Vijana Huuliza . . .
Kwa Nini Sikuzote Ni Kosa Langu?
“Baba yangu ana mzio na hulazimika kufanya kazi na watu wavutao sigareti. Ajapo nyumbani, nyakati fulani huwa amekasirika sana. Yeye hupoteza vitu na kunilaumu. Nimwambiapo kwamba ni yeye aliyevipoteza, yeye huwaka na kuniambia kwamba sikupaswa kumsahihisha.”—Msichana tineja.
JE, NYAKATI fulani wahisi kwamba wewe ndiwe msingiziwa wa familia? Je, yaonekana kwamba haidhuru ni kasoro gani inatokea, ni wewe unayelaumiwa? Yaonekana ndivyo ilivyo kwa Joy mwenye umri wa miaka 14. Yeye aishi katika nyumba yenye mzazi mmoja na mara nyingi huwatunza ndugu na dada yake mchanga. “Wakati mwingine niko kwenye orofa ya chini waanzapo kupigana,” alalamika Joy. “Wanatenda kipumbavu sana na kwa kukosa ukomavu, lakini baba ajapo nyumbani, ananipigia kelele kwa sababu sikuwapo kuwakomesha.”
Ikiwa wazazi wako hukutaja kuwa umeharibika, ni mvivu, au asiyechukua daraka kwa uzito au kukubandika majina mengine ambayo yanakufanya uonekane kuwa usiyeweza kurekebika, nyakati fulani huenda ikaonekana kana kwamba wanatarajia ushindwe. Familia ya Ramon ilimbandika jina profesa msahaulifu—jina la utani ambalo alilichukia sana. Huenda pia ukachukia jina la utani au jina la kubandikwa ambalo hukazia kasoro zako, hata likisemwa kwa njia ya upendo. Badala ya kukuchochea kujiboresha, majina ya kubandika yasiyofaa yaweza tu kukazia hisia ya kwamba ni wewe tu upasaye kulaumiwa sikuzote.
Lawama yaweza hasa kuwa yenye maumivu ionekanapo kuwa yatokezwa na ubaguzi. “Mimi ni mtoto wa katikati,” asema tineja aitwaye Frankie, “nami sikuzote hutendwa vibaya.” Huenda ikaonekana kwamba ndugu zako sikuzote hawaonwi kuwa na hatia bali kwamba wewe huonwa kuwa na hatia wakati wowote tatizo lianzapo kutokea.
Sababu Ifanyayo Wazazi Walaumu
Bila shaka, ni jambo la kawaida kwa wazazi kurekebisha watoto wao wanapokosea. Kwani, kutoa rekebisho lifaalo, lililo chanya ni mojawapo ya njia ambazo wazazi wenye kumhofu Mungu hulea watoto wao “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Ingawa hivyo, nyakati fulani hata wazazi bora zaidi wanaweza kutenda kwa kupita kiasi au hata kufikia mikataa ya haraka yenye makosa. Kumbuka jambo lililotukia wakati Yesu alipokuwa mchanga. Katika pindi hii Yesu alikuwa amepotea. Kumbe alikuwa katika hekalu la Mungu, akiwa katika mazungumzo ya Biblia. Hata hivyo, wazazi wake walipompata, mama yake aliuliza hivi: “Mtoto, kwa nini ulitutenda kwa njia hii? Tazama, baba yako na mimi tukiwa na taabu ya akilini tumekuwa tukikutafuta.”—Luka 2:48.
Kwa kuwa Yesu alikuwa mkamilifu, hakukuwa na hofu yoyote kwamba angekuwa akijihusisha katika mwenendo wa ukosaji. Lakini kama wazazi wote wenye upendo, mama yake alihisi akiwa na daraka kwa mtoto wake naye akaitikia kwa mkazo, labda akihofu kwamba masilahi ya mwana wake ilikuwa hatarini. Vivyo hivyo, huenda wazazi wako wakatenda kwa njia ya kupita kiasi nyakati nyingine, si kwa sababu wanajaribu kukusumbua au kuwa wakatili, bali kwa sababu tu wanakujali kikweli.
Tambua pia, kwamba twaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Wakifanya kazi na kutunza nyumba yenu, wazazi wako wanakuwa chini ya mkazo mwingi, na hilo laweza kuathiri jinsi wanavyokutenda. (Linganisha Mhubiri 7:7.) Mfanyakazi mmoja wa afya ya kiakili alionelea hivi: “Katika familia fulani, kunapokuwa na tatizo, wazazi waweza kukasirika na kufanya maamuzi ya haraka hata ingawa kwa kawaida wao ni watu wazuri.”
Wazazi wasio na mwenzi hasa wanaweza kuwa katika hali ya kuelekezea watoto wao mifadhaiko yao, kwa sababu tu hawana mwenzi wa kuzungumza naye mambo. Inakubalika kwamba kupata sehemu kubwa ya mifadhaiko ya kibinafsi ya mzazi hakuleti raha. Lucy mwenye umri wa miaka 17 asema: “Ikiwa nilifanya jambo na napasa kuadhibiwa, hiyo ni sawa. Lakini niadhibiwapo kwa sababu mama yangu yuko katika hali mbaya ya moyoni, hiyo si haki hata kidogo.”
Upendeleo ni jambo jingine. Ingawa kwa kawaida mzazi hupenda watoto wake wote, si jambo lisilo la kawaida kwake kumpenda zaidi mtoto mmoja.a (Linganisha Mwanzo 37:3.) Kuhisi kwamba wewe ni mtoto asiyependwa sana kunaumiza kwenyewe. Lakini ikionekana kwamba mahitaji yako yanapuuzwa au mara nyingi unalaumiwa kwa yale ambayo ndugu zako wamefanya, kitakachofuata kwa hakika ni chuki. “Nina huyu ndugu yangu, Darren,” asema Roxanne mchanga. “Mama amfikiria kwamba hawezi kufanya kosa lolote. . . . Sikuzote hunilaumu, hamlaumu Darren kamwe.”
Familia Zenye Matatizo
Katika familia nzuri lawama isiyo ya haki huenda ikatukia mara chache. Lakini katika familia zenye matatizo huenda kukawa na namna yenye kuendelea ya mzazi kulaumu, kuaibisha, na kufedhehesha. Nyakati fulani lawama hiyo hata huambatana na ‘uchungu wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi.’—Waefeso 4:31.
Je, kijana aweza kulaumiwa kwa mifoko hiyo ya mzazi? Ni kweli kwamba mwana au binti anayekosa kutii aweza kuwa “huzuni” kwa mzazi. (Mithali 17:25) Hata hivyo, ni wazazi ambao Biblia huwaambia: “Msiwe mkiwasumbua [kihalisi “kuchokoza ili kukasirisha”] watoto wenu.” (Waefeso 6:4) Kama ilivyo na Wakristo wote, ni lazima mzazi ajizoeze hali ya kujidhibiti, “akifuliza kujizuia mwenyewe chini ya uovu.” (2 Timotheo 2:24) Kwa hiyo mzazi apotezapo hali ya kujidhibiti, hawezi kulaumu makosa ya mtoto wake.
Mashambulizi ya maneno yaweza kuwa uthibitisho kwamba mzazi anapatwa na msononeko wa kihisia-moyo, mshuko-moyo, au kujiona kuwa bure. Huenda pia yakaashiria matatizo kama vile msononeko wa kindoa au uraibu wa alkoholi. Kulingana na chanzo kimoja, watoto wa wazazi walio waraibu mara nyingi huwa wasingiziwa. “Hakuna wafanyacho kilicho sawa. Huenda wakaitwa ‘mpumbavu,’ ‘mbaya,’ ‘mchoyo,’ na kadhalika. Kisha washiriki wa familia wamkazia fikira mtoto huyo (au watoto hao) kuwa ‘tatizo’ lililotambulishwa na wanakengeushwa kutoka kwenye hisia zao za kutostarehe na matatizo yao wenyewe.”
Kushughulika na Lawama Isiyo ya Haki
Dakt. Kathleen McCoy ataja: “Kubandika majina, kushusha na kuchambua utu wa mtoto . . . kwaweza kuwa jambo linalochangia kutojiheshimu sana, mshuko-moyo na kutowasiliana kwa tineja.” Au kama Biblia yenyewe isemavyo, kutendwa kwa ukali kwaweza ‘kuchochea watoto wakasirike’ na kuwafanya ‘washuke moyo.’ (Wakolosai 3:21) Huenda ukaanza kujihisi ukiwa mtu bure asiyefaa. Huenda pia ukasitawisha hisia hasi kuelekea wazazi wako. Huenda ukafikia mkataa kwamba kuna machache uwezayo kufanya ili kuwapendeza na kwamba hakuna sababu ya kujaribu. Hasira na chuki zaweza kuja, zikikufanya ukatae nidhamu—hata uchambuzi ujengao.—Linganisha Mithali 5:12.
Waweza kukabilianaje na hali? Mengi yatategemea hali yako hususa. Kwa nini usitue na kuipima kihalisi? Kwa kielelezo, je, ni kweli kabisa kwamba ni wewe sikuzote wa kulaumiwa? Au yaweza tu kuwa kwamba wazazi wako huelekea kuwa wachambuzi kupita kiasi kidogo nyakati fulani na kusema jambo baya? “Sisi sote hujikwaa mara nyingi,” yasema Biblia, na hiyo yatia ndani wazazi. (Yakobo 3:2) Kwa hiyo hata ikiwa wazazi wako wanatenda kupita kiasi kidogo pindi kwa pindi, je, wewe pia wahitaji kutenda kupita kiasi pia? Shauri la Biblia kwenye Wakolosai 3:13 laweza kutumika vema: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia.”
Hisia-mwenzi kwa wazazi wako yaweza kukusaidia ufanye hilo. Mithali 19:11 yasema hivi: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” Ikiwa baba yako aonekana kuwa awezaye kukasirika isivyo kawaida ajapo nyumbani kutoka kazini na akulaumu kwa jambo ambalo hukufanya, je, kuna uhitaji wa kukuza sana jambo hilo? Kutambua kwamba yaelekea ana mkazo na amechoka kwaweza tu kukusaidia ‘kusamehe makosa.’
Ingawa hivyo, namna gani ikiwa kulaumiwa isivyo haki si jambo la kukukasirisha pindi kwa pindi tu bali hufanywa daima na bila kukoma? Makala fulani ya wakati ujao itazungumzia njia za kuboresha hali yako.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kushughulika na Ndugu na Dada Yangu?” katika toleo letu la Julai 22, 1987, (la Kiingereza).
[Picha katika ukurasa wa 19]
Ni jambo la haki kwa mzazi kutoa shauri la kurekebisha lihitajikapo