Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Linda Watoto Wako Nilikutana na mwanamke mmoja kijana ambaye amewapa makao watoto waliotendwa vibaya kingono. Nilimtolea toleo la Oktoba 8, 1993, lililokuwa na mfululizo wa makala zenye kichwa “Linda Watoto Wako!” Nilipomtembelea tena, alisema: “Makala hizi zimenisaidia kukabiliana na hali hii mpya. Nilichukua hilo gazeti nilipokuwa na miadi ya kufika mahakama ya watoto na nililionyesha kwa kiongozi wa mashtaka. Yeye, na vilevile hakimu, walivutiwa na hizo makala wakataka kuzigawanya miongoni mwa mawakili wale wengine.” Mwanamke huyo kijana aliomba fasihi zaidi na sasa anajifunza Biblia pamoja nasi.
E. T. V., Brazili
Maradhi Yenye Kuua Asanteni kwa ule mfululizo wenye mambo mengi, wenye kueleweka na ulio sahihi juu ya “Maradhi Yenye Kuua—Vita Kati ya Mwanadamu na Vijiumbe-Maradhi.” (Februari 22, 1996) Sikung’amua kamwe utata mkubwa sana wa vijiumbe-maradhi na jinsi viwezavyo kudhuru kimwili.
C. L., Marekani
Gazeti hilo lilifika wakati barabara kabisa, kwa kuwa nilikuwa nimepatwa na nimonia nilipaswa nitumie viuavijasumu. Makala hizo zilinisaidia kuelewa ni kwa nini nilijihisi vibaya zaidi badala ya kuhisi nafuu baada ya kutumia dawa kwanza. Ninashukuru sana kwa habari hii, ambayo ilitolewa kwa njia iliyo rahisi kueleweka.
I. W., Ujerumani
EthiopiaBaada ya kusoma makala juu ya “Ethiopia Yenye Kupendeza” (Februari 22, 1996), moyo wangu umejawa na shukrani. Nina watu wengi wa ukoo Waethiopia ambao si Mashahidi wa Yehova. Makala hii ilikuwa nzuri sana hivi kwamba nina uhakika kwamba itaamsha kupendezwa kwao katika kujifunza juu ya Mungu wetu mkuu, Yehova.
J. R., Luxembourg
Geisha wa Zamani Niliguswa moyo sana na ile makala “Mtoto wa Chura.” (Februari 22, 1996) Kwa sababu ya uvutano wa mama yangu, nilisomea baleti bora tangu nilipokuwa mdogo sana. Nilipopata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, niliamua kuacha baleti, ijapokuwa niliipenda sana. Makala hii imenitia moyo. Ilinisaidia kuona kwamba kuna Wakristo wengine ambao wamefanya dhabihu kama hizo. Nawashukuru kwa moyo wangu wote.
Y. S., Japani
Sikuweza kujizuia kulia machozi nilipoangalia picha ya Sawako Takahashi akiwa na familia yake ya kitheokrasi, yenye furaha. Mateso yaliyonipata katika wakati uliopita yalikuwa yametawala maisha yangu kwa muda mrefu, na hali ya kujihisi kuonewa imeniletea huzuni kuu. Kung’amua kwamba Yehova atanisamehe kupungukiwa kwangu kwa wakati uliopita kumenipa moyo mkuu wa kujitahidi kuelekea kuwa Mkristo aliyebatizwa.
M. K., Japani
Hicho kilikuwa mojawapo visa vyenye kuarifu na vyenye kupendeza zaidi nilivyopata kuvisoma. Kilinisaidia kuelewa pia kinachotiwa ndani katika ibada ya wazazi wa kale. Sijaweza kamwe kufahamu namna hii ya ibada mpaka niliposoma habari hizi za maisha ya mtu huyo.
P. Y., Marekani