SOMO LA 22
Muujiza Katika Bahari Nyekundu
Muda mfupi tu baada ya kusikia kwamba Waisraeli wameondoka Misri, Farao alibadili mawazo yake kuhusu kuwaruhusu waondoke. Aliwaamuru hivi mashujaa wake wa vita: ‘Tayarisheni magari ya vita ili tuwafuate! Hatukupaswa kuwaruhusu waondoke.’ Farao na wanaume wake wakaanza kuwafuata Waisraeli.
Yehova alikuwa akiwaongoza watu wake kupitia wingu wakati wa mchana na nguzo ya moto wakati wa usiku. Aliwaongoza hadi kufikia Bahari Nyekundu, na kuwaambia wapige kambi.
Kisha Waisraeli wakaona Farao na jeshi lake wakiwafuatilia. Walijikuta wakiwa wamenaswa kati ya bahari na jeshi la Wamisri. Wakaanza kumlilia Musa na kusema, ‘Tutakufa! Ni bora ungetuacha Misri.’ Lakini Musa akawaambia: ‘Msiogope. Simameni imara muuone wokovu wa Yehova.’ Kwa kweli Musa alimtumaini Yehova, sivyo?
Yehova akawaambia Waisraeli wavunje kambi. Usiku huo, Yehova akalihamisha wingu na kuliweka katikati ya Wamisri na Waisraeli. Kukawa na giza upande wa Wamisri, lakini upande wa Waisraeli kukawa na mwangaza.
Yehova akamwambia Musa aunyooshe mkono wake juu ya bahari. Kisha Yehova akafanya upepo wenye nguvu uvume usiku kucha. Bahari ikagawanyika na kukawa na njia katikati yake. Idadi kubwa ya Waisraeli wakapita katikati ya bahari juu ya nchi kavu, huku maji yakiwa kama ukuta kando yao nao wakaelekea upande wa pili wa bahari.
Jeshi la Farao likawafuata Waisraeli ndani ya bonde la bahari. Kisha Yehova akavuruga jeshi hilo. Magurudumu ya magari yao ya vita yakaanza kutoka. Wanajeshi hao wakapiga kelele na kusema: ‘Tuondoke hapa, kwa kuwa Yehova anawapigania Waisraeli!’
Yehova akamwambia Musa: ‘Nyoosha mkono wako juu ya bahari.’ Ghafla kuta za maji zikaangukia jeshi la Wamisri. Farao na wanaume wake wote wakafa. Hakuna hata mmoja aliyeokoka.
Ng’ambo ile nyingine ya bahari, umati mkubwa ulikuwa ukimsifu Mungu kwa kuimba hivi: “Mwimbieni Yehova, kwa maana amekwezwa sana. Farasi na mpandaji wake amewavurumisha baharini.” Watu walipokuwa wakiimba, wanawake walikuwa wakicheza dansi wakiwa na matari. Kila mtu alikuwa na furaha kwa sababu sasa walikuwa huru kabisa.
“Ili tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?’”—Waebrania 13:6