Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 11/22 kur. 23-25
  • Kwa Nini Niishi Bila Wazazi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Niishi Bila Wazazi?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Si Kosa Lako
  • Jambo Lenye Kufadhaisha
  • Kupata Msaada
  • Kufurahisha Mioyo ya Wazazi Wako
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Vijana Mnagusa Mioyo ya Wazazi Wenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Wazazi—Wasaidieni Watoto Wenu Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 11/22 kur. 23-25

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Niishi Bila Wazazi?

“Maisha yalikuwaje bila wazazi? Naweza kusema yalikuwa yenye huzuni kwa sababu nyingi. Ni vigumu sana kukua bila shauku na upendo wa wazazi.”—Joaquín.

“Ugumu mkubwa niliopata ulikuwa wakati wazazi walihitaji kutia sahihi ripoti yangu ya shule. Nilihisi huzuni nyingi na upweke. Ningali nahisi hivyo nyakati fulani.” —Abelina mwenye umri wa miaka 16.

NI MSIBA wa nyakati zetu—mamilioni ya vijana kukua bila wazazi. Katika Ulaya Mashariki maelfu wamekuwa mayatima kwa sababu ya vita. Katika Afrika ugonjwa wa mlipuko wa UKIMWI umesababisha hali mbaya kama hiyo. Watoto fulani wametupwa tu na wazazi wao. Familia kadhaa zimetenganishwa na vita au msiba wa asili.

Hali kama hizi zilikuwa za kawaida pia katika nyakati za Biblia. Kwa kielelezo, hali mbaya ya yatima inatajwa tena na tena katika Maandiko. (Zaburi 94:6; Malaki 3:5) Katika nyakati hizo za kale vita na misiba mingineyo iligawanya familia pia. Hivyo, Biblia huzungumza juu ya msichana kijana aliyetenganishwa na wazazi wake alipochukuliwa na vikosi vya Washami.—2 Wafalme 5:2.

Labda wewe ni mmoja wa mamilioni ya vijana ambao vilevile hawana wazazi. Ikiwa ndivyo, unajua namna hali hiyo inavyoweza kutaabisha. Kwa nini jambo hili limekupata?

Si Kosa Lako

Je, wewe hujipata ukishangaa ikiwa Mungu anakutia nidhamu ya namna fulani? Au huenda ukawakasirikia wazazi wako kwa sababu walikufa—kana kwamba walifanya hivyo kimakusudi. Kwanza, uwe na uhakika kwamba Mungu hajakukasirikia. Wala wazazi wako hawakuamua kukuacha kimakusudi. Kifo ni fungu lenye kuhuzunisha la wanadamu wasiokamilika, na nyakati nyingine huwapata wazazi, watoto wao wakiwa wangali wachanga. (Waroma 5:12; 6:23) Inaonekana kwamba Yesu Kristo mwenyewe alipatwa na kifo cha baba yake mlezi aliyekuwa mpendwa wake, Yusufu.a Bila shaka jambo hili halikutukia kwa sababu ya dhambi yoyote aliyotenda Yesu.

Pia, tambua kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Jeuri, vita, na uhalifu zimeua kiholela mamilioni ya watu katika karne hii. Wengine wamekuwa wahasiriwa wa “wakati na tukio lisilotazamiwa,” linaloweza kumpata mtu yeyote. (Mhubiri 9:11, NW) Hata kifo cha wazazi wako kiwe kichungu namna gani, kwa wazi halikuwa kosa lako. Badala ya kujitesa kwa kujilaumu au kulemewa na kihoro, jipatie faraja katika ahadi ya Mungu ya ufufuo.b Yesu alitabiri: “Msistaajabie hili, kwa sababu saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Abelina, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, asema: “Nimesaidiwa sana na upendo wangu kwa Yehova na tumaini la ufufuo.”

Lakini vipi ikiwa wazazi wako wangali hai lakini wamekutupa? Mungu anawataka wazazi walee na kuwaandalia watoto wao. (Waefeso 6:4; 1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, kwa kusikitisha, wazazi fulani kwa njia yenye kushtua wameshindwa kuwaonyesha watoto wao “shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:3) Kwa wengine, kutupwa huwa ni tokeo la ufukara wa kupindukia, uraibu wa dawa za kulevya, kufungwa jela, au uraibu wa vileo. Kwa wazi, kuna wazazi ambao pia huwatupa watoto wao kwa sababu tu ya ubinafsi. Hata sababu iwe ni nini, kutenganishwa na wazazi ni jambo lenye kuvunja moyo. Lakini hii haimaanishi kwamba una kasoro fulani au kwamba unapaswa kujitesa kwa kuhisi hatia. Kwa kweli, ni wazazi wako wanaopaswa kumjibu Mungu kuhusu namna ambavyo umetendwa. (Waroma 14:12) Bila shaka, ikiwa wazazi wako wamelazimika kutengana nawe kwa sababu ya hali wasizoweza kuzidhibiti, kama vile msiba wa asili au ugonjwa, basi hakuna mtu apaswaye kulaumiwa! Kuna tumaini la kuunganishwa tena sikuzote, hata ikiwa tumaini hilo laonekana kuwa dogo sana nyakati fulani.—Linganisha Mwanzo 46:29-31.

Jambo Lenye Kufadhaisha

Kwa wakati huu, waweza kukabili matatizo mengi mazito. Uchunguzi uliofanywa na shirika la Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa, ulioitwa Children in War, wafunua hivi: “Watoto wasioambatana na mtu mzima ndio watoto wanaopatwa na madhara kwa urahisi—wale ambao . . . wanakabili hali ngumu sana ili kuokoka, hukosa utegemezo wa ukuzi wa asili na hutendwa vibaya. Kutenganishwa na wazazi kwaweza kuwa mojawapo ya hasara yenye kufadhaisha zaidi kwa mtoto.” Labda unajipata ukipigana na hisia za kuvunjika moyo na mfadhaiko.

Mkumbuke Joaquín, aliyetajwa hapo mapema. Wazazi wake walitengana na kuwatupa yeye na ndugu na dada zake. Wakati huo alikuwa na umri wa mwaka mmoja tu na alilelewa na dada zake wakubwa. Aeleza hivi: “Nilikuwa nikiuliza kwa nini hatukuwa na wazazi kama marafiki zangu. Na nilipoona baba akicheza na mwana wake, nilitamani kwamba angekuwa baba yangu.”

Kupata Msaada

Hata iwe vigumu namna gani kulelewa bila wazazi, haimaanishi kwamba utakosa kufaulu maishani. Kwa msaada na utegemezo, unaweza si kuishi tu bali kusitawi. Huenda likawa jambo gumu kuamini, hasa ikiwa unapambana na huzuni na kihoro. Hata hivyo, tambua kwamba hisia za namna hiyo ni za kawaida na kwamba hazitakusumbua milele. Katika Mhubiri 7:2, 3, twasoma: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu . . . Huzuni ni afadhali kuliko kicheko, maana simanzi ya uso ni faida ya moyo.” Naam, ni jambo la kawaida na la kiafya kulia na kuwa na huzuni upatwapo na msiba. Huenda ukaona kuwa inasaidia pia kumwambia siri rafiki anayeelewa hali au mshiriki aliyekomaa wa kutaniko na kumweleza maumivu unayohisi.

Kweli, waweza kushawishwa ujitenge. Lakini Mithali 18:1 yaonya: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.” Ni bora kutafuta msaada wa mtu mwenye fadhili na anayeelewa hali. Yasema Mithali 12:25: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” Unaweza kupata hilo “neno jema” tu ukimwambia mtu fulani kuhusu “uzito katika moyo wako.”

Unaweza kuongea na nani? Tafuta msaada ndani ya kutaniko la Kikristo. Yesu anaahidi kwamba hapo unaweza kuwapata “akina ndugu na akina dada na akina mama” watakaokupenda na kukuhangaikia. (Marko 10:30) Joaquín akumbuka hivi: “Kushirikiana na ndugu Wakristo kulinifanya nione maisha kwa njia tofauti. Hudhurio la mikutano la kawaida lilinifanya nimpende Yehova zaidi na kutaka kumtumikia. Ndugu wakomavu waliipa familia yetu msaada wa kiroho na shauri. Leo, baadhi ya ndugu zangu ni wahudumu wa wakati wote.”

Pia, kumbuka kwamba Yehova ni “baba wa yatima.” (Zaburi 68:5, 6) Nyuma katika nyakati za Biblia, Mungu aliwatia moyo watu wake washughulike na mayatima kwa njia ya rehema na ya haki. (Kumbukumbu la Torati 24:19; Mithali 23:10, 11) Hata sasa anahangaikia vijana wasiokuwa na wazazi kwa namna ileile. Kwa hiyo mwendee Mungu katika sala, ukiwa na uhakika wa kwamba anakujali na kwamba atakujibu. Mfalme Daudi aliandika: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake. Umngoje BWANA, uwe hodari, upige moyo konde.”—Zaburi 27:10, 14.

Ijapokuwa hivyo, kijana asiyekuwa na wazazi hukabili magumu mengi siku kwa siku. Utaishi wapi? Utajiruzukuje? Makala ya wakati ujao itazungumzia jinsi baadhi ya magumu hayo yanavyoweza kushindwa kwa mafanikio.

[Maelezo ya Chini]

a Kabla ya kifo chake, Yesu alimkabidhi mwanafunzi wake Yohana daraka la kumtunza mama yake, jambo ambalo haielekei lingetokea iwapo baba yake mlezi, Yusufu, angekuwa angali hai.—Yohana 19:25-27.

b Kwa habari kuhusu kukabiliana na kifo cha mzazi, ona makala za “Vijana Huuliza . . .” katika matoleo ya Amkeni! ya Agosti 22, na Septemba 8, 1994.

[Blabu katika ukurasa wa 24]

“Nimesaidiwa sana na upendo wangu kwa Yehova na tumaini la ufufuo”

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nyakati fulani waweza kujawa na hisia za upweke

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kuna marafiki wawezao kukusaidia na kukutia moyo kutanikoni

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki