Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 3/22 kur. 10-13
  • Mkazo Unaweza Kudhibitiwa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mkazo Unaweza Kudhibitiwa!
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jitunze Mwenyewe
  • Dumisha Mahusiano Mazuri
  • Weka Usawaziko Katika Maisha Yako
  • Uuone Mkazo kwa Njia Ifaayo
  • Sitawisha Hali ya Kiroho
  • Tumaini Hakika
  • Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko
    Amkeni!—2010
  • Mkazo Mzuri, Mkazo Mbaya
    Amkeni!—1998
  • Ninaweza Kukabiliana Jinsi Gani na Mikazo Shuleni?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Visababishi na Madhara ya Mfadhaiko
    Amkeni!—2005
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 3/22 kur. 10-13

Mkazo Unaweza Kudhibitiwa!

“Sikuzote kutakuwa na mkazo maishani, na kwa kweli jambo ambalo tunahitaji kuchunguza ni jinsi tunavyoitikia mkazo badala ya kujaribu kuuondoa.”—Leon Chaitow, mwandikaji mashuhuri wa masuala ya afya.

BIBLIA ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho,” kutakuwapo “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Uthibitisho waonyesha wazi kwamba tunaishi katika wakati huo, kwa sababu watu—kama tu unabii ulivyosema—ni “wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi.”—2 Timotheo 3:1-5.

Si ajabu kwamba ni vigumu sana kudumisha utulivu wa kadiri fulani! Hata wale wanaojaribu kuishi kwa amani waweza kuathiriwa. “Mateso ya mwenye haki ni mengi,” akaandika mtunga-zaburi Daudi. (Zaburi 34:19; linganisha 2 Timotheo 3:12.) Na bado, kuna mengi uwezayo kufanya ili kupunguza mkazo usije ukalemewa nao. Fikiria madokezo yafuatayo.

Jitunze Mwenyewe

Jihadhari na kile unachokula. Mlo wenye afya watia ndani protini, matunda, mboga, nafaka na mbegu nyinginezo, na vyakula vinavyotokana na maziwa. Jihadhari na unga mweupe uliochujwa na mafuta kifu. Jihadhari na ulaji wako wa chumvi, sukari iliyosafishwa, unywaji wa kileo, na kafeini. Boresha mlo wako, na huenda ukapunguza uwezekano wa wewe kushikwa na mkazo.

Mazoezi. “Mazoezi ya kimwili ni yenye manufaa,” Biblia yashauri. (1 Timotheo 4:8) Kwa kweli, mazoezi ya kiasi lakini yenye kudumu—wengine wanapendekeza mara tatu kwa juma—huimarisha moyo, huboresha mzunguko, hupunguza kolesteroli, na kupunguza uwezekano wa wewe kupatwa na mshiko wa moyo. Zaidi ya hiyo, mazoezi huendeleza hisia ya kuwa na afya njema, yaelekea kwa sababu ya endorphin ambazo huachiliwa wakati wa utendaji unaohitaji nguvu.

Pata usingizi wa kutosha. Ukosefu wa usingizi hutokeza uchovu na kupunguza uwezo wako wa kudhibiti mkazo. Ikiwa unapata matatizo ya usingizi, jaribu kudumisha wakati mmoja wa kawaida wa kwenda kulala na wa kuamka. Wengine hupendekeza kwamba usingizi mfupi wa mchana usipite dakika 30 ili usihitilafiane na usingizi mzuri wa usiku.

Kuwa mwenye mpango. Watu ambao hudhibiti wakati wao wanaweza kukabiliana na mkazo vizuri zaidi. Ili kuwa mwenye mpango, kwanza tambua ni madaraka yapi ambayo yanastahili kutangulizwa. Kisha, fanyiza ratiba ili madaraka hayo yasisahauliwe.—Linganisha 1 Wakorintho 14:33, 40 na Wafilipi 1:10.

Dumisha Mahusiano Mazuri

Pata tegemezo. Katika nyakati zenye mkazo wale ambao wana marafiki wengi na ambao wanajuana na watu wengi angalau hupata kadiri fulani ya ulinzi dhidi ya kushindwa. Kupata rafiki mmoja tu mwenye kutumainika ambaye mtu aweza kuongea naye kisiri kwaweza kusaidia sana. Mithali moja ya Biblia yasema: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

Tatua mahitilafiano. “Msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka,” akaandika mtume Paulo. (Waefeso 4:26) Hekima ya kusuluhisha tofauti haraka badala ya kufungia hasira inaonyeshwa katika uchunguzi mmoja wa waokokaji 929 wa mshiko wa moyo. Wale wenye viwango vya juu vya uhasama walikuwa na uwezekano wa mara tatu wa kufa kutokana na kuzimika kwa moyo katika miaka kumi ya kwanza baada ya mshiko wa moyo kuliko wenzao wenye hali ya upole. Waandishi wa uchunguzi huo wasema kwamba ingawa hasira inaonekana kuwa kisababishi kikubwa, hisia yoyote hasi yenye nguvu inayopeleka kiasi kikubwa cha homoni mwilini inaweza kuwa na tokeo ilo hilo. “Husuda ni ubovu wa mifupa,” yasema Mithali 14:30.

Panga kutumia wakati na familia yako. Wazazi Waisraeli waliamriwa watumie wakati na watoto wao, wakikazia kikiki kanuni nzuri katika mioyo yao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kifungo kilichotokea kiliendeleza muungano wa familia—jambo ambalo linakosekana sana leo. Uchunguzi mmoja ulifunua kwamba wenzi wa ndoa wenye kufanya kazi hutumia wastani wa dakika 3.5 pekee za kucheza na watoto wao kila siku. Lakini, familia yako yaweza kuwa chanzo kikubwa sana cha msaada mtu anapokabili mkazo. “Familia inakupa ushirika wa daima ikiwa kikundi kinachokujua vizuri sana na hata kukupenda,” chasema kitabu kimoja juu ya mkazo. “Kufanya kazi pamoja kwa familia ni njia bora zaidi ya kupunguza mkazo.”

Weka Usawaziko Katika Maisha Yako

Uwe mwenye kiasi. Mtu ambaye nyakati zote hujisukuma kupita kiasi kimwili na kihisia-moyo yaelekea atapatwa na uchovu mno na labda mshuko wa moyo. Jambo kuu ni usawaziko. ‘Hekima ya kutoka juu ni yenye kukubali sababu,’ akaandika mwanafunzi Yakobo. (Yakobo 3:17; linganisha Mhubiri 7:16, 17 na Wafilipi 4:5.) Jifunze kukataa madai ambayo yanazidi kile uwezacho kutimiza ifaavyo.

Usijilinganishe na mtu mwingine. Kitabu cha Wagalatia 6:4 chasema: “Acheni kila mmoja athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, na ndipo atakuwa na sababu ya mchachawo kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.” Ndiyo, hata katika mambo ya ibada, Mungu hafanyi ulinganishi usiofaa, akidai zaidi ya vile hali za kila mmoja ziruhusuvyo. Yeye hukubali zawadi zetu na dhabihu ‘kulingana na tulicho nacho, si kulingana na kile ambacho hatuna.’—2 Wakorintho 8:12.

Panga wakati wa pumziko. Hata Yesu, japo alikuwa mwenye bidii, alipanga wakati wa pumziko kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya wafuasi wake. (Marko 6:30-32) Mwandikaji aliyepuliziwa wa Mhubiri alihisi kwamba pumziko lenye kufaa lilinufaisha. Yeye aliandika: “Kisha nikaisifu furaha, kwa sababu mwanadamu hana neno lo lote lililo jema chini ya jua, kuliko kula, na kunywa, na kucheka; na yakuwa hilo likae naye katika amali yake, siku zote za maisha yake alizompa Mungu chini ya jua.” (Mhubiri 8:15) Raha zenye usawaziko zaweza kuburudisha mwili na kusaidia kuondoa mkazo.

Uuone Mkazo kwa Njia Ifaayo

Unapokabili nyakati zenye mkazo:

Usikate kauli kwamba umekataliwa na Mungu. Biblia yatuambia kwamba kwa miaka mingi, Hana, aliyekuwa mwanamke mwaminifu, alikuwa na ‘uchungu rohoni mwake’ (“alihuzunika sana,” Revised Standard Version). (1 Samweli 1:4-11) Katika Makedonia, Paulo “alikuwa na mkazo katika kila hali.” (2 Wakorintho 7:5, Byington) Kabla ya kifo chake, Yesu “alikuwa akiingia katika maumivu makali,” na mkazo wake ulikuwa mkubwa sana hivi kwamba “jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka kwenye ardhi.”a (Luka 22:44) Hao walikuwa watumishi waaminifu wa Mungu. Kwa hiyo, unapokabili mkazo hakuna sababu ya kukata kauli kwamba Mungu amekuacha.

Jifunze kutokana na hali zako zenye kutokeza mkazo. Paulo aliandika kwamba alilazimika kuvumilia “mwiba katika mwili,” bila shaka tatizo la afya ambalo lilikuwa limemsababishia mkazo sana. (2 Wakorintho 12:7) Lakini, miaka mitano baadaye, aliweza kusema hivi: “Katika kila jambo na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji. Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Wafilipi 4:12, 13) Paulo hakufurahia “mwiba katika mwili,” lakini kwa kuuvumilia, alijifunza jinsi ya kutegemea Mungu zaidi kwa ajili ya nguvu.—Zaburi 55:22.

Sitawisha Hali ya Kiroho

Soma na utafakari juu ya Neno la Mungu. “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho,” Yesu alisema. (Mathayo 5:3) Ni muhimu kusoma na kutafakari juu ya Neno la Mungu. Mara nyingi, kwa kutafuta kwa bidii katika Maandiko, tunapata neno lifaalo la kututia moyo ambalo tunahitaji ili kutusaidia katika siku hiyo. (Mithali 2:1-6) “Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu,” akaandika mtunga-zaburi, “faraja zako [za Mungu] zaifurahisha roho yangu.”—Zaburi 94:19.

Sali kwa ukawaida. Paulo aliandika: “Acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Ndiyo, “amani ya Mungu” yaweza kushinda hisia zenye mfadhaiko na kuzituliza, hata wakati ambapo “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” inapohitajiwa.—2 Wakorintho 4:7.

Hudhuria mikutano ya Kikristo. Kutaniko la Kikristo hutoa njia nzuri ya kutoa tegemezo, kwa sababu wale waliomo katika kutaniko wanahimizwa kwa bidii ‘wafikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora [kwa] kutiana moyo.’ Kwa sababu nzuri, Paulo aliwaambia Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza ‘wasiachilie mbali kukusanyika pamoja.’—Waebrania 10:24, 25.

Tumaini Hakika

Ni kweli kwamba kupunguza mkazo mara nyingi kunatia ndani mambo mengi kuliko kufuata tu utaratibu fulani sahili. Mara nyingi, badiliko kubwa katika njia ya kufikiri huhitajiwa. Kwa kielelezo, mtu aweza kuhitaji kujifunza njia mpya za kuitikia hali ili zisimlemeze. Katika visa vingine kurudia-rudia au kuzidi kwa mkazo kwaweza kufanya liwe jambo bora kutafuta matibabu mazuri.

Bila shaka, hakuna mtu leo ambaye maisha yake hayana kabisa mkazo mbaya. Hata hivyo, Biblia yatuhakikishia kwamba karibuni Mungu ataelekeza uangalifu wake kwa wanadamu na kuondoa hali ambazo hutokeza mkazo wenye kudhuru. Katika Ufunuo 21:4, twasoma kwamba Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” Baadaye, wanadamu waaminifu watakaa katika usalama. Nabii Mika alitabiri hivi: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.”—Mika 4:4.

[Maelezo ya Chini]

a Jasho lenye damu limeripotiwa kuwa limetukia katika visa fulani vya mkazo wa akili ulio mkali sana. Kwa kielelezo, katika hali ya hematidrosis, kuna kutoka kwa jasho lililochangamana na damu au rangi ya damu au umajimaji wa mwili uliochangamana na damu. Hata hivyo, haiwezi kusemwa kwa uhakika kabisa, jambo hususa ambalo lilitukia katika kisa cha Yesu.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Mkazo na Upasuaji

Matabibu fulani hufikiria kiwango cha mkazo cha wagonjwa wao kabla ya kuwapeleka katika chumba cha upasuaji. Kwa kielelezo, Dakt. Camran Nezhat, ambaye ni daktari-mpasuaji asema:

“Ikiwa mtu aliyeratibiwa kufanyiwa upasuaji aniambia kwamba alikuwa na wasiwasi siku hiyo na anaogopa kupasuliwa, mimi hufuta upasuaji huo.” Kwa nini? Nezhat aeleza: “Kila daktari-mpasuaji anajua kwamba watu ambao huogopa sana hawafanyi vizuri wakipasuliwa. Wao hutoka damu sana, wanapatwa na maambukizo na matatizo mengi zaidi. Ni vigumu zaidi kwao kupata nafuu. Ni afadhali zaidi ikiwa wametulia.”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusitawisha hali ya kiroho kwaweza kukufanya udumishe utulivu

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kutunza afya yako hupunguza mkazo

Pumziko

Mlo mzuri

Mazoezi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki