Tumaini na Upendo Zirudipo
WAZAZI, walimu, na wengine ambao hushughulika na vijana hutambua kwamba wao, vijana, au mtu yeyote yule hawezi kubadili ulimwengu. Kuna mavutano yafananayo na mawimbi ya bahari, ambayo hakuna mtu yeyote awezaye kuyazuia. Lakini, kuna mengi tunayoweza kufanya ili kusaidia vijana wawe wenye furaha zaidi, wenye afya zaidi, na wenye mahusiano mazuri na jamii.
Kwa kuwa kuzuia ni bora kuliko kuponya, wazazi wapaswa kufikiria kwa uangalifu jinsi mtindo wao wa maisha na mambo wanayotanguliza yawezavyo kuathiri mitazamo na tabia za watoto wao. Kuandaa mazingira yenye upendo na yenye kujali nyumbani hufanyiza usalama ambao unaweza kuzuia kwa njia bora zaidi tabia ya kujiharibu. Mojawapo ya mahitaji makubwa zaidi ya vijana ni kuwa na mtu wa kuwasikiliza. Wazazi wasipowasikiliza, labda watu wasiofaa watawasikiliza.
Jambo hilo lamaanisha nini kwa wazazi leo? Weka wakati wa kuwa na watoto wanapouhitaji—wakiwa wachanga. Hilo si rahisi kwa familia nyingi. Familia hujitahidi kupata riziki, wazazi wote wawili wakikosa namna ila tu kufanya kazi. Wale ambao wamekuwa tayari kufanya dhabihu hiyo, na wameweza kufanya hivyo, ili wapate wakati wa kuwa pamoja na watoto wao mara nyingi wamevuna thawabu ya kuona wana wao na binti zao wakifanikiwa maishani. Lakini, kama ilivyotajwa mapema, nyakati nyingine japo jitihada bora zaidi za wazazi, matatizo mazito yaweza kuwapata watoto wao.
Marafiki na Watu Wengine Wazima Waweza Kusaidia
Vita, ubakaji, na kutendwa vibaya kwa vijana huhitaji watu wazima wenye kuwajali vijana watie jitihada nyingi sana ili kushughulikia madhara ya vijana. Huenda hata jitihada za kuwasaidia vijana wenye kusumbuliwa na mambo mabaya kama hayo ziambulie patupu. Huenda hilo likamaanisha kutumia wakati mwingi sana na kujikakamua kwelikweli. Kwa hakika, si jambo la hekima wala lenye upendo kuwashushia hadhi wala kuwakana. Je, twaweza kukuza hisia zaidi ili tuonyeshe fadhili na upendo ili tuwasaidie wale walio hatarini?
Si wazazi tu bali pia marafiki na hata ndugu na dada zao wanahitaji hasa kuwa wenye tahadhari kuona mielekeo katika wachanga hao ambayo yaweza kuashiria hali dhaifu ya kihisia-moyo au isiyo na usawaziko. (Ona sanduku “Msaada wa Wataalamu Wahitajika,” ukurasa wa 8.) Ikiwa kuna dalili hizo, uwe mwepesi kusikiliza. Ikiwezekana, jaribu kuuliza vijana wenye matatizo maswali yenye fadhili na kuwahakikishia kwamba wewe ni rafiki wa kweli. Marafiki na watu wa ukoo wenye kutumainiwa wanaweza kuwategemeza wazazi katika kushughulikia hali ngumu; lakini, bila shaka, wawe waangalifu wasichukue daraka la wazazi. Mara nyingi mielekeo ya vijana kujiua ni ombi la dharura la kutaka uangalifu—uangalifu wa wazazi.
Mojawapo ya zawadi bora zaidi mtu yeyote aweza kuwapa vijana ni tumaini thabiti la wakati ujao wenye furaha, kichocheo cha kuishi. Vijana wengi wametambua ukweli wa ahadi za Biblia za ulimwengu bora ambao utakuja karibuni.
Waokolewa Wakifikiria Kujiua
Kutoka Japani, mwanamke mmoja mchanga ambaye mara nyingi alifikiria kujiua asema: “Ni mara nyingi kadiri gani nilitamani kujiua. Nilipokuwa mtoto mchanga, nilitendwa vibaya kingono na mtu niliyemtumaini. . . . Wakati uliopita, nilikuwa nimeandika habari nyingi sana zilizosema ‘Nataka kufa.’ Sasa nimekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na sasa natumikia nikiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote, lakini hali hiyo bado hunishika mara kwa mara. . . . Lakini Yehova ameniruhusu niendelee kuishi, naye anaonekana kana kwamba ananiambia kwa upole, ‘Endelea kuishi.’”
Msichana mmoja kutoka Urusi mwenye umri wa miaka 15 alieleza hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka minane, nilianza kuhisi kwamba hakuna mtu aliyenihitaji. Wazazi wangu hawakuwa na wakati wa kuzungumza nami, na nilijaribu kujisuluhishia matatizo yangu. Nikawa mnyamavu. Nikawa nagombana daima na watu wa ukoo. Kisha nikafikiria kujiua. Nilifurahi kama nini kukutana na Mashahidi wa Yehova!”
Na kutoka Australia kuna maelezo haya yenye kutia moyo ya Cathy, ambaye sasa yuko katika miaka ya 30, yanayoonyesha kwamba kukata tumaini kwaweza kugeuka kuwa tumaini: “Niliwaza na kuwazua jinsi ya kumaliza uhai wangu na hatimaye nikajaribu. Nilitaka niondoke ulimwengu huu, uliojaa uchungu, hasira, na ubatili. Kushuka moyo kukafanya iwe vigumu sana kuondokea hali hiyo niliyoona imeninasa kama ‘utando wa buibui.’ Basi, ikaonekana kama suluhisho ni kujiua.
“Niliposikia kwa mara ya kwanza uwezekano wa dunia kuwa paradiso, yenye maisha ya amani kwa wote, nikaitamani sana. Lakini ilionekana kama ndoto tu isiyoweza kutimia. Hata hivyo, polepole nilianza kuelewa maoni ya Yehova juu ya uhai na jinsi kila mmoja wetu alivyo na thamani machoni pake. Nikaanza kuwa na uhakika kwamba kuna tumaini kwa wakati ujao. Hatimaye, nilipata njia ya kutoka kwenye hali iliyokuwa imeninasa. Lakini ikawa vigumu sana kutoka. Nyakati nyingine kushuka moyo kungenishinda, nami ningehisi nimevurugika kwelikweli. Lakini, kwa kukaza fikira zangu kwa Yehova Mungu niliweza kumkaribia sana na kuhisi usalama. Namshukuru Yehova kwa yote ambayo amenifanyia.”
Hakuna Vifo vya Vijana Tena
Kwa kujifunza Biblia, kijana aweza kutambua kwamba kuna kitu bora cha kutazamia—kitu ambacho mtume Mkristo Paulo akiita “uhai ulio halisi.” Alimshauri kijana Timotheo: “Uwape maagizo wale walio matajiri . . . waweke tumaini lao, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu; kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, . . . wakijiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili wao wapate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.”—1 Timotheo 6:17-19.
Basi ni kama shauri la Paulo lamaanisha kwamba twapaswa kujihusisha na watu wengine, tukiwasaidia kuwa na tumaini thabiti la wakati ujao. “Uhai ulio halisi” ndio ambao Yehova ameahidi katika ulimwengu wake mpya wa “mbingu mpya na dunia mpya.”—2 Petro 3:13.
Vijana wengi ambao pindi moja walikuwa hatarini wamepata kuelewa kwamba kutumia dawa za kulevya na mitindo ya maisha yenye kukosa adili ni njia tu zenye kuongoza kwenye kifo, na kujiua kunakuwa njia tu ya mkato. Wametambua kwamba ulimwengu huu, ukiwa na vita vyake, chuki, mwenendo mbaya, na njia zake zisizo za upendo, karibuni utapotelea mbali. Wamejifunza kwamba ulimwengu huu hauwezi kuokolewa. Wameamini kwa dhati kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini la pekee, kwa kuwa utaleta ulimwengu mpya ambamo vijana na vilevile wanadamu watiifu hawatalazimika kufa kamwe—wala hata hawatataka kufa tena.—Ufunuo 21:1-4.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Msaada wa Wataalamu Wahitajika
Kitabu The American Medical Association Encyclopedia of Medicine chasema kwamba “zaidi ya asilimia 90 ya kujiua husababishwa na magonjwa ya akili.” Kinaorodhesha magonjwa hayo kuwa mshuko wa moyo mkali sana (asilimia 15 hivi), kuchanganyikiwa akili (asilimia 10 hivi), kutegemea kileo (asilimia 7 hivi), tatizo la kutopatana na watu (asilimia 5 hivi), na fadhaa (chini ya asilimia 5). Kinashauri hivi: “Majaribio yote ya kutaka kujiua yapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Asilimia 20 hadi 30 ya watu ambao wanajaribu kujiua hujaribu tena kujiua kwa muda wa mwaka mmoja.” Dakt. Jan Fawcett aandika: “Zaidi ya nusu ya watu wanaojiua [Marekani] hawakupata kumwona daktari wa matatizo ya akili.” Na kitabu kingine chasema: “Sehemu muhimu sana ya tiba ni kumwona daktari wa matatizo ya akili haraka iwezekanavyo ili kutibu mshuko wa moyo unaotokeza tatizo hilo.”