Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 12/1 kur. 10-13
  • Matendo ya Yehova ya Kuokoa Sasa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matendo ya Yehova ya Kuokoa Sasa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Upendo kwa Matendo
  • Udugu wa Ulimwenguni Pote
  • Chanzo cha Ulinzi wa Kweli
  • Kukua Pamoja Katika Upendo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Mambo Ambayo Kimbunga Andrew Hakingeweza Kuharibu
    Amkeni!—1993
  • Kitu Kisichoweza Kuharibiwa na Dhoruba
    Amkeni!—2003
  • Kazi ya Kutoa Msaada
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 12/1 kur. 10-13

Matendo ya Yehova ya Kuokoa Sasa

BIBLIA hutuambia hivi juu ya Yehova: “Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini BWANA [Yehova, NW] humponya nayo yote” na, “Bwana [Yehova, NW] ajua kuwaokoa watauwa na majaribu.”—Zaburi 34:19; 2 Petro 2:9.

Yehova huwasaidiaje watu wake wanapokuwa katika msononeko? Si kwa kutangua kani za asili kimuujiza au kwa tendo jingine linalozidi nguvu za kibinadamu, kama vile watu wengi hufikiri apaswa kufanya, lakini kwa kani nyingine ambayo watu walio wengi hawaelewi kikweli—upendo. Ndiyo, Yehova hupenda watu wake, na amekuza kati yao upendo kwa ajili ya mmoja na mwenzake ulio wenye nguvu sana hivi kwamba aweza kuwatimizia jambo ambalo karibu laonekana kuwa la kimuujiza.—1 Yohana 4:10-12, 21.

Huenda wengine wakatoa hoja kwamba katika wakati wa dharura, kinachohitajiwa ni chakula, dawa, na vifaa—si upendo. Bila shaka chakula, dawa, na vifaa ni vya maana. Hata hivyo, mtume Paulo atoa sababu hivi: “Nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.”—1 Wakorintho 13:2, 3.

Mara nyingi sisi husoma juu ya ugavi wa misaada ukiwa bandarini ukioza au ukiliwa na wanyama-watafunaji huku watu wenye uhitaji wakifa kutokana na magonjwa na njaa. Au vibaya zaidi, ugavi huo huenda ukaingia mikononi mwa watu wenye pupa na walio wabaya ambao wautumia kwa faida yao binafsi. Hivyo, ni rahisi kuwa na ugavi, lakini ni vigumu kuhakikisha kwamba wale walio katika msononeko wanufaika nao. Upendo na hangaiko la kweli laweza kuleta tofauti.

Upendo kwa Matendo

Katika Septemba 1992, Kimbunga Iniki kilipiga kisiwa cha Hawaii cha Kauai, chenye wakazi 55,000. Kikiwa na pepo zenye mwendo wa kilometa 210 kwa saa na dhoruba za ghafula zenye mwendo wa kilometa 260 kwa saa, kiliua watu 2 na kuwajeruhi 98, kikaharibu asilimia 75 ya nyumba, kuacha watu 8,000 bila makao, na kusababisha uharibifu wenye thamani iliyokadiriwa kuwa dola bilioni moja. Miongoni mwa wale walioishi katika kisiwa kidogo hicho walikuwa Mashahidi wa Yehova 800 hivi katika makutaniko sita. Wao walikabilianaje?

Kabla ya Iniki kupiga kihalisi, wazee wa kutaniko, chini ya mwelekezo wa mwangalizi asafiriye, walikuwa tayari wamewasiliana na washiriki wote wa makutaniko ili kuhakikisha kwamba walikuwa salama salimini, wakiwa tayari kwa ajili ya pigo hilo. Utunzi huo wenye upendo ulisaidia kuzuia majeruhi mabaya au kifo miongoni mwa Mashahidi.—Linganisha Isaya 32:1, 2.

Hata ingawa mawasiliano na usafiri ulikuwa umekatizwa vibaya sana, wawakilishi watatu wa ofisi ya tawi ya Watch Tower Bible and Tract Society katika Honolulu walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuwasili mahali hapo baada ya kimbunga, wakiwa wamepewa ruhusa ya pekee na idara ya ulinzi wa raia ya kusafiri kwa ndege hadi Kauai. Mara moja, asubuhi iliyofuata, waliwasiliana na Mashahidi wa mahali hapo, wakapanga mkutano ili kuratibisha utaratibu wa kutoa msaada. Halmashauri ya kutoa msaada ilifanyizwa ili kuchanganua mahitaji na kupata ugavi uliohitajiwa kupitia ofisi ya tawi katika Honolulu. Kwa kufanya kazi bila kukoma, walielekeza kazi ya kuwapelekea wenye uhitaji ugavi na kusafisha na kutengeneza nyumba zilizokuwa zimeharibika.

