Kutumaini au Kutotumaini
YAWEZA kuwa vigumu kujua ikiwa tutumaini au tusitumaini. Njia zote mbili zina hatari, hasa katika ulimwengu ambamo udanganyifu na usaliti zimeenea kila mahali. Hata hivyo sote twahitaji marafiki wenye kutumainiwa ambao watatutegemeza katika wakati wa taabu. (Mithali 17:17) Miaka elfu mbili hivi iliyopita, mwandikaji Mroma Phaedrus alieleza hali hiyo ya kutojua la kufanya hivi: “Kutumaini au kutotumaini, kutumaini ni hatari.”
Kutumaini Kwaweza Kuwa Hatari
Kwa nini kutumaini mtu mwingine huenda kukawa hatari? Fikiria onyo linalotolewa katika gazeti Psychology Today. Hilo hufafanua watu fulani ambao hutumia vibaya tumaini la watu kama “wawindaji” ambao “hutumia ujanja na ubadilikano kama wa kinyonga ili kudanganya na kuwatumia wanavyotaka wale walio karibu nao na kuharibu maisha zao.” Kwa wazi, kukiwa na wadanganyaji kama hao kotekote, kwa hakika kuwa mwenye kutumaini kupita kiasi ni hatari.
Mtu atumainiye kupita kiasi huenda akawa zuzu na, kama tokeo, adanganywe kwa urahisi na kutumiwa isivyofaa. Kielelezo kimoja halisi cha uzuzu kilikuwa Sir Arthur Conan Doyle, mbuni wa mpelelezi stadi mwenye kufikiri kwa utambuzi, Sherlock Holmes. Katika 1917 wasichana wawili wachanga, Elsie Wright na binamu yake, Frances Griffiths, walidai kwamba walikuwa wamecheza na viumbe vya kihekaya katika shamba la makao yao katika Cottingley, Uingereza. Hata walitoa picha za viumbe hao wa kihekaya ili kujaribu kuthibitisha jambo hilo.
Conan Doyle, ambaye alipendezwa sana na uwasiliani-roho baada ya kifo cha mwanaye, aliwatumaini na kuamini hadithi zao kuhusu viumbe hao wa kihekaya—kama ilivyokuwa na watu wengi wakati huo. Haikuwa hadi miaka 55 hivi baadaye kwamba wasichana hao wawili walikiri kwamba jambo hilo lilikuwa danganyo tu na kwamba walikuwa wamekata “viumbe hao wa kihekaya” kutoka kitabu fulani kabla ya kuwapiga picha. Frances Griffiths alishangaa kwamba mtu yeyote angeweza kuamini hadithi yao. Yeye alisema hivi: “Sikuzote sikuelewa jinsi ambavyo mtu angeweza kuwa zuzu mno kiasi cha kuamini kwamba viumbe hao wa kihekaya walikuwa halisi.”—Hoaxers and Their Victims.
Je, waweza kuona mtego ambao Conan Doyle aliangukia? Yeye alitumaini kabisa hadithi hiyo bila kushuku kwa sababu alitaka iwe kweli. Mtungaji vitabu Norman Moss asema hivi: “Twaweza kupumbazwa kwa sababu tu utambuzi wetu unafifishwa na zoea, nasi twatazama mambo kupitia macho yaliyofunguliwa nusu. . . . Nyakati fulani, twakubali jambo kuwa kweli kwa sababu ni jambo tutakalo liwe kweli.” (The Pleasures of Deception) Hilo larudia onyo lililotolewa na msemaji Mgiriki Demosthene miaka 350 hivi kabla ya Wakati wa Kawaida wetu: “Jambo rahisi kuliko yote ni kujidanganya, kwa kuwa kile mwanadamu hutamani kwa kawaida hukiamini kuwa kweli.” Kutumaini hisia zetu tu kwaweza kuwa hatari.
Bila shaka, huenda ukafikiri kwamba hicho ni kielelezo cha kupita kiasi na kwamba Conan Doyle alikuwa mpumbavu zaidi ya vile uwezavyo kuwa. Lakini si mazuzu tu walio hatarini mwa kudanganywa. Watu wengi waangalifu na ambao hutahadhari wamepumbazwa na kudanganywa na watu waonekanao kuwa wenye kutumainika.
Kutotumaini Kwaweza Kuwa Hatari
Hata hivyo, kuna hatari katika kutotumaini yeyote au chochote. Kutotumaini ni kama kutu yenye kuharibu. Inaweza kumomonyoa na kuharibu yale ambayo huenda yangekuwa mahusiano ya karibu, yenye furaha. Kutotumaini kwa madharau kusikobadilika kwaweza kukufanya uwe mtu asiye na furaha na asiye na rafiki. Kwaweza pia kuharibu sana mahusiano na watu wengine hivi kwamba mwandikaji Mwingereza Samuel Johnson aliandika, “ni jambo la furaha zaidi kuweza kudanganywa nyakati fulani kuliko kutotumaini.”
Kutotumaini kwaweza hata kuhatarisha afya yako ya kimwili. Huenda una habari kwamba hisia zenye nguvu kama hasira zaweza kukufanya upatwe na hatari ya mshiko wa moyo. Lakini je, ulijua kwamba utafiti fulani hudokeza kwamba kutotumaini kwaweza kufanya vivyohivyo? Gazeti Chatelaine lasema: “Si watu wanaofoka kwa hasira kwa urahisi pekee ambao waweza kuongeza hali zao za kupatwa na maradhi ya moyo kwa sababu ya tabia yao. Utafiti mpya waonyesha kwamba hata namna zilizofichika za uhasama, kama vile mwelekeo wa kudharau na kutotumaini, kwaweza kukuweka hatarini.”
Angalia Sana Uendavyo
Waweza kufanya nini? Biblia hutoa shauri zuri juu ya jambo hilo. “Mjinga [“Mtu yeyote asiye na uzoefu,” New World Translation] huamini kila neno,” husema Mithali 14:15. Huku si kudharau kunakodhuru. Ni kikumbusha cha kihalisi cha uhitaji wa kutahadhari. Ni mtu asiyejua chochote, asiye na uzoefu ambaye atatumaini bila kushuku kila neno alisikialo. Kwa sababu nzuri methali hiyo ya Biblia huendelea hivi: “Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” Mwandishi wa tamthilia Mwingereza William Shakespeare aliandika hivi: “Usitumaini mbao zilizooza.” Yeyote anayefikiria kwamba huenda ikawa mbao kwenye daraja lililo juu mno zimeoza, angekuwa mpumbavu kuzikanyaga. Basi, unaweza ‘kuangaliaje sana uendavyo’ ili usiweke tumaini lako mahali pasipofaa?
Biblia hututia moyo tujaribu yale wasemayo watu badala ya kukubali tu bila kushuku kila jambo tusikialo. “Sikio huyajaribu maneno, kama vile kaakaa lionjavyo chakula,” hiyo yasema. (Ayubu 34:3) Je, hilo si kweli? Je, sisi hatuonji chakula kabla ya kukimeza? Twapaswa pia kuyajaribu maneno na matendo ya watu kabla ya kuyakubali. Hakuna mtu ambaye ni mnyoofu atakayekasirika tukichunguza ustahili wake. Uhakika wa kwamba twapaswa kuchunguza ili kuona ikiwa kitu ni kinyoofu waungwa mkono na methali ya Scotland ambayo husema hivi: “Yeye anidanganyaye mara moja, aibu na iwe kwake; akinidanganya mara mbili, aibu na iwe kwangu.”
Mtume Paulo alishauri hivi: “Jaribuni mambo yote.” (1 Wathesalonike 5:21) Neno lililotumiwa na mtume Paulo kwa ‘jaribu’ lilitumiwa pia kuhusiana na kujaribu madini yenye thamani ili kuona ikiwa yalikuwa yenye thamani kikweli. Mtu mwenye busara sikuzote alijaribu ili kuona ikiwa kile alichonunua kilikuwa cha kweli. Sivyo angejipata akiwa na kile kilichoitwa dhahabu ya mpumbavu—kitu kilichofanana na dhahabu lakini kwa hakika hakikuwa na thamani.
Uwe Mwenye Kiasi na Usawaziko
Bila shaka, twataka kuwa na kiasi katika jambo hili na kutokuwa wenye kushuku wengine isivyofaa. (Wafilipi 4:5) Usifanye haraka kushuku wengine. Kusoma nia vibaya kwaweza kuwa njia ya haraka kupita zote ya kuvunja uhusiano bora wa karibu. Ni jambo bora kwa kawaida kudhania kwamba rafiki zako wanataka kufanya kile ambacho ni bora zaidi kwako badala ya kuwawekea nia mbaya hali ngumu zizukapo.
Ruhusu nafasi kwa ajili ya kutokamilika na makosa ya wengine. “Kusalitiwa na rafiki humaanisha kuvunjwa kwa tumaini,” asema mwandikaji Kristin von Kreisler. Hata hivyo, huenda usaliti huo haukunuiwa au huenda ulikuwa tokeo la udhaifu ambao unasikitikiwa sana sasa. Kwa hivyo, yeye aendelea: “Usikaze fikira zako kwenye huo usaliti—au kuacha ukuzuie kutumaini wengine.” Usiache maono machungu yaliyo hasi yakunyang’anye shangwe unazoweza kupata kutokana na kujenga mahusiano yenye tumaini na wengine.
Uwe na usawaziko. Huhitaji kuzuia utambuzi unapochanganua watu; mtu mwenye tahadhari hukaa chonjo. Kwa upande ule mwingine, Daktari Redford Williams adokeza kwamba tujaribu kudhania kwamba wengine wanafanya kadiri wawezavyo, jaribu kuelewa maoni yao, na “jizoeze kutumaini wengine” iwezekanapo. Huenda likawa jambo jema kutumaini mno kuliko kutotumaini kabisa.
Mwandikaji wa kitabu cha Biblia cha Mithali akubali kwamba “kuna waandamani wenye mwelekeo wa kuvunjana vipande-vipande”—yaani, watu ambao watajaribu kutumia vibaya tumaini lako. Dunia imejawa nao. Lakini wape wengine wakati na fursa ya kuonyesha kwamba wanaweza kuwa wenye kutumainika, nawe utapata marafiki ambao, kwa hakika, ‘huambatana karibu kuliko ndugu.’—Mithali 18:24, NW.
Basi, kuna yeyote au chochote ambacho unaweza kukitumaini kikamili, bila hofu yoyote kwamba tumaini lako litatumiwa vibaya au kusalitiwa? Ndiyo, kwa hakika kiko. Makala ifuatayo itazungumzia kifupi mahali ambapo waweza kuweka tumaini lako ukiwa na uhakika kamili.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Mjinga [“Mtu yeyote asiye na uzoefu,” NW] huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.”—Mithali 14:15
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ruhusu nafasi kwa ajili ya kutokamilika na makosa ya wengine