Vijana Huuliza . . .
Nifanye nini wazazi wangu wanapobishana?
LAZIMA utaathiriwa na ugomvi wa wazazi wako. Unawapenda na unawategemea. Hivyo, wakati ambapo hawapatani, huenda ukashikwa na wasiwasi fulani. Kwa nini nyakati nyingine inaonekana ni kama wazazi wako hawapatani?
Maoni Yanayotofautiana
Yesu alisema kwamba mwanamume na mwanamke wanapooana, wao huwa “mwili mmoja.” (Mathayo 19:5) Je, hilo linamaanisha kwamba baba na mama yako wana maoni yaleyale kuhusu kila kitu? Sivyo. Kwa kweli, watu wawili wowote, hata mume na mke walio na umoja, hawatakubaliana nyakati zote.
Wazazi wako wakiwa na maoni tofauti, hilo halimaanishi kwamba ndoa yao inavunjika. Inawezekana sana kwamba bado wazazi wako wanapendana sana, ingawa wao hukasirishana mara kwa mara. Kwa hiyo kwa nini wao hubishana? Huenda wana njia tofauti za kuona mambo fulani. Hilo si kosa, wala halimaanishi kwamba ndoa yao haitafaulu.
Kwa mfano: Umewahi kutazama sinema na marafiki wa karibu na ukaona kwamba maoni yako yalitofautiana sana na yao kuhusu yale mliyotazama? Jambo hilo linawezekana. Hata watu walio na uhusiano wa karibu wataona mambo kwa njia tofauti.
Huenda mambo yakawa hivyo kwa wazazi wako. Labda wote wanahangaishwa na pesa za familia, lakini kila mmoja ana maoni tofauti kuhusu zinavyopaswa kutumiwa; huenda wote wanataka kupanga likizo ya familia, lakini kila mmoja ana maoni yake kuhusu tafrija inayofaa; au huenda wote wangependa ufanye vizuri shuleni, lakini kila mmoja ana wazo tofauti kuhusu unavyopaswa kuchochewa. Tunalomaanisha ni, umoja haumaanishi kuwa na maoni yaleyale. Hata watu wawili waliounganishwa na kuwa mwili mmoja wanaweza kuona mambo kwa njia tofauti.
Lakini kwa nini nyakati nyingine wazazi wako huruhusu tofauti zao ziwafanye wabishane? Kwa nini kitu kidogo kama maoni ya mtu mwingine yageuze mazungumzo kuwa mabishano?
Jinsi Kutokukamilika Kunavyochangia
Mabishano mengi kati ya wazazi huchangiwa na kutokukamilika. Biblia inasema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2) Wazazi wako si wakamilifu kama vile wewe usivyo mkamilifu. Nyakati nyingine, sisi sote husema mambo tusiyotaka, na nyakati nyingine maneno yetu yanaweza kuumiza kama “upanga unaochoma.”—Methali 12:18.
Huenda umeona jambo kama hilo. Kwa mfano, je, unaweza kukumbuka wakati ulibishana kwa ukali na mtu unayempenda? Huenda unakumbuka. “Kila mtu hubishana na wengine,” anasema kijana anayeitwa Marie.a “Kwa kweli, watu ninaowapenda zaidi wanaweza kunikasirisha zaidi, labda kwa sababu ninatazamia mengi sana kutoka kwao.” Wenzi wa ndoa Wakristo hutazamia mengi kati yao kwa sababu Biblia huwawekea kiwango cha juu. (Waefeso 5:24, 25) Kwa kuwa wao si wakamilifu, lazima mmoja au wote wawili watakosea. Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23; 5:12.
Hivyo inatazamiwa kwamba kutakuwa na mvutano fulani kati ya wazazi wako. Kwa kweli, mtume Paulo aliandika kwamba watu waliooana watakuwa na “dhiki katika mwili” au, kama tafsiri ya The New English Bible inavyosema, “maumivu na huzuni.” (1 Wakorintho 7:28) Kuwa na mwajiri anayetazamia mengi, msongamano wa magari, au gharama za ghafula, ni baadhi tu ya mivutano inayoweza kuchochea matatizo nyumbani.
Kujua kwamba wazazi wako si wakamilifu na kwamba nyakati nyingine wanaweza kuwa wanakabili hali ngumu kunaweza kukusaidia kuelewa sababu inayowafanya wabishane. Marie aliona mambo kuwa hivyo. “Wazazi wangu hugombana sana siku hizi kuliko ilivyokuwa zamani,” anasema, “na nyakati nyingine mimi hujiuliza ikiwa wamechoka kuwa pamoja. Kisha ninajiambia, ‘Ukweli ndio huu—kuishi miaka 25 katika ndoa na kuwatunza watoto watano si kazi rahisi!’” Huenda wewe pia unaweza kuonyesha “hisia-mwenzi” kwa kutambua kwamba wazazi wako wana majukumu mengi ya kutimiza.—1 Petro 3:8.
Jinsi ya Kukabiliana na Hali Hiyo
Huenda ukakubali kwamba wazazi wako si wakamilifu, na unajua kwamba wanabishana kila siku. Lakini swali bado linabaki, Unaweza kufanya nini wanapobishana? Jaribu kufuata madokezo yanayofuata:
◼ Usiingilie. (Methali 26:17) Si kazi yako kuwa mshauri wa ndoa au kuwapatanisha wazazi wako. Kujaribu kwako kuingilia hakutafaulu. “Nimejaribu kuingilia, lakini mara nyingi mimi huambiwa nisijiingize katika mambo yao,” anasema Charlene mwenye umri wa miaka 18. Acha wazazi wako wasuluhishe tatizo lao.
◼ Angalia mambo kwa njia inayofaa. (Wakolosai 3:13) Kama ilivyotajwa awali, haimaanishi kwamba wazazi wako watatengana kwa kuwa tu wanabishana mara kwa mara. Kwa hiyo, usiruhusu ugomvi mdogo kati yao ukutie wasiwasi. Melanie, mwenye umri wa miaka 20 anasema hivi kuhusu wazazi wake: “Hata wanapobishana, mimi ninajua kwamba wanapendana na wanaipenda familia yetu. Watasuluhisha tofauti zao.” Mambo yanaweza kuwa hivyo pia wazazi wako wanapotofautiana.
◼ Sali kuhusu mahangaiko yako. Hupaswi kufungia wasiwasi wako. Biblia inasema: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Sala inaweza kukusaidia. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wafilipi: “Maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.
◼ Jitunze. Si jambo la hekima kufadhaishwa na jambo ambalo huwezi kudhibiti. Kufanya hivyo kunaweza kuathiri afya yako. Biblia inasema: “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname.” (Methali 12:25) Jaribu kupunguza wasiwasi wako kwa kuwa pamoja na marafiki wenye kutia moyo na kujihusisha katika utendaji unaofaa.
◼ Zungumza na wazazi wako. Ingawa huhitaji kujihusisha katika mabishano ya wazazi wako, unaweza kuwajulisha jinsi unavyoathiriwa. Tafuta wakati unaofaa wa kuzungumza na kila mmoja wao. (Methali 25:11) Zungumza kwa ‘upole na heshima kubwa.’ (1 Petro 3:15) Usimlaumu yeyote. Eleza tu jinsi unavyoathiriwa.
Jaribu kutumia madokezo hayo. Huenda wazazi wako wakafaidika kwa sababu ya jitihada zako. Hata wasipofanya hivyo, utaridhika kujua kwamba ingawa huwezi kuwadhibiti wazazi wako, unaweza kutenda kwa njia inayofaa wanapobishana.
[Maelezo ya Chini]
a Majina katika makala hii yamebadilishwa.
MAMBO YA KUFIKIRIA
◼ Kwa nini nyakati nyingine wazazi hawapatani?
◼ Unaweza kumwambia nini mdogo wako ambaye anaathiriwa na kubishana kwa wazazi wako?
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
TAARIFA KWA WAZAZI
Ni kawaida kwa wenzi wa ndoa kutofautiana. Hata hivyo, unaweza kuchagua jinsi ya kushughulikia hali kama hiyo. Vijana huathiriwa sana wazazi wao wanapobishana. Hilo ni jambo zito kwani ndoa yako ni kielelezo ambacho huenda watoto wako watafuata watakapofunga ndoa. (Methali 22:6) Kutofautiana kunapotokea, kwa nini usitumie pindi hiyo kuonyesha njia zinazofaa za kutatua matatizo? Jaribu kufanya mambo yafuatayo:
Sikiliza. Biblia inatuambia tuwe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema, si wepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Usiweke mafuta kwenye moto kwa ‘kulipa uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Hata mwenzi wako akionekana kuwa hataki kusikiliza, wewe sikiliza.
Jaribu kueleza badala ya kulaumu. Kwa utulivu, mwambie mwenzi wako jinsi mwenendo wake umekuathiri. (“Mimi huumia unapo . . . ”) Jizuie hata unapohisi unataka kumshutumu au kumlaumu. (“Wewe hunijali.” “Hunisikilizi hata kidogo.”)
Tulia Kwanza. Nyakati nyingine ni afadhali kuacha mazungumzo kisha uyarudie wakati hasira zimepungua. Biblia inasema: “Mwanzo wa ugomvi ni kama mtu anayefungulia maji; kwa hiyo kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.”—Methali 17:14.
Wazazi wanapaswa kuombana msamaha na inapofaa kuwaomba watoto msamaha. Brianne aliye na umri wa miaka 14 anasema: “Mara nyingine baada ya kugombana, wazazi huniomba mimi na kaka yangu msamaha kwa sababu wanajua jinsi tunavyoathiriwa.” Jambo moja muhimu zaidi unaloweza kuwafundisha watoto wako ni kusema “Samahani,” kwa unyenyekevu.
Kwa habari ya ziada, ona gazeti la Amkeni! la Januari 8, 2001 (1/8/2001), ukurasa wa 8-14, na Januari 22, 1994 (1/22/1994), ukurasa wa 3-12.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Usimlaumu yeyote. Eleza tu jinsi unavyohisi