Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 10/22 kur. 12-14
  • Naweza Kufanyaje Ukweli Uwe Mali Yangu Mwenyewe?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kufanyaje Ukweli Uwe Mali Yangu Mwenyewe?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jithibitishie Mwenyewe
  • Je, Una Shughuli Nyingi Sana Usiweze Kujifunza?
  • Shiriki Mambo Unayojifunza
  • Linda Mashirika Yako
  • Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Usiache Ukweli Ukuponyoke
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • “Nitatembea Katika Kweli Yako”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • ‘Endelea Kutembea Katika Kweli’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 10/22 kur. 12-14

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kufanyaje Ukweli Uwe Mali Yangu Mwenyewe?

“Nililelewa nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na sikuzote nilihisi kwamba ikiwa umelelewa namna hiyo, kwa kweli ulimjua Yehova. Jinsi nilivyokosea!”—Antoinette.

“KWELI ni nini?” Swali hilo maarufu liliulizwa na Pontio Pilato, aliyempeana Yesu ahukumiwe. (Yohana 18:38) Hata hivyo, kwa wazi Pilato alikusudia swali lake lenye dhihaka likatishe—badala ya kuanzisha—mazungumzo ya wazi. Kwa kweli hakupendezwa na “kweli.” Lakini vipi wewe? Je, wapendezwa na kweli?

Kwa muda mrefu wanafalsafa wamefikiria kwa uzito kweli ni nini, kukiwa na matokeo kidogo yenye kuaibisha juu ya jitihada zao. Hata hivyo, waweza kupata jibu la swali la Pilato. Yesu Kristo alifundisha kwamba Neno la Mungu ni kweli. Pia alijisema kuwa “kweli.” Na mtume Yohana aliandika: “Kweli zilikuja kuwa kupitia Yesu.” (Yohana 1:17; 14:6; 17:17) Kwa hiyo mafundisho yote ya Kikristo, ambayo baadaye yalikuja kuwa sehemu ya Biblia, pia yanaitwa “kweli” au “kweli ya habari njema.” (Tito 1:14; Wagalatia 2:14; 2 Yohana 1, 2) Mafundisho haya ya Kikristo yanatia ndani mambo kama vile jina la Mungu la kibinafsi, kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu, ufufuo, na fidia ya Yesu.—Zaburi 83:18; Mathayo 6:9, 10; 20:28; Yohana 5:28, 29.

Maelfu ya vijana wamefundishwa kweli ya Biblia na wazazi Wakristo. Lakini je, hili lamaanisha kwamba vijana hao ‘wanatembea katika kweli’? (3 Yohana 3, 4) Si lazima iwe hivyo. Kwa mfano, Jennifer mwenye umri wa miaka 20 alilelewa akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Akumbuka hivi: “Mama yangu alinipeleka kwenye mikusanyiko ya Mashahidi na kunigusia kwamba napaswa kufikiria ubatizo. ‘Singependa kamwe kuwa Shahidi,’ ndivyo nilivyofikiri. ‘Nataka kujifurahisha tu!’”

Vijana fulani huamini mambo waliyofunzwa, lakini wameshindwa kusitawisha uelewevu wenye kina wa kile ambacho Biblia hufundisha hasa. Kungeweza kutokea hatari gani? Yesu alionya kwamba watu fulani “hawana mizizi ndani yao wenyewe.” Watu kama hao waweza ‘kuendelea kuwako kwa wakati fulani; kisha mara tu dhiki au mnyanyaso utokeapo kwa sababu ya lile neno, wao hukwazika.’ (Marko 4:17) Wengine waweza kueleza imani yao inayotegemea Biblia kwa kiwango fulani, lakini hawajamjua Mungu kibinafsi. Mwanamke kijana anayeitwa Aneesa asema: “Sidhani kwamba nilikuwa na uhusiano halisi pamoja na Yehova nilipokuwa na umri mchanga zaidi . . . Nafikiri uhusiano huo ulitegemea uhusiano wa wazazi wangu pamoja na Yehova.”

Hali yako ikoje kwa habari hii? Je, Yehova ni Mungu wa wazazi wako tu? Au, je, waweza kusema kama mtunga-zaburi wa Biblia: “Mimi nakutumaini Wewe BWANA. Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu”? (Zaburi 31:14) Huenda ukahitaji ujasiri ili kukubali ukweli wa mambo. Kijana anayeitwa Alexander asema: “Hatua yangu ya kwanza ilikuwa kujichunguza kwa njia ya unyoofu.” Baada ya kujichunguza, huenda ukatambua kwamba hujapata kamwe kujithibitishia kweli (mafundisho yote ya Kikristo). Huenda ukakosa usadikisho imara, na hivyo maisha yako yakakosa kusudi, bila mwelekezo halisi.

Mara nyingi katika mikutano yao ya Kikristo, Mashahidi wa Yehova huimba wimbo wenye kichwa “Ufanye Ukweli Uwe Mali Yako Mwenyewe.”a Shauri hilo laweza kukufaa. Lakini waweza kufanyaje hivyo? Utaanzia wapi?

Jithibitishie Mwenyewe

Kwenye Waroma 12:2, twapata shauri la mtume Paulo: ‘Jithibitishie mwenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ Unaweza kufanyaje hivyo? Kwa kutwaa “ujuzi sahihi wa kweli.” (Tito 1:1) Wakazi wa kale wa jiji la Berea hawakukubali bila shaka yoyote mambo waliyosikia. Badala yake, ‘waliyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo [waliyokuwa wakijifunza] yalikuwa hivyo.’—Matendo 17:11.

Mkristo mchanga aliyeitwa Erin aliona uhitaji wa kufanya hivyo yeye mwenyewe. Akumbuka: “Nilifanya utafiti. Nilijiuliza, ‘Najuaje kwamba hii ndiyo dini ya kweli? Najuaje kwamba kuna Mungu anayeitwa Yehova?’” Kwa nini usianzishe programu yako mwenyewe ya funzo la kibinafsi? Waweza kuanza kwa kutumia kitabu chenye kutegemea Biblia Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele.b Kisome kwa uangalifu. Tazama Maandiko yote yaliyoonyeshwa na kuona jinsi yanavyohusiana na yale yanayosemwa. Waweza kushangaa kupata jinsi unavyohisi tofauti kuhusu kweli unapokuwa “mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli”!—2 Timotheo 2:15.

Mtume Petro alisema kwamba mambo fulani katika Biblia ni “magumu kuelewa,” na utapata jambo hili kuwa kweli. (2 Petro 3:16) Lakini roho ya Mungu yaweza kukusaidia ujue hata habari zilizo ngumu. (1 Wakorintho 2:11, 12) Sali ili kupata msaada wa Mungu unapokuwa na matatizo ya kuelewa jambo fulani. (Zaburi 119:10, 11, 27) Jaribu kufanya utafiti wa ziada katika vichapo vya Watch Tower Society. Ikiwa huna uhakika jinsi ya kufanya hivyo, omba msaada. Wazazi wako au labda washiriki fulani wakomavu wa kutaniko la Kikristo waweza kukusaidia.

Kumbuka, hujifunzi ili uwavutie wengine kwa ujuzi wako. Kijana anayeitwa Collin aeleza hivi: “Unapata kujua sifa za Yehova.” Chukua muda wa kutafakari yale unayosoma ili yapenye kabisa ndani ya moyo wako.—Zaburi 1:2, 3.

Jambo linaloweza kukusaidia pia ni kushirikiana na kutaniko kwenye mikutano ya Kikristo. Kwani, kama alivyoandika mtume Paulo, kutaniko ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Vijana fulani hulalamika kwamba mikutano ya Kikristo inachosha. “Lakini ikiwa hujitayarishi kwa ajili ya mikutano,” atukumbusha Collin mchanga, “basi hutanufaika kutokana nayo.” Kwa hiyo tayarisha habari kimbele. Mikutano hupendeza zaidi unapokuwa mshiriki—si mtazamaji tu.

Je, Una Shughuli Nyingi Sana Usiweze Kujifunza?

Ni kweli kwamba ni vigumu kupata wakati wa kujifunza ukiwa na kazi ya shule na kazi za nyumbani. Kijana anayeitwa Susan aandika: “Niling’ang’ana kwa miaka mingi kujua kwamba nilihitaji kujitayarisha kwa ajili ya mikutano na kufanya funzo la kibinafsi, na bado sikuweza kufanya hivyo.”

Susan alijifunza ‘kununua wakati’ kutokana na mambo yasiyo muhimu. (Waefeso 5:15, 16) Kwanza alitengeneza orodha ya mambo aliyohitaji kujifunza. Kisha akapanga wakati wa kujifunza mambo hayo. Lakini pia katika ratiba yake alitia ndani wakati fulani kwa ajili ya tafrija. Yeye ashauri: “Usipangie kila wakati jambo fulani. Sote twahitaji wakati wa kupumzika.” Yaelekea ratiba itakusaidia pia.

Shiriki Mambo Unayojifunza

Kutumia unayojifunza husaidia hasa kuyafanya yawe sehemu ya maisha yako. Jaribu kufundisha mtu mwingine. Mtunga-zaburi alisema: “Kinywa changu kitanena hekima, na fikira za moyo wangu zitakuwa za busara.”—Zaburi 49:3.

Ikiwa huziaibikii habari njema, hutasita kuzishiriki pamoja na wanashule na wengine uwezao kukutana nao. (Waroma 1:16) Kwa kutumia kwa faida fursa hizo kuongea na wengine kuhusu kweli, utakuwa ukitumia yale unayojifunza; na kwa njia hii utatia kweli ndani ya akili na moyo wako.

Linda Mashirika Yako

Wakristo fulani katika karne ya kwanza walifanya maendeleo mazuri ya kiroho. Lakini upesi mtume Paulo alihitaji kuwaandikia, akiwauliza: “Ni nani aliyewazuia msifulize kuitii kweli?” (Wagalatia 5:7) Jambo linalofanana na hilo lilimpata kijana anayeitwa Alex. Aungama kwamba jitihada zake za kujifunza Neno la Mungu zilidhoofishwa na “kushirikiana na mashirika mabaya.” Huenda pia ukahitaji kufanya mabadiliko fulani kwa habari hii ili ufanye maendeleo ya kiroho.

Kinyume cha hilo, mashirika mazuri yaweza kukusaidia kikweli ufanye maendeleo. Mithali 27:17 yasema: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.” Tafuta vigezo vizuri vya kuigwa—watu wanaoishi kupatana na kweli. Huenda ukawapata nyumbani kwenu kwenyewe. Jennifer mchanga akumbuka: “Babu alikuwa kielelezo changu kizuri zaidi. Sikuzote alitumia muda wa saa tatu akijitayarisha kwa ajili ya funzo letu la Biblia la kutaniko siku ya Jumapili. Aliangalia kila andiko kwenye somo katika tafsiri mbalimbali za Biblia na kuangalia maneno katika kamusi yake. Alikuwa stadi kuhusu mambo madogo yasiyojulikana sana ya Biblia. Ungemwuliza swali lolote na angepata jibu.”

Unapoifanya kweli iwe mali yako, unapata kitu chenye thamani—kitu ambacho huwezi kukidhabihu kwa hali yoyote ile. Kwa hiyo usiione kweli kuwa tu “dini ya wazazi wako” kamwe. Usadikisho wako wapaswa kuwa kama ule wa mtunga-zaburi aliyesema: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Kwa kujua kikweli yale yanayofundishwa na Biblia, kuyaamini, kushiriki itikadi zako na wengine, na zaidi ya yote, kuishi kwa kupatana na itikadi hizi, utaonyesha kwamba umeufanya ukweli uwe mali yako mwenyewe.

[Maelezo ya Chini]

a Kutoka kitabu cha wimbo Mwimbieni Yehova Sifa, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Jithibitishie mwenyewe kweli kwa kujifanyia utafiti na kuwa na funzo la kibinafsiy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki