Maoni ya Biblia
Je, Ni Vibaya Kula Nyama?
“TAZAMA, NIMEWAPA KILA MCHE UTOAO MBEGU, ULIO JUU YA USO WA NCHI YOTE PIA, NA KILA MTI, AMBAO MATUNDA YAKE YANA MBEGU; VITAKUWA NDIVYO CHAKULA CHENU.”—Mwanzo 1:29.
SUJATA mwenye umri wa miaka 18, ambaye ni wa familia ya Kihindu ya wala mboga, alikubaliana haraka na mashauri ya ulaji ya Mungu kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Lakini akauliza mara moja: “Kwa nini, basi, watu huua wanyama kwa ajili ya chakula wakati kuna vitu vingine vingi sana vya kula?”
Watu wengi kote ulimwenguni hujiuliza mambo haya. Mamia ya mamilioni katika Mashariki hula milo isiyo na nyama. Kwa kuongezea, idadi ya wala mboga katika Magharibi inaongezeka. Katika Marekani peke yake, karibu watu milioni 12.4 hudai kuwa wala mboga, karibu milioni 3 zaidi ya mwongo uliopita.
Kwa nini watu wengi sana hupendelea ulaji usio na nyama? Ni nini maoni yanayofaa kuhusu uhai wa wanyama? Je, kula nyama huonyesha kutoheshimu uhai? Kulingana na yale yaliyoandikwa kwenye Mwanzo 1:29, je, ni vibaya kula nyama? Kwanza, fikiria kwa nini wengine hawali nyama.
Kwa Nini Wengine Hawali Nyama?
Kwa Sujata, ulaji wake huhusisha itikadi zake za kidini. “Nililelewa nikiwa Mhindu, nikiamini katika fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine,” yeye aeleza. “Kwa kuwa nafsi ya kibinadamu yaweza kurudi ikiwa mnyama, nawaona wanyama kuwa sawa na mimi. Hivyo yaonekana kuwa vibaya kuwaua kwa chakula.” Dini nyinginezo pia hupendekeza ulaji wa mboga.
Mambo mengine zaidi ya itikadi za kidini pia huathiri machaguo ya watu ya vyakula. Kwa kielelezo, Dakt. Neal Barnard, asisitiza hivi: “Sababu tu za kula nyama ni tabia au kutokujua.” Msimamo wake thabiti unategemea maoni yake kuhusu hatari za kiafya za kula nyama, kama vile maradhi ya moyo na kansa.a
Katika Marekani, matineja wanasemekana kuwa sehemu inayokua haraka zaidi ya wala mboga. Sababu moja ikiwa hangaiko kwa wanyama. “Watoto hupenda wanyama,” asema Tracy Reiman wa shirika la Watu wa Kutetea Wanyama Watendewe Ifaavyo. “Waanzapo kujifunza juu ya linalowapata wanyama kabla hawajauawa kwa chakula inaongeza tu huruma wanayohisi.”
Wengi wanaohangaikia mazingira pia hufahamu uhusiano uliopo kati ya ulaji wao na dai kubwa mno linalofanywa juu ya mali ya asili katika kulea wanyama kwa ajili ya chakula. Kwa kielelezo, inachukua karibu lita 3,300 za maji kutokeza kilogramu moja tu ya nyama ya ng’ombe na lita 3,100 kwa kilogramu moja ya nyama ya kuku. Kwa wengine, hii inakuwa sababu ya kuepuka nyama.
Namna gani wewe? Je, wapaswa kujiepusha kula nyama? Kabla ya kujibu swali hilo, fikiria maoni mengine. Kama yapatikanavyo katika Zaburi 50:10, 11, Yehova Mungu, Mfanyi wa vitu vyote asema: “Kila hayawani ni wangu, na makundi juu ya milima elfu. Nawajua ndege wote wa milima, na wanyama wote wa mashamba ni wangu.” Kwa vile wanyama wote kwa kweli ni wa Mungu, ni jambo la maana kuelewa jinsi Muumba anavyohisi kuhusu uhai wa wanyama na wanadamu kuwatumia kwa chakula.
Je, Ni Vibaya Kuua Wanyama?
Wengine, kama Sujata, ambao huwaona wanyama kuwa sawa na wanadamu huhisi kwa nguvu kwamba kutoa uhai wa mnyama kwa sababu yoyote ni kosa — na hasa kuwaua kwa ajili ya chakula. Hata hivyo, Maandiko huonyesha kuwa Mungu hutofautisha kati ya uhai wa wanyama na uhai wa wanadamu nayo huruhusu uuaji wa wanyama kwa sababu mbalimbali. Kwa kielelezo, katika Israeli mnyama angeuawa ikiwa angekuwa tisho kwa uhai wa mwanadamu au mifugo ya mtu. — Kutoka 21:28, 29; 1 Samweli 17:34-36.
Tokea nyakati za zamani, Mungu aliidhinisha toleo la wanyama wakiwa dhabihu katika ibada. (Mwanzo 4:2-5; 8:20, 21) Pia aliwaagiza Waisraeli wakumbuke Kutoka kwao Misri kwa kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa kila mwaka, ambayo ilitia ndani kudhabihu kondoo au mbuzi na kula nyama yake. (Kutoka 12:3-9) Na chini ya Sheria ya Kimusa, kulikuwa na pindi nyingine kwa ajili ya dhabihu za wanyama.
Mwanamke mmoja Mhindu, mwenye umri wa miaka 70, alipoisoma Biblia kwa mara ya kwanza, alipata lile wazo la dhabihu za wanyama kuwa lisilopendeza. Lakini kadiri alivyoendelea katika ujuzi wake juu ya Maandiko, aliweza kuona kuwa dhabihu zilizoagizwa na Mungu zilikuwa na kusudi. Zilielekeza mbele kwenye dhabihu ya Yesu Kristo, ambayo ingetimiza takwa la kisheria kwa ajili ya msamaha wa dhambi. (Waebrania 8:3-5; 10:1-10; 1 Yohana 2:1, 2) Katika visa vingi yale matoleo yalitumika kama chakula kwa makuhani na nyakati nyingine kwa waabudu. (Mambo ya Walawi 7:11-21; 19:5-8) Mungu, ambaye kila kiumbe hai ni chake, angeweza kuweka kwa haki mpango kama huo kwa kusudi fulani. Bila shaka, Yesu alipokufa dhabihu za wanyama hazikuhitajika tena katika ibada. — Wakolosai 2:13-17; Waebrania 10:1-12.
Kutumia Wanyama kwa Chakula
Lakini, namna gani kuua wanyama kwa chakula? Ni kweli kwamba ulaji wa mwanadamu mwanzoni ulikuwa wa mboga. Lakini baadaye Yehova aliupanua akitia ndani nyama ya wanyama. Miaka 4,000 hivi iliyopita—katika siku za Noa mwadilifu—Yehova alileta gharika ya tufeni pote na akaleta mwisho wa uovu uliokuwapo duniani wakati huo. Noa, familia yake, na viumbe vilivyo hai alivyoviingiza ndani ya safina waliokoka hilo Furiko. Baada ya wao kutoka katika safina, Yehova alisema kwa mara ya kwanza: “Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapeni hivi vyote.” (Mwanzo 9:3) Hata hivyo, wakati uleule Mungu alitoa sheria: “Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu, maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu.” (Mwanzo 9:6) Kwa wazi, Mungu hakuweka wanyama katika kiwango kimoja na wanadamu.
Kwa hakika, usadikisho wa Sujata juu ya wanyama ulitegemea itikadi katika lile fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine. Kuhusu hili Biblia hueleza kwamba ingawa wanadamu na wanyama ni nafsi, nafsi si isiyoweza kufa. (Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4, 20; Matendo 3:23; Ufunuo 16:3) Wakiwa nafsi, wanadamu na wanyama hufa na hukoma kuwako. (Mhubiri 3:19, 20) Hata hivyo, wanadamu wana taraja la ajabu la ufufuo katika ulimwengu mpya wa Mungu.b (Luka 23:43; Matendo 24:15) Hili pia laonyesha kuwa wanyama hawako sawa na wanadamu.
“Hata hivyo, kwa nini badiliko hilo katika ulaji?” Sujata alitaka kujua. Yaonekana tabia ya nchi ilibadilika sana kwa sababu ya Furiko. Iwe Yehova aliongeza mlo wa nyama katika ulaji wa mwanadamu kwa sababu alitazamia mahitaji ya vizazi vya wakati ujao ambavyo vingeishi katika sehemu ambazo mboga zingekuwa chache, Biblia haisemi. Lakini Sujata angeweza kukubali kwamba Mmiliki wa vitu vyote vilivyo hai alikuwa na haki ya kuleta badiliko.
Kuonyesha Staha kwa Ajili ya Uhai wa Wanyama
Lakini, Sujata alistaajabu, ‘Hatupaswi angalau kuonyesha staha kwa uhai wa wanyama?’ Ndiyo, twapaswa. Na Muumba wa vitu vyote ametuambia tuwezavyo kufanya hivyo. “Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile,” lasema agizo lake kwenye Mwanzo 9:4. Kwa nini kuna katazo juu ya kula damu? “Kwa kuwa uhai wa mwili u katika hiyo damu,” Biblia husema. (Mambo ya Walawi 17:10, 11) Yehova ameweka masharti: ‘Imwageni damu ya mnyama aliyechinjwa juu ya nchi kama maji.’—Kumbukumbu la Torati 12:16, 24.
Hii haimaanishi kuwa kuruhusiwa kula nyama ni kibali cha kumwagamwaga damu ya wanyama bila sababu kwa ajili tu ya msisimuko wa kuwinda au kuonyesha ushujaa wa kibinafsi. Kwa wazi Nimrodi alifanya hivyo. Biblia humtambulisha kuwa “mwindaji mwenye nguvu katika kupingana na Yehova.” (Mwanzo 10:9, NW) Hata leo, msisimuko wa kuwinda na kuua wanyama waweza kukua kwa urahisi ndani ya wengine. Lakini roho kama hiyo huenda sambamba na kupuuza kikatili uhai wa wanyama, na Mungu hakubaliani nayo.c
Kuwa Wenye Huruma Kuelekea Wanyama
Wala mboga wengine pia wana moyo mweupe wa kuhangaikia jinsi wanyama wanavyotendwa na biashara za kisasa za nyama. “Biashara ya mifugo haipendezwi na silika za kiasili za wanyama,” chataja kitabu The Vegetarian Handbook. “Wakifugwa katika vyumba vilivyosongamana vibaya na mazingira yasiyo ya asili,” kitabu hicho chasema, “wanyama wa siku hizi hutumiwa vibaya zaidi kuliko wanyama wa wakati mwingine wowote.”
Ingawa Mungu hakatazi kutumia wanyama kwa chakula, anakataza kuwatenda kikatili. “Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake,” Biblia husema kwenye Mithali 12:10. Na Sheria ya Kimusa iliamuru wanyama watunzwe ifaavyo. — Kutoka 23:4, 5; Kumbukumbu la Torati 22:10; 25:4.
Je, Mkristo Apaswa Kuwa Mla Mboga?
Kama ilivyoonyeshwa mwanzoni, swali la kuwa mla mboga—au kuendelea kuwa mla mboga—kwa kweli ni uamuzi wa mtu binafsi. Kwa sababu ya afya, uchumi, ikolojia, au huruma kwa wanyama, mtu aweza kujichagulia kufuata kanuni za wala mboga. Lakini lazima atambue kuwa hiyo ni njia moja tu ya kula. Hapaswi kuchambua wale wachaguao kula nyama, kama vile yule alaye nyama hapaswi kumhukumu mla mboga. Kula nyama au kujizuia kuila hakumfanyi mtu kuwa bora zaidi. (Waroma 14:1-17) Wala ulaji wa mtu haupaswi kuwa hangaiko kuu maishani mwake. “Binadamu lazima aishi,” Yesu alisema, “si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.
Kuhusu ukatili kwa wanyama na kutumia vibaya mali ya dunia, Yehova ameahidi kuleta mwisho wa mfumo huu uliopotoka na wenye pupa na kuubadilisha na ulimwengu mpya atakaoufanyiza. (Zaburi 37:10, 11; Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13) Katika ulimwengu huo mpya, mwanadamu na wanyama watakuwa pamoja kwa amani ya milele, na Yehova ‘atakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zaburi 145:16; Isaya 65:25.
[Maelezo ya Chini]
b Ona Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1997, ukurasa wa 3-8, lililochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]
Punch