Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 4/22 kur. 17-19
  • Naweza Kuepukaje Kusongwa Sana na Rafiki Yangu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuepukaje Kusongwa Sana na Rafiki Yangu?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhitaji wa Kuwa na Wakati wa Kibinafsi na Faragha
  • ‘Panuka’
  • Tumia Wakati Pamoja na Rafiki Wanaofaa
  • Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
    Amkeni!—1996
  • Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Marafiki Wangu wa Kweli ni Nani?
    Amkeni!—2011
  • Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 4/22 kur. 17-19

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuepukaje Kusongwa Sana na Rafiki Yangu?

“Rafiki yangu alitenda kana kwamba alinimiliki. Hakuniruhusu niwe na wakati wa faragha.”—Hollie.

“YUKO rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu,” yasema mithali yenye hekima. (Mithali 18:24) Na ikiwa una rafiki mnayeshiriki usadikisho wako, ucheshi, au mapendezi, kiasili mwataka tu kuwa pamoja. Kijana aitwaye Caroline asema: “Ukaribu wa rafiki zangu fulani katika kutaniko la Kikristo ni tokeo la kushiriki utendaji pamoja.” Akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, Caroline huweka kando mwezi mmoja ambao yeye hupanga kutumia muda wa saa 60 katika kazi ya kueneza evanjeli. Rafiki zake hupanga ratiba zao ili waweze kumwunga mkono katika kazi hii!

Lakini ingawa kuwa pamoja kuna manufaa yake, wakati mwingine waweza kuhisi kana kwamba kumepita kiasi. Hollie, aliyetajwa mwanzoni, ahisi kusongwa sana na mmoja wa rafiki zake. Na hayuko peke yake katika kuhisi hivyo. Hollie aonelea: “Hilo laonekana kutendeka kwa vijana wengine pia. Karibu waishi katika mifuko ya mmoja na mwenzake hadi kunatokea mlipuko mkubwa. Kisha hawazungumzi kwa majuma kadhaa.”

Tatizo ni kwamba, kumwambia rafiki kuwa wahisi kusongwa sana na kwamba wahitaji wakati zaidi wa faragha si rahisi. Waweza kuhofu kuumiza hisia za rafiki yako. Waweza pia kuhofu kutahatarisha uhusiano wenu. Hata hivyo, kuweka nafasi ya kadiri katika urafiki wenu kwaelekea kusaidia badala ya kuumiza.

Kutoa kielezi: Katika bustani ya umma katika Sydney, Australia, mti mkubwa ulihitaji kuwekewa uzio wa mnyororo. Kwa nini? Kwa sababu vikosi vya wageni vilikuwa vikigandamiza udongo kwa ukawaida na kusonga mizizi. Ikiwa haukulindwa, mti huo ungekufa. Hilo pia laweza kuwa kweli kwa habari ya urafiki. Kuwa karibu sana kwaweza kusonga uhusiano. Mfalme Solomoni aliandika: “Mguu wako usiingie katika nyumba ya jirani yako ila kwa kiasi; asije akakukinai na kukuchukia.”—Mithali 25:17, chapa ya 1989.

Uhitaji wa Kuwa na Wakati wa Kibinafsi na Faragha

Kwa nini Solomoni alisema hivyo? Sababu moja ni kwamba, sote twahitaji wakati wa kibinafsi na faragha. Hata Yesu Kristo alikuwa na uhitaji huo. Ingawa alikuwa na ukaribu na wanafunzi wake, mara kwa mara angeenda “akiwa peke yake mwenyewe ili kusali.” (Mathayo 14:23; Marko 1:35) Isaka mwenye kumhofu Mungu vilevile alipata wakati wa kuwa peke yake. (Mwanzo 24:63) Wewe pia wahitaji wakati wa kibinafsi ili kushughulikia mambo kama vile mgawo wa masomo ya nyumbani, kazi za kila siku, na funzo lako la Biblia la kibinafsi. Na ikiwa rafiki zako waonyesha ukosefu wa ufikirio kwa kupuuza mahitaji yako katika jambo hili, uchungu wa moyo waweza kutokea.

Basi, usiogope, kumjulisha rafiki yako unapohitaji wakati wa kuwa peke yako. Kwa kuwa upendo wa Kikristo “hautafuti masilahi yao wenyewe,” rafiki wa kweli kwa kawaida atajaribu kuwa mwenye kuelewa. (1 Wakorintho 13:4, 5; Mithali 17:17) “Wakati wa kipindi kinachoelekea kwa mtihani wangu wa mwisho,” kijana mmoja aandika, “rafiki zangu walikuwa wenye utegemezo na wenye kuelewa sana. Nilijihisi starehe kuwaomba waondoke nilipohitaji wakati wa kujifunza. Kuwa mwenye kufuatia haki pamoja na rafiki zangu ni rahisi; wanajua kwamba sote tuna madaraka.”

Bila shaka ile Kanuni Bora yahitaji tuwafikirie rafiki zetu pia. (Mathayo 7:12) Mtu mchanga aitwaye Tamara aandika: “Kuwa kwangu na madaraka mengi kwa kweli kumenifanya niweze kutambua uhitaji wa rafiki yangu wa kuwa na wakati wake mwenyewe.” Na wakati Tamara anapokuwa na kazi nyumbani, rafiki zake hawamhimizi kuzifanya kwa haraka au kuziacha hadi wakati mwingine. Badala ya hivyo, Tamara asema, “kwa kawaida watanisaidia kufanya kazi yangu ili tuweze kufanya mambo pamoja baadaye.” Rafiki wasio na ubinafsi ni hazina iliyoje—na kutumia wakati kwenye hivyo pamoja nao kwafaa kama nini!

‘Panuka’

Kuna sababu nyingine kwa nini ni jambo la hekima kuacha nafasi kati ya urafiki. Tunapotoa wakati na hisia zetu zote kwa urafiki mmoja tu, huenda tukaelekea kupuuza uhusiano mwingine wa muhimu—kama vile uhusiano wetu na wazazi wetu na ndugu zetu wa kimwili na Wakristo wengine. Pia twazuia sana ukuzi wetu wa kihisia-moyo na kiroho. Biblia husema: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.” (Mithali 27:17) Bila shaka waweza ‘kunolewa’ kidogo sana kwa kushirikiana na mtu mmoja tu—hasa ikiwa mtu huyo ni wa rika lako.

Hivyo, Biblia huvunja moyo kuwa katika kikundi cha watu wenye mawazo yanayofanana, kuwa wenye uzuifu, au bila kuhusisha wengine katika uchaguzi wetu wa marafiki. Inatuhimiza ‘tupanuke.’ (2 Wakorintho 6:13) “Hata kama una uhusiano wa pekee na mtu fulani,” chashauri kitabu Moods and Feelings, “ni jambo la maana kuwa na wakati wa kuwaona rafiki wengine pia.”

Kwa kawaida ushauri kama huu si rahisi kuutumia. Kijana Mkristo aitwaye Michael asema: “Troy nami tulikuwa tukifanya kila kitu pamoja, katika kutaniko na hata mambo mengine ya kirafiki. Hatukuweza kutengana. Kisha kijana mwingine Shahidi akahamia kutaniko letu. Yeye nami tulitaka kutumika pamoja tukiwa waeneza-evanjeli wa wakati wote, kwa hiyo tukaanza kutumia wakati pamoja.” Tokeo likawa nini? “Troy aliacha kuzungumza nami,” asema Michael, “na baada ya kufanya jitihada bila kufanikiwa ili kurekebisha mambo, niliacha kuzungumza naye. Hili liliendelea kwa muda wa mwaka mmoja.” Alieleza urafiki wao kuwa “umiliki wenye wivu.”

Hata hivyo, katika uhusiano mzuri na wenye usawaziko, marafiki hawatendeani kama mali. Kwa hiyo ikiwa rafiki athibitika kuwa mwenye kukinza jitihada zako za kupanuka, wahitaji kuwa na mazungumzo ya ana kwa ana pamoja naye. Labda rafiki yako ahitaji tu uhakikishio kwamba ungali wathamini sana urafiki wake. Mhakikishie kuwa mtaendelea kufanya mambo pamoja.

Kwa kukiri wazi, yaweza kuchukua wakati kwa rafiki yako kujirekebisha kwa maoni hayo. Kwa kielelezo, Zaneta mwenye umri wa miaka 16, alihisi wivu wakati rafiki yake wa karibu alipoanza kutumia wakati na wengine. Lakini Zaneta asema kwamba alishinda hisia hizo, “kwa msaada wa sala na funzo la Biblia la kibinafsi.” Kwa njia hiyo aliweza kudumisha uhusiano wa karibu na rafiki yake. Rafiki ya Michael, Troy, pia aliweza kushinda wivu wake wa kwanza na wakawa marafiki wazuri tena. Labda rafiki yako atafanya vivyo hivyo. Kwa kweli, mwishowe, kupanuka humfaidi kila mmoja anayehusika. Debbie mwenye umri wa miaka 17 hupata kwamba wakati rafiki zake wanapopata rafiki wapya, “kwa kawaida wao huwa rafiki zangu pia.”

Namna gani ikiwa, rafiki yako akataa tu kukubali mabadiliko haya katika urafiki wenu? Huenda ikawa hutakuwa na la kufanya ila tu kutengana. Hata hivyo, kabla ya kuamua kwamba huo ndio mwisho wa urafiki wenu, kwa nini usiwaombe wazazi wako maoni yao kuhusu jambo hilo? Hata hivyo, wazazi wanaomhofu Mungu kwa kweli ndio rafiki zako wa karibu zaidi. Na wanaweza kuwa na madokezo fulani yenye kutumika ambayo yaweza kuokoa urafiki wenu bila kuridhiana uhitaji wako wa nafasi.

Tumia Wakati Pamoja na Rafiki Wanaofaa

Neno la hadhari: Kupanuka hakumaanishi kuwa usiwe na uteuzi katika uchaguzi wako wa marafiki. Kitabu kuhusu urafiki husema: “Ni jambo la asili kuwa kama watu unaotumia wakati mwingi nao. Wakati mwingine hili laweza kutokea bila wewe kujua kuwa latokea. Waweza kuanza kufikiri na kutenda kama marika wako bila kujali unavyohisi. Katika njia hii marika wako wanaweza kuwa wanakudhibiti.” Biblia ilitaja hoja hiihii maelfu ya miaka iliyopita iliposema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.”—Mithali 13:20.

Unapokuwa shuleni au kazini, huenda utalazimika kutumia wakati pamoja na watu ambao hawapendezwi kumtumikia Yehova. Lakini unapowachagua waandamani wa karibu, kumbuka shauri la Biblia: “Waandamani wabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Wakorintho 15:33, Today’s English Version.

Pia, kumbuka kwamba urafiki wa maana zaidi kuliko urafiki wowote wa kibinadamu ni urafiki na Muumba wetu, Yehova Mungu. Debbie, aliyetajwa mapema, ana rafiki kadhaa wazuri. Na bado shauri lake ni “kuhakikisha kwamba kila wakati Yehova huja kwanza.” Mwanamume mwaminifu Abrahamu wa zamani alifanya hivyo, na hasa Yehova alimwita “rafiki yangu.” (Isaya 41:8) Na fikiria hili: Yehova haoni wivu unapowapatia wakati rafiki zako wengine ambao pia wanampenda; kwa hakika, yeye hutia moyo ufanye hivyo. Ni Rafiki wa kweli namna gani!

[Picha katika ukurasa wa 18]

Rafiki za kweli hutambua uhitaji wa mmoja na mwenzake wa kuwa na wakati wa faragha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki