Wakati Ujao Mzuri kwa Watoto Wetu
TANGU mwisho wa Vita ya Ulimwengu wa Pili, serikali za ulimwengu zimetayarisha na kutia sahihi mikataba mingi ya kuwalinda raia wakati wa vita. Miongoni mwa hiyo kuna mikataba ambayo inaruhusu mavazi pamoja na ugavi wa kitiba na chakula kuwafikia watoto. Mapatano ya kimataifa huahidi kukinga watoto dhidi ya kutumiwa vibaya kingono, kuteswa, na ujeuri. Mapatano pia yamepiga marufuku kusajiliwa kwa mtu yeyote aliye chini ya umri wa miaka 15 jeshini.
Ripoti moja ya Shirika la Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa The State of the World’s Children 1996, yazisifu sheria hizo kuwa “maendeleo makubwa” na kuongezea: “Wanasiasa wajuao kwamba kuna viwango ambavyo katika hivyo wao waweza kuhukumiwa waelekea zaidi kuvifikiria katika mipango yao.”
Bila shaka, wanasiasa pia hutambua kwamba jumuiya ya kimataifa mara nyingi hukosa uwezo na nia ya kutekeleza sheria. Basi, ripoti hiyo yakiri kwamba “kwa kufikiria kadiri ambayo kanuni hizi zimepuuzwa, ni rahisi kudharau shirika lililopo sasa la kutunza sheria ya kimataifa.”
Kisha kuna suala la pesa. Katika mwaka wa 1993, mapambano yaliwaka katika mataifa 79. Kati ya hayo mataifa 65 yalikuwa maskini. Mataifa hayo maskini yalipataje silaha za kupigana? Hasa kutoka kwa mataifa matajiri. Na ni mataifa yapi yanayoongoza katika kusafirishia nchi zinazoendelea silaha? Ni yale mataifa matano yaliyo yanachama ya kudumu ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa!
Wale Wanaojali
Bila shaka, kuna wale ambao hujali sana hali za watoto vitani. Watu mmoja-mmoja na vilevile mashirika huwasaidia wahasiriwa wa vita. Kwa kielelezo, Mashahidi wa Yehova, ambao bila shaka hawashiriki katika vita, wamefanya hivyo. Lakini, kuondoa kuhasiriwa kwa watoto katika vita kwa kweli kwamaanisha kuondoa vita yenyewe, tazamio ambalo huenda likaonekana kama haliwezekani. Kwa sababu ya historia ndefu ya mizozo na mapambano ya wanadamu, wengi hukata kauli kwamba wanadamu hawataleta kamwe amani ya duniani pote. Kwa maoni hayo, wanasema kweli.
Watu pia hukata kauli kwamba Mungu hatayaingilia kamwe mambo ya mataifa wala hataleta amani ya kudumu kwenye sayari hii. Kwa maoni haya, wamekosea.
Muumba wetu, Yehova Mungu, hujali sana kuhusu mambo yatendekayo duniani. Katika Neno lake, Biblia, Yehova auliza: “Je! mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu . . . si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi?” Mungu ajibu kwa mkazo: “Sikufurahii kufa kwake afaye.”—Ezekieli 18:23, 32.
Ebu fikiria: Ikiwa Muumba wetu mwenye huruma-nyororo ataka hata watu wazima walio waovu kutubu na kufurahia maisha, kwa hakika yeye ataka watoto vilevile waishi na kufurahia maisha! Lakini, Mungu wetu mwenye upendo hatavumilia waovu kwa muda usio dhahiri. “Watenda mabaya wataharibiwa,” Neno la Mungu laahidi. “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo.”—Zaburi 37:9, 10.
Yesu Kristo, ambaye alionyesha kwa ukamili utu wa Baba yake wa kimbingu, aliwapenda watoto na kusema kwamba “ufalme wa mbingu ni wa walio kama hao.” (Mathayo 19:14) Dhabihu za watoto kwa miungu ya vita huchukiza Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 18:10, 12.
Ahadi ya Mungu ya Wakati Ujao Mzuri
Mungu ameruhusu vita na kuteseka katika karne ambazo zimepita ili ile kweli iliyotajwa na nabii Yeremia iweze kuthibitishwa kwa umilele wote ujao: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Upesi, Biblia yaahidi, Yehova atatetea enzi kuu yake kwa ‘kuvikomesha vita hata mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9) Uliotabiriwa pia katika Biblia ni wakati ambapo “[watu] watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza tena vita kamwe.”—Isaya 2:4.
Ni nini kitakachowapata wale ambao wameuawa na vita? Je, kuna tumaini lolote kwao? Yesu aliahidi ufufuo wa wafu kwenye dunia isiyo na vita, akisema: ‘Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Vilevile, mtume Paulo alisema hivi kwa uhakika: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.
Ahadi za Mungu hakika zitatimia. Yeye ana nguvu na azimio la kutekeleza kile ambacho amekusudia. (Isaya 55:11) Yehova asemapo kwamba ataondoa vita, yeye atafanya vivyo hivyo. Aahidipo kuwafufua kwenye uhai wale ambao wamekufa, atafanya hivyo. Kama alivyosema malaika Gabrieli, “kwa Mungu hakuna tangazo lolote litakalokuwa lisilowezekana.”—Luka 1:37.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wakati ambapo vita havitakuwapo tena, watoto wote watafurahia maisha mazuri