazo zinaweza kutumiwa na viongozi wadanganyifu.” Akiendelea alisema: “Tunajua kutokana na historia jinsi kushindwa kiuchumi na kijamii kwaweza kutoa nguvu kwa watu wenye kupita kiasi kama hao. Pia tunajua kwamba hata itukie wapi, utukuzo wa taifa wa aina hiyo ni hatari.”
Ulimwengu mpya wa Mungu unahakikisha upatano na amani kati ya watu wa makabila na mataifa yote kwa sababu wataelimishwa katika njia za Yehova za kutokuwa na upendeleo na zenye upendo. Isaya alitoa unabii hivi: “Na watoto wako wote watafundishwa na BWANA [Yehova, NW]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Na mtume Petro Mkristo alisema: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
Bila shaka yoyote, kutakuwa na matukio ya kutazamisha katika wakati ujao ulio karibu katika ulimwengu kama tuujuao. Hata hivyo, mabadiliko yaliyo makuu zaidi, ya kudumu na yenye kunufaisha, ni yale ambayo Mungu ameahidi kuleta, na yeye ‘hawezi kusema uongo.’—Tito 1:2.
[Maelezo ya Chini]
a Milki ya ulimwengu ya dini bandia inatambulishwa katika Biblia kuwa “Babeli Mkuu, Mama wa Makahaba” malkia aliyemwaga damu ambaye “dhambi zake zimefika hata mbinguni.” (Ufunuo 17:3-6, 16-18; 18:5-7) Kwa maelezo mengi juu ya utambulisho wa Babeli Mkuu, ona kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, kurasa 368-71, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kwa maelezo mengi kuhusu matukio hayo yaliyotolewa unabii katika Biblia, ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! sura 30-42, kilichotangazwa katika 1988 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.