Maoni ya Biblia
Unaweza Kutumaini Uongozi wa Nani?
“NI WAKATI wa kwenda!” baba amwambia mwana wake mwenye umri wa miaka mitano. Baba anyoosha mkono, na bila kusita mwana huyo anyoosha na kuviringisha mkono wake mdogo katika vidole vya baba yake. Bila kujali safari yaelekea wapi, mtoto huyo autumaini uongozi wa mzazi wake na aufuata akiwa na uhakika. Lolote litakalotokea, mtoto aendelea kushika kwa imara.
Kwa vile tunaishi katika siku zisizo na uhakika wa kiuchumi, kisiasa na kibinafsi, je, usingekaribisha mkono wenye kuongoza kutoka chanzo ambacho ungekitumaini kabisa? Lakini twaishi katika nyakati ambazo watu wasio wanyoofu hutumia vibaya watu wasio na uzoefu. Hivyo, kuna sababu ya kweli ya kuwa wenye tahadhari kwa mtu tumwaminiye. Katika nyakati za nyuma, labda ulitamaushwa kabisa ulipotegemea mtu fulani kwa uongozi lakini akakutamausha.
Hata hivyo, Biblia yatutia moyo kuweka tumaini letu katika Mungu. “Kwa maana mimi, BWANA, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope, mimi nitakusaidia,” alirekodi nabii Isaya. (Isaya 41:13) Na mtume Petro alishauri: “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”—1 Petro 5:6, 7.
Hata hivyo, kwa haki waweza kuuliza, ‘Nina sababu gani kuweka tumaini langu katika Mungu kwa ajili ya uongozi?’ Sababu thabiti zifuatazo zinapatikana katika rekodi ya Waisraeli wa kale.
Mkono wa Yehova Waongoza Watu Wake
Mfululizo wa matukio ambayo yalifikia upeo katika Nisani 14, 1513 K.W.K., yalivunja azimio la Farao mkatili na mwenye kupiga ubwana na la Wamisri, hivi kwamba waliwaachilia watu wa Mungu, Waisraeli, kutoka utumwani. (Kutoka 1:11-13; 12:29-32) Katika Nisani 15, taifa la Israeli lenye shangwe lilielekea jangwani likiwa njiani kwenda Bara Lililoahidiwa. Njia ya moja kwa moja zaidi ilikuwa ile yenye kuelekea kaskazini ya Nofu, kando-kando ya pwani ya Mediterania, karibu na bara lililokaliwa na Wafilisti walioogopwa, na kuingia katika Bara Lililoahidiwa. Hata hivyo, Mungu alifikiria njia nyingine.—Kutoka 13:17, 18; Hesabu 33:1-6.
Kwa taifa la kale Israeli, Mungu aliandaa uongozi wenye kuonekana, ambao ulitokea kama nguzo ya wingu wakati wa mchana na nguzo ya moto wakati wa usiku. (Kutoka 13:21, 22) Pamoja na tukio hilo la ajabu linalozidi uwezo wa mwanadamu, Yehova alimtumia mwakilishi wake wa kidunia, Musa mwaminifu. (Kutoka 4:28-31) Basi, wakati huo kulikuwa na uthibitisho wa wazi kabisa kwamba mkono wa Mungu ulikuwa unawaongoza Waisraeli.
Katika kambi yao ya pili, Ethamu “kwenye mpaka wa ile jangwa,” Yehova alimwelekeza Musa arudi nyuma na kupiga kambi katika pwani ya Bahari Nyekundu katika Pi-hahirothi. (Kutoka 13:20) Hatua hii isiyoweza kuelezeka ilimchochea Farao kufikia mkataa kwamba Waisraeli “wametatanishwa katika nchi.” Akipata ujasiri, Farao akabadili maoni yake. Sasa akiwa ameazimia kuwafanya Waisraeli watumwa tena, alikusanya jeshi lake akaanza kuwafuata.—Kutoka 14:1-9.
Kwa kulipeleka taifa hilo katika njia nyingine katika lile ambalo kwa wazi lilikuwa bonde linaloelekea Bahari Nyekundu, ilionekana Musa alikuwa anawaweka Waisraeli katika mtego katikati ya milima iliyokuwa pande mbili za kambi ya Pi-hahirothi, Bahari Nyekundu na jeshi la Farao linalosonga mbele. Ilionekana kwamba Waisraeli walikuwa wamekuwa katika hali rahisi ya kushindwa au kuangamizwa.
Hili lilikuwa na matokeo gani kwao? Je, wao wangeonyesha tumaini lao kwa uongozi wa Yehova? Ilionekana kana kwamba hakukuwa na matumaini. Hivyo basi, wengine wakawa na wasiwasi. Na bado wengine walianza kunung’unika dhidi ya Musa. Baadhi yao walikuwa hata tayari kujisalimisha na kurudi kwa utumwa wa Kimisri.—Kutoka 14:10-12.
Shika kwa Imara Mkono wa Mungu!
Katika hali hii Waisraeli walihitaji kuonyesha tumaini kama la mtoto kwa Mweza Yote. Taifa lote kwa ujumla halikujua kwamba Yehova alikuwa na sababu nzuri ya kumwelekeza Musa kuvuka Bahari Nyekundu katika Pi-hahirothi. Kwa kuanzisha safari ya Waisraeli ya kuingia Bara Lililoahidiwa kupitia kusini mwa bara la Wafilisti, Yehova alionyesha ufahamu wa kina wenye upendo. Baada ya kuwa Misri kwa miaka 215, hakukuwa na shaka kwamba Waisraeli hawakuwa wamejitayarisha kwa vita na taifa lenye wanajeshi wakali. Hivyo basi, Yehova alichagua njia ambayo ingeepusha pambano kama hilo.a—Kutoka 13:17, 18.
Kuokolewa kwa taifa hilo na kushindwa kwa Farao na jeshi lake katika Bahari Nyekundu kwatoa uthibitisho wa ajabu katika uwezo wa Mungu wa kuokoa. Na zaidi, Waisraeli walikuwa wenye shukrani kama nini, na ingawa hawakujua sababu ya Mungu kuwaongoza katika njia fulani hususa, hawakuacha mkono wa Mungu! Walishikamana kwa imara na kuona miujiza ya kugawanyika kwa Bahari Nyekundu na pia kuangamizwa kwa maadui wao. Tumaini lao kwa uongozi wa Yehova lilithawabishwa.—Kutoka 14:19-31.
Tena wacha turudie mfano wa mtoto anayeshika mkono wa mzazi wake. Mtoto awapo na wasiwasi, yeye hufanyaje? Badala ya kuacha au kupunguza mshiko wake, mtoto huyo atakaza mkono wake mdogo katika vidole vya mzazi wake. Kwa kufanya hivyo, aonyesha tumaini lake lisiloyumba-yumba kwamba mzazi huyo ataandaa uongozi usioshindwa na nguvu katika magumu.
Hali kadhalika, tupatapo mikazo katika maisha yetu, twapaswa kukaza mshiko wetu, tukitumaini hata zaidi katika uongozi wa Mungu! Neno lake, Biblia, laweza kuwa nuru ya kutuongoza. (Zaburi 119:105) Pia, kumbuka kwamba pamoja na tumaini huja subira. Kwa sababu hiyo, twapaswa kumpa Yehova wakati ili asuluhishe matatizo, hata ikiwa kwa kipindi fulani cha wakati hatuwezi kuelewa sana kwa nini anatuongoza katika njia fulani. Naam, twaweza kutumaini uongozi wa Mungu.—Kutoka 15:2, 6; Kumbukumbu la Torati 13:4; Isaya 41:13.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu Pi-hahirothi, ona Insight on the Scriptures, Buku 2, kurasa 638-639, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.