Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 1/8 kur. 11-27
  • Wazazi Wangu Wanaachana—Je! Napaswa Kufanya Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazazi Wangu Wanaachana—Je! Napaswa Kufanya Nini?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuongoza Dhoruba
  • Matarajio Bandia
  • Hatari ya Chuki
  • Kunaswa Katikati
  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Naweza Kushindaje Hali Baada ya Wazazi wangu Kuachana?
    Amkeni!—1992
  • Nishughulikeje na Mzazi Wangu Aliyeondoka Nyumbani?
    Amkeni!—1992
  • Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?
    Amkeni!—2009
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 1/8 kur. 11-27

Vijana Wanauliza. . .

Wazazi Wangu Wanaachana—Je! Napaswa Kufanya Nini?

“Usiku mmoja baba yangu alituchukua akatununulie sisi watoto wanne aisi-kirimu. Kwa ghafula, sauti yake ikawa ya hali rasmi sana. Akatuambia hivi: ‘Mama yenu nami twaona mambo kwa jinsi tofauti, kwa hiyo nitaondoka. Huenda nikarejea wakati wa kiangazi.’ Hakuna mmoja aliyesema jambo lolote. Ni lazima iwe alikuwa amekwishapanga mikoba yake, kwa kuwa alipoturudisha nyumbani kwa gari, hakuingia. Tulitoka ndani ya gari tukasimama katika barabara ya faraghani kuelekea nyumba tukiwa tunalia kwa sauti baba yangu alipokuwa akiendesha kwenda zake.”—Tom.a

WAZAZI wa Tom hawakurejeana tena kamwe. Lakini kwa wakati huo, Tom hakujua kama wangefanya au wasingefanya hivyo.

Kwa upande mwingine, wazazi wa Randy waliachana mara nyingi zaidi ya anavyoweza kukumbuka. “Baba angeondoka labda kwa mwezi mmoja au miwili,” akumbuka. “Halafu angerejea, na mambo yangekuwa mazuri kwa muda. Halafu, kwa ghafula, angeondoka tena.”

Talaka huwa kikata-maneno. Lakini wazazi wako wakiwa wameachana tu, na bado hujui kama watatalikiana au sivyo, ukosefu huo wa hakika waweza kutatiza sana. Wazazi wengi, kama wa Randy, hurejeana lakini huachana tena baadaye. Kulingana na kitabu Divorced Families, kadiri ya asilimia 50 ya mitengano huishia katika angalau patanisho la muda. Lakini kama vile wachunguzi wa habari za talaka Judith Wallerstein na Sandra Bakeslee wanavyosema: “Talaka mara nyingi hutangulizwa na mitengano kadha, ambayo kila mmoja huonekana thabiti lakini hugeuka kuwa usio wa mwisho kabisa. Hiyo yaweza kuvuruga watoto na kuwaongoza kutarajia patanisho.”

Maneno, ‘Huenda nikarejea,’ huonekana kuwa yenye taraja sana. Lakini maswali yasiyojibiwa hubakia hewani yakiumiza mno. Wewe wajiuliza hivi: ‘Wazazi wangu watataliki mwishowe? Je! naweza kukabilianaje na maoni ambayo yananihangaisha hivi sasa?’

Kuongoza Dhoruba

Mara ya kwanza, huenda ukajipata ukiona mshuko wa moyo, uchovu, usiweze kukaza fikira, au hata mara nyingine ukiwa mwenye mshindo wa hasira. Au huenda ukajisikia mlegevu tu. Haya yote ni matendo-itikio ya kawaida kwa hali iliyo ngumu sana—moja inayotukia mara nyingi zaidi siku hizi. Ingawa Neno la Mungu hutia moyo wenzi wa ndoa kubaki pamoja na kutatua matatizo yao, mwelekeo wa ulimwengu kwa ndoa umepunguka thamani sana sana. (1 Wakorintho 7:10-16) Leo, nyakati nyingine ndoa haina taraja la zaidi ya asilimia 50 ya kuokoka. Kama vile Biblia ilivyotabiri zamani za kale, kizazi chetu kimeona upungufu mkubwa katika “shauku ya asili” iliyokuwa ya kawaida sana katika familia wakati mmoja.b—2 Timotheo 3:3, NW.

