Waweza Kumtumaini Mungu
WAWEZA kumtumaini Mungu na Neno lake, Biblia, kikamili. Baada ya kumtumaini Mungu muda wote wa maisha yake, mwanamume mmoja, aliyepita miaka 100, alitoa sababu hii ya uhakika wake: “Angalieni!” yeye akasema, “mimi leo ninakwenda njia ile waendayo watu wote wa ulimwengu; nanyi nyote mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA, Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu hapana neno lo lote mlilopungukiwa.”—Yoshua 23:14, italiki ni zetu.
Mwanamume huyu, Yoshua, kiongozi wa Israeli la kale alijionea hali ya kutegemeka ya Mungu na Neno lake. Kila kitu ambacho Mungu aliahidi Israeli kilitimia. Ukipata kujua mengi kumhusu Muumba na Neno lake, unaweza kukuza tumaini lilo hilo. Mwabudu wa baadaye wa Mungu, Mfalme Daudi, alieleza jambo hilo kwa njia hii: ‘Wakujuao jina lako watakutumaini Wewe, maana Wewe, BWANA hukuwaacha wakutafutao.’—Zaburi 9:10.
Mungu Hatakosa Kamwe Kufanya Uliyotumaini
Kadiri upatavyo ‘kujua jina la Mungu’ na kile kimaanishwacho na jina hilo—makusudi yake, utendaji wake, na sifa zake—ndivyo utakavyozidi kumtumaini. Yeye ni Rafiki mwenye kutegemeka ambaye hatakosa kamwe kufanya uliyotumaini au kukosa kutimiza ahadi yake. Usivunjwe moyo na unafiki wa wale wadaio kuwa wawakilishi wake na kisha hushughulika na wengine kwa hila. Watu wa namna hiyo hutambulishwa na Biblia kuwa wasiotumainika. Wanafiki wa kidini husema jambo na kufanya kinyume. Kama alivyoonya mtume Petro, wao hutumia vibaya makundi yao. Petro aliandika: “Kwa sababu ya hao ile njia ya kweli itasemewa vibaya. Pia, kwa choyo watawatumia nyinyi kujifaidi kwa maneno bandia.”—2 Petro 2:2, 3, NW.
Watu kama hao hawamwakilishi Mungu. Wao hukosa kuliheshimu Neno lake. Kwa nini usijichunguzie rekodi na simulizi la Mungu mwenyewe kama lipatikanavyo katika Biblia? ‘Lakini,’ huenda ukauliza, ‘kwa nini nitumaini Biblia zaidi kuliko kitabu kinginecho chote?’ Ni kweli kwamba kumekuwa na ubandia mwingi wa kidini katika historia yote, lakini Biblia ni tofauti. Fikiria sababu zifuatazo za kuitumaini Biblia.
Sababu za Kuitumaini Biblia
Waweza kuitumaini Biblia kwa kuwa ahadi na unabii wayo sikuzote hutimia. Hapa pana kielelezo kimoja tu. Ingawa lingeonekana jambo lisiloweza kuaminika kwa Israeli lililotekwa, Yehova Mungu, mtungaji wa Biblia, alikuwa ameahidi kwamba angewaweka huru kutoka utekwa wa Babiloni lenye nguvu na kuwarudisha Yerusalemu. Lilionekana kuwa tumaini lisiloelekea kutimia kwa sababu Babiloni lilikuwa mamlaka kuu ya ulimwengu ya siku hiyo na lilikuwa limeharibu Yerusalemu kabisa. Lakini miaka mia mbili hivi kimbele, Yehova hata alikuwa ametaja jina la mtawala wa Uajemi, Koreshi, kuwa yule ambaye angepindua Babiloni na kuweka watu Wake huru naye akatabiri jinsi ngome za mto za Babiloni zingeshindwa. Waweza kusoma simulizi hilo kwenye Isaya 44:24–45:4.
Kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko chaeleza jinsi ahadi hiyo ilivyotimizwa: “Koreshi alikuwa hajazaliwa unabii ulipoandikwa. . . . Unabii huu ulitimia moja kwa moja kuanzia 539 K.W.K. Koreshi aligeuza maji ya Mto Frati kuwa ziwa lililofanyizwa na binadamu, malango ya mto ya Babuloni yaliachwa wazi kizembe wakati wa karamu ya mji huo, Babuloni ukaangushwa na Wamedi na Waajemi chini ya Koreshi. Baada ya hapo, Koreshi akawakomboa Wayahudi wahamishwa na kuwarudisha Yerusalemu pamoja na maagizo ya kujenga upya hekalu la Yehova huko.”a Kila ahadi kama hii iliyotolewa na Mungu, kila unabii ulio ndani ya Biblia, umetimia bila kukosea.
Kielelezo kingine cha unabii uliotimizwa ni uhakika wa kwamba tumaini limefifia katika karne yetu. Biblia ilitabiri hili kuwa kionyeshi cha wakati tunaoishi, kwa kuwa hiyo huuita muhula ulioanza na Vita ya Ulimwengu 1 katika 1914 “siku za mwisho” nayo husema zitakuwa ‘nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo.’ Ilijulisha kwamba katika siku zetu watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . . wenye kujitanguliza, wenye kiburi, . . . wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya asili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, . . . wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujitutumua kwa majivuno.” Ilitabiri hivi pia: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.” (2 Timotheo 3:1-4, 13, NW) Hilo ndilo tumeona katika wakati wetu.
Waweza kuitumaini Biblia kwa kuwa ni yenye uasilia kabisa. Hakuna mtu yeyote amepata kamwe kupinga kwa mafanikio uasilia wa Biblia. Mwanasayansi ajulikanaye sana Sir Isaac Newton alisema hivi: “Napata alama zaidi za hakika za uasilia katika Biblia kuliko historia yoyote ya kilimwengu.” Hakuna madanganyo kama yale ya orodha ya matukio ya Hilter hapa! Nayo Biblia hulinganikaje na maandishi mengine ya kale? The Bible From the Beginning chasema hivi: “Katika hati-kunjo kadhaa za kale zinazohakikisha usahihi wa uandishi, na katika miaka iliyopita kati ya zile za awali na zinazohakikisha usahihi wa hati-kunjo, Biblia ina manufaa iliyoamuliwa kupita maandishi ya Kigiriki na Kiroma ya kale [yale ya Homer, Plato, na wengine]. . . . Kwa ujumla hati-kunjo za Kigiriki na Kiroma ni chache tu zikilinganishwa na za Kibiblia. Hakuna kitabu chochote cha kale ambacho kimehakikishwa kama Biblia.” Kila kitu kuhusu Biblia huonyesha kwamba hiyo ni ya kweli kabisa.
Waweza kuitumaini Biblia kwa sababu hiyo ni sahihi kabisa katika taarifa zayo zote. Biblia husema kwamba Mungu “hutandaza kaskazi juu ya nafasi isiyo na kitu, na kuutundika ulimwengu pasipo kitu.” (Ayubu 26:7) Badala ya kurudia dhana za kimawazo tu zilizoenea sana siku hizo, kama vile dunia kuwa imetegemezwa na tembo, Biblia ilitaarifu kile ambacho hatimaye kimethibitishwa kuwa ukweli wa kisayansi—kwamba dunia ‘imetundikwa’ katika utupu. Kwa kuongezea hilo, zaidi ya miaka elfu mbili kabla ya wakati wa Columbus, Biblia ilitaarifu wazi kwamba dunia ni duara.—Isaya 40:22.
Waweza kuitumaini Biblia kwa sababu ya unyoofu na uwazi wayo. Waandishi wa Biblia hawakufanya chochote kiwe uwongo. Hata wakati ambapo kile walichosema kilionyesha ubaya wao wenyewe, ubaya wa wenzao, ubaya wa watawala wao, kwa unyoofu wao waliripoti mambo ya hakika. Kwa kielelezo, katika gospeli yake Mathayo alikiri waziwazi kwamba mitume wa Yesu Kristo nyakati fulani walikosa imani, wakapigania ukuu miongoni mwao, na hata kumwacha Yesu wakati aliposhikwa.—Mathayo 17:18-20; 20:20-28; 26:56.
Sababu nyingine yenye kutokeza ya kuitumaini Biblia ni kwamba shauri la Biblia sikuzote limethibitika kuwa lenye kutumika na lenye manufaa wakati wowote ambapo watu walilitumaini kiasi cha kulitumia. (Mithali 2:1-9) Shauri la Biblia juu ya kukabili matatizo ya maisha hutofautiana kwa njia yenye kutazamisha na shauri la wanaojiita “wataalamu” ambalo mara nyingi halina uthabiti. Kuhusu wanasafu wengi watoao shauri kama hilo katika magazeti mengi ya kitaifa ya habari, The Sunday Times la London lauliza: “Je, maelfu ya watu kila mwaka hueleza mawazo na hisia zao za ndani kabisa kwa wanasafu hawa ambao hutoa shauri bila kufikiri?” Waandikaji wa Biblia hawakuwa wakitoa mashauri bila kufikiri. Wao walirekodi shauri lenye kutumainika, lililopuliziwa na Mungu ambalo limethibitika kuwa lenye kutegemeka katika historia yote.—2 Timotheo 3:16, 17.
“Shauri la Biblia lilinilinda kutokana na mwendo ambao ungaliharibu maisha yangu,” asema Ellen, ambaye sasa yuko katika miaka ya 30 na katika ndoa yenye furaha. “Wazazi wangu ambao walikuwa wametalikiana, hawakuonyesha uaminifu-mshikamanifu sana katika mpango wa ndoa, nao hasa walinitia moyo niishi tu na mtu badala ya kufunga ndoa naye. Ninapofikiria juu ya uthabiti ambao kufuata kanuni za Biblia kumepatia maisha yangu, nafurahi kwamba niliitumaini Biblia hata zaidi ya shauri la wazazi wangu wenyewe.”—Ona Waefeso 5:22-31; Waebrania 13:4.
“Nilikuwa na umri wa miaka 14 tu nilipoanza kujifunza kile ilichosema Biblia kuhusu mambo,” asema Florence. “Sasa niwaziapo nyuma katika miaka ya 1960 na taabu ambayo marika wangu walijisababishia kwa kufuata viwango na maadili ya wakati huo, ninashukuru sana ulinzi ambao shauri la Biblia ulinipa nikiwa mwanamke mchanga, asiye na uzoefu.”—Ona 1 Wakorintho 6:9-11.
“Katika kisa changu,” asema James, “nilijihusisha na uchezaji kamari, uvutaji sigareti, na unywaji.” Yeye aendelea hivi: “Najua uharibifu ambao hili limesababisha kwa watu wengi mno na familia zao. Mwanzoni sikufahamu umaana wa Biblia kwa matatizo yangu. Lakini sasa naona waziwazi jinsi ilivyokuwa na uvutano kwa kufikiri kwangu kuzuri na kunisaidia kudumisha mtindo-maisha bora zaidi.”—Ona 2 Wakorintho 7:1.
Mary Anne alifikiria kujiua kwa sababu ya misongo ya maisha na magumu ya kihisia-moyo yaliyotokana na maisha ya mbeleni yenye matatizo. “Kujiua kulionekana kuwa suluhisho pekee kwa wakati huo,” yeye asema. “Lakini Biblia ilirekebisha kufikiri kwangu. Ilikuwa tu kwa sababu ya kile nilichosoma katika Biblia kwamba sikujiua.”—Ona Wafilipi 4:4-8.
Ni nini kilichowasaidia watu wote hao? Wao walikuza tumaini kamili katika Mungu na katika Neno lake, Biblia. Mungu akawa kama rafiki mpendwa mwenye kutumainiwa ambaye alinong’oneza shauri masikioni mwao wakati wa magumu. (Linganisha Isaya 30:21.) Wao walijifunza kanuni za Biblia ambazo ziliwasaidia kukabili misongo na matatizo ya maisha. Nao walijifunza kutumaini ahadi nzuri ajabu kutoka kwa Mungu ambaye hawezi kusema uwongo—ahadi kama ile ya “dunia mpya” yenye kupendeza isiyo na hila, uwongo, utumiaji kwa kujifaidi, na usio na huzuni, magonjwa, na hata kifo!—2 Petro 3:13; Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 21:4, 5.
Waweza kukuza tumaini lilo hilo. Ulimwengu leo waweza kuvunja tumaini lako, lakini waweza kuwa na uhakikisho kwamba tumaini lako katika Mungu na katika Neno lake halitavunjwa kamwe. Watangazaji wa gazeti hili watafurahi kupanga ili mtu akusaidie kumjua Mungu na Neno lake Biblia, vyema zaidi.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Miaka 200 hivi kimbele, nabii wa Mungu alitabiri jinsi Babiloni lingepinduliwa
[Picha katika ukurasa wa 9]
Sir Isaac Newton aliiona Biblia kuwa yenye kutumainika