Uwe Mteuzi Unapochagua Vitumbuizo
Vitumbuizo huathirije watoto? Alvin Poussaint, mwalimu aliye pia daktari ambaye ameshughulika na watoto kwa miaka 30 hivi, amesadiki kwamba kutazama sinema zenye ngono na ujeuri hufundisha vijana kwamba hizo ni tabia za kawaida. Yeye ataja hatari nyingine pia: “Nimeona watoto wakitoka kuona sinema kama hizo wakiwa na hofu—au wakiwa wakali sana. Nimeona wengine wakirudia kushika-shika mama au kunyonya kidole au kukojoa kitandani.” Kulingana na daktari huyo, wataalamu wameandika matukio mengine ambayo yanaweza kusababisha tabia hizo—kutendwa vibaya kimwili au kingono au kuishi katika eneo la vita, tukitaja machache tu. “Hakuna mtu yeyote kati yetu ambaye angeweka mtoto kimakusudi katika hali hizo,” yeye aeleza, “lakini hatuwazuii kutazama sinema za mambo ambayo yangetuogofya kama wangeyatazama yakiwa halisi.”
Wakristo wana sababu nzuri za kuwa wateuzi na kuhakikisha kwamba vitumbuizo wanavyochagua havivunji kanuni za Biblia. Kwa mfano, Zaburi 11:5 yasema: “BWANA humjaribu mwenye haki; bali nafsi yake humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu.” Na mtume Mkristo Paulo aliandika: “Kwa hiyo, fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa . . . Yawekeni mbali nanyi hayo, hasira ya kisasi, hasira, ubaya, usemi wenye kuudhi, na maongezi yenye aibu kutoka katika kinywa chenu.”—Wakolosai 3:5, 8.
Basi, wazazi wapaswa kutahadhari ili vitumbuizo wanavyowachagulia watoto wao—na kujichagulia—visiwe vyenye kuendeleza “kazi za mwili.” (Wagalatia 5:19-21) Wao wapaswa kuwa wateuzi, wakifikiria ubora na wingi wa vitumbuizo.—Waefeso 5:15-17.