Maoni ya Biblia
Je, Roho Waovu Ni Halisi?
KATIKA karne ya 17 na ya 18, kampeni ya mnyanyaso wenye kichaa dhidi ya wachawi ilifanywa katika sehemu nyingi za Ulaya. Wengi ambao walishukiwa kuwa wachawi walipatwa na mateso makali sana. Wengine ambao walishtakiwa kimakosa waliungama kuzoea uchawi ili tu waepe mateso. Idadi zisizohesabika zilifishwa chini ya msingi wa uvumi au shuku.
Ingawa kwa kijuujuu hatua dhidi ya uchawi, namna ya ibada ya roho waovu, zilikuwa na msingi wa Maandiko, kwa wazi hazikuwa za kiakili. Wakristo hawakupewa daraka la kutesa au kufisha wachawi au wowote wanaozoea uwasiliani-roho. (Waroma 12:19) Mtazamo ulio wa kawaida leo ni upi?
Mtazamo Wenye Utulivu
Leo watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo hawachukui mazoea ya namna hiyo ya uwasiliani-roho kwa uzito. Wakichochewa na udadisi, huenda wengine wakajichovya katika unajimu, mizungu, uaguzi, na uchawi, lakini hawaoni mazoea haya ya kifumbo kuwa ibada ya roho waovu. Nyakati nyingine, watumbuizaji, wanamichezo, na wanasiasa hukiri waziwazi kujihusisha kwao na mambo ya kifumbo. Sinema na vitabu fulani huonyesha wachawi na walozi kuwa “wenye kuvutia, kuwa watu ambao kidogo si wa kawaida [na] ambao utendaji wao upitao uwezo wa kibinadamu haudhuru mtu yeyote,” yasema ensaiklopedia moja. Habari ambayo imekusudiwa itumbuize na kuelimisha watoto huenda ikaendeleza habari za kifumbo.
Mtazamo wa namna hiyo ulio mtulivu na wa kawaida kuelekea ibada ya roho waovu waweza kuongoza kwenye kutoitikadi kuwapo kwa roho waovu. Je, unaamini kuwa roho waovu wako na kwamba wanajaribu kwa bidii kutudhuru? Kwa vyovyote, watu wengi leo wangesema kwamba hawajapata kamwe kuwa na uhusiano na roho waovu au kushuhudia utendaji wao. Je, roho waovu ni halisi?
Kutosadiki Hutokeza Utatanishi
Wale wanaodai kuikubali Biblia lakini ambao hutilia shaka uhalisi wa roho waovu wanakabiliwa na utatanishi. Ikiwa hawaamini kuwa roho waovu ni halisi wanaonyesha kiasi fulani cha ukosefu wa imani katika Biblia. Kwa nini? Kwa sababu dhana ya viumbe roho waovu walio na nguvu zipitazo za kibinadamu inafundishwa katika Neno la Mungu, Biblia.
Kitabu chake cha kwanza, Mwanzo, husimulia jinsi kiumbe mwenye akili alivyotumia nyoka kudanganya Hawa na kumfanya aasi dhidi ya Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, humtambulisha mlaghai huyu mwovu, “nyoka wa awali,” kuwa “yeye aitwaye Ibilisi na Shetani, anayeiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Shetani alifanikiwa kuwashawishi malaika wengine waingie katika uasi. (Yuda 6) Katika Biblia malaika hawa walioasi wanaitwa roho waovu. Wanatenda katika ujirani wa dunia na ni wenye hasira sana kuelekea Mungu na wale wanaomtumikia.—Ufunuo 12:12.
Shetani na roho waovu wana uwezo wa kushawishi, kudhuru, na kuwasiliana na wanadamu. (Luka 8:27-33) Wamechunguza asili ya binadamu kwa maelfu ya miaka. Wanajua jinsi ya kutumia kwa faida yao udhaifu wa kibinadamu. Biblia huripoti visa ambavyo walipagaa, au kudhibiti kikamili, wanaume, wanawake, na watoto. (Mathayo 15:22; Marko 5:2) Wanaweza kusababisha maradhi au udhaifu wa kimwili kama vile upofu. (Ayubu 2:6, 7; Mathayo 9:32, 33; 12:22; 17:14-18) Pia wanaweza kupofusha akili za watu. (2 Wakorintho 4:4) Roho waovu wanazidi kutenda kazi, kama kiongozi wao, Shetani, ambaye ni kama “simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Biblia ina masimulizi mengi yanayoonyesha kuwapo kwa roho waovu. Ikiwa unaiamini Biblia, basi unakubali uhalisi wa viumbe roho waovu wasioonekana.
Wadanganyifu Wenye Uovu
Lakini ni jinsi gani roho waovu wenye nguvu wangekuwako leo bila kusababisha hali yenye tisho la daima katika ulimwengu? Kwa nini kuwapo kwao na matendo yao si dhahiri zaidi? Biblia hujibu: “Shetani mwenyewe hufuliza kujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Ibilisi ni mdanganyi. Mara nyingi utendaji wa roho waovu huonekana kwa hila kuwa jambo lisilodhuru au hata lililo jema. Kwa sababu hiyo, ni vigumu kuutambua.
Shetani na roho waovu wake wanaendelea kutaabisha watu kwa njia mbalimbali, kama walivyofanya katika nyakati za Biblia. Wengine ambao sasa ni Wakristo wa kweli wakati mmoja walijihusisha na mambo ya kifumbo; wanaweza kushuhudia mashambulizi yenye kutisha ya roho waovu. Leo, labda kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko wakati uliopita, roho waovu wanatumia nguvu zao zipitazo za kibinadamu kushawishi watu wajiingize katika matendo ya moja kwa moja ya mazoea ya kifumbo. Nguvu yao haipasi kudharauliwa. Hata hivyo, wanatimiza mengi kwa kuvuta watu mbali kutoka kwa Mungu kuliko kuwatisha. Shetani na roho waovu “wanaiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa,” husema Biblia. (Ufunuo 12:9) Wanakusudia kudhoofisha hali ya kiroho kwa njia zenye hila, zenye kudhuru kwa siri.
Roho waovu ni halisi. Ni jinsi gani kiu isiyoisha ya damu na uharibifu ulio wazi leo miongoni mwa watu ingeweza kuelezwa? Kiasili wanadamu wanataka kuishi kwa amani na furaha. Lakini roho waovu huendeleza ubaya na wana uwezo wa kuathiri na kufisidi akili ya kibinadamu.
Lakini, Yehova ndiye Mungu mweza yote—aliye na nguvu zaidi kuliko roho waovu. Yeye hutoa nguvu na ulinzi wake dhidi ya “mbinu za Ibilisi.” (Waefeso 6:11-18) Hatuhitaji kuwa na hofu isiyofaa ya roho waovu, kwani Mungu anaahidi: “Basi, jitiisheni wenyewe kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.”—Yakobo 4:7.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]
Sipa Iconoy