Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 3/8 kur. 14-16
  • Naweza Kushindaje Hali Baada ya Wazazi wangu Kuachana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kushindaje Hali Baada ya Wazazi wangu Kuachana?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kubadili Jambo Unalokazia Fikira
  • Waendee Wengine
  • Fuata Kawaida ya Kiroho
  • Wazazi Wangu Wanaachana—Je! Napaswa Kufanya Nini?
    Amkeni!—1992
  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?
    Amkeni!—2009
  • Marafiki Wazuri na Wabaya
    Amkeni!—2004
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 3/8 kur. 14-16

Vijana Wanauliza . . .

Naweza Kushindaje Hali Baada ya Wazazi wangu Kuachana?

“Wazazi wangu walipoachana, ilikuwa lazima tuhame. Hatukuwa na gari tena, kwa hiyo mama alilazimika kusafiri kotekote kwa basi na kutupeleka kwa mtunza-watoto. Kisha tukaweza kuona mabadiliko nyumbani. Baba alitakiwa alipe gharama za kuruzuku watoto, lakini mara nyingi hakufanya hivyo, na mama alilazimika kulipa gharama za mahitaji fulani. Hatimaye baba hakulipa chochote.”—Anne.a

BAADA ya miaka 14, wazazi wa Anne wangali wameachana ingawa hawajatalikana. Iwapo umepitia hali hii ya kuhuzunisha ya kuona wazazi wako wakiachana huenda ukaelewa vizuri anavyohisi. Huenda ikawa kwamba majuma, miezi, au miaka ya kutosha imepita ikapunguza ule mshtuko wa kwanza. Lakini mara nyingine huenda ukashangaa utawezaje kuendelea kuishi namna hiyo. Bado hakuna talaka wala patano; bado ukosefu wa uhakika unatoa dalili zinazosumbua maisha yako.

Upweke huenda ukawa mwingi pia. Baada ya wazazi wa Brad kuachana, mama yake alianza kufanya kazi mbili na kwenda shuleni kujifunza kazi fulani. Brad alisikitika sana kwa kutoweza kuwa pamoja naye. Akumbuka hivi: “Usiku mmoja nilijificha ndani ya gari ili kwenda kazini naye. Lakini nilipofika huko, nikamsumbua sana. Ikabidi mtu fulani anipeleke nyumbani. Kwa kweli, watoto wengi wa wazazi walioachana huhisi kana kwamba kuachana huko kumewanyang’anya wazazi wote wawili, si mmoja tu. Kama kijana mwingine, Mike asemavyo: “Tulinyang’anywa baba yetu na mwanamke mwingine, na kisha tukanyang’anywa mama yetu kwa kazi zake.”

Upweke, kutokuwa na uhakika, hali ya uchumi iliyobadilika—matatizo kama hayo ndiyo unahitaji kukabiliana nayo ikiwa wazazi wako wameachana. Unaweza kuwaje na mtazamo chanya (mzuri)?

Kubadili Jambo Unalokazia Fikira

Vita hivi, kama vingine vingi, huanza na akili na moyo wako mwenyewe. Huenda ukakazia fikira sana kuachana kwa wazazi wako, ukikuhangaikia mno, na hata kuingia katika kipindi cha kujihurumia ambacho ni vigumu kukipona. Hata hivyo, unaweza kujilinda usilemewe na wasiwasi.

Katika makala yetu iliyotangulia katika mfululizo huu, tulifananisha kushinda hali ya kuachana kwa wazazi wako na kukabiliana na dhoruba maishani mwako.b Inapendeza kwamba, Biblia huzungumza juu ya vile mtume Petro alivyojipata katika dhoruba halisi baharini. Kwenye upeo wa dhoruba hiyo, alimwona Yesu Kristo akitembea juu ya bahari bila kupata dhara! Yesu hata alimwalika Petro atembee juu ya bahari kumwelekea. Lakini Petro hakuweza kwenda mbali kabla ya kuanza kuzama. Kwa sababu gani?

Mathayo 14:30 yasema hivi: “Lakini alipouona upepo [Petro] akaogopa; akaanza kuzama.” Jambo alilohitaji Petro ni imani, si woga. Lakini alipokaza fikira zake kwenye dhoruba, ikiwa na mawimbi yenye kukumba, yaliyovumishwa na upepo, akaanza kuogopa. Akaacha kukaza fikira zake kwa Yesu, yeye ambaye angeweza kumsaidia asizame. Jambo hilo laweza kukupata wewe pia. Kadiri unavyokaza fikira zaidi juu ya matatizo yako, ndivyo yanavyoonekana kuwa yenye kuogofya zaidi kwako. Badala ya hiyo kaza fikira kwenye masuluhisho.

Meg, ambaye wazazi wake wameachana, aeleza hivi: “Usikaze sana fikira juu ya hali yako ya sasa. Huwezi kuibadili kwa vyovyote.” Randy akariri wazo hilo: Unapofikiria mambo yasiyofaa, unaingia kwenye hali ya kurudiarudia mawazo yale yale, kama lori lililokwama katika matope.” Unaweza kujitoaje katika hali hiyo?

Waendee Wengine

Meg asema hivi: “Ongea jambo hilo na mtu mwenye ujuzi wenye kutumika na aliyekomaa kwelikweli kiroho, mtu anayeweza kukusaidia kuona mambo waziwazi.” Rafiki wa namna hiyo aweza kukusaidia kukaza mawazo yako katika njia iliyo chanya zaidi. Kama Mithali 17:17 isemavyo: “Marafiki huonyesha upendo wao sikuzote. Ndugu ni wa nini ikiwa si wa kushiriki magumu?” (Today’s English Version) Kwa hiyo unapojitahidi kushindana na kuachana kwa wazazi wako, na hasa na upweke unaoufuata, huenda ukahitaji kuwaendea marafiki wako na kuwategemea zaidi ya wakati mwingineo wote.

Hata hivyo, kuna neno la hadhari. Si rafiki wote watakusaidia kufaulu katika jambo hilo. Wengine watakuongezea tu matatizo. Mike akumbuka hivi: “Baada ya wazazi wangu kuachana, nilijifungamanisha na marafiki wangu kwa njia iliyokaribia sana kutokuwa ya kiasili. Tulikuwa na wakati wa furaha pamoja, lakini mara nyingi sana tulijiingiza matatani pamoja—kama vile dawa za kulevya na mapigano. Kwa muda fulani nilikuwa nikifikiri kwamba nikipoteza marafiki wangu, ningepoteza yote. Hilo, niligundua baadaye, lilikuwa wazo la uwongo, kwa sababu kwa kweli hawakuwa washikamanifu. Walinigeuka. Mmoja wao hata alijifanya kuwa ndiye mimi alipokamatwa na polisi akiharibu ovyoovyo jengo la shule.”

Hapana, si marafiki wote walio marafiki wa kweli. Kama Mithali 18:24 isemavyo: “Kunao marafiki wanaoongoza mtu katika uharibifu, wengine ni wa karibu kuliko ndugu.” (The Jerusalem Bible) Kwa kupendeza, Baadaye Mike alipata marafiki wa namna ifaayo. Akumbuka mmoja hasa: “Alikuwa kama ndugu mkubwa kwangu. Alijifunza Biblia pamoja nami, na kufanya mambo mengine pamoja nami pia. Hata nilienda kazini pamoja naye. Naye hakunifanya kamwe nihisi kwamba kufanya hivyo kulikuwa jambo la kuchosha kwake. Hadi leo hii, najua hilo liliathiri maisha yangu. Kama singeonana naye, sijui leo ningekuwa nini.”

Unaweza kupata wapi marafiki wa namna hiyo? Yesu aliahidi kwamba kundi la Kikristo lingeweza kuandaa “ndugu na dada na mama na watoto” wengi kwa wale ambao hawakuwa na wowote. (Marko 10:30, NW) Hivyo, Mike alipata rafiki kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova.

Ndivyo na Tom. Akumbuka hivi: “Ndugu mmoja katika kundi alinichukua niishi naye kana kwamba nilikuwa mwana mkubwa wake. Na dada mmoja mwenye umri mkubwa akawa kama nyanya kwetu. Kundi lilitupenda kwelikweli sikuzote, na inastaajabisha jinsi hilo liwezavyo kukutimizia mengi.” Kwa hiyo, Tom asema hivi: “Ikiwa huna baba, pata mmoja kundini. Kwa sasa, imarisheni uhusiano wowote wa kifamilia mlio nao, na karibianeni pamoja.” Ndugu, dada, babu na nyanya, na watu wengine wa ukoo waweza kuwa marafiki waaminifu kwako.—Mithali 13:20.

Lakini urafiki mkubwa zaidi utakaofanya wakati wowote ni ule wa Muumba wako, Yehova. Wazazi wanapoachana, ahadi kwenye Yakobo 4:8 inakuwa hasa yenye kufariji: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”

Fuata Kawaida ya Kiroho

Kwenda kwenye mikutano ya Kikristo kwa ukawaida kutakusaidia ufanye hilo hasa—umkaribie Mungu, kwa kujifunza juu yake. Mikutano itakusaidia pia upate rafiki wapya. (Waebrania 10:24, 25) Lakini mikutano na shughuli nyinginezo za Kikristo zaweza pia kuyapa maisha yako utaratibu na kawaida. Hilo hasa ni la muhimu iwapo kuachana kumeharibu sana kawaida zako za kifamilia, kukijaza siku zako ukosefu wa uhakika.

Kweli, huenda ukahisi tamaa hatari ya kuasi dhidi ya kawaida zote zenye utaratibu sasa hivi. Shule hasa huenda ikaonekana kuwa yenye kulemea. Mike akumbuka hivi: “Nilichukua mtazamo wa ‘mimi sijali.’ Nilianza kufanya vibaya shuleni, nami nikafikiri, ‘Ikiwa baba na mama yangu hawajali vya kutosha kuendeleza umoja wa familia yetu, basi mimi sijali pia.’ Kuachana kwao kukawa sababu yangu ya kutojaribu.”

Lakini usifanye kosa la kutumia kuachana huko kuwa udhuru wako wa kutojali mambo ambayo yatakusaidia hasa. Kitabu Surviving the Breakup kinasema kwamba kwa watoto wa talaka “shule ilikuwa yenye faida hasa kwa sababu ilitokeza utaratibu . . . Kulikuwa na ushuhuda kwamba watoto wengi walitegemezwa na shule katika njia hiyo ya msingi, bila kujali ubora wa kutenda kwao kimasomo na kijamii darasani.”

Shule inaweza pia kukusaidia usitawishe sifa na ujuzi na nidhamu ambazo zaweza kukusaidia katika muda wote wa maisha yako—hata kukufanya ustahili zaidi kupata kazi ya kuajiriwa. Ikiwa familia yako inaumia kifedha kwa sababu ya mwachano, kama vile familia nyingi huathiriwa, labda unaweza kuona faida ya kujitayarisha sasa ili upate kazi ambayo itakusaidia kutosheleza mahitaji yako katika wakati ujao.

Kwa vyovyote vile, wakati ujao wako, si usioweza kudhibitika. Unaweza kushinda hali ya kuachana kwa wazazi wako. Umetayarishwa kufanya hivyo. Watafiti wa talaka wamepata kwamba vijana wengi wameshinda hali ya kuachana kwa wazazi wao bila kupatwa na dhara. Wengi wao hata hujifunza kutokana na makosa ya wazazi wao na kwa hiyo katika njia fulani wanaimarishwa na yaliyowapata.c

Si lazima wakati wako ujao uwe bila uhakika. Si lazima uwe na upweke. Ukiendea marafiki wa namna ifaayo, ushikamane na kawaida ya kiroho yenye utaratibu, na ukatae kukaza fikira mno juu ya tatizo lako, wakati ujao wako waweza kuwa wenye uhakika kabisa. Bila shaka, unaweza kuwa mrefu na wenye furaha.—Mithali 3:1, 2.

[Maelezo ya Chini]

a Majina mengine yamebadilishwa.

b Makala “Vijana Wanauliza . . . Wazazi Wangu Wanaachana—Je! Napaswa Kufanya Nini?” katika toleo la Amkeni! la Januari 8, 1992, lilizungumzia baadhi ya mitego ya kuepuka, kama vile kushindwa na roho ya hasira, ya kutaka kisasi.

c Makala “Vijana Wanauliza . . . Je! Talaka ya Wazazi Wangu Itaharibu Maisha Yangu?” katika toleo la Amkeni! la Desemba 22, 1987 (Kiingereza), linaonyesha kwamba hujahukumiwa kuyarudia makosa ya wazazi wako.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazazi wako wakiachana, huenda ukahitaji marafiki zaidi ya wakati mwingine wowote. Unaweza kupata wapi marafiki wa namna ifaayo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki