Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Misitu ya Mvua Asanteni kwa habari iliyo wazi na yenye kufariji mliyochapisha kuhusu misitu ya mvua. (Mei 8, 1998) Inasikitisha kuona jinsi ambavyo kichaa na pupa ya binadamu zinaharibu sayari yetu pamoja na wanyama na mimea yake yenye thamani. Ninafurahi ninapofikiri kwamba upesi Muumba wetu Mtukufu, Yehova, ataingilia mambo na kulinda kito hiki chenye thamani pamoja na viumbehai vyake.
F. A., Brazili
Ninafurahi kusema kwamba makala yenu imekuwa yenye kuelimisha sana juu ya matatizo mengi na masuala yanayohusu kuharibiwa kwa misitu ya mvua leo. Ningependa kuwashukuru hasa kwa kuandaa habari iliyo katika fungu la mwisho—uhakika wa kwamba kuna tumaini kwa misitu yetu inayobaki na kwamba kizazi kinachokuja cha misitu ya mvua kwa kweli kitasitawi.
J. T., Australia
Nimemaliza tu kusoma makala bora ya gazeti la Amkeni! nililopewa na mgeni mwenye urafiki ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mimi ni mshiriki wa Sosaiti ya Ikolojia ya Chuo Kikuu cha Edinburgh, nikiwa nimepokea digrii ya elimu-misitu kwenye Chuo Kikuu cha Edinburgh katika mwaka wa 1939. Tulifundishwa mambo mengi kuhusu msitu wa mvua wa kitropiki. Ninawapongeza pamoja na wasaidizi wenu kwa mfululizo wa makala bora “Je, Misitu Yetu ya Mvua Yaweza Kuokolewa?” Nilisoma makala hizo kikamili. Tengenezo lenu la kidini na lisitawi! Litasitawi.
L. M., Uingereza
Mwaka wa 2000 Makala “Maoni ya Biblia: Mwaka wa 2000 Ni Wenye Maana Kadiri Gani?” katika toleo la Amkeni! la Mei 8, 1998 ilikuwa kikumbusha chenye kufurahisha. Ninathamini jinsi ambavyo mnapinga kwa wazi mwelekeo wowote wa kukisia na ufuatiaji-haki wenu katika kueleza taarifa zilizopita kuhusu mpangilio wa siku ya Yehova.
S. W., Marekani
Washindi Wajapokabiliwa na Kifo Ni furaha kuwaandikia na kuwashukuru kwa kuchapisha masimulizi ya maisha ya ndugu zetu wakati wa vita ya ulimwengu ya pili na baadaye, makala kama zile zilizo katika mfululizo “Washindi Wajapokabiliwa na Kifo.” (Mei 8, 1993) Mfululizo huo wa makala ulinichochea niendelee kumtumikia Yehova, nikifuata hatua za Mashahidi wake washindi. Hata tisho la kifo halikuwazuia kumpenda Yehova.
A. A., Albania
Uhai na Kifo Katika Kambodia Asanteni kwa makala “Safari Yangu Ndefu Kutoka Katika Uhai na Kifo Katika Kambodia.” (Mei 8, 1998) Inafurahisha kumtumikia Yehova kwa uaminifu na kujua kwamba kama Wathana Meas, ambaye akiwa askari-jeshi aliwaua wengine ili aokoke, wengi wanamtumikia Yehova licha ya kumbukumbu zenye kuhuzunisha. Nilishtuka kusoma kwamba alitumia miezi mitatu akiwa amefichwa ndani ya shimo. Hakutambua kwamba baada ya muda mfupi angepata pendeleo kubwa zaidi maishani mwake—kumjua Yehova!
C. M. S. L., Brazili
Je, Wewe Huhukumu kwa Kutazama Sura? Sura zaweza kudanganya, kama ilivyotolewa kielezi na hadithi kuhusu Nasreddin Hoja. (Mei 8, 1998) Asanteni kwa kutukumbusha kwamba hatupaswi kuwahukumu wengine ifaavyo au isivyofaa kwa kutegemea tu sura yao—na kwamba Yehova hutuhukumu kwa kutegemea hali yetu ya moyo, si kwa kutazama sura zetu.
A. O. F. A., Brazili
Upendo Haushindwi Kamwe Natoa shukrani zangu kutoka moyoni kwa makala fupi, iliyo bora “‘Upendo Haushindwi Kamwe’—Je, Wewe Hushindwa Kuuonyesha?” (Mei 8, 1998) Mawazo yaliyotokezwa kuhusiana na pande mbalimbali za upendo wa kweli yalinichochea sana na kunitia moyo, hasa kwa sababu makala hiyo ilifika wakati tu nilipohitaji msaada. Sasa nimesadikishwa kwamba licha ya hali zozote, upendo wa kweli haushindwi kamwe.
S. G., Ufaransa