Ni Nani Anayepaswa Kuamua Ukubwa wa Familia?
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA BRAZILI
AKIWA ameishi kwa siku tatu tu, huyo mvulana aliachwa ndani ya mfuko wa plastiki katika stesheni ya gari-moshi la chini ya ardhi. Lakini gazeti moja la Brazili lilisema kwamba familia kadhaa zilijitolea kumwasilisha huyo mtoto.
Ingawa kisa kama hicho ni nadra kutokea, idadi ya watoto wasiotakikana na kutupwa inaongezeka ulimwenguni kote. Mara nyingi hakuna uzazi wenye kuchukua mambo kwa uzito. Je, suluhisho ni vizuia-mimba? Je, lingekuwa kosa kwa mtu kupanga ukubwa wa familia yake?
Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, karibu asilimia 50 za mimba hazijapangiwa. Mara nyingi mimba haipangiwi wala haitakikani.
engi hujaribu kuepuka mimba, labda kwa sababu za afya, nyumba, au matatizo ya kazi. Hivyo, njia za kuzuia mimba, kama vile vibonge vya kudhibiti uzazi au kondomu, ziko kwa wingi. Utoaji-mimba na kufunga uzazi pia hutumiwa kuwa njia za kudhibiti uzazi. Kuhusu utoaji-mimba katika Brazili, gazeti O Estado de S. Paulo laripoti: “Shirika la Afya Ulimwenguni lakadiria kwamba kila mwaka wanawake milioni 5 kati ya wale milioni 13 ambao hushika mimba katika Brazili huharibu mimba hizo kisiri.” Pia, gazeti Time liliripoti kwamba asilimia 71 ya wanawake wa Brazili wenye umri wa kuweza kuzaa wanaoishi na wenzi hudhibiti uzazi. Kati ya hao, asilimia 41 hutumia vibonge na asilimia 44 wamefungwa uzazi.
Uchunguzi mmoja waonyesha kwamba asilimia 75 ya Wabrazili hufikiri kwamba ni lazima kupanga idadi ya watoto. Wengine hukataa kupanga uzazi kwa sababu ya kuitikadi ajali au kwa sababu ya kufikiri kwamba ni mapenzi ya Mungu kwamba familia iwe na ‘watoto wengi kadiri Mungu anavyotoa.’ Ni nani anayepaswa kuamua ukubwa wa familia—je, ni wenzi wa ndoa au ni mapendezi ya kitaifa au ya kidini?
Kudhibiti Uzazi—Kwa Nini Ni Suala Lenye Kubishaniwa?
Ingawa linaruhusu njia ya kutofanya ngono wakati mwanamke anapoelekea kushika mimba, Kanisa Katoliki la Kiroma, ambalo ni dini kubwa zaidi katika Brazili, linakataa njia za kudhibiti uzazi, ziwe ni za kutoa mimba au la. Papa Paul 6 alisema hivi: “Kila tendo la kujamiiana ni lazima liruhusu kupitishwa kwa uhai.” Papa John Paul 2 alisema: “Vizuia-mimba, vikitazamwa vizuri, ni vya haramu sana hivi kwamba haviwezi kwa njia yoyote ile kuonwa kuwa halali.” Matokeo ni kwamba Wakatoliki wengi husita kudhibiti ukubwa wa familia yao, wakiona kutumia vizuia-mimba kuwa dhambi.
Kwa upande mwingine, jarida la kitiba Lancet latangaza hivi: “Mamilioni yataishi bila elimu, bila kazi, bila makao mazuri na bila mfikio wowote kwa vifaa vya msingi vya afya, bila utumishi wa kijamii na wa kuondoa taka, na ongezeko lisilodhibitiwa la watu ndilo kisababishi kikubwa cha mambo hayo.” Kwa sababu hiyo, zikihofu kuwa na idadi nyingi kupita kiasi na umaskini, serikali fulani zinapendekeza kupanga familia, japo mateto ya kanisa. Kwa kielelezo, “Kosta Rika ilipunguza wastani wa idadi ya watoto [katika kila familia] kutoka 7 hadi 3,” asema mwanabiolojia Paul Ehrlich.
