Upendo (Agape)—Usivyo na Ulivyo
“Tieni . . . katika upendano wa ndugu [shauku yenu ya kidugu, NW], upendo.”—2 PETRO 1:5, 7.
1. (a) Biblia hutanguliza sifa gani? (b) Ni maneno gani ya Kigiriki manne ambayo hutafsiriwa “upendo” mara nyingi, na ni jipi linalorejezewa kwenye 1 Yohana 4:8?
SIFA au wema-adili mmoja hasa unaotangulizwa zaidi katika Neno la Mungu, Biblia, ni upendo. Katika Kigiriki, lugha ya awali ya Maandiko ya Kikristo, kuna maneno manne ambayo mara nyingi hutafsiriwa “upendo.” Upendo tunaozungumzia si ule wa eʹros (neno ambalo halipatikani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo), unaotegemea uvutano wa kingono; wala si ule wa stor·geʹ, hisia inayotegemea uhusiano wa damu; wala si phi·liʹa, upendo mchangamfu wa urafiki unaotegemea kustahiana, uliozungumziwa katika makala iliyotangulia. Badala ya hivyo, ni a·gaʹpe—upendo unaotegemea kanuni, ambao waweza kusemwa kuwa sawa na hali ya kutokuwa na ubinafsi, ule upendo ambao mtume Yohana alirejezea aliposema: “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
2. Ni nini limesemwa vema juu ya upendo (a·gaʹpe)?
2 Kuhusiana na upendo huo (a·gaʹpe), Profesa William Barclay asema hivi katika kitabu chake New Testament Words: “Agapē linahusiana na akili: si hisia inayotokea katika mioyo yetu bila kuamshwa humo [kama vile phi·liʹa iwezavyo]; ni kanuni ambayo sisi tunaishi kwayo kimakusudi. Agapē linahusiana zaidi sana na nia. Ni ushindi wa kuzidia nguvu kitu chenye ukinzani, ushindi wa mafanikio, na utimizo wa mradi. Hakuna mmoja ambaye amepata kupenda adui zake kiasili. Kupenda adui za mmoja ni ushindi wa kuizidi nguvu mielekeo na mibetuko yetu ya kiasili na hisia-moyo zetu. Hiyo agapē . . . kwa uhakika ni uwezo wa kupenda kisichopendeka, kupenda watu ambao sisi hatufurahii.”
3. Yesu Kristo na Paulo walikaziaje upendo?
3 Naam, miongoni mwa mambo yanayotofautisha ile ibada safi ya Yehova Mungu na zile namna nyinginezo zote za ibada ni kukazia kwayo upendo wa aina hiyo. Yesu Kristo alitaja kwa kufaa zile amri mbili zilizo kuu zaidi: “Ya kwanza ndiyo hii, . . . Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho [nafsi, NW] yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote. Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi.” (Marko 12:29-31) Mtume Paulo alikazia upendo vivyo hivyo katika sura ya 13 ya 1 Wakorintho. Baada ya kukazia kwamba upendo ulikuwa ndiyo sifa kuu iliyo ya lazima, alimalizia kwa kusema hivi: “Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.” (1 Wakorintho 13:13) Yesu alisema kwa kufaa kwamba upendo ungekuwa ndiyo alama ya kuwatambua wafuasi wake.—Yohana 13:35.
Mambo Yanayoonyesha Jinsi Upendo Usivyo
4. Paulo ataja mambo mangapi yasiyofaa na mangapi yafaayo juu ya upendo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8?
4 Imesemwa kwamba ni rahisi zaidi kusema jinsi upendo usivyo kuliko jinsi ulivyo. Kuna kadiri fulani ya kweli katika hilo, kwani katika sura yake juu ya upendo, 1 Wakorintho 13, katika mistari 4 hadi 8, mtume Paulo ataja mambo tisa yanayoonyesha jinsi upendo usivyo na mambo saba yanayoonyesha jinsi upendo ulivyo.
5. “Wivu” unafasiliwaje, nao unatumiwaje kwa namna ifaayo katika Maandiko?
5 Jambo la kwanza ambalo Paulo ataja kuonyesha jinsi upendo usivyo ni kwamba “si wenye wivu.” (NW) Hilo lahitaji kuelezwa kidogo kwa sababu wivu una hali zifaazo na zisizofaa. Kamusi moja yafasili “wivu” kuwa “kutovumilia ushindani” na “kudai ujitoaji kamili.” Hivyo, Musa alisema hivi kwenye Kutoka 34:14: “Hutamwabudu mungu mwingine, kwa kuwa BWANA [Yehova, NW], ambaye jina lake ni mwenye wivu, ni Mungu mwenye wivu.” Kwenye Kutoka 20:5, Yehova asema hivi: “Mimi, BWANA [Yehova, NW] Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [anayedai ujitoaji kamili, NW].” Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika: “Nawaonea wivu, wivu wa Mungu.”—2 Wakorintho 11:2.
6. Ni vielelezo vipi vya Kimaandiko vinavyoonyesha sababu kwa nini upendo si wenye wivu?
6 Hata hivyo, kwa ujumla, “wivu” una maana mbaya, ambayo kwa sababu hiyo unaorodheshwa pamoja na kazi za mwili kwenye Wagalatia 5:20. Naam, wivu huo ni wenye ubinafsi nao watokeza chuki, na chuki ni kinyume cha upendo. Wivu ulimfanya Kaini amchukie Habili kufikia hatua ya kumwua kimakusudi, na uliwafanya ndugu-nusu kumi wa Yusufu wamchukie kufikia hatua ya kutaka kumwua. Upendo hauhusudu kwa wivu mali au faida za wengine, kama vile Mfalme Ahabu alivyohusudu kwa wivu shamba la mizabibu la Nabothi.—1 Wafalme 21:1-19.
7. (a) Ni tukio gani linaloonyesha kwamba Yehova hapendezwi na kujigamba? (b) Kwa nini upendo haujigambi hata bila kufikiri?
7 Kisha Paulo atuambia kwamba upendo “haujigambi.” (NW) Kujigamba huonyesha ukosefu wa upendo, kwani kwamfanya mtu ajiweke mwenyewe juu ya wengine. Yehova hapendezwi na wenye kujigamba, kama inavyoweza kuonwa kutokana na njia aliyomnyenyekeza Mfalme Nebukadreza alipojigamba. (Danieli 4:30-35) Mara nyingi kujigamba hufanywa bila kufikiri kwa sababu ya mtu kupendezwa mno na mafanikio yake au na mali zake mwenyewe. Huenda wengine wakawa na mwelekeo wa kujivunia mafanikio yao katika huduma ya Kikristo. Wengine ni kama yule mzee aliyehisi ni lazima awapigie simu marafiki wake kuwaambia juu ya lile gari jipya alilonunua lenye thamani ya karibu dola 50,000. Hayo yote hayaonyeshi upendo kwa sababu yamwonyesha mwenye kujigamba kuwa mkuu kuliko wasikilizaji wake.
8. (a) Mtazamo wa Yehova ni nini kuelekea wale wanaojivimbisha? (b) Kwa nini upendo hautendi kwa njia hiyo?
8 Kisha twaambiwa kwamba upendo “haujivimbishi kwa kiburi.” (NW) Mtu ambaye amejivimbisha, au ni mwenye kiburi, hujikweza juu ya wengine bila upendo. Mtazamo huo wa akilini si wenye hekima hata kidogo kwa sababu “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.” (Yakobo 4:6) Upendo hutenda kinyume kabisa; huwaona wengine kuwa wakuu zaidi. Paulo aliandika hivi kwenye Wafilipi 2:2, 3: “Ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja, wenye roho [nafsi, NW] moja, mkinia mamoja. Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.” Mtazamo huo wa akilini huwafanya wengine wahisi kustareheka, ilihali mwenye kiburi huwafanya wengine wasihisi kustareheka kwa sababu ya ushindani.
9. Kwa nini upendo hautendi kwa njia ikosayo adabu?
9 Paulo aendelea kusema kwamba upendo “haukosi kuwa na adabu.” Kamusi hufasili “-kosa adabu” kuwa “-a kutofaa au -a kuudhi sana adabu au adili.” Mtu anayetenda bila adabu (bila upendo) hupuuza hisia za wengine.” Fasiri nyingi za Biblia hutafsiri neno hilo la Kigiriki kuwa “fidhuli.” Mtu wa jinsi hiyo hudharau kinachoonwa kuwa chenye kufaa na chenye kupendeza. Kwa hakika, ufikirio wenye upendo kuelekea wengine ungemaanisha kuepuka mambo yote yenye ufidhuli au yakosayo adabu, mambo yanayoudhi na huenda hata yakashtua.
Mambo Mengine Yanayoonyesha Jinsi Upendo Usivyo
10. Upendo hautafuti mambo yake kwa njia gani?
10 Kisha twaambiwa kwamba upendo “hautafuti mambo yake,” yaani, kunapokuwa swali juu ya mapendezi yetu binafsi na yale ya wengine. Mtume asema hivi kwingineko: “Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.” (Waefeso 5:29) Lakini, mapendezi yetu yanaposhindana na mapendezi ya mwingine na hakuna kanuni nyingine ya Biblia inayohusika, twapaswa kufanya kama vile Abrahamu alivyofanya na Loti, kumruhusu kwa upendo yule mtu mwingine atangulie.—Mwanzo 13:8-11.
11. Inamaanisha nini kwamba upendo hauwi wenye kuchokozeka?
11 Upendo hauudhiki upesi. Kwa hiyo Paulo atuambia kwamba upendo “hauwi wenye kuchokozeka.” (NW) Si wenye kukasirika upesi. Huzoea kujidhibiti. Waume na wake waliooana ndio wanaohitaji hasa kutia onyo pole hilo maanani kwa kujilinda dhidi ya kupaaza sauti zao bila subira au kupigiana makelele. Kuna hali inapokuwa rahisi kuchokozeka, ndiyo sababu Paulo alihisi uhitaji wa kumshauri Timotheo hivi: “Haimpasi mtumwa wa Bwana kuwa mgomvi; bali kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu”—naam, hachokozeki—“akiwaonya kwa upole wao washindanao naye.”—2 Timotheo 2:24, 25.
12. (a) Upendo hauhesabu mabaya kwa njia gani? (b) Kwa nini si jambo la hekima kuhesabu mabaya?
12 Akiendelea na mambo yanayoonyesha jinsi upendo usivyo, Paulo ashauri hivi: “Upendo . . . hauhesabu mabaya.” Hilo halimaanishi kwamba upendo hauoni mabaya hata kidogo. Yesu alionyesha namna tupaswavyo kushughulikia mambo wakati ambapo tumeumizwa vibaya sana. (Mathayo 18:15-17) Lakini upendo hauturuhusu tuendelee kuwa na chuki, kuweka kinyongo. Kutohesabu mabaya kwamaanisha kuwa mwenye kusamehe na kusahau mara jambo hilo limeshughulikiwa kwa njia ya Kimaandiko. Naam, usijitese mwenyewe wala kujihuzunisha kwa kufikiria kosa fulani daima, kuhesabu mabaya!
13. Ni nini maana ya kutofurahia ukosefu wa uadilifu, na kwa nini upendo haufanyi hivyo?
13 Zaidi ya hayo, tunaambiwa kwamba upendo “haufurahii udhalimu [ukosefu wa uadilifu, NW].” Ulimwengu hufurahia ukosefu wa uadilifu, kama inavyoweza kuonwa kutokana na kule kupendwa sana kwa fasihi, sinema na programu za televisheni zenye jeuri na mambo ya kingono. Kufurahia kote kwa jinsi hiyo ni ubinafsi, kutoheshimu hata kidogo kanuni za Mungu zenye uadilifu wala hali njema ya wengine. Kufurahia kote huko kwa ubinafsi ni kupanda kwa mwili na hatimaye kutavuna uharibifu kutoka katika mwili.—Wagalatia 6:8.
14. Kwa nini yaweza kusemwa kwa hakika kwamba upendo haushindwi kamwe?
14 Sasa jambo la mwisho ambalo upendo haufanyi: “Upendo haushindwi kamwe.” Kwanza, upendo haushindwi au kuisha kamwe kwa sababu Mungu ni upendo, naye ndiye “Mfalme wa milele.” (1 Timotheo 1:17) Kwenye Warumi 8:38, 39, tunahakikishiwa kwamba upendo wa Yehova kwetu hautashindwa kamwe: “Nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Pia, upendo haushindwi kamwe kwa sababu haupatikani kamwe umepungukiwa. Upendo waweza kukabiliana na pindi yoyote, ugumu wowote.
Mambo Yanayoonyesha Jinsi Upendo Ulivyo
15. Kwa nini Paulo aorodhesha ustahimilivu kwanza miongoni mwa mambo yafaayo juu ya upendo?
15 Sasa akija kwenye upande ufaao, mambo yanayoonyesha jinsi upendo ulivyo, Paulo aanza hivi: “Upendo ni mstahimilivu.” (NW) Imesemwa kwamba ushirika wa Kikristo hauwezekani bila ustahimilivu, yaani, bila kuchukuliana kwa subira. Ni hivyo kwa sababu sisi sote ni watu wasiokamilika, na kutokamilika kwetu na udhaifu wetu mbalimbali huwajaribu wengine. Si ajabu kwamba mtume Paulo aorodhesha sehemu hii kwanza kuonyesha jinsi upendo ulivyo!
16. Washiriki wa familia waweza kuonyeshana fadhili kwa njia zipi?
16 Paulo asema kwamba upendo ni “wenye fadhili.” (NW) Yaani, upendo ni wenye kusaidia, wenye kufikiri, wenye kuwahangaikia wengine. Fadhili hujidhihirisha katika mambo makubwa na madogo. Bila shaka yule Msamaria mwenye ujirani alikuwa akionyesha fadhili kwa yule mwanamume aliyekuwa ameshambuliwa na wanyang’anyi. (Luka 10:30-37) Upendo hufurahia kusema “tafadhali.” Kusema, “Pitisha mkate” ni kuamuru. Kutanguliza hilo na “tafadhali” hulifanya liwe ombi. Waume ni wenye fadhili kwa wake zao wanapotii lile shauri kwenye 1 Petro 3:7: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” Wake ni wenye fadhili kwa waume zao ‘wanapowastahi.’ (Waefeso 5:33) Akina baba ni wenye fadhili kwa watoto wao wanapofuata lile shauri kwenye Waefeso 6:4: “Akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana [Yehova, NW].”
17. Ni zipi njia mbili ambazo katika hizo upendo hufurahi pamoja na kweli?
17 Upendo haufurahii ukosefu wa uadilifu bali “hufurahi pamoja na kweli.” Upendo na kweli huambatana—Mungu ni upendo, na wakati uleule, yeye ni “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Upendo hufurahi kuona kweli ikishinda na kufunua uwongo; hilo huchangia kwa sehemu lile ongezeko kubwa linalotukia katika idadi ya waabudu wa Yehova leo. Hata hivyo, kwa kuwa kweli hutofautishwa na ukosefu wa uadilifu, wazo laweza kuwa pia kwamba upendo hufurahi pamoja na uadilifu. Upendo hufurahia ushindi wa uadilifu, kama vile waabudu wa Yehova wanavyoamriwa kufanya wakati wa anguko la Babuloni Mkubwa.—Ufunuo 18:20.
18. Upendo huhimili yote katika maana gani?
18 Paulo atuambia pia kwamba upendo “huhimili yote.” (NW) Kama vile Kingdom Interlinear ionyeshavyo, wazo ni kwamba upendo hufunika mambo yote. ‘Haumsingizii’ ndugu, kama vile waovu wanavyoelekea kufanya. (Zaburi 50:20; Mithali 10:12; 17:9) Naam, wazo hapa ni sawa na lile kwenye 1 Petro 4:8: “Upendano husitiri wingi wa dhambi.” Bila shaka, uaminifu-mshikamanifu ungemzuia mtu asifiche dhambi nzito dhidi ya Yehova na dhidi ya kutaniko la Kikristo.
19. Upendo huamini yote kwa njia gani?
19 Upendo “huamini yote.” Upendo ni sifa ifaayo, si sifa isiyofaa. Hiyo haimaanishi kwamba upendo ni wenye kudanganyika. Si mwepesi kuamini taarifa za ajabu-ajabu. Lakini ili mtu aweze kupata imani katika Mungu, ni lazima awe na nia ya kuamini. Kwa hiyo upendo si wenye kutia shaka, wenye kuchambua isivyofaa. Haujizuii usiamini, kama vile mtu asiyeamini kuwako kwa Mungu, anayesema kwa ushupavu kwamba hakuna Mungu, wala si kama Mwagnosti, anayedai kwa ushupavu kwamba haiwezekani hata kidogo kujua tulikotoka, sababu ya sisi kuwa hapa, na jinsi wakati ujao utakavyokuwa. Neno la Mungu hutupa sisi uhakikishio kuhusiana na mambo hayo yote. Upendo uko tayari pia kuamini kwa sababu unatumaini, hauwi wenye kushuku isivyofaa.
20. Upendo huhusianaje na tumaini?
20 Mtume Paulo aendelea kutuhakikishia kwamba upendo “hutumaini yote.” Kwa kuwa upendo ni sifa ifaayo, si sifa isiyofaa, ina tumaini lenye nguvu katika yote yaliyoahidiwa katika Neno la Mungu. Twaambiwa hivi: “Alimaye nafaka ni haki yake kulima kwa matumaini; naye apuraye nafaka ni haki yake kutumaini kupata sehemu yake.” (1 Wakorintho 9:10) Kama vile upendo ni wenye kuitibari, huo ni wenye tumaini pia, ukitumaini yaliyo bora zaidi sikuzote.
21. Kuna uhakikishio gani wa Kimaandiko kwamba upendo huvumilia?
21 Mwishowe, tunahakikishiwa kwamba upendo “huvumilia yote.” (NW) Unaweza kufanya hivyo kwa sababu ya yale ambayo mtume Paulo atuambia kwenye 1 Wakorintho 10:13: “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili [kuvumilia, NW].” Upendo utatufanya tutazame vile vielelezo vingi katika Maandiko vya watumishi wa Mungu ambao wamevumilia, mkuu wao akiwa Yesu Kristo, kama tunavyokumbushwa kwenye Waebrania 12:2, 3.
22. Tukiwa watoto wa Mungu, ni lazima tuhangaike kudhihirisha sifa gani kuu?
22 Kwa kweli, upendo (a·gaʹpe) ndio sifa kuu ambayo sisi tukiwa Wakristo, Mashahidi wa Yehova, twahitaji kusitawisha, kuhusiana na jinsi usivyo na pia kuhusiana na jinsi ulivyo. Tukiwa watoto wa Mungu, na tuhangaike kudhihirisha tunda hilo la roho ya Mungu sikuzote. Kufanya hivyo ni kuwa wenye mfano wa Mungu, kwani, kumbuka kwamba, “Mungu ni upendo.”
Je! Wakumbuka?
◻ Yesu Kristo na Paulo wanaonyeshaje ukuu wa upendo?
◻ Upendo si wenye wivu katika maana gani?
◻ Upendo ‘huhimilije yote’?
◻ Kwa nini yaweza kusemwa kwamba upendo haushindwi kamwe?
◻ Upendo hufurahi pamoja na kweli kwa njia zipi mbili?
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
UPENDO (AGAPE)
Usivyo
1. Si Wenye Wivu
2. Haujigambi
3. Haujivimbishi
4. Haukosi adabu
5. Hautafuti mambo yake
6. Hauwi wenye kuchokozeka
7. Hauhesabu mabaya
8. Haufurahii ukosefu wa uadilifu
9. Haushindwi kamwe
Ulivyo
1. Mstahimilivu
2. Wenye Fadhili
3. Hufurahi pamoja na kweli
4. Huhimili yote
5. Huamini yote
6. Hutumaini yote
7. Huvumilia yote
[Picha katika ukurasa wa 18]
Yehova alimnyenyekeza Nebukadreza kwa sababu ya kujigamba