Maoni ya Biblia
Furiko—Kweli au Hekaya?
‘Na wanyama wakaingia katika safina alimo Noa, wawili wawili.’—Mwanzo 7:8, 9.
NI NANI ambaye hajasikia furiko la siku za Noa? Labda umejua masimulizi hayo kutoka utotoni. Kwa kweli, ukienda katika maktaba ya mahali penu kuchunguza habari ya Furiko, waweza kupata kwamba vitabu vingi zaidi juu ya jambo hilo vimeandikwa kwa ajili ya watoto kuliko kwa ajili ya watu wazima. Hivyo, waweza kuamua kulichukulia elezo la Furiko kuwa hadithi ya kusomea watoto wakati wa kulala. Wengi wahisi kwamba elezo la Furiko la Noa, pamoja na sehemu nyingine ya Biblia ni hekaya tu, kwa vyovyote, ni somo la maadili lililotungwa na mwanadamu.
Kwa kushangaza, hata baadhi ya watu wadaio kutegemeza imani zao za kidini juu ya Biblia watilia shaka ikiwa Furiko lilitokea kweli. Kasisi wa Kikatoliki Edward J. McLean wakati fulani alitaja kwamba masimulizi ya Noa yalipaswa yafafanuliwe, si yakiwa historia, bali yakiwa “fumbo au jambo la kusoma tu.”
Walakini, je, maelezo ya Furiko katika Biblia ni fumbo tu, ambayo kamwe hayakupaswa kuchukuliwa kihalisi? Je, Biblia yenyewe yaruhusu maoni kama hayo?
Maelezo ya Ndani Yastahiliyo Kuaminiwa
Kwanza, fikiria rekodi iliyofanywa na Musa katika kitabu cha Mwanzo. Hapo, twapata mwaka, mwezi, na siku hususa mvua ilipoanza kunyesha, safina ilipotua, na dunia ilipokauka. (Mwanzo 7:11; 8:4, 13, 14) Ingawa tarehe hususa hazirekodiwi kwa ukawaida katika sehemu nyingine za Mwanzo, tarehe hizo zinazohusiana na Furiko hukazia uhakika wa kwamba Musa aliona Furiko kuwa tukio halisi. Tofautisha maelezo ya Biblia ya kweli na maneno ya kufungua ya hekaya nyingi, “Hapo zamani za kale . . . ”
Kwa mfano mwingine, fikiria safina yenyewe. Biblia yaeleza juu ya chombo chenye urefu wa meta 133, huku urefu ukishinda kimo kwa uwiano wa 10 kwa 1 na urefu ukishinda upana kwa uwiano wa 6 kwa 1. (Mwanzo 6:15) Sasa angalia, Noa hakuwa muunda-meli. Na kumbuka, hili lilitukia zaidi ya miaka 4,000 iliyopita! Hata hivyo, safina ilitengenezwa kwa uwiano ambao ulifaa sana kwa utendaji wayo kikiwa chombo cha kuelea. Kwa kweli, wabuni wa vyombo vya kisasa vya majini wamepata uwiano unaofanana na huo kuwa hufaa kwa uimara katika bahari. Ingawa Biblia haionyeshi muda halisi aliotumia Noa kujenga safina, kulingana na maelezo ya Mwanzo, ujenzi ulichukua labda miaka 50 au 60. (Mwanzo 5:32; 7:6) Kweli hizo zinatofautiana sana na hekaya inayojulikana sana iliyopatikana katika Utenzi wa Kibabiloni wa Gilgameshi. Utenzi huo husimulia mchemraba mkubwa, usiovutia wa karibu meta 60 kila upande ambao ulijengwa kwa siku saba tu. Tofauti na hekaya hiyo ya Kibabiloni, maelezo ya Biblia ya Gharika yatokeza uhakika katika usahihi wayo.
Mbali na maelezo ya Mwanzo, Maandiko humrejezea Noa au Gharika ya tufeni pote mara kumi. Je, marejezo yote hayo huonyesha kwamba waandishi waliopuliziwa waliona Furiko kuwa historia ya kweli au hekaya tu?
Uasilia Wathibitishwa
Katika Maandiko, Noa aonekana katika nasaba mbili za taifa la Israeli, ya pili ikifikia Yesu Kristo. (1 Mambo ya Nyakati 1:4; Luka 3:36) Ezra na Luka, wakusanyaji wa nasaba hizi, wote wawili walikuwa wanahistoria stadi na bila shaka waliamini kwamba Noa alikuwa mtu halisi.
Katika sehemu nyingine ya Biblia, Noa anaorodheshwa pamoja na watu wa kihistoria, akitajwa kuwa mwadilifu na mwenye imani. (Ezekieli 14:14, 20; Waebrania 11:7) Je, lingekuwa jambo la akili kwa waandishi wa Biblia kumhusisha mtu wa kingano kuwa kielelezo cha kufuata? Hapana, kwa sababu hii ingeongoza kwa urahisi wale wanaosoma Biblia kufikia uamuzi kwamba imani haiwezi kufikiwa na nguvu za wanadamu na inaweza kuonyeshwa tu na watu wa kitabu cha hadithi. Noa na wanaume na wanawake wengine wa imani waliorodheshwa kwa sababu walikuwa wanadamu wenye udhaifu na hisia kama zetu.—Waebrania 12:1; linganisha Yakobo 5:17.
Katika marejezo yaliyobaki ya Maandiko, Noa na Furiko wanarejezewa katika muktadha wa uharibifu ambao Mungu alileta juu ya kizazi kisicho na imani ambacho kilimzunguka Noa. Angalia rejezeo la Yesu juu ya Gharika, lililorekodiwa katika Luka 17:26, 27: “Sawa na vile ilivyotukia katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa pia katika siku za Mwana wa binadamu: walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, wanaume walikuwa wakioa, wanawake walikuwa wakiozwa, hadi siku ile ambayo Noa aliingia katika safina, na furiko likawasili na kuwaangamiza wote.”
Yesu Kristo alikuwa shahidi aliyejionea kwa macho matukio aliyoyaeleza, kwani aliishi mbinguni kabla ya maisha yake ya duniani. (Yohana 8:58) Ikiwa Gharika ilikuwa hekaya tu, basi Yesu alionyesha kwamba kuwepo kwake kwa wakati ujao kulikuwa kusikoaminika au alikuwa akisema uwongo. Kila mmoja wa mikataa hiyo miwili haipatani na sehemu nyingine ya Maandiko. (1 Petro 2:22; 2 Petro 3:3-7) Kwa sababu hiyo, kutokana na mambo ambayo Yesu Kristo alijionea mwenyewe, aliamini maelezo ya Biblia ya Furiko ya tufeni pote kuwa historia ya kweli. Kwa Wakristo wa kweli, bila shaka huu ndio ushahidi mkubwa kabisa kwamba Furiko la siku ya Noa lilikuwa la kweli, si hekaya.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
L. Chapons/Illustrirte Familien-Bibel nach der deutschen Uebersetzung Dr. Martin Luthers