Kichapo cha UM Facts for Life—A Communication Challenge chasema: “Baada ya mwanamke kuzaa watoto wanne, mimba zifuatazo huhatarisha zaidi uhai na afya za mama na mtoto. Hasa ikiwa mimba za awali zilifuatana-fuatana kwa muda upunguao miaka miwili-miwili, mwili wa mwanamke waweza kuchoka kwa urahisi kwa mfululizo wa mimba, kuzaa, kunyonyesha, na kutunza watoto wadogo.”
Kungali kuna familia nyingi zilizo kubwa ambamo vitoto vichanga hufa kwa wingi, hasa katika maeneo ya mashambani ya Afrika, Asia, na Amerika ya Latini. Kwa nini? Wengi hawafahamu njia za kuzuia mimba. Kisababishi kimoja katika maeneo fulani chaweza kuwa kwamba, kama mtunga-sheria mmoja alivyosema, “mwanamume angali anajiona kuwa mwanamume halisi ikiwa tu mke wake anapata mimba kila mwaka.” Gazeti Jornal da Tarde lataja jambo jingine liwezalo kuchangia jambo hilo, hasa kutokana na maoni ya mwanamke: “Watoto ni vyanzo vyao vilivyo nadra vya furaha nao huwapa hisia za kwamba wametimiza kitu.” Pia, Paulo Nogueira Neto, aliyekuwa zamani katibu wa mazingira katika Brazili, alisema hivi: “Mtoto ndiye usalama wa kijamii wa walio maskini.”
Kile Ambacho Biblia Yasema
Je, ulijua kwamba Neno la Mungu, Biblia, huachia mume na mke jukumu la kuamua ukubwa wa familia yao? Pia yaonyesha kwamba ndoa inafaa, ama kwa uzazi ama kwa kuonyeshana upendo kwa ngono yenye staha.—1 Wakorintho 7:3-5; Waebrania 13:4.
Lakini, je, Mungu hakuwaambia Adamu na Hawa katika Paradiso ‘wazaane, wakaongezeke, wakaijaze nchi’? (Mwanzo 1:28) Ndiyo, lakini hakuna jambo katika Biblia linaloonyesha kwamba sisi tumo chini ya amri hiyo leo. Mwandikaji Ricardo Lezcano alisema hivi: “Laonekana kuwa jambo la kujipinga kutumia sheria ile moja iliyotumika kwa wanadamu wawili tu wa dunia kwa [mabilioni ya] wanadamu.” Hata ikiwa uamuzi ni kutozaa kamwe, hilo ni chaguo la kibinafsi ambalo lapaswa kuheshimiwa.
Kwa kupendeza, New Catholic Encyclopedia yasema kwamba maoni ya Mashahidi wa Yehova yanategemea Biblia. Hiyo yasema: “Ila tu kwa habari ya kudhibiti uzazi, jambo ambalo wao huachia wenzi wa ndoa wenyewe waamue, maadili yao ya ngono ni thabiti sana.” Nayo yaongezea hivi: “Wao huona Biblia kuwa chanzo chao cha pekee cha itikadi na cha kanuni ya mwenendo.”
Je, njia zote za kudhibiti ukubwa wa familia ni halali? La. Kwa kuwa uhai ni mtakatifu, Sheria ya Mungu kwa Israeli iliamuru kwamba mtu ambaye alisababisha mimba itoke alipaswa kuonwa kama muuaji kimakusudi. (Kutoka 20:13; 21:22, 23) Kuhusu kuondolewa uwezo wa kuzaa, kama vile kukatwa kwa mrija wa shahawa, uamuzi unategemea dhamiri ya mtu binafsi, kwa kuwa jambo hilo halitajwi moja kwa moja katika Biblia. “Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5)a Na kwa kuwa kuna njia kadhaa za kudhibiti uzazi, mwongozo wa kitiba waweza kusaidia wenzi waamue iwapo wanataka kutumia njia fulani au hapana.
Fanya Maamuzi Ambayo Unaweza Kuishi Kupatana Nayo
Si kila kitu maishani kinaweza kupangiwa. Lakini, je, ungeweza kununua gari au nyumba bila kufikiria kwa uzito mambo yanayohusika? Gari ama nyumba yaweza kuuzwa tena, lakini watoto hawawezi. Basi, wanapopanga mimba, je, uwezo wa mume na mke wa kumwandalia mtoto mahitaji ya maisha haupasi kufikiriwa?
Hakika, hatutaki familia yetu ikose lishe, wala hatutaki kuwa mzigo wa kulemea wengine. (1 Timotheo 5:8) Kwa wakati uo huo, mbali na chakula na makao, watoto wanahitaji elimu, maadili, na upendo.
Kwa kuongezea kupanga kile kinachohitajika kwa habari ya kazi, fedha, na subira, afya ya mke ni lazima ifikiriwe. Kupanga mimba kwa hekima ili zisiwe karibu-karibu huokoa uhai na kuendeleza afya njema. Facts for Life chasema: “Mojayapo njia zenye matokeo zaidi za kupunguza hatari za mimba na kuzaa kwa mama na kwa mtoto ni kupanga vizuri mimba zisiwe karibu-karibu. Hatari za kuzaa ni kubwa zaidi ikiwa mwenye kutarajia kuzaa ni mwenye umri wa chini ya miaka 18 au ana umri unaozidi miaka 35, au amepata kuwa na mimba nne au zaidi, au wakati pengo ni dogo kuliko miaka miwili tangu azae mara ya mwisho.”
Wenzi wa ndoa wanaofikiri kuhusu kuwa na watoto wanapaswa kukumbuka kwamba, kama Biblia ilivyotabiri, tumezingirwa na ulimwengu uliojaa uhalifu, njaa kuu, vita, na uchumi dhaifu. (Mathayo 24:3-12; 2 Timotheo 3:1-5, 13; Ufunuo 6:5, 6) Upendo wa kweli kwa watoto utawasaidia wenzi wa ndoa waone mambo kihalisi kuhusu ulimwengu tunamoishi, wakitambua kwamba ni vigumu kulea watoto katika wakati wetu. Hivyo, badala ya kuachilia tu mambo na kuzaa watoto wengi iwezekanavyo wakitumaini kwamba mambo yote yatakuwa shwari, wengi hupendelea kuamua ukubwa wa familia zao ili watoto wao wafurahie kadiri fulani ya furaha na usalama.
Mbali na kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima kwa masuala ya familia, Neno la Mungu latupa tumaini thabiti kwa wakati ujao. Biblia inaonyesha kwamba ni kusudi la Muumba kwa wanadamu kuishi milele katika amani na furaha kwenye dunia iliyo paradiso. Ili kutimiza jambo hilo, karibuni Mungu atamaliza mfumo huu mwovu wa mambo. Kisha, katika ulimwengu mpya wenye uadilifu usio na umaskini na idadi kubwa ya watu yenye kupita kiasi, watoto hawatatupwa tena eti kwa sababu hawatakikani.—Isaya 45:18; 65:17, 20-25; Mathayo 6:9, 10.
Kwa wazi, ufikirio kwa kila mmoja na kwa watoto, pamoja na maoni yenye usawaziko kuhusu kuzaa, utasaidia wenzi wa ndoa kuamua ukubwa wa familia zao. Badala ya kuachilia tu mambo, wao wapaswa kutafuta mwongozo wa Mungu kupitia sala. “Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—Mithali 10:22.
[Maelezo ya Chini]
[Picha katika ukurasa wa 12]
Mamilioni ya watoto hutupwa
[Picha katika ukurasa wa 13]
Watoto wanahitaji utunzi wenye upendo