Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 1/15 kur. 35-39
  • Sifa za Kimungu za Upendo na Chuki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sifa za Kimungu za Upendo na Chuki
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIFA YA KIMUNGU YA UPENDO
  • SIFA YA KIMUNGU YA CHUKI
  • “Wakati wa Kupenda na Wakati wa Kuchukia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Watu Wafundishwao Kupenda
    Amkeni!—1997
  • Upendo (Agape)—Usivyo na Ulivyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Njia Pekee ya Kukomesha Chuki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 1/15 kur. 35-39

Sifa za Kimungu za Upendo na Chuki

“Yachukieni mabaya; yapendeni mema.”​—Amosi 5:15.

1. Je! inafaa Mkristo apende na kuchukia pia?

UPENDO na chuki. Je! mtu aweza kuwa na sifa hizi zilizo tofauti akampendeza Mungu? Ndiyo, kulingana na mwandikaji wa Biblia Amosi. Aliongozwa kwa roho awaamuru watu wa kale wa Mungu, taifa la Israeli: “Yachukieni mabaya; yapendeni mema.” (Amosi 5:15) Katika maana ile ile mwandikaji wa mapema zaidi wa Biblia, Sulemani, alisema kuna “wakati wa kupenda, na wakati wa kuchukia.”​—Mhu. 3:8.

2. (a) Watu wengi wanaonyeshaje upendo na chuki? (b) Mtu anapata maoni yafaayo juu ya upendo wa kimungu wapi?

2 Upendo na chuki ni maneno yanayoeleweka vibaya mara nyingi leo. Hakuna neno jingine lo lote ambalo habari zake zimeandikwa, zikazungumzwa na kuimbwa kama neno “upendo,” lakini je! ni watu wangapi wawezao kukuambia maana yake hasa? Watu wanasemekana kupenda michezo, televisheni, magari, na hata mapaka na mbwa. Kwa upande mwingine, watu wanasemekana kuchukia mambo kama vile kushindania utajiri, Ukomunisti, utawala wa kutumia nguvu na namna nyingine za serikali. Wanachukia kodi na mamlaka pia. Mara nyingi kunakuwa na chuki nyingi kati ya watu wa mataifa na makabila mbalimbali, kati ya matajiri na wafanya kazi, kati ya matajiri na maskini. Je! hii ndiyo namna ya upendo na chuki ambayo waandikaji wa Biblia wanazungumza juu yake? Je! wewe kama Mkristo umeongozwa na maoni ya ulimwengu yaliyopotolewa juu ya upendo na chuki? Sasa tunapozichunguza sifa za kimungu za upendo na chuki, utasaidiwa ulione jibu. Kwanza, na tuichunguze sifa ya kimungu ya upendo kwa kirefu, kama inavyoelezwa na mtume Paulo kwa uongozi wa roho katika 1 Wakorintho 13:4-8.

SIFA YA KIMUNGU YA UPENDO

3. Eleza matendo ya mtu ‘mvumilivu na mfadhili’ yalivyo.

3 “Upendo huvumilia, hufadhili” Hii maana yake si kuvumilia ugumu tu bali kuvumilia hali zisizofaa bila kuchoka. Katika jamaa, Wakristo wenye upendo wa kimungu hawavumilii makosa ya mtu na mwenzake tu. Ndiyo, bila kuchoka ‘wanachukuliana na kusameheana mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake.’ (Kol. 3:13) Hata katika uhusiano wa karibu kama ule wa mume na mke, maoni yanayotofautiana yanahitaji kuonyeshwa kwa upendo huu. Kwa mfano, huenda mwenzi mmoja akafurahia kutembelea rafiki fulani au watu wa jamaa mara kwa mara. Huenda hili lisiwe linampendeza sana yule mwingine. Je! tusisitizie kufuata njia yetu wenyewe, au twende pamoja kwa manung’uniko, tukiufanya wakati huo usiopendeza kwa wote? Mtu mwenye upendo wa kimungu atasitawisha kupendezwa na kufurahia linalompendeza mwenzake. Nje ya kundi la Kikristo mtu anaweza kupata nafasi zaidi kuonyesha uvumilivu anapozungumza na majirani na wengine juu ya habari njema za Biblia. Huenda wengine wakaitikia kwa kukosa adabu au kwa jeuri sana juu ya mazungumzo yanayomhusu Yehova Mungu na makusudi yake. Je! mhudumu wa Kikristo mwenye upendo atataka alipize kisasi kwa maneno makali au yasiyo ya adabu? Sivyo, kwa maana yeye ni ‘mvumilivu na mfadhili.’

4. Ni kwa njia gani wivu unavyoweza kujionyesha wazi, na upendo una maoni gani juu ya mambo?

4 “Upendo hauhusudu.” Hali za watu wa Yehova ni nyingi na za namna mbalimbali, wengine wakiwa maskini wa vitu vya kimwili huku wengine wakiwa wenye fedha. Wale walio maskini na wale wenye mali pia wako sawa machoni pa Yehova. Kwa hiyo je! kuna sababu yo yote kwa wasio na mali kutamani vitu vya kimwili vya ndugu zao, au imewapasa wawaonee ndugu zao uchungu kwa sababu hiyo? Nia hiyo yaweza kupenya katika Mkristo polepole ikiwa anahusudu au ni mwenye wivu. Kumbuka, Biblia haikatazi fedha, bali “kupenda fedha.” (1 Tim. 6:9, 10; Ebr. 13:5) Au, katika maana tofauti, pengine ndugu yako wa Kikristo amepewa mapendeleo fulani kundini. Wewe ulipitwa, ijapokuwa sikuzote ulijisikia ulikuwa na uwezo mwingi kumpita yeye. Sasa wajisikiaje? Je! unaona wivu kidogo tu? Upendo wa Mungu hauoni wivu. Hautatufanya tuwaone ndugu zetu kama adui; bali, tutafurahia kuona wengine wakifanya maendeleo. Tu wenye furaha tu na twaridhika kuwa na mahali katika tengenezo la Yehova.

5. Unyenyekevu unajionyeshaje wazi?

5 “Upendo hautakabari; haujivuni.” Tunaozungumza juu yao au mambo tunayoyazungumza ni njia nzuri ya kuona namna tulivyo katika habari hii. Je! unaona kwamba unazungumza juu yako mwenyewe kidogo, sikuzote ukijaribu kwa werevu kusimamia mazungumzo huku ukijaribu kujifanya kwamba hutaki fikira zikazwe kwako mwenyewe? Je! sikuzote wewe ndiye mwenye kusimulia mambo yaliyoonwa, ukisimulia mambo uliyoyatimiza maishani? Je! nia yako ya kusimulia mambo hayo yaliyoonwa ni kwa sababu unajaribu kuwatia ndugu zako moyo, au unajaribu kujionyesha? Bila shaka ni jambo jema kusimulia mambo yaliyoonwa juu ya utumishi wa shambani, nako hata kwastahili kutiwa moyo, lakini Mkristo mwenye upendo hataonyesha kwamba yeye ndiye aliyewasaidia wengine hasa. Bali, sikuzote atampa Yehova sifa. Ni huruma na inafaa kama nini kuuliza wengine waseme na kusikia watakavyosema! Ni wonyesho wa unyenyekevu, ambalo ni jambo mojawapo la kuonyesha upendo wa kimungu.​—1 Pet. 4:11.

6, 7. Huenda kukosa adabu kukajionyeshaje wazi?

6 Upendo “haukosi kuwa na adabu.” Tafsiri nyingine zinasema, Upendo si “jeuri,” “haushtui watu.” (New English Bible; Byington) Kuna mambo mengi yanayokosa adabu kabisa, kama vile uasherati, uchafu na hasira za ghafula. (Rum. 13:13) Walakini, je! umepata kufikiri kwamba tabia mbaya zinakosa adabu? Kwa mfano, watoto mara nyingi wanaruhusiwa waseme kupita kiasi penye mazungumzo watu wazima wakiwapo, au kuyakatiza kwa kukimbia-kimbia hapo wakipiga kelele. Nyakati nyingine wanapaka-paka peremende wanazotafuna katika viti au kuandika kuta au viti katika jumba la kukutania la Kikristo. Je! huku si kukosa adabu? Wazazi wapendao watoto wao hawawaruhusu ‘wakose kuwa na adabu’ hata katika njia hizi.​—Linganisha Kumbukumbu la Torati 23:14.

7 Katika maandiko upendo na ukarimu vinashirikishwa sana. (Ebr. 13:1, 2; 1 Pet. 4:8, 9) Kwa hiyo je! twawaonaje wale wanaohamia kundi letu? Pengine wameuza nyumba yao na kuacha kazi zao waje na kulisaidia kundi la mahali petu. Huenda hata wakawa wanatumia wakati wao wote kuhubiri waziwazi. Je! ‘tunakosa kuwa na adabu’ kwa kuwatendea kwa uadui? Je! tunakuwa wenye mashaka kwa sababu huenda wakasema kwa lafudhi tofauti au kuvalia kwa mtindo tofauti kidogo? Upendo wa kimungu unatuongoza tuonyeshe ukarimu wenye uchangamfu wa Kikristo. Tunaongozwa tufanye tuwezayo kusaidia na kuwafanya wajisikie wamestarehe.​—Rum. 12:13.

8. Upendo wa kimungu unatafuta faida za nani? Toa mfano.

8 Upendo “hautafuti mambo yake”; bali, unaongozwa na kanuni iliyotajwa mapema na Paulo: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.” (1 Kor. 10:24) Penye makusanyiko ya Kikristo je! unasukuma au kukumba wengine ili utangulie? Je! unajiwekea viti vya akiba bila ya kuwafikiria wengine? Au katika kundi la mahali petu huenda yakawako maeneo fulani mtaani ambayo yamekuwa yenye matokeo sana ziara zilipofanywa nyumbani katika kazi ya kuhubiri huku sehemu nyingine huenda zikajulikana kama zisizo na watu wenye kupendezwa. Je! sikuzote tunasisitizia kupata sehemu zinazofaa zaidi kwa kazi yetu ya kuhubiri? Je! tunaziona kama zetu, tusitake wengine wazuru katika maeneo haya? Je! twaweza kumwazia Kristo Yesu akiwa na maoni hayo juu ya mambo? Upendo wa kimungu utatufanya tuweke faida zetu wenyewe nyuma.

9. Toa mfano wa namna upendo wa kimungu utatusaidia tuwe na maoni yafaayo juu ya matendo ya wengine.

9 Upendo “hauoni uchungu.” Unaposafiri kwa gari, unaonaje mtu fulani akipita mbele yako kwa haraka? Wewe unafanyaje unaposimamishwa na taa za kuongoza magari na mwendeshaji aliye nyuma yako anapiga honi wakati ule ule tu inapokuja taa ya rangi nyingine? Je! unakwenda polepole sana ati umwonyeshe mtu huyo kwamba hakuna faida ya kutosubiri? Mtu mwenye upendo wa kimungu hajiachi aone uchungu kwa sababu ya adabu mbaya zinazoonyeshwa na ulimwengu huu. Kwa sababu gani Mkristo achukie kwa sababu kodi zinapanda na utumishi mwingi unaharibika? Je! huu si ushuhuda zaidi ya mambo? Katika kundi, haiwapasi wazee na watumishi wa huduma wakasirike au kuona uchungu kwa sababu wengine wanakosa kutoa ripoti fulani wakati ufaao wala kwa sababu wengine hawaelekei kuthamini kabisa ujumbe wa Neno la Mungu Biblia. Upendo wa kimungu unaachilia kutokamilika kwa kibinadamu na kukubali haki ya kila mtu kuamua atakavyouitikia upendo wa Mungu.

10. Upendo unatusaidiaje katika uhusiano wetu na Yehova na ndugu zetu?

10 Upendo “hauhesabu mabaya.” Je! wewe unakumbuka jambo fulani ulilotendwa miaka mitano au kumi iliyopita? Pengine uliudhiwa, lakini haipatani kabisa na Neno la Mungu kufuatia mambo hayo wala kukumbusha-kumbusha yaliyopita. Mtu anayefuatia makosa aliyotendwa na kuweka kinyongo moyoni hajifaidi mwenyewe wala wengine. Maoni yake yasiyofaa yanamfanya akose furaha mwenyewe na walio karibu naye pia. Uhusiano wake wenyewe na Yehova unahusika, kwa maana mtu kama huyo awezaje kusali, “Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu”? (Mt. 6:12) Kama vile asemavyo Yakobo: “Kwa maana yeye asiyezoea rehema atapata hukumu yake bila rehema.” (Yak. 2:13, NW) Lo! ni jambo jema namna gani, mwishoni mwa siku tunapomfikia Yehova katika sala na kuuomba msamaha wake, kujua kwamba sisi hatukuhesabu mabaya!​—Mt. 18:21, 22; Efe. 4:26.

11. Ni nini kinachomtambulisha mtu ambaye “hufurahi pamoja na kweli”?

11 Upendo “haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli.” Mtu anayelithamini jambo hili la upendo wa kimungu hatafuti kujifurahisha kwa vitabu, vipindi vya televisheni, au sinema zinazoonyesha uovu. Bali, watu hao wanaonyesha kwamba ‘wanafurahi pamoja na kweli’ kwa wanayoyazungumza kila siku na nyakati za kuburudika. Yesu alisema: “Maana, kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.”​—Mt. 12:34.

12. Kwa sababu gani Mkristo “huvumilia yote”? Toa mfano.

12 Upendo “huvumilia yote.” Usemi huu unamaanisha kwa halisi “mambo yote unayafunika.” (1 Kor. 13:7, Interlinear) Unafunika kama dari isiyopenywa na maji, ikilinda vilivyoko chini. Unakinga, unazuia. Kwa hiyo neno hilo lamaanisha pia kustahimili. (1 Kor. 9:12; 1 The. 3:1, 5) Upendo wa kimungu unaona mambo kama yalivyo; hautazamii ukamilifu kwa watu wasiokamilika. Una nia ya kuvumilia mengi nao hauna wepesi wa kukasirika. Wakati mshiriki wa jamaa yetu au wa kundi la Kikristo afanyapo kosa, badala ya kulitangaza, upendo wa kimungu utatufanya tujaribu kusahau na kumlinda mwenye kukosa ikiwa kosa zito halihusiki. Tunapotendwa vibaya kama Wakristo katika utumishi wa shambani, kazini petu au shuleni, upendo “huvumilia yote.”​—Mit. 10:12; 17:9.

13. Limeonekanaje kuwa jambo lenye faida kwa Mkristo kumwamini Yehova na tengenezo lake?

13 Upendo “huamini yote.” Hii haimaanishi kwamba Wakristo wanadanganywa kwa vyepesi. Maana ni kwamba Wakristo wanamtumaini Baba yao wa kimbinguni kabisa; wao hawatilii mashaka anayowaambia kupitia kwa Neno lake lililoandikwa na tengenezo lake. Mambo yanakuwa mazuri kwa wale wanaoambatana na njia ya Mungu ya kufanya mambo kwa matumaini. Kwa mfano, kwa miaka mingi Yehova amewaonya watu wake juu ya madhara ya kutumia tumbako kupitia kwa tengenezo lake, nao wale waliolitii shauri hili walifaidika kwa kimwili na kiroho pia. Pengine wengine hawakufahamu sababu gani wasitumie tumbako. Lakini iliwafaidi ‘kuamini yote’ ijapokuwa hawakuelewa vizuri sababu yake, ya Maandiko au ya kimwili. Leo tunayo sababu ya Maandiko na uhakika pia wa kwamba matabibu wanaitambua sababu ifaayo ya kuepuka matumizi ya tumbako.​—2 Kor. 7:1.

14. Kwa sababu gani haimpasi mtu akate tumaini kamwe?

14 Upendo “hutumaini yote.” Pengine tumekuwa tukiwazuru watu katika eneo fulani katika kazi ya Kikristo ya kuhubiri bila ya kuona matokeo mengi. Upendo wa kimungu utatufanya tuwafikie tukiwa na hakika na uchangamfu tukitumaini kwamba wengine watausikiliza ujumbe na kujifunza kweli. Kwa upande mwingine pengine umeishi na mwenzi asiyeamini miaka mingi. Upendo wa kimungu haukati tumaini kwamba asiyeamini hataikubali kweli siku moja. Imekuwa lazima wengine waweke mfano wa uaminifu kwa miaka kumi, ishirini au zaidi kabla asiyeamini hajaikubali kweli. Usikate tumaini kamwe. Ni msaada mwema wa utumishi mwaminifu unaoiendeleza furaha yetu na kutufanya tutazamie mema wakati ujao tukipatwa na msiba.​—Rum. 8:24, 25.

15. Ni nini kimewasaidia ndugu zetu waendelee kuwa imara walipopatwa na mateso?

15 Upendo “hustahimili yote.” Jambo hili la upendo ni la lazima zaidi kwa sababu ya maneno haya: “Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.” (2 Tim. 3:12) Tangu Uwanja wa Michezo wa Rumi ya kale hata kwenye kambi za mateso za Nazi ya Ujeremani, mashahidi wa kweli wa Kikristo wa Yehova hawakuvunja ukamilifu, ijapokuwa wamekuwa “vyombo vya chuki ya mataifa yote.” (Mt. 24:9, NW) Karibuni zaidi nchi za Wakomunisti na zenye watawala wa kutumia nguvu zimejitahidi sana ziwaharibu mashahidi wa Yehova kabisa. Jitihada hizi, pamoja na nyingine kali zenye chuki za mataifa ya kidemokrasi, zimeshindwa kutimiza kusudi lao kwa maana upendo “hustahimili yote.”

16. Taja sehemu fulani ambazo upendo bila shaka utasaidia bila kushindwa.

16 Lakini kweli inawezekana kwamba upendo wa kimungu waweza kutusaidia kwa njia zote tulizozizungumza? Je! waweza kusaidia wenzi wa ndoa kweli wakae pamoja, wakimtumikia Mungu kwa furaha? Je! waweza kutusaidia tutazamie mema wakati ujao tukipatwa na msiba, bila kuona uchungu tunapotendwa vibaya, na pia bila ya kuwa wachoyo na wasiosamehe? Je! waweza kufanya yote haya? Ndiyo! “Upendo haushindwi kamwe (NW).”

SIFA YA KIMUNGU YA CHUKI

17. Je! chuki inapatana na utu wa Kikristo?

17 Umeona faida ya upendo wa kimungu, lakini je! unajua namna ya kuchukia? Mtunga zaburi wa Biblia alijua, naye alisema hivi: “Enyi mmpendao [Yehova], uchukieni uovu.” Pia, alisema hivi: “Je! [Yehova], nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? Nawachukia kwa ukomo wa chuki, wamekuwa adui kwangu.” (Zab. 97:10; 139:21, 22) Maneno haya makali yenyewe yaonyesha chuki ya kimungu, nawe pia lazima uwe na sifa hii upate kumpendeza Mungu.

18. Chuki ya kimungu ni ulinzi kwa njia gani? Toa mfano.

18 Chuki inakutia karaha ndani yako. Unakirihi na kukidharau unachokichukia. Kukifikiria tu kunakushtusha. Wakati mke wa bwana wake alipomshawishi na kumwomba na hata kumshika Yusufu kwa makusudi ya ufisadi, yeye hakusimama na kujaribu kufikiria atakalolifanya. Dakika moja tu ya kukawia ingalimfanya auharibu uhusiano wake na Yehova. Yeye alikimbia tu. Kuchukia kwake mabaya kulimfanya atende mara moja na kuilinda dhamiri yake njema na Mungu. (Mwa. 39:7-12) Vivyo hivyo leo, kama vile chuki inavyotenganisha watu, chuki ya kimungu itakutenganisha wewe na matendo mabaya.

19. Ni mambo gani mengine ayachukiayo Mungu, nawe wayaonaje?

19 Kwa sababu gani usijiulize juu ya unavyoyaona mambo yamchukizayo Yehova? “Kuna vitu sita anavyovichukia [Yehova]; naam. viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; moyo uwazao mawazo mabaya; miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; shahidi wa uongo asemaye uongo; naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.” (Mit. 6:16-19) Maoni yako juu ya mambo haya yaonyesha ni kwa kadiri gani ulivyo na chuki ya kimungu.

20. Haitupasi tuchukie nani wakati wo wote? Kwa sababu gani?

20 Chuki ya kimungu si juu ya ndugu zetu wa Kikristo, hata wawe wasiokamilika namna gani. Mtume Yohana alisema hivi: “Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji: nanyi mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake.” (1 Yohana 3:15) Hata wakiwa wamehusika katika kosa zito, twawaonyesha ndugu zetu wa Kikristo huruma na rehema. Watenda mabaya wenye kutubu wakiruhusiwa wakae katika kundi la Mungu, nasi pia yatupasa tuwakubali.​—Mt. 18:18.

21. Chuki ya kimungu yaonyeshwaje?

21 Chuki ya kimungu haivumilii maovu. Hii haimaanishi kwamba Wakristo wanatumia nguvu za kimwili kupinga dini ya uongo au serikali zenye upotovu, kwa maana wanajua kwamba hili ni jambo ambalo Mungu amejiwekea mwenyewe. Chuki ya Mkristo juu ya mambo hayo yaonyeshwa na bidii yake kuwaeleza wengine linayoyasema Neno la Mungu juu ya wakati ambao ufalme wa Mungu utakuwa ndiyo serikali ya pekee yenye kuitawala dunia hii. Chuki ya kimungu inaonyeshwa zaidi kwa kudharau mambo kama vile kusema uongo, kuiba, ufisadi. Mazungumzo ya Mkristo, njia ya maisha na uchaguzi wake wa burudisho vinahakikisha kabisa yeye anasimama wapi kwa habari ya mambo haya.​—Efe. 5:3-5.

22. Kwa sababu gani ni lazima kuzizoea sifa za kimungu zenye maana sana za upendo na chuki?

22 Huu ndio wakati wa kusitawisha kabisa sifa za kimungu za upendo na chuki. Kuyapenda ayapendayo Yehova na kuyachukia ayachukiayo Yehova kutatulinda na mazoea ya ulimwengu huu mwovu. Sifa ya kimungu ya upendo ni nguvu kuu ya kutenda haki. Sifa ya kimungu ya chuki ni ulinzi na kutenda mabaya nayo yatusaidia tuendelee kutembea katika njia ya Yehova. Upendo wetu na chuki yetu ni ya kweli kadiri gani? Ubora na ustahili wa maisha yetu yote waweza kuonyeshwa ni wa kadiri gani na jibu letu.

​—Kutoka The Watchtower, July 15, 1974.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki