Jumba la Hifadhi ya Uangamizo na Mashahidi wa Yehova
UTAWALA mkatili wa Nazi uliangamiza mamilioni ya watu, hasa Wayahudi na Waslavi. Hata hivyo, kikundi kimoja cha kidini—Mashahidi wa Yehova—kilikataa kwa umoja kujitiisha kwa utawala wa Nazi, si kwa sababu ya rangi au taifa, bali kwa sababu ya kushikamana na kanuni za Biblia kwa kudhamiria.—Yohana 17:14, 16.
Taifa la Nazi lilielekeza mnyanyaso mkatili juu ya Mashahidi wa Yehova—shambulizi kubwa sana dhidi yao. Kwa nini? Kwa sababu za kidini, Mashahidi walikataa kushiriki na kutumika katika Chama cha Wafanyakazi cha Ujerumani na kukataa kuapa kuwa Hitler ni Mwokozi. Kwa hiyo, Wanazi waliwapiga marufuku wakiwa tengenezo katika Aprili 1933. Wakishtakiwa kwa kuasi sheria ya kiraia na kidini, walikuwa miongoni mwa vikundi vya kwanza kutupwa katika kambi za mateso. “Hatimaye, mashahidi zaidi ya 30,000 walinyanyaswa na Wanazi,” yasema karatasi moja ya habari ya jumba la hifadhi.
Jumba la Hifadhi ya Ukumbusho wa Uangamizo la United States, lililopo katika Washington, D.C., limejitolea kueleza masimulizi ya vikundi vyote vilivyonyanyaswa na Wanazi, kutia ndani Mashahidi wa Yehova. Chanzo kimoja cha habari kinasema kwamba jumba hilo la hifadhi “lapaswa lipendeze hasa Waamerika na wageni wanaozuru wa dini za Kiyahudi na Mashahidi wa Yehova waliokuwa ndio shabaha kuu ya uangamizo wa utawala wa Hitler.” Kupitia vitu vya kale, hati, ushuhuda wa shahidi aliyejionea ulionaswa katika vidio, picha za kihistoria, na sinema, maono ya wakati wa vita ya vikundi kadhaa vilivyonyanyaswa vyote vinatiwa ndani katika sehemu za onyesho, maktaba, na mahali pa hati za jumba hilo la hifadhi. Jumba hilo limenasa katika vidio mahoji 74 ya Mashahidi wa Yehova walionyanyaswa na utawala wa Nazi. Jumba hilo lilifunguliwa kwa umma katika Aprili 1993.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]
Courtesy of United States Holocaust Memorial Museum