SURA YA 24
Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
Je, wazazi wako hubishana mbele yako? Ikiwa ndiyo, ni nini kati ya mambo yafuatayo wanayogombania mara nyingi?
□ Pesa
□ Kazi za nyumbani
□ Watu wa ukoo
□ Wewe
Ungependa kuwaambia wazazi wako nini kuhusu jinsi hilo linavyokuathiri? Andika maelezo yako hapa chini.
․․․․․
HUWEZI kuepuka usumbufu unaotokana na ugomvi kati ya wazazi wako. Unawapenda na unawategemea. Kwa hiyo, huenda ukafadhaika sana unapowasikia wakibishana. Huenda ukakubaliana na msichana anayeitwa Marie, aliyesema: “Ni vigumu kwangu kuwaheshimu wazazi wangu kwa kuwa inaonekana hawaheshimiani.”
Unapowaona wazazi wako wakigombana, unalazimika kukubali jambo hili lenye kuumiza: Wazazi wako si wakamilifu kama ulivyofikiri. Kujua hivyo huenda kukakutia wasiwasi. Mabishano hayo yanapozidi kuongezeka na kuwa makali zaidi, huenda ukawa na wasiwasi kwamba ndoa yao inaelekea kuvunjika. Marie anasema: “Ugomvi unapozuka kati ya wazazi wangu, ninawazia kwamba watatalikiana nami nitalazimika kuchagua nitakayeishi naye. Pia ninaogopa kwamba nitatenganishwa na ndugu na dada zangu.”
Kwa nini wazazi hugombana, nawe unapaswa kufanya nini ugomvi unapozuka?
Chanzo cha Ugomvi
Huenda wazazi wako ‘wanavumiliana katika upendo.’ (Waefeso 4:2) Hata hivyo, Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Wazazi wako si wakamilifu. Kwa hiyo, usishangae hasira zao zinapopanda na hata nyakati nyingine kutokeza ugomvi.
Kumbuka pia kwamba tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Mkazo wa kuchuma pesa, kulipia gharama mbalimbali, kushughulika na hali ngumu za kazini—yote hayo hulemea ndoa. Na ikiwa wazazi wote wawili wanafanya kazi ya kuajiriwa, huenda ikawa vigumu kuamua ni nani atakayefanya kazi fulani za nyumbani.
Lakini uwe na hakika kwamba hata wazazi wako wanapokosa kuelewana, haimaanishi kwamba ndoa yao inavunjika. Haikosi wazazi wako bado wanapendana—ijapokuwa huenda wakawa na maoni tofauti kuhusu mambo fulani.
Kwa mfano: Umewahi kutazama sinema pamoja na rafiki zako, kisha baadaye ukaona kwamba maoni yako kuhusu sinema hiyo ni tofauti kabisa na maoni yao? Inawezekana. Hata watu walio na uhusiano wa karibu huona mambo kwa njia tofauti. Huenda ikawa hivyo pia na wazazi wako. Labda wote wanahangaikia matumizi ya pesa za familia, lakini kila mmoja wao ana maoni tofauti kuhusu bajeti ya familia. Huenda wangependa familia iende tafrija, lakini kila mmoja wao ana maoni tofauti kuhusu tafrija itakayofaa. Au, huenda wangependa ufanye vizuri shuleni, lakini kila mmoja ana wazo tofauti kuhusu njia bora ya kukusaidia.
Somo ni: Kuwa na maoni tofauti hakumaanishi kwamba hakuna umoja. Watu wawili wanaopendana wanaweza kuwa na maoni tofauti. Hata hivyo, bado hungependa kusikia wazazi wako wakibishana. Ni nini kinachoweza kukusaidia?
Mambo Unayoweza Kufanya
Uwe na heshima. Ni rahisi kukasirishwa na ugomvi wa wazazi. Wao ndio wanaopaswa kukuwekea kielelezo kizuri. Hata hivyo, kumdharau mzazi kutazidisha tu matatizo katika familia. Isitoshe, Yehova Mungu anakuamuru uwaheshimu wazazi wako—hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo.—Kutoka 20:12; Methali 30:17.
Lakini, unaweza kufanya nini ikiwa jambo ambalo wazazi wako wanabishania linakuhusu? Kwa mfano, tuseme kwamba mzazi wako mmoja ni Mkristo na yule mwingine si mwamini. Huenda hali fulani zikatokea na kukulazimu kuchukua msimamo upande wa uadilifu pamoja na mzazi anayemwogopa Mungu. (Mathayo 10:34-37) Sikuzote fanya hivyo kwa “tabia-pole na heshima kubwa.” Huenda siku moja mfano wako unaweza kumvutia mzazi wako asiyeamini.—1 Petro 3:15.
Usiwe na upendeleo. Unaweza kufanya nini wazazi wako wakitaka uwaunge mkono katika jambo ambalo halikuhusu moja kwa moja? Usiegemee upande wowote. Labda unaweza kuondoka na kusema kwa heshima: “Mama na Baba, ninawapenda nyote wawili. Lakini, tafadhali msiniombe niunge mkono upande mmoja au mwingine. Hilo ni kati yenu wawili.”
Zungumza nao. Wajulishe wazazi wako jinsi unavyohisi wanapobishana. Tafuta wakati ambao unajua watakusikiliza, kisha uwaeleze kwa heshima kwamba kubishana kwao kunakufadhaisha, kunakuudhi, na hata kukuogopesha.—Methali 15:23; Wakolosai 4:6.
Mambo ya Kutofanya
Usijifanye mshauri wa ndoa. Ukiwa kijana, si kazi yako kutatua tofauti za wazazi wako. Kwa mfano: Wazia unasafiri katika ndege ndogo na unasikia rubani na msaidizi wake wakibishana. Huenda ukawa na wasiwasi. Itakuwaje ukiamua kuwafundisha marubani hao jinsi ya kuendesha ndege au hata kujaribu kuiendesha wewe mwenyewe?
Vivyo hivyo, kujaribu ‘kuendesha mambo’ kwa kujihusisha katika matatizo ya ndoa ya wazazi wako kutaharibu mambo hata zaidi. Biblia inasema: “Kwa sababu ya kimbelembele mtu husababisha tu pambano, lakini wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” (Methali 13:10) Wazazi wako wanaweza kutatua matatizo yao vizuri zaidi wakiwa peke yao.—Methali 25:9.
Usijitupe ulingoni. Tayari kelele za watu wawili wanaogombana zinaudhi. Mbona uongeze sauti yako? Hata ikiwa unaona kwamba unahitaji kuokoa jahazi, ukweli ni kwamba ni jukumu la wazazi wako—bali si lako—kutatua matatizo yao. Katika mambo yasiyokuhusu kama hayo, jitahidi kufuata shauri hili la Biblia: ‘kazia akili mambo yako mwenyewe.’ (1 Wathesalonike 4:11) Usikubali kuhusishwa katika mabishano.
Usiwagonganishe. Vijana fulani huchangia mabishano kati ya wazazi wao kwa kuwachezea shere. Mama akisema hapana, wanajaribu kumshawishi Baba aseme ndiyo. Huenda ukapata uhuru kidogo kwa sababu ya ujanja wako, lakini mwishowe, kufanya hivyo kutazidisha tu matatizo katika familia.
Usiruhusu mwenendo wao uathiri mwenendo wako. Kijana anayeitwa Peter alikuwa akijiendesha isivyofaa eti kwa sababu baba yake ni mkatili. Peter anasema: “Nilitaka aone uchungu. Nilimchukia sana kwa sababu ya vile alivyonitendea mimi, mama yangu na dada yangu.” Hata hivyo, muda si muda utalazimika kuvuna ulichopanda. Hivyo, kujiendesha isivyofaa kutaongeza tu matatizo nyumbani.—Wagalatia 6:7.
Andika hapa chini mambo unayohitaji kufanyia kazi zaidi kati ya mambo yaliyozungumziwa katika sura hii. ․․․․․
Ni wazi kwamba huwezi kuwazuia wazazi wako wasigombane. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anaweza kukusaidia kukabiliana na mfadhaiko ambao ugomvi wao unakusababishia.—Wafilipi 4:6, 7; 1 Petro 5:7.
Jitahidi kutumia madokezo yaliyozungumziwa. Mwishowe, huenda wazazi wako wakachochewa kufikiria kwa uzito jinsi wanavyoweza kutatua matatizo yao. Huenda hata wakaacha kugombana.
Unaweza kushughulikia jinsi gani magumu ya kulelewa katika familia ya mzazi mmoja?
MAANDIKO MUHIMU
“Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.”—Wakolosai 4:6.
PENDEKEZO
Ikiwa wazazi wako wanagombana vikali karibu kila siku, wapendekezee kwa heshima watafute usaidizi.
JE, WAJUA . . .?
Hata watu wanaopendana wanaweza kukosana nyakati nyingine.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Wazazi wangu wakianza kugombana, nita ․․․․․
Mmoja wa wazazi wangu akitaka nimuunge mkono, nitasema ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini wazazi hugombana?
● Kwa nini huwezi kulaumiwa kwa sababu ya matatizo ya wazazi wako?
● Unaweza kujifunza nini kutokana na mwenendo wa wazazi wako?
