Upendo wa Kikristo Kati ya Misiba Katika Mexico
GAZETI moja la habari la Mexico City liliripoti hivi: “Kwa siku 20 zilizopita, msiba wa asili—vimbunga na tetemeko la dunia—umekumba pwani za Mexico ukiacha matokeo ya kifo na uharibifu.”—El Financiero, Oktoba 17, 1995.
Majimbo ya Mexico ya Campeche, Quintana Roo, na Tabasco yaliharibiwa vibaya mno na Kimbunga Opal mapema katika Oktoba. Watu karibu 200 waliuawa, zaidi ya 150 walijeruhiwa, 500,000 wakapata hasara, na maelfu ya nyumba yakaharibiwa nusu au kabisa.
Mara tu ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Mexico iliposikia juu ya uharibifu huo, mtu fulani alitumwa kuona jinsi Mashahidi walivyokuwa wakiendelea katika maeneo yaliyoathiriwa. Ilijulikana kwamba zaidi ya 2,500 kati yao walikuwa wamelazimika kuacha nyumba zao. Hawa walikaribishwa kwa fadhili katika nyumba za Mashahidi wenzao.
Vitovu vya kutuliza vilipangwa. Chakula, mavazi, na fedha ziliandaliwa kwa waliokuwa na uhitaji. Baada ya maji ya furiko kupwa, Mashahidi hao walianza kujenga upya nyumba za ndugu zao Wakristo.
Oktoba 9, tetemeko la dunia lenye nguvu sana lililokuwa na kiwango cha 7.6 kwenye kipimo cha Richter liliharibu majimbo ya Mexico ya Colima na Jalisco. Majumba ya Ufalme manane ya Mashahidi wa Yehova yaliharibiwa vibaya mno. Nyumba zao 12 ziliporomoka, na 65 hivi kuharibiwa. Kwa mara nyingine tena, halmashauri ya utulizaji ilipangwa, na msaada ukatolewa.
Kisha, Oktoba 20, tetemeko jingine la dunia likapiga, likitikisa jimbo la Chiapas. Nyumba za Mashahidi wengine 88 ziliharibiwa, na 38 kuharibiwa vibaya mno. Majumba ya Ufalme mawili yaliharibiwa kabisa, na mengine manne yakaharibiwa vibaya. Karibu wakati sawa na huo, mafuriko yaliyohusiana na Kimbunga Roxanne yaliharibu nyumba za Mashahidi 80 hivi katika jimbo la Veracruz. Nyumba nne ziliharibiwa kabisa. Hazina ya utulizaji iliyoanzishwa na Mashahidi wa Yehova pia iliandalia majeruhi hawa kwa haraka.
Ingawa Mashahidi fulani walichubuka na kuvunjika mifupa, hakuna aliyekufa katika misiba hii ya asili. Kwa ujumla, tani zipatazo 24 za chakula na tani 4 za mavazi zilipelekewa waliokuwa na uhitaji. Watazamaji wengi walipendezwa na kazi ya utulizaji. Mwanamke mmoja katika Colima alisema: “Nilikuwa nimesikia tu kwamba Mashahidi wa Yehova ni wenye muungano, lakini sasa naweza kuuona kwa macho yangu mwenyewe.”
Mara kwa mara watu walisema hivi kuhusu Mashahidi na kazi yao ya utulizaji: “Hawa kwa kweli ni ndugu.” “Ni kikundi kilichopangwa vizuri zaidi.” Wengine hata walisikika wakisema: “Ikiwa vikundi vyote vya kutuliza vilivyokuja kusaidia vingefanya kazi kama Mashahidi wa Yehova, mji wote ungekuwa safi tayari.”
Sasa zaidi ya Mashahidi 440,000 wanashiriki habari njema za Ufalme wa Mungu pamoja na Wamexico wenzao. Upendo waliodhihirishiana wakati wa misiba hii ya asili ulitoa ushahidi wenye nguvu sana.—Yohana 13:34, 35.