Maoni ya Biblia
Je, Wakristo Wachukie Wagoni-Jinsia-Moja?
KATIKA mwaka wa 1969 neno linalofafanua hofu isiyofaa au chuki kubwa dhidi ya wagoni-jinsia-moja lilitungwa katika lugha ya Kiingereza. Neno hilo ni “homophobia,” yaani kuhofu wagoni-jinsia-moja. Lugha nyingi hazina neno mahususi kama hilo, lakini kwa maelfu ya miaka, watu wa mataifa mengi na lugha nyingi wamedhihirisha chuki dhidi ya wagoni-jinsia-moja.
Hata hivyo, katika nyakati za karibuni zaidi, ugoni-jinsia-moja umekuzwa sana kuwa tu njia ya badala ya kuonyesha hisia za kingono. Mwanahistoria Jerry Z. Muller karibuni aliandika juu ya “dai linaloongezeka la kutaka kutambuliwa na umma na kustahiwa kwa ugoni-jinsia-moja jinsi ulivyo.” Alieleza kwamba wagoni-jinsia-moja “wanazidi kuungana pamoja ili kutangaza zoea lao kuwa lenye kustahili sifa, na kudai kwamba wengine wafanye kama wao.” Hili laonekana hasa katika nchi za Magharibi. Hata hivyo, katika sehemu nyingi za ulimwengu, hata zile zinazoitwa eti nchi zenye kupendelea mabadiliko, wengi bado hulaumu na kukataa ugoni-jinsia-moja.
Wagoni-jinsia-moja na wale wanaoshukiwa kwa ugoni-jinsia-moja mara nyingi huwa shabaha ya maneno yenye madharau, kuudhiwa, na kufanyiwa ujeuri. Hata viongozi wa kidini wamedhihirisha chuki kama hiyo. Wengine wameanzisha ile inayoonekana kuwa vita vyao wenyewe dhidi ya wagoni-jinsia-moja. Kwa mfano, fikiria maelezo yaliyotolewa na askofu wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki na ambayo yalitangazwa hivi karibuni kwenye radio ya taifa la Ugiriki. Alitaarifu: “Mungu atachoma wagoni-jinsia-moja milele katika shimo la helo lenye kuwaka moto. Mayowe ya vinywa vyao vyenye uchafu wa kuchukiza yatavuma hadi umilele wote. Miili yao iliyopotoka itapatwa na mateso yasiyovumilika.” Je, hii ni kweli? Mungu anahisije juu ya wagoni-jinsia-moja?
Maoni ya Mungu
Biblia haitoi uangalifu mahususi kwa wagoni-jinsia-moja kuwa kikundi kinachopasa kutengwa ama kuchukiwa na Wakristo. Zaidi ya hilo, haifundishi kwamba Mungu ataadhibu wagoni-jinsia-moja—au viumbe vyake vyovyote—kwa kuwachoma milele katika helo iliyo kama moto.—Linganisha Waroma 6:23.
Hata hivyo, Maandiko hutokeza viwango vya adili vya Muumba wetu, ambavyo mara nyingi hupingana na mielekeo ya kiadili ya kisasa. Matendo ya ugoni-jinsia-moja, ngono ya jinsia tofauti kati ya watu wasiofunga ndoa, na ngono na wanyama zote hulaumiwa katika Biblia. (Kutoka 22:19; Waefeso 5:3-5) Mungu aliharibu Sodoma na Gomora kwa sababu ya mazoea ya kingono kama hayo.—Mwanzo 13:13; 18:20; 19:4, 5, 24, 25.
Kwa habari ya matendo ya ugoni-jinsia-moja, Neno la Mungu lasema hivi wazi: “Hili ni chukizo.” (Mambo ya Walawi 18:22, The New Jerusalem Bible) Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilisisitiza: “Mtu mume akilala pamoja na mtu mume, kama alalavyo na mtu mke, wote wawili wamefanya machukizo; hakika watauawa.” (Mambo ya Walawi 20:13) Adhabu hiyohiyo iliagizwa kwa waliofanya ngono na mnyama, ngono ya maharimu, na uzinzi.—Mambo ya Walawi 20:10-12, 14-17.
Mtume Paulo alipuliziwa kueleza matendo ya ugoni-jinsia-moja kuwa maonyesho ya “hamu za ngono yenye kufedhehesha” na yaliyo “kinyume cha asili.” Aandika: “Hiyo ndiyo sababu Mungu aliwaacha kwenye hamu za ngono yenye kufedhehesha, kwa maana watu wao wa kike walibadili utumizi wa kiasili wa wao wenyewe kuwa ule ulio kinyume cha asili; na hivyohivyo pia hata watu wa kiume waliacha utumizi wa kiasili wa aliye wa kike na kuwakiana tamaa kali katika uchu wao kuelekea mtu na mwenzake, watu wa kiume kwa watu wa kiume, wakifanya yaliyo yenye aibu na kupokea katika wao wenyewe malipo kamili, yaliyostahili kosa lao. Na kama vile hawakukubali kuwa na Mungu katika ujuzi sahihi, Mungu aliwaacha katika hali ya kiakili iliyokataliwa, ili wafanye mambo yasiyofaa.”—Waroma 1:26-28.
Maandiko hayatolei udhuru, hayaridhiani, wala kutatanisha mambo; mazoea ya ugoni-jinsia-moja, uzinzi, uasherati, yote hayo ni yenye kukirihi machoni pa Mungu. Kulingana na hayo, Wakristo wa kweli hawapunguzi umaana wa msimamo wa Biblia juu ya “hamu za ngono yenye kufedhehesha” ili tu wawe wenye kupendwa zaidi na wengi ama wenye kukubalika zaidi na utamaduni wa kisasa. Wala hawakubaliani na chama chochote kilichojitoa ili kuendeleza ugoni-jinsia-moja kuwa mtindo-maisha wa kawaida.
“Uchukieni Uovu”
Biblia inaonya kwa upole: “Enyi mmpendao BWANA, uchukieni uovu.” (Zaburi 97:10) Kwa sababu hiyo, Wakristo wanatarajiwa wachukie kila zoea linalovunja sheria za Yehova. Watu fulani huenda hata wakaitikia kwa hisia zenye chuki kubwa zaidi ama kukirihi ugoni-jinsia-moja kuliko aina nyinginezo za ukosefu wa adili, wakiuona ugoni-jinsia-moja kuwa upotovu wa kingono usio wa asili. Hata hivyo, je, Wakristo wachukie watu mmoja-mmoja wanaozoea mambo kama hayo?
Mtunga-zaburi atoa nuru fulani kwenye suala hili katika Zaburi 139:21, 22: “Je! BWANA nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? Nawachukia kwa ukomo wa chuki, wamekuwa adui kwangu.” Uaminifu-mshikamanifu wetu kwa Yehova na kanuni zake wapaswa kukuza ndani yetu chuki kubwa kwa wale wanaomwasi Yehova kimakusudi na ambao wanachukua msimamo wa kuwa maadui wa Mungu. Shetani na roho waovu ni baadhi ya maadui wa Mungu wa hakika. Wanadamu fulani pia waelekea kuwa katika kikundi hiki. Bado, yaweza kuwa vigumu sana kwa Mkristo kutambulisha watu kama hao kwa sura za nje. Hatuwezi kusoma mioyo. (Yeremia 17:9, 10) Lingekuwa kosa kufikiri ya kwamba mtu ni adui wa Mungu asiyeweza kubadilika kwa sababu ya kuzoea mabaya. Katika visa vingi wakosaji hawafahamu tu viwango vya Mungu.
Kwa sababu hiyo, kusema kwa ujumla, Wakristo hawawi wepesi kuchukia wanadamu wenzao. Hata wakiwa na hisia zenye kukirihi kabisa aina fulani za mitindo-maisha, hawajaribu kudhuru wengine, wala hawaweki chuki wala kuwafungia kinyongo. Badala ya hivyo, Biblia inashauri Wakristo wawe “wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:9, 17-19.
“Mungu Si Mwenye Ubaguzi”
Yehova atamsamehe mtu ambaye atubu kikweli, hata huyo mtu awe amekuwa akitenda ukosefu gani wa adili. Hakuna uthibitisho wowote wa kwamba Yehova huona aina moja ya ukosefu wa adili kuwa mbaya zaidi ya nyingine. “Mungu si mwenye ubaguzi.” (Matendo 10:34, 35) Kwa mfano, fikiria kisa cha kutaniko la karne ya kwanza katika Korintho. Mtume Paulo aliwaandikia: “Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.” Kisha Paulo akakiri kwamba baadhi ya waliokuwa waasherati, wazinzi, wagoni-jinsia-moja, na wezi walikuwa wamekubaliwa katika kutaniko la Kikristo la Korintho. Alieleza: “Na hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa. Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.
Bila shaka, Yehova havumilii kuendelea na kudumu kokote kwa kuvunjwa kwa viwango vyake vya adili vilivyo vikamilifu. Kwa wazi anachukia kutostahi kwa ukaidi kanuni zake. Hata hivyo, yeye yuko tayari kwa mapatano. (Zaburi 86:5; Isaya 55:7) Kwa kupatana na hayo, Wakristo hawafanyi wagoni-jinsia-moja, au mtu mwingine yeyote, kuwa shabaha ya uadui, dhihaka, ama wa kusumbuliwa. Wakristo wa kweli huona wanadamu wenzao kuwa watu wawezao kuwa wanafunzi wa Kristo, wakiwatendea kwa njia yenye staha na hadhi. Biblia husema: “Hili ni bora na lenye kukubalika machoni pa mwokozi wetu, Mungu, ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4.
Wakristo Hukaribisha Wenye Kutubu
Tena na tena, Biblia hutangaza kwamba Mungu ni mwenye kusamehe. Inamfafanua kuwa ‘Mungu aliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi, si mwepesi wa hasira, aliye mwingi wa rehema.’ (Nehemia 9:17; Ezekieli 33:11; 2 Petro 3:9) Zaidi Biblia humfananisha na baba katika mfano wa Yesu wenye somo kuhusu mwana mpotevu, ambaye alifuja mali yake kwa kuishi maisha ya ufasiki katika nchi ya mbali. Baba alingoja kwa shangwe kumkaribisha mwana wake wakati mwana huyo aliporudiwa na fahamu zake, akatubu, na kurejea nyumbani mwa familia yake.—Luka 15:11-24.
Ndiyo, inawezekana kwa mkosaji kubadilika. Maandiko hukiri hili kwa kuwatia watu moyo wavue utu wa zamani na kuvaa utu mpya na ‘kufanywa upya katika kani inayotendesha akili.’ (Waefeso 4:22-24) Wale ambao wanazoea lililo baya, kutia ndani wagoni-jinsia-moja, wanaweza kufanya mabadiliko ya msingi katika namna yao ya kufikiri na kuenenda, na wengi kwa kweli wamefaulu katika kufanya mgeuzo huu.a Yesu mwenyewe alihubiria watu kama hao; na walipoonyesha toba, walikubalika naye.—Mathayo 21:31, 32.
Wakristo hukaribisha watu wenye kutubu kutoka hadhi mbalimbali za maisha. Baada ya kuacha mazoea ya ukosefu wa adili, bila kujali walikuwaje, wote waweza kufurahia manufaa kamili za msamaha wa Mungu kwa sababu “BWANA ni mwema kwa watu wote, na rehema zake zi juu ya kazi zake zote.”—Zaburi 145:9.
Wakristo wako tayari kutoa msaada unaohitajiwa wa kiroho, hata kwa wale ambao bado wanapigana na mielekeo ya ugoni-jinsia-moja. Hili lapatana na onyesho la Mungu mwenyewe la upendo, kwa kuwa Biblia husema: “Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.”—Waroma 5:8.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Naweza Kuzifanyaje Hisia Hizi Ziondoke?,” katika toleo la Amkeni! la Machi 22, 1995.
[Blabu katika ukurasa wa 14]
Wakristo hawapunguzi umaana wa maoni ya Biblia juu ya ugoni-jinsia-moja
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]
Punch