Waweza kukabilianaje? Unayoyapitia yaweza kulinganishwa na dhoruba maishani mwako. Kuyafikiria kwa njia hiyo kwaweza kukusaidia kwa njia mbili. Kwanza, hakuna dhoruba idumuyo milele. Msukosuko wa maoni ya moyoni unaoona sasa utupungua kwa wakati, kama vile dhoruba zote hufanya. Na pili, unaweza kuongoza njia yako kupitia dhoruba hiyo. Huhitaji ‘kuzama.’ Lakini kama vile meli katika dhoruba lazima ijiepushe na miamba, kuna hatari fulani kama miamba ambazo zaweza kumaanisha taabu kikweli. Acha tuzungumze chache yazo.

Matarajio Bandia

Mojapo ya hatari kama hizo ingekuwa kukaza moyo juu ya kufanya wazazi wako warejeane. Anne akumbuka hivi: “Baada ya wao kuachana, wazazi wangu bado wangetutembeza pamoja, nyakati nyingine. Dada yangu nami tulikuwa tunanong’onezeana hivi, ‘Acha tukimbie mbele tukawaache wale wawili pamoja.’ Lakini,” ahema akisikitika kwamba, “Naona ilikuwa bure tu. Hawakurejeana kamwe.”

Kama Mithali 13:12 inavyosema: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” Kumbuka, huwezi kudhibiti yale wazazi wako wanayofanya. Si wewe uliyesababisha kuachana kwao, na ni yamkini kwamba huwezi kuingilia na kutengeneza ndoa yao.—Ona pia Mithali 26:17.

Hatari ya Chuki

Hasira na chuki huenda ikawa hasa ndiyo “miamba” hatari zaidi utakayokabili katika dhoruba hiyo. Tom akumbuka maoni yake akiwa na umri wa miaka 12: “Nilianza kuona hasira kikweli kuelekea baba yangu. Sipendi kutumia neno ‘chuki,’ lakini nilikuwa na kinyongo kibaya. Sikuona jinsi angeweza kujali juu yetu ikiwa alituacha. Na nafikiri nilikuwa nikisema ndani yangu kwamba ni zamu yangu kujulisha yeye jinsi mimi ninavyoona.”

Kuachana kwa ndoa mara nyingi si uamuzi wa wote wawili; kwa hiyo kwa asili mzazi mmoja huenda akaonekana kuwa mwenye kulaumika zaidi machoni mwako. Huenda hata ikawa kwamba mzazi wako mmoja alivunja sheria ya Mungu juu ya kuwa mwaminifu kwa mwenzi wa ndoa. (Waebrania 13:4) Lakini kwa vyovyote, ushughulikeje na mzazi aliye na hatia zaidi? Je! ni lazima umchukie mzazi huyo au kujaribu kumlipia kisasi mzazi aliyekosewa?

Kumbuka kwanza kwamba si kawaida mwachano kuwa ni jambo rahisi kama tu mzazi mmoja kuwa ni “mbaya” sana na mwingine ni “mzuri” sana. Wazazi wako labda hawajakuambia yote juu ya ndoa yao au mvunjiko wao; huenda hata hawauelewi wao wenyewe. Kwa hiyo epuka kuhukumu hali ambayo huna maelezo yote juu yayo. (Mithali 18:13) Kwa kupendeza, Mungu ndiye Hakimu wa mambo yote kama hayo. Hakuchagui kuwa hakimu wala mwadhibu wa wazazi wako. Nacho ni kitulizo kama nini! Ni nani kati yetu ambaye kwa kweli angeweza kushughulikia daraka kama hilo?—Warumi 12:19.

Ni kweli, ni vigumu kuzuia hasira; na ni jambo la kiasili kwako kuudhika sana wakati huu. Lakini kuweka hasira na roho ya kulipa kisasi kwaweza kuharibu utu wako pole kwa pole. Biblia yasema kwamba “moyo ulio mzima ni uhai wa mwili.” Hakika, moyo mtulivu haujawi na uchungu. Si ajabu kwamba Biblia hutuambia ‘tukomeshe hasira, tuache ghadhabu.’ (Mithali 14:30; Zaburi 37:8) Zaidi ya hayo, amri ya Biblia kuheshimu wazazi wako hata hutumika kwa kuheshimu wazazi ambao wamekuvunja moyo.—Luka 18:20.

Kwa hiyo Tom amerekebisha hasira yake. Sasa asema hivi: “Ni rahisi kuwa na kinyongo na kufikiri ‘Yeye ndiye alifanya kosa. Ni jambo la haki nikimchukia.’ Lakini nikaanza kujiuliza, ‘Je! hilo kweli ni jambo la haki?’ Na niliona kwamba, la, sivyo. Ukiwa Mkristo, huwezi kuwa na vinyongo.”