[Blabu katika ukurasa wa 201]
“Kutambua kwamba wazazi wangu si wakamilifu na kwamba wana matatizo kama mimi kumenisaidia kuvumilia wanapogombana.’’—Kathy
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 206, 207]
Namna gani wazazi wangu wakitengana?
Wazazi wako wakitengana, unaweza kutendaje kwa hekima licha ya hasira kali ambayo huenda ukawa nayo? Fikiria mapendekezo yanayofuata:
● Usitarajie mambo yasiyowezekana. Huenda jambo la kwanza ambalo ungetaka kufanya ni kuwaunganisha tena wazazi wako. Anne anakumbuka: “Baada ya kutengana, bado wazazi wetu walikuwa wakitupeleka matembezi mara kwa mara. Mimi na dada yangu tulikuwa tukinong’onezeana, ‘Tukimbie tuwaache pamoja.’ Lakini wapi! Hawakurudiana.”
Andiko la Methali 13:12 linasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Ili kujiepusha na mkazo usio wa lazima, kumbuka kwamba huwezi kuwafanyia maamuzi wazazi wako. Kwa kuwa si wewe uliyefanya watengane, basi utawezaje kuwafanya warudiane?—Methali 26:17.
● Epuka chuki. Kufungia kinyongo na chuki moyoni kumwelekea mzazi mmoja au wote wawili kunaweza kukuletea madhara makubwa. Tom anakumbuka alivyohisi alipokuwa na umri wa miaka 12: “Nilianza kumchukia baba yangu. Sipendi kutumia neno ‘chuki,’ lakini nilikuwa na kinyongo kwelikweli. Sikuelewa jinsi angeweza kudai kwamba anatujali na wakati uleule atuache.”
Hata hivyo, kutengana hakutokei kwa sababu mzazi mmoja ni malaika na yule mwingine ni mwovu. Ukweli ni kwamba, huenda wazazi wako hawajakuambia mambo yote yaliyosababisha watengane; huenda hata wao wenyewe hawaelewi. Kwa hiyo, epuka kukata kauli kwa kuwa kuna mambo ambayo hujui. (Methali 18:13) Ni kweli kwamba si rahisi kuepuka kukasirika, na kwa kawaida utakuwa na hasira kali kwa muda fulani. Lakini kuendelea kuwa na hasira na kisasi kunaweza kuharibu utu wako. Biblia ina sababu nzuri ya kutuambia: “Acha hasira na uache ghadhabu.”—Zaburi 37:8.
● Uwe na usawaziko. Badala ya kumchukia mzazi aliyeondoka, vijana fulani hupita mipaka kwa kuanza kumwabudu. Kwa mfano, baba ya kijana mmoja alikuwa mlevi na mwasherati aliyeiacha familia yake mara nyingi na mwishowe akapata talaka. Hata hivyo, kijana huyo anakumbuka kwamba kwa sababu moja au nyingine, bado alimhusudu sana baba yake!
Visa kama hivyo ni vya kawaida. Katika nchi fulani, asilimia 90 ya watoto ambao wazazi wao wametalikiana wanaishi na mama yao na kumtembelea baba yao mara kwa mara. Hivyo, mama ndiye mwenye jukumu la kuwatunza watoto kila siku—kutia ndani kuwatia nidhamu. Ijapokuwa baba anamtegemeza kwa kulipia gharama fulani, mara nyingi uwezo wa kifedha wa mama hupungua sana baada ya talaka. Kwa upande mwingine, huenda uwezo wa kifedha wa baba ukaongezeka. Matokeo: Watoto wanapomtembelea Baba wanapata zawadi na mambo mengi yenye kuwafurahisha! Wanaporudi kwa Mama hali ni ngumu na sheria chungu nzima. Inasikitisha kwamba, vijana fulani hata wamemwacha mzazi Mkristo na kwenda kuishi na mzazi asiye mwamini ambaye ana mali nyingi zaidi na anawaruhusu kufanya wapendalo.—Methali 19:4.
Ikiwa uko katika hali kama hiyo, fikiria mambo yaliyo ya maana zaidi. Kumbuka kwamba unahitaji nidhamu na mwongozo unaofaa wa kiadili. Hakuna kingine chochote ambacho mzazi anaweza kukupa kitakachokuwa na matokeo makubwa zaidi katika utu wako na maisha yako kuliko nidhamu na mwongozo wa kiadili.—Methali 4:13.
[Picha katika ukurasa wa 202, 203]
Kijana anayewaambia wazazi wake namna ya kutatua matatizo yao ni kama abiria anayewaambia marubani namna ya kuendesha ndege