Vielelezo vya Unyenyekevu vya Kuiga
“Na unyenyekevu wako umenikuza.”—ZABURI 18:35.
1. Ni ithibati ipi ya unyenyekevu iliweza kuonwa katika mmoja aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society?
JOSEPH F. RUTHERFORD alikuwa mwenye kuvutia, akiwa na kimo cha zaidi ya sentimeta 180 na uzito wa zaidi ya kilo 90. Pia alikuwa na sauti yenye nguvu, aliyotumia si kujulisha jina la Yehova tu kwa kadiri lisivyopata kamwe kujulishwa bali pia kufunua unafiki wa viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo, akiita dini yao “mtego na hila.” Lakini ingawa hotuba zake zilikuwa zenye nguvu sana, aliposali pamoja na familia ya Betheli ya makao makuu, alisikika akiwa kama mvulana mdogo tu anayeongea na babake, hivyo akitoa ithibati ya uhusiano wake wa karibu sana na Mfanyi wake na ya unyenyekevu wake pia. Ndiyo, alikuwa mnyenyekevu kama vile mtoto mdogo.—Mathayo 18:3, 4.
2. Watumishi wa Yehova hutofautiana kabisa na watu mmoja-mmoja katika ulimwengu kwa habari gani hasa?
2 Bila shaka, watumishi wote wa kweli wa Yehova Mungu ni wanyenyekevu. Kwa habari hiyo wao hutofautiana kabisa na watu wa ulimwengu. Leo, kuliko wakati mwingine wowote, umejaa watu mmoja-mmoja wenye kiburi. Watu wenye vyeo vya juu na walio na uweza, matajiri na wenye elimu, na hata wengi walio maskini na wale wanaopungukiwa katika njia nyinginezo ni wenye kiburi.
3. Ni nini chaweza kusemwa juu ya matunda ya kiburi?
3 Kiburi husababisha ugomvi na huzuni nyingi sana. Kwa kweli, ole wote katika ulimwengu wote mzima ulianza kwa sababu malaika fulani alikuwa mwenye kiburi, akitaka kuabudiwa kwa njia iliyomstahili Muumba, Yehova Mungu, pekee. (Mathayo 4:9, 10) Zaidi ya hayo, yule aliyejifanya mwenyewe Ibilisi na Shetani, alifanikiwa katika kumshawishi mwanamke wa kwanza, Hawa, kwa kuvutia kiburi chake. Alimwahidi kwamba ikiwa angekula lile tunda lililokatazwa, yeye angeweza kuwa kama Mungu mwenyewe, akijua mema na mabaya pia. Kama angalikuwa mnyenyekevu, yeye angalisema, ‘Kwa nini nitake kuwa kama Mungu?’ (Mwanzo 3:4, 5) Tufikiriapo ile hali mbaya sana ambayo ainabinadamu imo ndani yayo, kimwili, kiakili, na kiadili, kiburi ni jambo lisilofaa kama nini kwa upande wa wanadamu! Si ajabu twasoma kwamba Yehova huchukia “kiburi na majivuno”! (Mithali 8:13) Tofauti kabisa na wenye kiburi wote ni vielelezo vya unyenyekevu vinavyopatikana katika Neno la Mungu, Biblia.
Yehova Mungu Ni Mnyenyekevu
4. Ni maandiko gani huonyesha kwamba Yehova ni mnyenyekevu?
4 Yehova Mungu—aliye Juu Kabisa, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, Mfalme wa umilele—ni mnyenyekevu. (Mwanzo 14:22) Je! hilo lawezekana? Bila shaka, ndiyo! Mfalme Daudi alisema, kama ilivyorekodiwa kwenye Zaburi 18:35: “Umenipa ngao ya wokovu wako, mkono wako wa kuume umenitegemeza, na unyenyekevu wako umenikuza.” Kwa wazi, Mfalme Daudi aliuona unyenyekevu wa Yehova kuwa ndiyo sababu ya kukuzwa kwake, Daudi. Kisha tena, twasoma kwenye Zaburi 113:6 kwamba Yehova ‘anyenyekea kutazama mbinguni na duniani.’ Tafsiri nyinginezo husoma, “ainama chini kutazama,” (New International Version) “ajidhili kutazama chini sana.”—The New English Bible.
5. Ni matukio gani ambayo hushuhudia unyenyekevu wa Yehova?
5 Kwa hakika Yehova Mungu alijinyenyekeza katika njia aliyoshughulika na Abrahamu, akimruhusu Abrahamu kumwuliza juu ya uadilifu Wake katika kukusudia kuharibu majiji maovu ya Sodoma na Gomora.(Mwanzo 18:23-32) Na Yehova alipoeleza nia yake ya kuharibu taifa la Israeli—wakati mmoja kwa sababu ya ibada ya sanamu, na wakati mwingine kwa sababu ya uasi—katika kila pindi Musa alisababu na Yehova kana kwamba alikuwa akiongea na binadamu mwingine. Kila mara Yehova aliitikia kwa kukubali. Kujibu sihi za Musa kwa niaba ya watu Wake Israeli kulionyesha unyenyekevu. (Kutoka 32:9-14; Hesabu 14:11-20) Vielelezo vingine vya Yehova akishughulika na wanadamu kwa unyenyekevu, kana kwamba mtu kwa mtu, vyaweza kuonwa katika mahusiano yake na Gideoni na Yona, kama yalivyorekodiwa kwenye Waamuzi 6:36-40 na Yona 4:9-11.
6. Ni sifa gani ya Yehova hufunua unyenyekevu wake zaidi?
6 Kwa kweli, Yehova anasemwa angalau mara tisa, kuwa “wa polepole kukasirika.”a Uthibitisho mwingine wa kwamba Yehova ni mnyenyekevu ni kule kuwa kwake mstahimilivu na wa polepole kukasirika katika kushughulika na viumbe vya kibinadamu visivyokamilika, kwa muda wote wa maelfu ya miaka iliyopita. Watu wenye kiburi hawana subira, ni wepesi kuonyesha hasira, tofauti sana na ustahimilivu. Unyenyekevu wa Yehova hufanya kiburi cha wanadamu wasiokamilika kionekane cha kipumbavu kama nini! Kwa kuwa tunaambiwa ‘tuwe waigaji wa Mungu kama watoto wapendwa,’ ni lazima tuwe wanyenyekevu kama vile alivyo mnyenyekevu.—Waefeso 5:1, NW.
Kielelezo cha Yesu cha Unyenyekevu
7, 8. Maandiko husema nini juu ya unyenyekevu wa Yesu Kristo?
7 Kielelezo cha pili cha unyenyekevu chenye kutokeza zaidi cha kuigwa na sisi kinatajwa kwenye 1 Petro 2:21: “Kwa sababu ndio mlioitwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.” Muda mrefu kabla hajaja duniani akiwa binadamu, unabii ulitolewa kuhusu yeye kwenye Zekaria 9:9: “Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; tazama, mfalme wako anakuja kwako; ni mwenye haki, naye ana wokovu; ni mnyenyekevu, amepanda punda.” Ikiwa Yesu Kristo angalikuwa mwenye kiburi, yeye angaliweza kwa urahisi kukubali toleo la Ibilisi la kumpa yeye falme zote ulimwenguni kwa kubadilishana na tendo moja la ibada. (Mathayo 4:9, 10) Alionyesha unyenyekevu wake pia kwa kumhesabia Yehova sifa yote kwa ajili ya mafundisho yake, akisema: “Mtakapokuwa mmekwisha kumwinua Mwana wa Adamu, ndipo mtakapofahamu ya kuwa mimi ndiye; na ya kuwa sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.”—Yohana 8:28.
8 Aliweza ifaavyo kuwaambia wasikilizaji wake hivi: “Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu.” (Mathayo 11:29) Naye aliweka kielelezo chema kama nini cha unyenyekevu kwa kuiosha miguu ya mitume wake katika jioni ya mwisho aliyokuwa pamoja nao akiwa binadamu! (Yohana 13:3-15) Kwa kufaa kabisa, kwenye Wafilipi 2:3-8, mtume Paulo awashauri Wakristo wawe na “unyenyekevu wa akili,” (NW) akitaja Yesu Kristo kuwa kielelezo: “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba [mti wa mateso, NW].” Alipokabiliwa na ugumu ulio mkubwa zaidi maishani mwake, alisali kwa Baba yake kwa unyenyekevu, hivi: “Si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.” (Mathayo 26:39) Kwa hakika, ili tuwe waigaji wa Yesu Kristo, tukifuata nyayo zake kwa ukaribu, ni lazima tuwe wanyenyekevu.
Mtume Paulo, Kielelezo Chema cha Unyenyekevu
9-12. Mtume Paulo aliweka kielelezo chema cha unyenyekevu katika njia zipi?
9 Mtume Paulo aliandika hivi: “Mwe waigaji wa mimi, kama nilivyo wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1, NW) Je! mtume Paulo alimwiga Yesu Kristo kwa kuwa mnyenyekevu wa akili, hivyo akitupa sisi kielelezo kingine cha unyenyekevu cha kuiga? Bila shaka alifanya hivyo. Kwanza, alikiri kwa unyenyekevu kwamba yeye alikuwa mtumwa wa Yesu Kristo. (Wafilipi 1:1) Aliwaambia wazee wa Efeso juu ya yeye ‘kumtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi, na majaribu yaliyompata kwa hila za Wayahudi.’ (Matendo 20:17-19) Kama asingalikuwa mnyenyekevu, yeye asingaliandika kamwe maneno haya yapatikanayo kwenye Warumi 7:18, 19: “Najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema . . . Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.”
10 Pia jambo lionyeshalo unyenyekevu wa Paulo ni yale aliyowaandikia Wakristo katika Korintho, kama ilivyorekodiwa kwenye 1 Wakorintho 2:3: “Nalikuwako kwenu katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi.” Akirejezea kwa unyenyekevu mwendo wake wa wakati uliopita kabla ya kuwa Mkristo, aliandika hivi: “Hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri. . . . Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi.”—1 Timotheo 1:13, 15.
11 Jambo jingine zaidi linaloonyesha unyenyekevu wake ni yeye kumpa Yehova Mungu sifa kwa ajili ya mafanikio yake yote katika jitihada zake. Aliandika hivi kuhusu huduma yake: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.” (1 Wakorintho 3:6, 7) Pia aliwaomba ndugu zake wasali kwa ajili yake ili aweze kutoa ushahidi mzuri, kama tusomavyo kwenye Waefeso 6:18-20: “Mkisali . . . kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi . . . hata nipate ujasiri katika hiyo kunena [ile siri takatifu ya habari njema] jinsi inipasavyo kunena.”
12 Paulo alionyesha unyenyekevu wake pia kwa njia aliyoshirikiana na mitume wengine: “Yakobo, na Kefa, na Yohana, . . . walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika; ili sisi tuende kwa Mataifa, na wao waende kwa watu wa tohara.” (Wagalatia 2:9) Alionyesha zaidi nia yake ya kushirikiana na wazee wa kutaniko kwa kuandamana na wanaume wachanga wanne hadi kwenye hekalu na kulipia gharama zao walipotimiza nadhiri.—Matendo 21:23-26.
13. Ni nini kilichofanya unyenyekevu wa Paulo uwe wenye kutokeza sana?
13 Unyenyekevu wa Paulo ni wenye kutokeza zaidi sana tuangaliapo jinsi alivyotumiwa sana na Yehova Mungu. Kwa kielelezo, twasoma kwamba “Mungu a[li]fanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida.” (Matendo 19:11, 12) Zaidi ya hayo, alipewa njozi na ufunuo mbalimbali unaozidi uwezo wa kiasili. (2 Wakorintho 12:1-7) Pia hatupaswi kupuuza kule kupuliziwa kwake ili kuandika vitabu (kwa kweli barua) 14 kati ya vile 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hayo yote hayakumfanya awe na kichwa kikubwa. Aliendelea kuwa mnyenyekevu.
Vielelezo vya Ki-Siku-Hizi
14-16. (a) Msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society alikuwaje kielelezo chema cha unyenyekevu? (b) Kielelezo chake chatofautiana kabisa na kile cha nani?
14 Kwenye Waebrania 13:7, twasoma shauri hili la mtume Paulo: “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.” Kwa kufuatia kanuni hiyo, twaweza kuchukua kama kielelezo cha ki-siku-hizi msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society, Charles Taze Russell, ambaye twaweza kufuata imani yake. Je! alikuwa mtu mnyenyekevu? Bila shaka alikuwa! Kama ilivyoonelewa vema, katika maandishi yake Studies in the Scriptures, yale mabuku sita yenye kurasa 3,000 hivi, yeye hakujirejezea hata mara moja. Vichapo vya Watch Tower Bible and Tract Society leo hufuata kanuni hiyo kwa kutoelekeza fikira kwa wanadamu kwa kutambulisha waandikaji wa makala mbalimbali.
15 Wakati mmoja katika Mnara wa Mlinzi, Russell aliandika kwamba hakujua jambo lolote liitwalo “Uruseli” na “Mwanaruseli,” majina ambayo wapinzani wake walitumia lakini ambayo yeye alikataa kabisa. Aliandika hivi: “Kazi yetu . . . imekuwa kukusanya vipande vya kweli vilivyotawanyika kwa muda mrefu na kuvitoa kwa watu wa Bwana—si kama ni mpya, si kama ni yetu wenyewe, bali kama ya Bwana. . . . Kazi ambayo katika hiyo Bwana amependezwa kutumia kipawa chetu chenye unyenyekevu imekuwa sana-sana kazi ya kuunda upya, kurekebisha, kupatanisha kuliko kuwa kazi ya kuanzilisha.” Kwa kweli, aliyatamka maoni ya mtume Paulo, kama yapatikanavyo kwenye 1 Wakorintho 3:5-7.
16 Mtazamo wake ulikuwa kinyume kabisa cha ule wa Charles Darwin. Katika chapa yake ya kwanza ya The Origin of Species katika 1859, mara kwa mara Darwin alirejezea nadharia “yangu,” akipuuza yale ambayo wengine kabla ya yeye walikuwa wamesema juu ya mageuzi. Mwandikaji mmoja mashuhuri wa karne hiyo, Samuel Butler, alimshambulia Darwin kwa maneno makali, akionyesha kwamba wengine wengi hapo mbele walikuwa wameendeleza nadhariatete (fikira dhanifu isiyothibitishwa) ya mageuzi; Darwin hakuwa mwenye kuianzisha hata kidogo.
17. Ni nini vielelezo vingine zaidi vya unyenyekevu wa Ndugu Rutherford?
17 Mtumishi mwingine mwaminifu katika nyakati za ki-siku-hizi ambaye Yehova Mungu alimtumia sana alikuwa Joseph F. Rutherford, aliyetajwa mwanzoni. Alikuwa mteteaji mwenye ujasiri wa kweli ya Biblia na hasa wa jina la Yehova. Ingawa alijulikana na wengi kuwa Hakimu Rutherford, yeye alikuwa mtu mnyenyekevu moyoni. Kwa kielelezo, wakati mmoja alitoa taarifa alizoona kuwa za kweli kabisa kuhusu yale ambayo Wakristo wangeweza kutazamia katika 1925. Matukio yaliposhindwa kuunga mkono matazamio yake, aliambia kwa unyenyekevu familia ya Betheli ya Brooklyn kwamba alikuwa ameamua mambo isivyofaa. Mkristo mmoja mpakwa aliyekuwa amekuwa na ushirika wa karibu naye alishuhudia kwamba mara kwa mara yeye alimsikia Ndugu Rutherford akiomba radhi katika namna ya Mathayo 5:23, 24, hadharani na faraghani pia, kwa sababu ya kumwudhi Mkristo mwenzake kwa maneno fulani yasiyofaa. Unyenyekevu wahitajiwa kwa upande wa mtu katika cheo cha mamlaka kuomba radhi kutoka kwa wale walio chini yake. Ndugu Rutherford aliwekea waangalizi wote kielelezo chema, iwe ni katika kutaniko, katika kazi ya kusafiri, au katika mojayapo matawi ya Sosaiti.
18. Msimamizi wa tatu wa Sosaiti alitoa elezo jipi lililofunua hali ya akili yenye unyenyekevu?
18 Msimamizi wa tatu wa Watch Tower Bible and Tract Society, Nathan H. Knorr, alionyesha pia kwamba, ingawa alikuwa mashuhuri miongoni mwa watu wa Yehova, yeye hakujihisi amekwezwa kwa sababu ya cheo chake. Ingawa alishinda wote katika uwezo wa kitengenezo na katika kutoa hotuba hadharani, alistahi sana yale ambayo wengine walifanya. Hivyo, wakati mmoja alimtembelea mshiriki mmoja wa Idara ya Uandikaji ofisini mwake na kusema hivi: “Huku ndiko kazi ya maana zaidi na pia iliyo ngumu zaidi hufanywa. Ndiyo sababu sifanyi kiasi kikubwa chayo.” Ndiyo, yeye alikuwa akitumia kwa unyenyekevu lile shauri kwenye Wafilipi 2:3, kwamba ‘kwa unyenyekevu wa akili kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.’ Alitambua kwamba ingawa kutumikia kama msimamizi wa Sosaiti kulikuwa jambo la maana, kazi nyinginezo zilikuwa za maana pia. Unyenyekevu ulihitajiwa kwa upande wake ili kuhisi hivyo na kueleza hilo kwa wazi sana. Yeye alikuwa kielelezo kingine chema cha kuigwa na wote, hasa wale ambao huenda wakawa wana cheo mashuhuri cha uangalizi.
19, 20. (a) Ni kielelezo kipi cha unyenyekevu kilichowekwa na msimamizi wa nne wa Sosaiti? (b) Makala ifuatayo itatupa sisi msaada gani kwa habari ya kuzoea kwetu unyenyekevu?
19 Msimamizi wa nne wa Sosaiti, Fred W. Franz, alikuwa kielelezo chema cha unyenyekevu pia. Akiwa makamu wa msimamizi wa Sosaiti kwa miaka 32 hivi, yeye alifanya sehemu kubwa ya uandikaji kwa ajili ya magazeti na kwa ajili ya programu za mkusanyiko; na bado kwa habari hiyo alibaki nyuma sikuzote, bila kujaribu kamwe kupata umashuhuri. Kielelezo cha kale kinachofanana na hicho chaweza kutajwa. Yoabu alipowashinda Waamoni katika Raba, alihakikisha kwamba Mfalme Daudi ndiye alihesabiwa ushindi huo.—2 Samweli 12:26-28.
20 Kwa kweli, kuna vielelezo vingi vyema, vya wakati uliopita na vya sasa, vinavyotupa sisi sababu zenye nguvu za kuwa wanyenyekevu. Hata hivyo, tuna sababu nyinginezo nyingi za kuwa wanyenyekevu, na hizo pamoja na misaada ya kutusaidia tuwe wanyenyekevu zitachunguzwa katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Kutoka 34:6; Hesabu 14:18; Nehemia 9:17; Zaburi 86:15; 103:8; 145:8; Yoeli 2:13; Yona 4:2; Nahumu 1:3, NW.
Je! Wakumbuka?
◻ Matokeo ya kiburi yamekuwa nini?
◻ Ni nani ameweka kielelezo chema zaidi cha unyenyekevu?
◻ Ni nini chaonyesha yule aliye na kielelezo kikuu zaidi cha pili cha unyenyekevu?
◻ Mtume Paulo aliweka kielelezo kipi chema cha unyenyekevu?
◻ Tuna vielelezo vipi mashuhuri vya unyenyekevu vya ki-siku-hizi?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Yesu alitoa wonyesho mzuri wa unyenyekevu
[Picha katika ukurasa wa 16]
Paulo aliweka kielelezo chema cha unyenyekevu
[Picha katika ukurasa wa 17]
Ndugu Russell hakujisifu mwenyewe kwa yale aliyoandika