Bila shaka, wakati Biblia inaposema kuacha hasira, haidokezi kwamba ujifanye kwamba hasira yako haiko. Kama vitendo vya wazazi wako vimekuumiza, kwa nini usijaribu kuzungumza nao kuhusu hilo, ukiwafahamisha kwa heshima maoni yako?—Ona Mithali 15:22, 23; 16:21.

Kunaswa Katikati

‘Lakini nitashughulikaje na hisia hii ya kuwa nimefarakana kati ya wazazi wangu?’ huenda ukauliza. Hiyo huenda ikawa hasa “mwamba” wenye hila wa kuepuka. Randy akumbuka: “Jambo nililohofia zaidi juu ya kutembelea babangu ni kwamba mamangu alikuwa ananihoji mno baada ya kila ziara. Naye alisema mambo ya kuchukiza kweli kweli dhidi yake. Ningesema, ‘Lakini mama! Mbona wafanya hivi? Usinisumbue!’ Naye alikuwa akiwaka na kunilazimisha nimjibu maswali yake yote.”

Nyakati nyingine wazazi hutumia watoto wao kupitishia habari za hasira kutoka kwa mmoja kuelekea mwingine au hata kupelelezana! Mwanamke mmoja alitaka kujua ni pesa ngapi mume wake aliyeishi mbali naye alikuwa nazo. Kwa hiyo yeye na mwana wake wa miaka kumi walitumia ufito uliojikunja nchani kufungua dirisha kwenye nyumba ya baba yake, na mvulana akapanda ndani kuiba kitabu cha cheki cha baba yake. “Tutamgundua!” mvulana huyo akasema kwa uchangamfu ulio wazi.

Si tendo la haki kwa wazazi wako kujaribu kukutumia kuwa chombo cha kulipizia kisasi. Lakini kumbuka kwamba wanapitia msukosuko mwingi ajabu wa maoni ya moyoni. Kwa hiyo uwe mwenye saburi nao iwezekanavyo. Zungumza nao. Labda ungeweza kusema kwa asili, ‘Mama na Baba, nawapenda nyote wawili. Kwa hiyo tafadhali msinitumie kuumizana.’ Si kwamba uwe asiyeshirikiana, kukataa kuwasilisha habari yoyote kutoka kwa mmoja hadi kwa mwingine. Lakini ikiwa wazazi wako wanakuwa wenye ukali na wenye kutaka kisasi, huo ndiyo wakati wa kutoka katikati yao.—Mithali 26:17.

Vilevile lingekuwa jambo la kinafiki kutumia mzazi mmoja dhidi ya mwingine kwa ajili ya manufaa yako, kwa kusema mambo kama vile: “Nataka kwenda kuishi na mama. Yeye huniacha nifanye nitakavyo.” Baada ya mwachano huenda wazazi wakajisikia wenye hatia sana kuhusu mkazo ambao wamesababishia watoto wao wakaambatana nao kwa kukata tamaa. Vijana ambao wanatambua uwezo ambao wanashikilia sasa juu ya wazazi wao huenda wakashawishwa kuutumia. Lakini hakika wewe hutaki kuwa mwelekeza mambo kwa hila.

Lakini kuna mengine zaidi ili kuokoka dhoruba, kuliko tu kuepuka miamba. Makala ya wakati ujao itazungumzia matendo mazuri mengine unayoweza kufanya yakusaidie ukabiliane.

[Maelezo ya Chini]

a Majina mengine yamebadilishwa.

b Kwa habari ya visababishi vya mvunjiko wa ndoa, ona makala “Kwa Nini Mama na Baba Waliachana?” katika toleo la Oktoba 22, 1987 la Amkeni! katika Kiingereza. Ona pia makala “Vijana Wanauliza . . . ” katika matoleo ya Desemba 22, 1987, na Mei 22, 1988 katika Kiingereza.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Unayoyapitia yaweza kulinganishwa na dhoruba maishani mwako. Kuyafikiria kwa njia hiyo kwaweza kukusaidia kuyashinda, kwa sababu hakuna dhoruba idumuyo milele

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Ni vigumu kuzuia hasira; na ni jambo la kiasili kwako kuudhika sana wakati huu. Lakini kuweka hasira na roho ya kulipiza kisasi kwaweza kuharibu utu wako pole kwa pole

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki