Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 8/8 kur. 20-21
  • Mavazi na Mapambo Yako—Je, Ni ya Maana kwa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mavazi na Mapambo Yako—Je, Ni ya Maana kwa Mungu?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jambo la Kibinafsi
  • “Pamoja na Kiasi na Utimamu wa Akili”
  • Kwa Nini Mavazi na Mwonekano Wetu Ni Muhimu?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Mavazi Yenye Mpangilio Mzuri Humstahi Mungu
    Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Kuvaa na Kujipamba kwa Kiasi
    Huduma Yetu ya Ufalme—2002
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 8/8 kur. 20-21

Maoni ya biblia

Mavazi na Mapambo Yako—Je, Ni ya Maana kwa Mungu?

“Kama vile faharisi huonyesha yaliyomo katika kitabu, . . . ndivyo na sura ya nje na mavazi ya mwanamume au mwanamke, hutuonyesha mwelekeo wake wa akili.”—Mwandishi wa tamthilia Mwingereza Philip Massinger.

KATIKA karne ya tatu W.K., mwandikaji wa kanisa Titus Clemens aliandika orodha ndefu ya sheria za kudhibiti mavazi na mapambo. Madoido na mavazi yenye mapambo ya kupendeza na ya rangi-rangi yalikatazwa. Wanawake hawakupaswa kupaka nywele zao rangi wala “kupaka nyuso zao rangi kwa njia zenye ujanja na za kunasa,” yaani, “kujipodoa.” Wanaume waliagizwa kunyoa nywele zao kwa sababu “nywele fupi . . . huonyesha heshima,” lakini ndevu hazikupasa kuguswa, kwani “zinaufanya uso uonekane kuwa wenye mamlaka ya kibaba.”a

Karne kadhaa baadaye kiongozi Mprotestanti John Calvin alitunga sheria zilizofafanua kihususa rangi na aina ya mavazi ambayo wafuasi wake wangeweza kuvalia. Vito na lesi vilichukiwa, na mwanamke angeweza kutiwa gerezani kwa kusuka nywele zake “kwa njia isiyo ya adili.”

Maoni ya namna hiyo yenye kupita kiasi, ambayo yamedhihirishwa na viongozi wa kidini katika miaka ambayo imepita, yamefanya watu fulani wenye moyo mweupe wajiulize, Je, mavazi yangu ni ya maana kwa Mungu? Je, yeye hukataza mitindo fulani au kujipodoa? Biblia hufundisha nini?

Jambo la Kibinafsi

Kwa kupendeza, kama ilivyorekodiwa katika Yohana 8:31, 32, Yesu alisema hivi kwa wanafunzi wake: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, . . . mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” Ndiyo, kweli zilizofundishwa na Yesu zilikusudiwa kuwakomboa watu kutokana na mizigo yenye kulemea iliyotokezwa na mapokeo na mafundisho bandia. Kweli hizo zilikusudiwa kuwaburudisha wale ‘waliomenyeka na kulemezwa mizigo.’ (Mathayo 11:28) Wala Yesu wala Baba yake, Yehova Mungu, hawana tamaa yoyote ya kudhibiti maisha ya watu kwa kiwango ambacho watu hawawezi kujifanyia mambo yao na kutumia akili zao kwa mambo ya kibinafsi. Yehova awataka wawe watu wakomavu ambao “kupitia utumizi, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.”—Waebrania 5:14.

Hivyo, Biblia haitoi sheria zenye mambo mengi za kuonyesha namna ya kuvalia na kujipamba au kujipodoa, isipokuwa amri za Sheria ya Musa, zilizowataka Wayahudi wavae mavazi fulani hususa ili kuwasaidia kujitenga na mataifa yaliyowazunguka na athari yao isiyo ya kiadili. (Hesabu 15:38-41; Kumbukumbu la Torati 22:5) Ndani ya mpango wa Kikristo, kwa msingi mavazi na kujipamba ni mapendezi ya kibinafsi.

Hata hivyo, jambo hili halidokezi kwamba Mungu hajali tunachovaa au kwamba ‘akubali kila kitu.’ Kinyume cha hilo, Biblia ina miongozo yenye kiasi inayoonyesha maoni ya Mungu kuhusu mavazi na mapambo.

“Pamoja na Kiasi na Utimamu wa Akili”

Mtume Paulo aliandika kwamba wanawake Wakristo wanapaswa “wajirembe wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mvao ulio ghali sana.” Vivyo hivyo, Petro aonya dhidi ya “kusuka nywele kwa nje na wa kuvalia madoido ya dhahabu.”—1 Timotheo 2:9; 1 Petro 3:3.

Je, mitume Petro na Paulo wanaonyesha kwamba wanawake na wanaume Wakristo hawapaswi kujirembesha? Sivyo hata kidogo! Kwa kweli, Biblia hutaja wanaume na wanawake waaminifu waliojivika vito au kutumia vipodozi na manukato. Mbele ya watazamaji wake na Mfalme Ahasuero, Esta alirembwa kwelikweli na kupakwa manukato na kukandwa. Na Yusufu alivikwa mavazi ya kitani nzuri na mkufu wa dhahabu.—Mwanzo 41:42; Kutoka 32:2, 3; Esta 2:7, 12, 15.

Fungu la maneno “utimamu wa akili,” kama litumiwavyo na Paulo, hutusaidia kuelewa onyo hilo la upole. Neno la awali la Kigiriki huonyesha kuwa mwenye kiasi na mwenye kujithibiti. Linadokeza kujifikiria jinsi ulivyo kihalisi, si kujielekezea uangalifu isivyofaa. Tafsiri nyingine za Biblia hufasili neno hili kuwa “kwa busara,” “-a akili,” “safi,” au “-enye kujizuia.” Sifa hii ni takwa la maana kwa wazee Wakristo.—1 Timotheo 3:2.

Hivyo, kwa kutuambia kwamba mavazi na mapambo yetu yapaswa kuwa yenye kiasi na yenye mpangilio mzuri, Maandiko hututia moyo tujiepushe na mitindo yoyote ya kupita kiasi ambayo ingewaudhi wengine na kusuta mwenendo wetu na wa kutaniko la Kikristo. Badala ya kukazia uangalifu kwa sura zao kupitia mapambo ya kimwili, wale wanaodai kumstahi Mungu wapaswa kuwa wenye utimamu wa akili na kukazia “yule mtu wa siri wa moyoni katika vao lisilofisidika la roho ya utulivu na ya upole.” Hii, amalizia Petro, “ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:4.

Wakristo ni “kitu cha kutazamwa mahali pa michezo kwa ulimwengu.” Wanahitaji kutambua wanatokeza maoni ya aina gani kwa wengine, hasa kwa kufikiria sharti lao la kuhubiri habari njema. (1 Wakorintho 4:9; Mathayo 24:14) Kwa hiyo hawangetaka kuruhusu kitu chochote, kutia ndani sura yao, iondoshe fikira za wengine wasisikilize ujumbe huo wa maana.—2 Wakorintho 4:2.

Ingawa mitindo hutofautiana sana katika sehemu mbalimbali, Biblia hutolea kila mtu mwongozo ulio wazi, wa kiasi unaowasaidia kufanya uchaguzi kwa hekima. Maadamu watu wanafuata kanuni hizi, Mungu huwaruhusu wote kwa upendo wachague mavazi na mapambo yanayowapendeza.

[Maelezo ya Chini]

a Majaribio yalifanywa ili kuimarisha vizuizi hivi kwa kupotoa Maandiko. Ingawa Biblia haisemi jambo lolote kama hilo, mwanatheolojia mwenye uvutano Tertullian alifundisha kwamba kwa kuwa mwanamke ndiye aliyesababisha “dhambi ya kwanza, na makuruhu . . . ya kuteseka kwa wanadamu,” wanawake wanapaswa “kutembea kama Hawa wakiomboleza na kutubu.” Hata alisisitiza kwamba mwanamke mrembo kiasili hata apaswa kuficha urembo wake.—Linganisha Waroma 5:12-14; 1 Timotheo 2:13, 14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki