Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Teketezo la Umati Sikuzote nilikuwa nimejiuliza ni kwa nini hakuna mtu aliyesema kwa ujasiri kuhusu lile Teketezo la Umati. Ule mfululizo “Lile Teketezo la Umati—Ni Nani Waliosema kwa Ujasiri?” (Agosti 22, 1995) ulijibu swali langu. Mashahidi wa Yehova walisema kwa ujasiri, nami naonea fahari Mashahidi wenzangu!
C. B., Marekani
Acheni mimi—nisiye mshiriki wenu—niwapongeze kwa kushughulikia habari ya Teketezo la Umati. Jinsi mlivyoshughulikia wonyesho huu mwovu wa hali ya kinyama ya mwanadamu kwa mwanadamu mwenzake ilinielimisha kiroho na kiakili zaidi ya zote ambazo nimepata kuona. Moyo mkuu wa Mashahidi wenzenu wakati huo ni jambo ambalo, kwa kuhuzunisha, ulimwengu haujui sana.
L. B., Uingereza
Baba yangu alipoteza uhai wake katika Sachsenhausen. Ndugu yangu mkubwa pia alipoteza uhai wake kutokana na kifungo cha Nazi. Bado nina kumbukumbu lililo dhahiri la mnyanyaso wa Nazi juu ya Mashahidi wa Yehova. Hivyo nimechochewa kuonyesha uthamini wangu kwa makala hizo. Pongezi!
F. D. J., Kanada
Nilipendezwa sana na hizo makala. Lakini sikubali kwamba Mashahidi wa Yehova ndio walikuwa tu “sauti moja katikati ya unyamavu.” Wakomunisti pia walionya watu dhidi ya Hitler kabla hajaanza kutawala. Wengi walijikuta katika kambi za mnyanyaso.
B. W., Ujerumani
“Amkeni!” hukubali haraka kwamba Hitler alikuwa na wapinzani wengi wa kisiasa. Hata hivyo, makala hizo zilirejezea hasa kushindwa kwa matengenezo ya kidini, ambayo mengi yayo yalishirikiana na utawala wa Nazi. Wanazi wenyewe waliwatambulisha Mashahidi wa Yehova kuwa wapingamizi wao wakuu wa kidini. Hivyo Mashahidi walikuwa kikundi cha kidini pekee kilichopewa alama yao wenyewe ya utambulishi katika kambi ya mateso—umbo la pembe tatu la zambarau lenye sifa mbaya.—MHARIRI.
Tetemeko la Dunia la Japani Nililia niliposoma ile makala “Msiba wa Ghafula wa Japani—Jinsi Watu Walivyoukabili.” (Agosti 22, 1995) Nilimpoteza dada yangu Mkristo mpendwa katika msiba wa tetemeko la dunia. Alikuwa mwenye bidii sana. Najua atafufuliwa nami nitaweza kumwona tena. Nashukuru sana kwa usaidizi wote wa kiroho na kimwili tuliopokea kutoka kutaniko na Sosaiti pia. Ingawa hivyo, bado mimi hulia, ninapofikiria yaliyotokea siku hiyo.
T. M., Japani
Hatua iliyopangwa vizuri na kuchukuliwa haraka na Mashahidi ilinishangaza kabisa. Niliposoma ujumbe wenye kujali kutoka ndugu katika kutaniko la Korea, niliendelea kulia tu. Nilifurahi kuwazia kwamba nimo katika tengenezo hilo lenye kuonyesha shauku.
M. K., Japani
Kuudhiwa Kingono Asanteni kwa makala yenu “Vijana Huuliza . . . Kuudhiwa Kingono—Naweza Kujilindaje?” (Agosti 22, 1995) Nina umri wa miaka 17, nami nilikutana na mvulana asiye Mkristo shuleni. Nilimtumaini, lakini baadaye yeye na rafiki zake waliniudhi kwa madokezo na vitisho vya ukosefu wa adili. Ilinibidi niache shule hiyo ili nitoke katika hali hiyo. Nilijifunza mengi kutokana na makala hii. Sasa najua la kufanya kuhusu jinsi ya kushughulika na mtu wa jinsia tofauti.
T. G., Ureno
Niliudhiwa kingono na kutishwa na mfanyakazi mwenzangu. Kwa kuwa nilitendwa vibaya nikiwa mtoto, mara nyingi mimi huona vigumu kujitetea. Hata hivyo, kwa kurudiarudia nilimwambia aniache. Mwishowe nilimripoti kwa waajiri wetu, kisha akaniacha. Nathamini makala hiyo kwelikweli. Wanawake wanahitaji kujua jinsi ya kushughulikia tatizo hili.
V. A., Marekani