Watu Wote Watakapopendana
KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo alitaja wakati ambapo watu wote watakapopendana. Akitoa utangulizi wa maneno yake, Yesu alinukuu Zaburi ya 37, akisema: “Wabarikiwa ni wapole: kwa kuwa watairithi nchi.” Zaburi hiyo ya Biblia pia inafafanua jinsi ambavyo hali hiyo nzuri ajabu itapatikana, ikisema: “Waovu watakatiliwa mbali; lakini wale wamngojeao Yehova, wao watairithi nchi.”—Mathayo 5:5; Zaburi 37:9; American Standard Version.
Hilo litakuwa badiliko lenye kutokeza kama nini—waovu wote kuondolewa duniani na watu tu wanaopendana wabaki! Jambo hilo laweza kutokeaje? Katika mahubiri yake yenye kujulikana sana, Yesu aliendelea kuonyesha jinsi ambavyo jambo hilo lingetokea alipotufundisha tusali hivi: “Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatendeke, kama ilivyo mbinguni, na pia duniani.” (Mathayo 6:10, AS) Ona mahali ambapo mapenzi ya Mungu yatafanywa. Si mbinguni tu. “Twasali, mapenzi yako yatendeke, duniani kama ilivyo mbinguni,” ikakazia makala moja katika The Christian Century.
Basi, Ufalme wa Mungu ambao Yesu alitufundisha tusali ni nini? Kwa wazi, hiyo ni serikali halisi, ambayo inatawala kutoka mbinguni. Hiyo ndiyo sababu inaitwa “Ufalme wa mbingu.” (Mathayo 10:7) Mtawala aliyewekwa rasmi wa Ufalme huo, au serikali, ni Mwana wa Mungu, Yesu Kristo.
Muda mrefu kabla ya Yesu kuzaliwa na Mariamu, nabii wa Yehova Isaya alikuwa ametabiri kuhusu tukio hilo la muujiza na mambo ambayo hatimaye yangefuata: “Kwetu mtoto amezaliwa, tumepewa mwana; na serikali itakuwa begani pake: na jina lake litakuwa Ajabu, Mshauri, Mungu Mwenye Uweza, Baba wa Milele, Mkuu wa Amani. Usitawi wa serikali yake na amani hautakuwa na mwisho.” (Isaya 9:6, 7, AS) Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, yeye aliketi pamoja na Baba yake mbinguni, akingojea apewe amri ya kuanza kutawala akiwa Mfalme.—Zaburi 110:1, 2; Waebrania 10:12, 13; Ufunuo 11:15.
Basi, nini ambacho hatimaye kitapata ulimwengu huu uliojaa chuki? Ona jinsi ambavyo Biblia inajibu swali hilo. Nabii wa Mungu Danieli alitabiri: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Kwa wazi, unabii huu wa Biblia waelekezea wakati ambapo kutakuwa na badiliko kubwa sana katika mambo ya wanadamu. Mfumo wote wa mambo, ambao unatia ndani wale wa ulimwengu huu ambao wanakataa kishupavu kunyenyekea utawala wa Mungu, wataondolewa kwenye dunia! Ebu fikiria hali ambayo itachukua mahali pa mfumo huu.
Maisha Katika Ulimwengu Mpya Wenye Uadilifu
Ulimwengu huu wa kale uishapo, kutakuwa na waokokaji. Biblia yaeleza hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yohana 2:17) Ndiyo, wale wanaofanya mapenzi ya Mungu wataokoka katika ulimwengu mpya, kama vile Noa na familia yake walivyookoka ulimwengu wa siku zao. Mtume Petro aliandika: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi [ya Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:5-7, 11-13.
Kuhusu wakati ambapo serikali ya pekee inayotenda ni Ufalme wa Mungu, Biblia inaahidi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Waadilifu watafurahia maisha katika ulimwengu uliosafishwa. Huo utakuwa wakati bora kama nini! Ikiwa hujazichunguza baraka zinazofafanuliwa katika Biblia ambazo zimeonyeshwa kwenye kurasa zinazotangulia, tafadhali zichunguze sasa.
Je, moyo wako hauchangamki kujua kwamba Muumba wetu anaahidi mambo ya ajabu kama hayo kwa manufaa ya wale wote ambao wanamwabudu? Kwa hakika, hilo lilikuwa kusudi la Mungu alipowaumba wanadamu wa kwanza wawili na kuwaweka katika paradiso ya dunia! Ona maneno ambayo Mungu aliwaambia: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”—Mwanzo 1:27, 28.
Adamu na Hawa walipaswa kuzaa watoto, na watoto hao walipokuwa watu wazima, wao walipaswa kushiriki katika kazi hii nzuri ya kudumisha Paradiso ya kidunia. Ebu fikiria shangwe ya kupanua bustani ya Edeni kwa kadiri ambavyo familia ya kibinadamu iliongezeka! Kwa wazi, lilikuwa ni kusudi la Mungu kwa dunia nzima kuwa paradiso. Je, kusudi hilo litapata kutimizwa? Kwa hakika litatimizwa, kwa kuwa neno la Mungu mwenyewe lasema hivyo! Yeye aahidi: “Nimenena, . . . nami nitafanya.”—Isaya 46:11; 55:11.
Je, ungefurahia kuishi milele katika Paradiso ya duniani ambayo imefafanuliwa katika maandiko na ambayo imeonyeshwa kwenye kurasa zilizotangulia? Kwa wazi, si kila mtu ataruhusiwa kuishi milele. Kuna matakwa. Ni matakwa yapi hayo?
Kustahili Kuishi Milele
Kwanza kabisa, wale wanaoishi katika ulimwengu mpya wa Mungu ni lazima wajifunze kupendana, kama tunavyofundishwa na Mungu. Biblia yasema: “Nyinyi wenyewe hufundishwa na Mungu kupendana.” (1 Wathesalonike 4:9) Tunafundishwaje jambo hili na Mungu?
Hasa ni kwa kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia. Hilo linamaanisha kwamba ili kuishi milele, ni lazima tukubali mafundisho ya Mungu katika Biblia. Mwanafunzi mmoja wa Biblia wa nchi za Mashariki alisema: “Natazamia wakati ambapo, kama Biblia ilivyoahidi, watu wote watajifunza kupendana.”
Akisali kwa Baba yake, Yesu alitambulisha takwa muhimu. Yeye alisema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Broshua yenye kurasa 32 Mungu Anataka Tufanye Nini? itakusaidia kupata ujuzi huu. Unaweza kupata broshua hiyo kwa kujaza karatasi iliyo kwenye ukurasa wa 32 na kuipeleka kwa I.B.S.A., Box 47788, Nairobi, Kenya, au kwa kutumia anwani ihusuyo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8-10]
Ahadi za Mungu
Udugu wa Ulimwenguni Pote Wenye Upendo
“Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.
Hakuna Uhalifu Wala Vita Tena Kamwe
“Waovu watatengwa na nchi.”—Mithali 2:22.
“[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:9.
Chakula Kizuri Tele
“Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.
Amani Kati ya Watu na Wanyama
“Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; . . . na mtoto mdogo atawaongoza.”—Isaya 11:6.
Ugonjwa, Uzee, na Kifo Zitaondolewa
“[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.
Ufufuo Kwenye Dunia wa Wapendwa Wetu Waliokufa
“Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [ya Yesu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.