Mashahidi katika visiwa vingine waliitikia upesi ndugu zao wenye uhitaji. Mara uwanja wa ndege katika Kauai ulipofunguliwa, Mashahidi 70 walisafiri kwa ndege hadi hapo ili kusaidia. Ugavi wa misaada wenye thamani ya dola 100,000 kutia ndani majenereta, meko yanayochukulika, taa, na chakula, ulisafirishwa kwa meli. Mojayapo Majumba ya Ufalme katika kisiwa hicho lilitumiwa likiwa depo; hata hivyo, kulikuwa na hofu kwamba huenda likaporwa. Kisha malori ya Jeshi yakaingia maegeshoni mwa Jumba la Ufalme hilo, na madereva wakaomba kama wangeweza kuegesha malori yao hapo. Askari-jeshi waliopewa mgawo wa kulinda malori hayo waliondosha pia tatizo la uporaji wa ugavi wa misaada.

Akina ndugu waliyachukua majenereta hayo nyumba kwa nyumba, wakiyawasha kwenye kila nyumba kwa muda wa saa mbili au tatu ili kuwasaidia watu wadumishe friza zao katika hali ya kufanya kazi. Vikundi vya akina ndugu vilitumwa kwenye nyumba mbalimbali ili kusaidia kuzisafisha na kuzitengeneza zilikoharibika. Walipofanyia kazi nyumba ya dada fulani ambaye mume wake alikuwa amempinga vikali wakati uliopita, mume alivutiwa sana hivi kwamba lile tu aliloweza kufanya ni kutazama na kulia machozi. Mgeni mmoja kutoka bara kuu aliyeona kikundi kingine cha Mashahidi kikifanya kazi alivutiwa sana na mwenendo na utaratibu wao hivi kwamba aliwaendea na kuwauliza kilichowafanya wawe tofauti sana. Ndugu mmoja alipoeleza kwamba ni kwa sababu ya kupenda kwao Mungu na Wakristo wenzao, mtu huyo aliitikia hivi: “Naweza kupataje kumjua Mungu?” (Mathayo 22:37-40) Kisha akaongeza hivi: “Nyinyi watu ni wenye utaratibu sana yaelekea mtakuwa na mtu akingojea nyumbani kwangu nirudipo Florida!”

Kwa jumla, Mashahidi wa Yehova walisaidia kusafisha na kutengeneza nyumba 295 zilizoharibika katika Kauai. Kati yazo, 207 zilihitaji kutengenezwa kidogo-kidogo, lakini 54 zilikuwa zimeharibika sana, na 19 zilikuwa zimeharibiwa kabisa. Kazi yao ilitia ndani pia kutembelea kila Shahidi aliyejulikana katika kisiwa hicho ili kuhakikisha kwamba kila mmoja alikuwa ametunzwa. Ugavi ulipopelekewa dada fulani, jirani mmoja wa Dini ya Buddha alionelea kwamba hakuwa amepokea hata kifuko cha majani-chai kutoka kwa kikundi chake. Mwanamke mwingine, ambaye nyumba yake ilisafishwa na kikundi cha Mashahidi, alisema hivi: “Nyinyi mmekuwa mkija mlangoni pangu kwa muda mrefu, na niliwaona kuwa majirani wazuri, lakini wonyesho huu wa upendo wa kijirani wanionyesha jinsi tengenezo lenu lilivyo. Asanteni kwa kazi yenu yote yenye bidii.”

Zaidi ya kutunza mahitaji ya kimwili ya Wakristo wenzao wote, wale waliosimamia utoaji wa msaada walihangaikia vilevile hali njema yao ya kiroho. Siku zilizopungua mbili baada ya kimbunga hicho, makutaniko kadhaa yalikuwa tayari yakifanya mikutano yao. Upesi, vikundi vidogo vya funzo la kitabu vilikuwa vimeanza kutenda tena. Wazee kumi waliotoka visiwa vingine walikuja Kauai kusaidia wazee wa hapo ili ziara za uchungaji ziweze kufanyiwa kila Shahidi katika kisiwa hicho. Jumapili iliyofuata, makutaniko yote sita yalifanya Funzo la Mnara wa Mlinzi, hotuba ya muda wa dakika 30 juu ya taratibu za kutoa msaada iliyotolewa na mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Kutoa Msaada, na hotuba ya kumalizia ya muda wa dakika 30 iliyotolewa na mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Tawi aliyekuwa amekuja kutoka Honolulu kwa kusudi hilo. Ripoti ya mtu aliyejionea mwenyewe yale yaliyotukia yasema hivi: “Wote walifarijiwa na ule mwelekezo mzuri uliotolewa wakahisi wakiwa tayari kiroho kushughulikia matatizo yao yaliyobaki. Wengi kati ya wasikilizaji walikuwa wakidondokwa machozi programu ilipomalizika, na kupiga makofi mara moja.”

Udugu wa Ulimwenguni Pote

Upendo na hangaiko hilo ni alama ya watu wa Yehova ulimwenguni pote. Tufani Val ilipokumba Samoa ya Magharibi karibu mwaka mmoja kabla ya hapo, ilisababisha uharibifu mwingi, lakini Mashahidi wa Yehova katika sehemu nyinginezo za ulimwengu walikuja upesi kuwasaidia wale walioathiriwa na furiko. Baadaye, serikali ilipoandalia dini zote fedha—kutia na Mashahidi wa Yehova—ili kutengeneza majengo yazo yaliyoharibika, Mashahidi walirudisha fedha hizo pamoja na barua iliyosema kwamba majengo yao yote yaliyoharibika yalikuwa tayari yametengenezwa, na fedha hizo zingeweza kutumiwa ili kutengeneza majengo mbalimbali ya serikali yaliyoharibika. Hatua yao iliripotiwa katika gazeti la habari la mahali hapo. Akiona hilo, ofisa mmoja wa serikali alimwambia Shahidi mmoja kwamba alihisi aibu kidogo juu ya kanisa lake mwenyewe kwa sababu lilikuwa limekubali fedha hizo kutoka kwa serikali hata ingawa majengo yalo yote yaliyokuwa yameharibika wakati wa tufani yalikuwa yamelipiwa na bima.

Vivyo hivyo, katika Septemba 1992, Mto Ouvèze katika kusini-mashariki mwa Ufaransa ulipofurika na kuharibu Vaison-la-Romaine na jumuiya 15 zilizo karibu na hapo, Mashahidi waliitikia upesi. Usiku kucha, furiko lilikuwa limeua watu 40, kuharibu kabisa nyumba 400, na kuharibu kwa sehemu mamia nyinginezo, na kuacha maelfu ya familia bila maji au nguvu za umeme. Mapema asubuhi iliyofuata, Mashahidi kutoka katika makutaniko ya hapo walikuwa wa kwanza kuja kuwasaidia ndugu zao. Wale waliohitaji makao walikaribishwa kwa upendo na familia za Mashahidi katika mkoa huo. Mamia ya Mashahidi walikuja kutoka sehemu mbalimbali ili kutoa msaada. Halmashauri ya kutoa msaada ilifanyizwa katika jiji la karibu la Orange ili kuratibu jitihada za vikundi vinne vya wenye kujitolea, walioondoa matope na kusafisha nyumba, kufua nguo nyingi sana zilizokuwa zimelowa matope, na walitayarisha na kupeleka chakula na maji ya kunywa kotekote katika maeneo yaliyoathiriwa. Hata walijitolea kusafisha shule ya hapo na majengo kadhaa ya manispaa. Jitihada zao nyingi zilithaminiwa na ndugu zao na watu katika jumuiya hiyo pia.

Katika mahali penginepo pengi, Mashahidi wa Yehova wamepatwa na misiba kama vile, mafuriko, dhoruba, na matetemeko ya dunia, sawa na kila mtu mwingine yeyote. Wakielewa kwamba hayo ni matokeo ya hali zisizotazamiwa au zisizozuilika, wao hawamlaumu Mungu wala mtu mwingine yeyote. (Mhubiri 9:11) Badala ya hivyo, wana hakika kwamba ule upendo wenye kujidhabihu wa waamini wenzao utawaokoa haidhuru ni hali zipi mbaya ziwezazo kuwapata. Matendo hayo yenye upendo ni tokeo la imani wanayoshiriki pamoja. Mwanafunzi Yakobo aeleza hivi: “Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, na mtu wa kwenu akawaambia, Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini? Vivyo hivyo na imani isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake.”—Yakobo 2:15-17.

Chanzo cha Ulinzi wa Kweli

Badala ya kutazamia miujiza kwa namna ya mwingilio wa kimungu wa namna fulani, Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba ulinzi unapatikana katika udugu wao wa Kikristo wa ulimwenguni pote. Kwa kweli, kile kiwezacho kutimizwa na udugu huo katika nyakati za msononeko chakaribia sana kuwa cha kimuujiza. Wao hukumbuka maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 17:20: “Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.” Ndiyo, vizuizi vilivyo kama mlima hutoweka wakati imani ya kweli ya Kikristo, pamoja na upendo, zitendapo kazi.

Watu wa Yehova ulimwenguni pote huhisi mkono wa Mungu wao wenye kutoa ulinzi katika nyakati hizi zenye msukosuko na zenye hatari. Wao huhisi kama mtunga-zaburi alivyohisi: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, BWANA [Yehova, NW], peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.” (Zaburi 4:8) Kwa uhakika, wao hukazia fikira zao kazi iliyopo: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Nao hutazama mbele kwa hakika kwenye utimizo wa ahadi ya Yehova ya ulimwengu mpya mwadilifu, wenye amani, ambao katika huo hawatapatwa tena na misiba ya aina yoyote, yenye kusababishwa na binadamu au ya asili.—Mika 4:4.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mashahidi walikuja kutoka sehemu mbalimbali ili kuwasaidia wale walioathiriwa na furiko

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki