Uthibitisho Uonekanao wa Yale Maangamizo
UNAPOINGIA MAHALI PANAPOONYESHA HALI iliyo mbaya kabisa ya kibinadamu, yaonekana kuwa ajabu sana kupata maneno haya yanayotoka katika Biblia Takatifu yakiwa yamechongwa kwenye jiwe: “Ninyi ni Mashahidi Wangu.” Lakini, labda hapa ndipo mahali pafaapo pa kuweka nukuu ya Biblia, angalau mstari huo hasa.—Isaya 43:10.
Jumba la Hifadhi ya Ukumbusho wa Maangamizo la United States katika Washington, D.C., lililozinduliwa mnamo Aprili 22, 1993, ni ukumbusho halisi na wenye uzito wa tekinolojia iliyopinduliwa na viongozi wasio na adili kuwa mashine ya kifo isiyo na kifani. Orodha ya watu wasio na kinga waliouawa na ukatili wa Nazi yahofisha sana—Wayahudi wapatao milioni sita na mamilioni ya watu wengine, kutia ndani Wapolandi, Waslavi, Mashahidi wa Yehova, Wajipsi, wagoni wa jinsia-moja, na watu wasiojiweza.
Matembezi Yenye Kukumbukwa
Matembezi hayo yaanza katika lifti ya rangi ya kijivu yenye baridi kidogo inayokuchukua kutoka Jumba la Ushahidi lililoko katika orofa ya kwanza hadi kwenda orofa ya nne. Kutoka huko, wageni wanaposhuka kuelekea orofa za chini, wao wapita vithibitisho vya kila aina ya yale Maangamizo, kutokea propaganda za Nazi hadi kuanza kutawala kwa Hitler, kushikwa kwa watu hadi kukombolewa kutoka kambi za kifo. Matembezi hayo yafika ndani ya Jumba la Ukumbusho, ambamo kuna moto uwakao milele. Ushuhuda wa watu waliojionea wenyewe, sinema za picha na zenye kusonga, muziki na michoro—zote zatumiwa kusaidia kueleza simulizi hilo lenye kuogofya sana.
Wageni washuhudia sehemu tatu za vithibitisho vyenye kudumu vyenye kuhuzunisha sana na vyenye kuamsha hisia sana. Vithibitisho vingine vyenye kusikitisha sana vimefichwa nyuma ya kuta zenye faragha zenye kimo cha meta moja na nusu, ambazo ni ndefu mno kwa watoto kuweza kutazama.
Jumba la Hifadhi la Kuelimisha
Taasisi ya Utafiti wa Maangamizo ya jumba hilo la hifadhi latia ndani maktaba kubwa na hati nyingi za kihistoria. Itatumika pia ikiwa kituo cha kimataifa kwa masomo ya yale Maangamizo. “Tumejitoa kufundisha na kuelimisha umma,” asema Dakt. Elizabeth Koenig, mkurugenzi wa Maktaba ya Jumba la Hifadhi. Maktaba hiyo itakuwa na habari juu ya baadhi ya vikundi vidogo vya watu vilivyokuwa katika kambi za mateso. “Tayari tuna habari nyingi juu ya Mashahidi wa Yehova,” yeye asema.
Katika 1933, Hitler alianzisha kampeni ya kuangamiza Mashahidi wa Yehova. Maelfu ya Mashahidi—kutoka Ujerumani, Austria, Polandi, ile iliyokuwa Chekoslovakia, Uholanzi, Ufaransa, na nchi nyinginezo—walipelekwa kwenda kambi za mateso. Wao walinyanyaswa kwa msingi wa kidini tu. Wawili kati ya wale waliookoka kambi hizo walialikwa katika kufunguliwa kwa jumba hilo la hifadhi.
Waokokaji wa Yale Maangamizo
Mwokokaji mmoja, Franz Wohlfahrt, mwenye miaka 73, aliona jumla ya washiriki 15 wa familia wa karibu zaidi na watu wa ukoo wakishikwa kwa sababu walikuwa Mashahidi. “Saba kati yao waliuawa, wengi wao kwa kukatwa vichwa. Mmoja aliuawa kwa gesi, na wengine wakafa katika kambi za mateso na magereza ya [polisi] wa Gestapo,” yeye asimulia.
Je! alikuwa akifikiria kama kweli angeokoka kambi hizo? “Nilikuwa nina shaka sana,” asema Franz. “Karibu kila siku walinzi walinikumbusha kwamba iwapo Ujerumani itashindwa katika vita, bado wangebaki na silaha za kutosha kuniua.”
Je! anasikitika kwamba alikuwa amekuwa mfungwa kwa ajili ya itikadi zake za kidini? “La! La!” asema Franz, kana kwamba wazo hilo lilikuwa madharau kwa azimio lake. “Kila wakati tulikuwa wenye furaha. Mara nyingi nilikuwa nikisimamishwa na walinzi ambao wangeuliza hivi: ‘Ijapokuwa huzuni hii yote, ungali unatabasamu? Ni nini mbaya na wewe?’ Nilikuwa nikijibu: ‘Nina sababu ya kutabasamu kwa sababu tuna tumaini linalopita wakati huu mgumu—tumaini katika Ufalme wa Mungu wakati ambapo kila kitu kitarudishwa kwa uzuri wacho na kila kitu kifanywe kiwe kizuri kwa ajili ya mambo yale ambayo ni lazima tupitie leo.’”
Joseph Schoen, aliyezaliwa katika 1910, alikuwa na shughuli nyingi katika kazi ya kuchapa na kugawanya vichapo vya Biblia katika Austria, kila wakati akiepa polisi wa Gestapo—mpaka 1940, walipomshika. Kutokea 1943 hadi 1945, alitishwa kwa kifo nyakati zote. Katika 1943 mkuu wa kambi hiyo ya mateso, wakiwa mbele ya watu wote waliokusanyika, alimwelekezea fikira Joseph na kumpigia kelele akisema, “Bado washikana na yule Mungu Yehova?”
“Naam,” akajibu Joseph.
“Basi utakatwa kichwa!”
Mwaka wa 1945 ulimpata Joseph akiwa katika ule msafara wa kifo kwenda Dachau. “Kimwili, nilikuwa nimedhoofika sana,” yeye akumbuka. “Lakini sikuwa nimepata kuwa na imani yenye nguvu zaidi kama ile niliyokuwa nayo katika msafara huo wa kifo.”[6b]
Sasa, akitembelea jumba hilo la hifadhi na akikumbuka siku zake akiwa mfungwa, yeye asema: “Wakati huo sikuogopa kamwe. Yehova hukupa kile unachohitaji, wakati unapokihitaji. Ni lazima ujifunze jinsi ya kumtegemea Yehova na kuona jinsi alivyo halisi wakati mambo yanapokuwa mabaya zaidi. Sifa zote zamwendea. Hakuna mtu yeyote kati yetu aliyekuwa shujaa. Sisi tulimtegemea Yehova tu.”[6c]
Thamani ya Jumba Hilo la Hifadhi
“Nafikiri jumba hilo la hifadhi lina umuhimu mkubwa sana,” asema mwanahistoria Dakt. Christine Elizabeth King, kaimu-msimamizi wa Chuo Kikuu cha Staffordshire katika Uingereza. “Kwanza kabisa, hilo ndilo rekodi [ya mambo yaliyotukia]. Na lipo ili kupinga wale wanaosema: ‘Hayo [yale maangamizo] hayakutokea kamwe.’ Kuna ushuhuda mwingi sana, na vilevile kuna wale walio hai walioushuhudia ambao waliokoka yale Maangamizo. Pili, jumba hilo la hifadhi ni chombo bora kabisa cha kufundisha.”[7]
“Kwa habari ya Mashahidi wa Yehova,” yeye aendelea kusema, “ni jambo la maana kwao kuweza kuona ndugu na dada zao waliokuwa wameumia na waliokuwa wamekufa na ambao walikuwa wametoa uhai wao. Kuona kwamba mambo hayo yalirekodiwa ni jambo la kipekee sana.”[7a]
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
Andiko kwenye ukuta lasema hivi:
“MASHAHIDI WA YEHOVA”
“Mnyanyaso wa Nazi kwa Mashahidi wa Yehova ulianza katika 1933. Kwa sababu walikataa utumishi wa kijeshi na kukataa kuapa utii kwa utawala huo, mara nyingi Mashahidi walishtakiwa kwa vitendo vya ujasusi na hila dhidi ya taifa. Wanazi waliona matabiri ya Mashahidi juu ya mvurugo wa wakati ujao wa ulimwengu kuwa tisho la kimapinduzi, na unabii wao mbalimbali kuhusu kurudi kwa Wayahudi Palestina, kuwa taarifa za [Kiyahudi].
“Hata hivyo, Mashahidi waliendelea kukutana, kuhubiri, na kugawanya fasihi. Walipoteza kazi zao, malipo yao ya kustaafu, na haki zote za kibinadamu, na kuanzia 1937 walipelekwa katika kambi za mateso. Huko, Wanazi waliwaita ‘wafungwa wa hiari’: Mashahidi wa Yehova waliokana itikadi zao wangeweza kuachiliwa. Hakuna hata mmoja aliyekana imani yake.”
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
“Ni Simulizi la Maana Kusimuliwa”
“Mashahidi wa Yehova ni moja ya masimulizi yenye kutokeza sana. Kwa sababu ya itikadi zao za kidini, walikuwa mojawapo dini za kwanza kupigwa marufuku . . . na serikali ya Ujerumani ya Nazi katika 1933. Hilo lilitukia kwa sababu tu waliona ibada yao na wajibu wao uwe kwa sheria iliyo juu zaidi, sheria ya Mungu. Kama tokeo, walinyanyaswa kikatili kama vile Wayahudi na Wajipsi na kuwekwa katika kambi za mateso ambamo wengi wao walikufa.
“Ni simulizi la maana la kusimuliwa. Labda jambo lenye kusikitisha zaidi [lilikuwa] lile la watoto wa Mashahidi wa Yehova. Baba yao alipolazimika kupelekwa katika kambi ya mateso na mama yao kushikwa, wangewekwa katika mstari wa nyuma shuleni, wakiwa pamoja na watoto wa Kiyahudi na Wajipsi. Watoto hao walipokataa kusema salamu ya ‘Heil Hitler!’ au kukataa kuabudu Taifa la Nazi kwa njia yoyote nyingine, walionwa kuwa watoto wahalifu kwa ajili tu ya itikadi zao. Na watoto hao, bila shaka hawakulipia tu uhalifu bandia na wa kuwaziwa tu wa wazazi wao, ambao ulikuwa uhalifu unaohusu dhamiri, bali pia walilipia jambo la kwamba walikuwa watoto wao [wa Mashahidi].”—Dakt. Sybil Milton, mwanahistoria mkuu wa jumba hilo la hifadhi.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Koti za kambi za mateso zenye beji za pembetatu za rangi ya zambarau zilitambulisha Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 17]
Waokokaji wa yale Maangamizo Franz Wohlfahrt (kushoto) na Joseph Schoen wakiwa na mwanahistoria Dakt. Christine King katika kithibitisho cha “Waliodhulumiwa”
[Picha katika ukurasa wa 17]
Magari yafananayo na hili yaliwapeleka Wohlfahrt na Schoen kwenye kambi za mateso
[Picha katika ukurasa wa 18]
Juu: Waokokaji Wohlfahrt (kushoto) na Schoen wakiwa katika wonyesho wa vidio ya historia juu ya “Adui za Taifa” unaotia ndani Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 18]
Chini: Maria na Franz Wohlfahrt wakiwa kwenye kithibitisho kinachotia ndani Biblia ya Johann Stossier, ndugu ya Maria. “Kwa njia fulani Johann aliificha Biblia hiyo kwa muda mrefu kabla igunduliwe,” asema Franz. “Biblia hiyo ilikuwa ndicho kitu chake pekee kilichorudishwa kwa mama yake baada ya kuuawa kwake”[10]
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kando ya Biblia hiyo inayoonyeshwa, andiko lasema hivi: “Biblia hii ilikuwa ya Johann Stossier, Shahidi wa Yehova aliyefungwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen. Stossier alikufa muda mfupi kabla ya majeshi ya Sovieti kukomboa kambi hiyo”[11]
[Picha katika ukurasa wa 19]
“Ulinzi wa ustaarabu ni dhaifu kama nini,” akasema Rais wa U.S. Clinton wakati wa kuwekwa wakfu kwa jumba hilo la hifadhi. “Yale Maangamizo yatukumbusha milele kwamba ujuzi bila kanuni zifaazo zaweza kuongeza tu hofu kuu ya binadamu, kwamba kichwa bila moyo si ubinadamu”