Watu Wafundishwao Kupenda
UPENDO ni shauku inayotegemea uvutio, nia ya kutenda mema, au kuwa na mapendezi yaliyo sawa. Upendo ni ufungamano mchangamfu. Upendo hauna ubinafsi, ni wenye uaminifu-mshikamanifu, nao waonyesha hangaiko la kutendea wengine mema. Upendo ni kinyume kabisa cha chuki. Mtu achochewaye na chuki hujishughulisha mno na harara zake; mtu achochewaye na upendo huwafikiria wengine.
Upendo au chuki—ni ipi hudhibiti maisha yako? Hili ni swali la kufaa sana kwa sababu wakati wako ujao udumuo milele wategemea hilo jibu. Ingawa wanaishi katika ulimwengu ufundishwao kuchukia, mamilioni ya watu wanajifunza kupenda. Wao hufanya hivyo kwa kujivika utu mpya. Wao hawazungumzi tu kuhusu upendo; wanajitahidi sana kuzoea kuonyesha upendo.
Ikiwa umepata kuhudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova, huenda ukawa ulivutiwa na yale uliyoyaona. Bila kujali mtu ni wa taifa gani, Mashahidi wa Yehova wameungana katika ibada. Wao wamefanyiza udugu wa kweli wa kimataifa. Hii yaweza kuonekana katika makutaniko ya kwao na katika mikusanyiko yao lakini labda mahali bora zaidi ni katika zile waziitazo familia za Betheli. Hivi ni vikundi vya wajitoleaji ambao huishi na kufanya kazi pamoja, wakiwa familia, wakitokeza na kugawanya fasihi za Biblia. Katika kila nchi, baadhi yao wanasimamia kazi ifanywayo na Mashahidi wa Yehova huko. Hiyo si kazi rahisi, kwa kuwa inahusisha—kufikia mwaka wa 1997—zaidi ya makutaniko 82,000 katika nchi 233. Ili kujazia uhitaji huo, zaidi ya watu 16,000 hutumikia katika familia za Betheli ulimwenguni kote, kutia ndani makao makuu na majengo kadhaa madogo-madogo ya ofisi ya tawi katika nchi 103.
Familia nyingi za Betheli zimefanyizwa hasa kwa wenyeji wa nchi ambamo ofisi hiyo ya tawi imo. Lakini si wote ni wenyeji. Familia nyingine za Betheli zimefanyizwa kwa Mashahidi wa mataifa, makabila, au jamii mbalimbali na vilevile watu ambao zamani walikuwa na malezi tofauti ya kidini. Kwa kielelezo, katika familia ya Betheli ya karibu watu 1,200 iliyoko Selters, Ujerumani, mataifa yapatayo 30 yamewakilishwa. Ni nini huwawezesha kuishi, kufanya kazi, na kuabudu pamoja kwa amani na muungano, katika mazingira yasiyo na chuki? Hao wanafuata shauri la Biblia katika Wakolosai 3:14, lisemalo:
“Jivikeni Wenyewe Upendo”
Hakuna mtu azaliwaye akiwa amejivika kabisa, wala mtu hajiviki kwa kuzungumza tu juu ya kujivika. Kuvaa kwatia ndani kufanya maamuzi hususa na kisha kujikakamua kuvaa. Vivyo hivyo, mtu hazaliwi akiwa amejivika upendo. Kuzungumza tu juu ya upendo hakutoshi. Jitihada inahitajika.
Kujivika hutumikia makusudi kadhaa. Hulinda mwili, husitiri sehemu za mwili zisizopendeza au kutokamilika, na kwa kadiri fulani hufunua utu wa mtu. Na ndivyo ilivyo na upendo. Hiyo hutumika kuwa ulinzi kwa sababu kupenda kanuni zenye uadilifu na ushirika ufaao huchochea mtu aepuke ushirika au mahali mbalimbali pawezapo kuwa hatari. Huo hutumika kulinda mahusiano ya kibinafsi, ambayo tunapaswa kuyapenda. Yeye apendaye aelekea zaidi kupendwa, na yule ambaye hujiepusha kudhuru wengine aelekea zaidi kutodhuriwa mwenyewe.
Upendo husitiri pia sehemu za utu wetu zisizopendeza, ambazo huenda zikawa zenye kuudhi wanadamu wenzetu. Je, haielekei zaidi kwamba tunapuuza mapungufu madogo-madogo ya watu ambao ni wenye upendo kuliko ya watu ambao ni wenye kiburi, wenye kujigamba, na wakosao upendo?
Watu ambao hujivika upendo hufunua uzuri wa utu ulio kama wa Kristo. Ingawa uzuri wa kimwili ni wa kijuujuu tu, uzuri wa kiroho huenea kote katika mtu. Labda unajua watu ambao unawaona kuwa wazuri, si kwa sababu ya sura zao, bali kwa sababu ya utu wao ambao kwa kweli ni mchangamfu. Kwa upande mwingine, wengi wetu tumekutana na wanawake wazuri au wanaume wenye sura nzuri ambao hawatuvutii tena kamwe mara tu utu wao halisi ulipodhihirika. Inapendeza kama nini kuwa na watu ambao wamejivika upendo!
Kubadilisha Chuki na Upendo
Jambo la kwamba chuki yaweza kubadilishwa na upendo laonyeshwa na uchunguzi uliofanywa katika mwaka wa 1994 kati ya Mashahidi wa Yehova 145,958 walio nchini Ujerumani.
Kunywa kupindukia, matumizi mabaya ya madawa, uhalifu, kucheza kamari, na tabia za kutopatana na watu au zenye ujeuri, zote kwa njia moja au nyingine, ni maonyesho ya ubinafsi, ambayo yaweza kutokeza chuki kwa urahisi. Lakini asilimia 38.7 kati ya wale waliohojiwa walisema kwamba ili kufikia viwango vya juu vya Biblia vinavyotetewa na Mashahidi, walikuwa wameshinda moja au zaidi kati ya matatizo hayo. Kumpenda Mungu na viwango vyake vyenye uadilifu vya mwenendo kuliwachochea wafanye hivyo. Msaada wenye upendo ulitolewa na Mashahidi wa Yehova, mara nyingi ana kwa ana. Katika miaka mitano ambayo imepita (1992-1996), watu 1,616,894 katika nchi 233 walisaidiwa kufanya mabadiliko, wakishinda chuki kwa upendo wenye kushinda mambo yote.
Kwa kutumia upendo usio na ubinafsi katika ndoa zao, Mashahidi wa Yehova hupata mahusiano thabiti. Katika nchi fulani ndoa moja kati ya kila ndoa mbili au tatu huishia talaka. Lakini huo uchunguzi uliotajwa hapo juu ulionyesha kwamba kwa wakati huu ni asilimia 4.9 pekee ya Mashahidi ambao wametaliki au wametengana na wenzi wao. Lakini, isisahaulike kwamba idadi kubwa kati ya hao walitaliki kabla ya wao kuwa Mashahidi wa Yehova.
Kwa kuwa Mungu wa upendo ni Mfunzi Mtukufu ambaye huwafundisha njia zake wale wampendao, Mashahidi wa Yehova huelekeza upendo wao, kwanza kabisa, kwake. Tofauti na watu wengine, ambao huenda wakawa wenye ‘kupenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu,’ Mashahidi wa Yehova humtanguliza Mungu. (2 Timotheo 3:4) Tofauti na njia za ulimwengu huu zisizo na kanuni, Shahidi wa kawaida hutumia muda wa saa 17.5 kila juma katika utendaji mbalimbali wa kidini. Kwa wazi Mashahidi hufikiria mambo ya kiroho. Hilo ndilo jambo liwafanyalo wawe na furaha. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.”—Mathayo 5:3.
Mtumishi wa kweli wa Mungu, asema mwandikaji wa Zaburi 118, hahitaji kuhofu wanadamu. “BWANA yuko upande wangu, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?” (Mstari wa 6) Itibari kabisa katika Mungu huondosha mojawapo ya visababishi vya kuchukia na kuhofu wanadamu wengine.
Mkristo, akijua kwamba Mungu ni “mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli,” atajitahidi kuondosha hasira maishani mwake, kwa kuwa hiyo inaweza kuwa kisababishi kingine cha chuki. Kusitawisha matunda ya roho ya Mungu, kutia ndani upole na kujidhibiti, kutamsaidia atimize jambo hili.—Zaburi 86:15; Wagalatia 5:22, 23.
Mkristo wa kweli ni mnyenyekevu naye hajifikirii zaidi kuliko impasavyo. (Waroma 12:3) Yeye husitawisha upendo anaposhughulika na wengine. Kwa kutofautisha na chuki, upendo “haupati kuwa wenye kuchokozeka. Hauweki hesabu ya ubaya.”—1 Wakorintho 13:5.
Ndiyo, hofu, hasira, au hisia ya kupatwa na madhara zaweza kuwafanya watu kuchukia. Lakini upendo, kwa kuiondoshea chuki msingi wake, huishinda. Kwa kweli, upendo ndio kani yenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote mzima kwa sababu “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
Karibuni Chuki Itatoweka Milele
Kwa kuwa ubinafsi na chuki si sehemu ya utu wa Yehova Mungu, hizo haziwezi kudumu milele. Kuna haja ya kwamba ni lazima ziondolewe, zikabadilishwe na upendo, ambao utadumu milele. Ikiwa ulimwengu usio na chuki, na uliojaa upendo, ndio aina ya ulimwengu unaotamani, acha Mashahidi wa Yehova wakuelezee kutoka kwenye Biblia matakwa ya kuweza kuishi ili kuuona.
Ndiyo, kila mmoja wetu angefanya vizuri kuuliza, ‘Ni sifa ipi inayodhibiti maisha yangu, upendo au chuki?’ Hili ni swali la kufaa sana. Mtu amfuataye mpinzani wa Mungu, mungu wa chuki, hataishi kwa muda mrefu. Mtu amfuataye Yehova, Mungu wa upendo, ataishi milele!—1 Yohana 2:15-17.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Hata leo watu waweza kujivika upendo